Msongo wa Marika—Je, Waweza Kutumiwa kwa Manufaa Yako?
Sisi sote tunazaliwa na tamaa ya msingi ya kutaka kukubaliwa na marika wetu. Hakuna mtu asiyetaka kupendwa, atakaye kukataliwa. Hivyo, marika wetu hutuathiri kwa viwango vyenye kutofautiana.
RIKA hufafanuliwa kuwa “mtu anayelingana na mwingine, . . . mtu wa kikundi kilekile cha kijamii, hasa ikitegemea umri, cheo, au hadhi.” Hivyo basi, msongo wa marika ni kani inayotuathiri kutoka kwa marika, hivi kwamba, iwe twajua au hatujui, twajikuta tukifikiri au kutenda kama wao. Msongo wa marika mara nyingi huonwa vibaya. Hata hivyo, kama tutakavyoona, twaweza kuutumia kwa manufaa yetu.
Uvutano kwa Watu wa Kila Umri
Msongo wa marika si kwa vijana tu; huathiri watu wa kila umri. Uvutano wake huonekana tunapojiuliza maswali kama haya: “Wengine wanafanya jambo hilo, kwa nini mimi nisifanye?” “Kwa nini lazima sikuzote niwe tofauti?” “Wengine watafikirije au watasemaje?” “Rafiki zangu wote wanawekeana miadi ya kijinsia na kuoa, lakini mimi sivyo. Kwani nina kasoro gani?”
Ijapokuwa kupatanishwa kulingana na msongo huathiri watu wa kila umri, yaelekea huathiri sana wakati wa kubalehe. Kichapo The World Book Encyclopedia chasema kwamba “wabalehe wengi hujiingiza kabisa katika rika lao—yaani, kikundi cha rafiki zao na watu wanaowafahamu. Matineja hawa hutafuta kibali cha rika lao, badala ya kibali cha wazazi wao, na huenda wakabadili tabia yao ili kupata kibali hicho.” Chaongeza kusema kwamba matineja “hudhania wanaendelea kama kawaida marika wao wakiwakubali na kuwapenda.” Kwa sababu hiyo wao “hukazia mambo wanayofikiri yanaathiri kupendwa kwao, kama vile mtindo wa kuvaa kwao, uwezo wa kuongoza, na kufanikiwa katika miadi ya kijinsia.”
Huenda wenzi waliooana wakagundua kwamba maamuzi yao kuhusu aina ya nyumba watakayonunua au kupangisha, aina ya gari la kununua, kama wawe na watoto au wasiwe nao, na mambo mengine mengi yanatokana na uvutano wa msongo wa marika—jambo linalokubalika katika jamii yao, miongoni mwa washiriki wao au kabila lao. Familia nyingine hata hujitia katika deni kubwa ili tu waweze kushindana na jirani na marika wao katika kupata vitu vya kimwili. Ndiyo, miradi yetu, kufikiri kwetu, na maamuzi yetu mara nyingi huonyesha dhahiri nguvu yenye hila ya msongo wa marika. Kwa kufikiria nguvu hiyo, je, twaweza kushughulika na msongo wa marika kwa manufaa yetu, kutusaidia twelekee tunakotaka kwenda? Bila shaka twaweza!
Kutumia Vizuri Uvutano wa Marika Unaofaa
Madaktari na wataalamu wengine wa afya wanajua thamani ya kuwazingira wagonjwa wao na watu wenye mwelekeo unaofaa na kwa uvutano mwingine wenye kujenga. Mazingira hayo yanaweza kuchochea kupona. Kwa mfano, watu ambao wamepoteza kiungo mara nyingi husaidiwa kupitia utaratibu wa kuwezeshwa kuishi maisha ya kawaida na kupona kihisia-moyo kwa kielelezo kizuri na kitia-moyo cha wengine ambao wamepatwa na jambo hilohilo. Ni dhahiri kwamba, kujiingiza katika mazingira yenye kujenga yanayotia ndani vigezo vya kuigwa vyenye mtazamo unaofaa, ni njia mojawapo ya kutumia vizuri aina ifaayo ya msongo wa marika.
Kanuni hii yatumika vilevile katika kutaniko la Kikristo, kwa kuwa uvutano wa marika ufaao ni mojawapo ya sababu ambazo Yehova ameelekeza watu wake wakutane kwa ukawaida. Mungu hutuhimiza ‘tuchocheane kwenye upendo na kazi zilizo bora na kutiana moyo.’ (Waebrania 10:24, 25) Kitia-moyo hicho ni chenye thamani kwa sababu ya misongo mingi isiyojenga na yenye kuumiza katika ulimwengu wa leo. Kwa sababu ya misongo hii, Wakristo lazima ‘wajikakamue kisulubu’ ili wadumu wakiwa na nguvu kiroho. (Luka 13:24) Kwa hiyo, twahitaji na kuthamini tegemezo lenye upendo kutoka kwa waamini wenzetu. Kwa kuongezea, huenda wengine wakahitaji kuvumilia ‘miiba katika mwili,’ labda ugonjwa au ulemavu. (2 Wakorintho 12:7) Huenda ikawa wengine wanang’ang’ana kushinda mazoea mabaya au mshuko wa moyo, au huenda wakaona kuwa jambo gumu kuendelea kushughulikia mahitaji ya maisha. Kwa hiyo, tutakuwa wenye hekima tukishirikiana na watu wanaomkaribia Yehova Mungu na ambao wanafurahia kumtumikia. Marika wa aina hiyo watatuchangamsha na kutusaidia ‘kuvumilia kwa uaminifu hadi mwisho.’—Mathayo 24:13.
Kwa kuchagua marika wanaofaa, ndipo tutakapoweza kudhibiti uvutano wao kwetu. Kwa kuongezea, chakula kizuri cha kiroho na mwongozo unaofaa tunaopata kwenye mikutano ya Kikristo huimarisha kitia-moyo tupatacho kutoka kwa marika wetu.
Bila shaka, kufika kwenye mikutano ya Kikristo si rahisi sikuzote. Huenda wengine wakategemezwa kidogo au hata wasitegemezwe na wenzi wao wa ndoa, huenda wengine wakalazimika kutayarisha watoto, na usafiri waweza kuwa tatizo la wengine pia. Lakini fikiria: Usiporuhusu vizuizi hivi vikuzuie, kielelezo chako chaweza kuchochea wengine ambao huenda wakawa wanashindana na hali kama hizo. Yaani, wewe na wengine wanaofanana nawe huweka kielelezo chema na vilevile aina ijengayo ya msongo wa marika—bila kudokeza kwamba walazimishwa.
Kwa kweli, mtume Paulo, ambaye yeye mwenyewe alishindana na magumu na vizuizi vingi, alitia moyo Wakristo waige kielelezo chake na kile cha Wakristo wengine wakomavu. Alisema hivi: “Kwa muungano iweni waigaji wangu, akina ndugu, na fulizeni kuwaangalia wale wanaotembea katika njia ilinganayo na kielelezo mlicho nacho katika sisi.” (Wafilipi 3:17; 4:19) Wakristo wa mapema katika Thesalonike waliiga kielelezo kizuri cha Paulo. Paulo aliandika hivi kuwahusu: “Mkawa waigaji wetu na wa Bwana, kwa vile mlilipokea neno chini ya dhiki nyingi pamoja na shangwe ya roho takatifu, hivi kwamba nyinyi mlipata kuwa kielelezo kwa waamini wote katika Makedonia na katika Akaya.” (1 Wathesalonike 1:6, 7) Mtazamo wetu na kielelezo chetu kinachofaa chaweza kuwa na matokeo hayohayo kwa wale tunaoshirikiana nao.
Epuka Uvutano Usiojenga
Ikiwa twataka kuepuka msongo wa marika usiojenga, lazima tukinze uvutano wa ‘wale wenye kutembea kupatana na mwili.’ (Waroma 8:4, 5; 1 Yohana 2:15-17) Tusipofanya hivyo, msongo wa marika wenye kuumiza utatupeleka mbali na Yehova na shauri lake lenye hekima. Mithali 13:20 husema: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” Je, waweza kufikiri juu ya mtu aliyeumia kwa sababu ya msongo wa marika usiojenga? Kwa mfano, Wakristo wengine wameongozwa kwenye ufuatiaji wa vitu vya kimwili, ukosefu wa adili, au matumizi mabaya ya dawa za kulevya na kileo kwa sababu ya uvutano wa marika wao.
Hata katika kutaniko la Kikristo, twaweza kuwa chini ya uvutano wa msongo wa marika usiojenga tukichagua watu waliodhoofika kiroho wawe washiriki wetu. (1 Wakorintho 15:33; 2 Wathesalonike 3:14) Watu kama hao mara nyingi hawaelekei kuzungumza mambo ya kiroho; huenda hata wakawadhihaki wale wanaofurahia mazungumzo kama hayo. Tukichagua watu hao wawe washiriki wetu wa karibu, msongo wa marika waweza kutulazimisha kuwa na tabia hizohizo, na upesi huenda tukaona kufikiri kwetu na mtazamo wetu ukiwa kama wao. Hata huenda tukaanza kudharau wale walio na imani ya kweli na ambao wanajaribu kufanya maendeleo ya kiroho.—1 Timotheo 4:15.
Inafaa kama nini kusitawisha urafiki na wale wanaojitahidi kumpendeza Yehova, ambao hufurahia mambo ya kiroho! Mashirika hayo yatatusaidia tuonyeshe “hekima ya kutoka juu.” Ambayo “kwanza kabisa ni safi kiadili, yenye kukubali sababu, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, . . . si ya kinafiki.” (Yakobo 3:17) Hiyo haimaanishi kwamba watu wenye kufikiria mambo ya kiroho hawawezi kuongea mambo mengine isipokuwa ya kiroho tu. Sivyo kamwe! Hebu wazia habari mbalimbali zinazozungumziwa katika vichapo vya Watch Tower kama vile gazeti Amkeni! Habari zenye kujenga za mazungumzo kwa kweli ni nyingi zaidi, na kwa kupendezwa na aina mbalimbali za habari hizo, twaonyesha kupenda uhai na kazi za Yehova mwenyewe.
Kama vile mchezaji wa tenisi aboreshavyo mchezo wake kwa kucheza na wachezaji wengine wazuri, mashirika yanayofaa yatakuza hali yetu ya kiakili, kihisia-moyo, na kiroho. Kwa upande mwingine, mashirika mabaya yanaweza kutuongoza kwenye mwendo wa unafiki yakitutia moyo kuishi maisha maradufu. Inafaa kama nini kufurahia dhamiri safi pamoja na kujistahi!
Wengine Walionufaika
Watu walio wengi huona kwamba kujifunza mafundisho ya Biblia na adili na matakwa yake ya kiroho si vigumu sana. Hata hivyo, jambo linaloweza kuwa gumu ni kutenda mambo hayo. Kama ionyeshwavyo na vielelezo vifuatavyo, uvutano ujengao wa msongo wa marika waweza kutusaidia tumtumikie Yehova kwa nafsi yote.
Shahidi mmoja aliye katika utumishi wa wakati wote pamoja na mke wake alisema kwamba vielelezo vya marika wake viliathiri miradi yake maishani. Alipokuwa akikua, alilazimika kukabiliana na uvutano usiojenga. Lakini alichagua marafiki waliomtia moyo awe wa kawaida katika huduma na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Kushikamana na mashirika haya kulimsaidia katika njia ya ukomavu wa kiroho.
Shahidi mwingine aandika hivi: “Baada ya mimi na mke wangu kuoana, tulihamia kwenye kutaniko ambamo kulikuwa na wenzi wa ndoa wenye umri kama wetu waliokuwa mapainia wa kawaida. Kielelezo chao kilichangia kuingia kwetu katika huduma ya wakati wote. Kisha sisi pia tukajitahidi kuingiza roho ya upainia katika kutaniko. Tokeo likawa kwamba, wengi walijiunga nasi wakiwa mapainia.”
Kushirikiana na wale walio na miradi ya kitheokrasi kwaweza kufanya utii kwa Yehova uwe rahisi zaidi. Hii ni manufaa nyingine ya uvutano wa marika unaofaa. Shahidi aliyeanza huduma ya wakati wote akiwa mwanamume mchanga na baadaye akawa mwangalizi asafiriye sasa anatumikia kwenye mojawapo ya ofisi za tawi za Watch Tower Society. Yeye aandika hivi: “Baadhi ya kumbukumbu zangu za mapema na zenye kupendeza zaidi za utotoni ni watumishi wa wakati wote waliokuwa wakitutembelea nyumbani. Sikuzote kulikuwako nafasi ya wageni kwenye chumba chetu cha kulia. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alinipa mkoba wa mahubiri nilipokuwa na umri wa miaka kumi. Mpaka leo hii, nauthamini mkoba huo.”
Akifikiria miaka yake ya utineja, Shahidi huyo aongezea kusema: “Vijana wengi katika kutaniko walitaka kujihusisha na mambo ya kutaniko, na kielelezo chao kilivutia wengine wetu tutamani kufanya vivyo hivyo.” Marika wenye kujenga walimsaidia kijana huyo, kama chipukizi, awe mwanamume mzuri Mkristo, aliye kama mti. Wazazi, je, mwakaribisha nyumbani kwenu wale wanaoweza kuwa na uvutano mzuri, wenye kujenga kwa watoto wenu?—Malaki 3:16.
Bila shaka, sisi sote hatuwezi kushiriki katika huduma ya wakati wote kama watu waliotoka kutajwa. Lakini sisi sote twaweza kujifunza kumpenda Yehova ‘kwa moyo wetu wote, kwa nafsi yetu yote, na kwa akili yetu yote.’ (Mathayo 22:37) Uchaguzi wetu wa marika hutimiza fungu kubwa katika kusitawisha upendo huo, na hivyo, katika tazamio letu la uhai wa milele.
Mtunga-zaburi alitoa njia ya mafanikio ya kweli maishani: “Heri mtu yule asiyekwenda katika shauri la wasio haki; wala hakusimama katika njia ya wakosaji; wala hakuketi barazani pa wenye mizaha. Bali sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku. Naye atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.”—Zaburi 1:1-3.
Huo ni uhakikisho mzuri ajabu kama nini! Hata ingawa sisi ni wasio wakamilifu na hufanya makosa, maisha yetu yatafanikiwa tukimwacha Yehova atuongoze na tukitumia kwa uhuru hazina hiyo kutoka kwa Mungu ya uvutano wa marika wenye kujenga—“ushirika mzima wa ndugu [zetu] katika ulimwengu.”—1 Petro 5:9.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Kutaniko huwa na uvutano wa marika wenye kujenga
[Picha katika ukurasa wa 25]
Wazazi, tieni moyo watoto wenu wachangamane na marika wenye kujenga