Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 5/15 kur. 25-28
  • Kutaniko la Kikristo—Chanzo cha Msaada Wenye Kutia Nguvu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutaniko la Kikristo—Chanzo cha Msaada Wenye Kutia Nguvu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Utegemezo na Msaada
  • Msaada wa Waangalizi Wenye Upendo
  • Msaada wa Kweli Katika Wakati Unaofaa
  • Hekima Kutoka Juu
  • Tianeni Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Kutaniko na Lijengwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kutaniko na Limsifu Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Fanya Zaidi ya Kusema Tu: ‘Ukaote Moto na Kushiba’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 5/15 kur. 25-28

Kutaniko la Kikristo—Chanzo cha Msaada Wenye Kutia Nguvu

POPI, mwanamke ambaye ana umri wa miaka 20 hivi, alikuwa amevunjika moyo kwa sababu ya hali yenye kusababisha uchungu inayohusu ukosefu wa mawasiliano yenye unyoofu pamoja na wazazi wake.a Baada ya kuongea kindani na mzee Mkristo na mke wake, yeye aliwaandikia hivi: “Asanteni sana kwa kutumia wakati wenu kuzungumza nami. Hamjui jinsi ninavyohisi kwa sababu mnanijali. Namshukuru Yehova kwa kunipa watu ninaoweza kutumaini na kuzungumza nao.”

Toula, mwanamke aliyefiwa na mume hivi karibuni na aliye na watoto wawili matineja, alikuwa na matatizo yenye kusumbua ya kihisia-moyo na ya kifedha. Yeye na watoto wake walitembelewa kwa ukawaida na kutiwa nguvu na wenzi Wakristo kutoka kutanikoni. Baada ya kukabiliana na hali yake kwa mafanikio, aliwapelekea wenzi hao kadi, iliyosema: “Mimi huwakumbuka katika sala zangu sikuzote. Nakumbuka jinsi mlivyonisaidia na kunitegemeza mara nyingi.”

Je, nyakati nyingine wewe huhisi kwamba ‘umelemezwa mizigo’ na misongo inayoongezeka ya ulimwengu huu? (Mathayo 11:28) Je, “wakati na tukio lisilotazamiwa” limetia maisha yako mambo yenye kuumiza? (Mhubiri 9:11, NW) Basi si wewe peke yako. Wewe pia unaweza kupokea msaada unaofaa katika kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova, kama vile ambavyo maelfu ya watu wenye kusononeka tayari wameona. Katika karne ya kwanza W.K., mtume Paulo aliona kwamba baadhi ya waamini wenzake walikuwa ‘msaada wenye kutia nguvu’ hasa kwake. (Wakolosai 4:10, 11) Wewe pia waweza kutiwa nguvu hivyo.

Utegemezo na Msaada

Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno “kutaniko” hutafsiriwa kutoka kwa neno la Kigiriki ek·kle·siʹa, linalomaanisha kikundi cha watu waliokutanishwa pamoja. Kiasili neno hilo humaanisha umoja na kutegemezana.

Kutaniko la Kikristo hutegemeza kweli ya Neno la Mungu na hutangaza habari njema za Ufalme wake. (1 Timotheo 3:15; 1 Petro 2:9) Hata hivyo, kutaniko huandaa pia utegemezo wa kiroho na msaada kwa wale wanaoshirikiana nalo. Katika kutaniko mtu aweza kupata kikundi cha marafiki wenye upendo, wanaomhangaikia, na wanaojali, walio tayari na wanaopenda kusaidia na kufariji wengine nyakati za shida.— 2 Wakorintho 7:5-7.

Sikuzote waabudu wa Yehova wamepata usalama katika kutaniko. Mtunga-zaburi alisema kwamba alifurahi na kuhisi akiwa salama miongoni mwa kutaniko la watu wa Mungu. (Zaburi 27:4, 5; 55:14; 122:1) Vivyo hivyo leo, kutaniko la Kikristo ni ushirika wa waamini wenzi wanaojengana na kutiana moyo.—Mithali 13:20; Waroma 1:11, 12.

Washiriki wa kutaniko hufundishwa ‘kufanya lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zao.’ (Wagalatia 6:10) Elimu inayotegemea Biblia wanayopokea huwachochea kudhihirisha upendo wa kidugu na shauku nyororo kwa mtu na mwenzake. (Waroma 12:10; 1 Petro 3:8) Ndugu na dada wa kiroho katika kutaniko huchochewa kuwa wenye fadhili, wenye kufanya amani, na wenye huruma nyororo. (Waefeso 4:3) Badala ya kuwa tu waabudu wasiotenda, wao huonyesha wengine hangaiko lenye upendo.— Yakobo 1:27.

Kwa hiyo, wale waliopondeka hupata hali changamfu yenye mazingira ya kifamilia ndani ya kutaniko. (Marko 10:29, 30) Hisia ya kuwa katika kikundi chenye umoja na upendo huwatia nguvu. (Zaburi 133:1-3) Kupitia kutaniko, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huandaa ‘chakula kinachotia nguvu kwa wakati ufaao.’—Mathayo 24:45.

Msaada wa Waangalizi Wenye Upendo

Washiriki wa kutaniko la Kikristo wanaweza kutarajia kupata kutanikoni wachungaji wenye upendo, uelewevu, na wenye sifa ya kustahili ambao huandaa utegemezo wa kiroho na kitia-moyo. Wachungaji wenye sifa hizo ni kama “mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba.” (Isaya 32:1, 2) Wazee au waangalizi waliowekwa rasmi na roho, hutunza watu wa Mungu wenye mfano wa kondoo, huwatia moyo walio wagonjwa na wenye kushuka moyo, nao hujaribu kuwarudisha katika hali nzuri wale waliotenda dhambi.—Zaburi 100:3; 1 Petro 5:2, 3.

Bila shaka, baraza la wazee la kutaniko si kikundi cha wanatiba wa kitaaluma, wanaoweza kuponya magonjwa ya kimwili na ya kiakili ya waamini wenzao. Katika mfumo huu wa mambo, wale wanaougua bado ‘wanahitaji tabibu.’ (Luka 5:31) Hata hivyo, wachungaji hawa wanaweza kuwasaidia wale walio wagonjwa kiroho. (Yakobo 5:14, 15) Iwezekanapo, wazee hupanga pia kutoa msaada wa aina nyingine.—Yakobo 2:15, 16.

Ni nani mwanzilishi wa mpango huo wenye upendo? Yehova Mungu mwenyewe! Nabii Ezekieli amwonyesha Yehova akitangaza hivi: “Nitawafuta kondoo zangu, na kuwaulizia. . . . Nitawaokoa katika mahali pote walipotawanyika . . . Mimi mwenyewe nitawalisha kondoo zangu, nami nitawalaza.” Mungu anahangaikia pia kondoo walio wanyonge na dhaifu.— Ezekieli 34:11, 12, 15, 16.

Msaada wa Kweli Katika Wakati Unaofaa

Je, kweli msaada halisi unaweza kupatikana katika kutaniko la Kikristo? Ndiyo, na mifano ifuatayo inatoa kielelezo cha hali mbalimbali ambapo kutaniko huthibitika kuwa lenye msaada.

◆ Kumpoteza mpendwa katika kifo. Mume wa Anna alikufa baada ya kuugua kwa muda mrefu. “Tangu wakati huo, nimekuwa nikionyeshwa upendo mchangamfu na udugu wa Kikristo,” yeye asema. “Maneno yenye fadhili na yenye kutegemeza na kitia-moyo kutoka kwa waamini wenzangu, kutia ndani makumbatio yao machangamfu, yamenitia nguvu na kuniepusha na mshuko-moyo, na namshukuru Yehova. Upendo wao umenifanya nihisi nimetegemezwa sana, nimetiwa moyo hatimaye, na kutunzwa kwa wororo.” Wewe pia huenda umepatwa na mfadhaiko wa kumpoteza mpendwa wako katika kifo. Katika pindi hizi, washiriki wa kutaniko wanaweza kuandaa faraja na utegemezo wa kihisia-moyo unaohitajiwa sana.

◆ Ugonjwa. Arthur, mwangalizi asafiriye kutoka Poland, alizuru kwa kawaida makutaniko katika Asia ya Kati ili kuyatia nguvu kiroho. Katika mojawapo ya ziara hizo, akawa mgonjwa sana na alipokuwa akipata nafuu matatizo makubwa yakaibuka. “Ninataka kuwaambia jinsi ambavyo ndugu na dada katika [mji mmoja huko Kazakhstan] walivyonitunza,” Arthur akumbuka akiwa na uthamini mkubwa. “Akina ndugu na dada, ambao hata sikujua wengi wao—na hata watu wenye kupendezwa—waliniletea fedha, vyakula, na dawa. . . . Nao walifanya hivyo kwa shangwe kuu.

“Wazia jinsi nilivyohisi nilipopokea bahasha iliyokuwa na fedha na barua ifuatayo: ‘Ndugu Mpendwa, pokea salamu zangu changamfu. Mama alinipa fedha ili ninunue aiskrimu, lakini nimeamua kukupa fedha hizo ili ununue dawa. Tafadhali pata nafuu haraka. Yehova anatuhitaji kwa muda mrefu. Pokea salamu zangu. Na utusimulie hadithi nyinginezo nzuri, na zenye kufundisha. Vova.’” Naam, kama mfano huu unavyoonyesha, watoto wachanga na watu wazima katika kutaniko wanaweza kuandaa msaada wenye kutia nguvu nyakati za ugonjwa.—Wafilipi 2:25-29.

◆ Mshuko-moyo. Teri alikuwa na tamaa ya moyoni ya kutumikia akiwa painia, au mpiga-mbiu wa Ufalme wa wakati wote. Hata hivyo, kwa sababu ya magumu alilazimika kuacha upainia. “Nilihisi hatia kubwa sana kwa kujaribu kutumikia nikiwa painia na nisiweze hata kudumu kwa mwaka mzima,” yeye asema. Teri aliamini kwa makosa kwamba kibali cha Yehova kilitegemea kiasi cha utumishi wake kwake. (Linganisha Marko 12:41-44.) Akiwa ameshuka moyo sana, alijitenga na wengine. Kisha akapata msaada wenye kuburudisha kutoka kwa kutaniko.

Teri asema: “Dada mmoja painia mwenye umri mkubwa alinisaidia kwa kunisikiliza nilipokuwa nikimweleza ninavyohisi. Nilipotoka kwake, nilihisi kana kwamba nilikuwa nimeondolewa uzito mkubwa. Kuanzia wakati huo na kuendelea, dada huyu painia na mumewe, aliye mzee katika kutaniko, waliandaa msaada wenye manufaa. Walinipigia simu kila siku kunijulia hali. . . . Kuna pindi ambazo wamenikaribisha katika funzo lao la familia, jambo ambalo limekazia akilini mwangu umuhimu wa familia kuwa pamoja.”

Ni jambo la kawaida kwa wengi—hata kwa Wakristo waliojiweka wakfu— kushuka moyo, kuvunjika moyo, na kuhisi upweke. Tunapaswa kuwa wenye shukrani kama nini kwa kuwa msaada wenye upendo na usio na ubinafsi hupatikana ndani ya kutaniko la Mungu!—1 Wathesalonike 5:14.

◆ Misiba na aksidenti. Jitie katika hali ya familia moja ya watu wanne iliyopoteza mali zote wakati nyumba yao ilipochomeka. Baada ya muda walipata kile walichokiita “jambo lenye kutia moyo litakalogusa moyo wetu milele na ambalo lilikazia akilini mwetu upendo wa kweli miongoni mwa watu wa Yehova.” Wao waeleza: “Punde si punde tulipokea simu kutoka kwa ndugu na dada zetu wa kiroho wenye moyo mweupe wakitoa utegemezo na kutuliwaza. Simu ililia daima. Hangaiko na upendo halisi kutoka kwa kila mtu ulitugusa sana hivi kwamba tulitokwa na machozi ya shukrani.”

Muda si muda, wazee wa kutaniko walipanga kikundi kikubwa cha akina ndugu, na baada ya siku chache wakajengea familia hii nyumba mpya. Jirani mmoja alisema hivi kwa mshangao: “Unapaswa kuona! Watu wa kila aina wanafanya kazi hapo—wanaume, wanawake, weusi, na watu wa Kihispania!” Huu ulikuwa uthibitisho wa wazi wa upendo wa kidugu.—Yohana 13:35.

Wakristo wenzi waliipa pia familia hiyo mavazi, chakula, na fedha. Baba yao asema hivi: “Huu ulikuwa wakati wa msimu wa Krismasi wakati ambapo kila mtu anatoa zawadi, lakini tunaweza kusema kwa unyoofu kwamba hakuna mtu awaye yote aliyefurahia ukarimu mkubwa na wa moyo mweupe kama sisi.” Nao waongezea hivi: “Kumbukumbu za moto huo sasa zinaondolewa na kumbukumbu nzuri sana za matendo yenye fadhili na marafiki wema. Twamshukuru sana Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo, Yehova, kwa sababu tuna familia yenye kustaajabisha, na yenye umoja ya ndugu duniani, nasi tunashukuru sana kwa sababu ya kuwa sehemu yake!”

Bila shaka, haiwezekani kuandaa, wala kutarajia, msaada kama huo kila msiba unapotukia. Lakini kisa hiki chatoa mfano wa utegemezo ambao kutaniko laweza kuandaa.

Hekima Kutoka Juu

Watu wengi wamepata chanzo kingine cha msaada na nguvu katika kutaniko la Kikristo. Chanzo hicho ni kipi? Vichapo vinavyotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Vyenye kutokeza miongoni mwa vichapo hivyo ni majarida ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ili kuandaa shauri lenye hekima na maagizo yanayotumika, vichapo hivi hutegemea hasa hekima ya kimungu inayopatikana katika Biblia. (Zaburi 119:105) Kuongezea habari za Kimaandiko zinazozungumziwa, utafiti wenye kina na wenye kutegemeka hufanywa juu ya habari kama vile mshuko wa kiakili, kupata nafuu baada ya kutendwa vibaya, matatizo mbalimbali ya kijamii na kiuchumi, magumu yanayowapata vijana, na magumu yapatikanayo hasa katika nchi zinazositawi. Na zaidi ya yote, vichapo hivi hutegemeza njia ya Mungu kuwa ndiyo njia bora zaidi ya maisha.— Isaya 30:20, 21.

Kila mwaka, Watch Tower Society hupokea maelfu ya barua za kuonyesha uthamini. Kwa mfano, kuhusu makala moja juu ya kujiua kwenye Amkeni!, kijana mmoja huko Urusi aliandika hivi: “Kwa sababu ya mwelekeo wangu wa kushuka moyo, . . . Mara nyingi nimefikiria kujiua. Makala hii ilitia nguvu itikadi yangu ya kwamba Mungu atanisaidia kukabiliana na matatizo yangu. Anataka niishi. Namshukuru yeye kwa sababu ya utegemezo alioutoa kupitia makala hii.”

Taabu za ulimwengu huu ziongezekapo na kuonekana kuwa ngumu kushughulika nazo, uwe na uhakika wa kwamba kutaniko la Kikristo ndilo mahali salama. Kwa kweli, ikiwa hali ngumu ya mfumo huu usio na upendo inakudhoofisha, unaweza kupata chanzo cha nguvu katika tengenezo la Yehova. Baada ya kupata utegemezo huo, huenda ukahisi kama mwanamke mmoja Mkristo aliyekabiliana kwa mafanikio na ugonjwa mbaya wa mume wake na kuandika hivi: “Kwa sababu ya upendo tulioonyeshwa na utunzaji tuliopewa, ninahisi kana kwamba Yehova alitubeba kwenye kitanga cha mkono wake kupitia kwa tatizo hili. Jinsi nilivyo mwenye shukrani kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova lenye utukufu!”

[Maelezo ya Chini]

a Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Tunaweza kuandaa msaada wenye kuimarisha wagonjwa, waliofiwa, na wengineo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki