Yehova Hutaka Nini Kutoka Kwetu Leo?
“Sauti kutoka katika lile wingu, [ikasema]: ‘Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye mimi nimemkubali; msikilizeni yeye.’”—MATHAYO 17:5.
1. Sheria ilitimiza kusudi lake lini?
YEHOVA alipatia taifa la Israeli Sheria, pamoja na sehemu zake mbalimbali. Kuzihusu, mtume Paulo aliandika hivi: “Hayo yalikuwa matakwa ya kisheria yenye kuhusiana na mwili na yaliamriwa hadi wakati uliowekwa ili kunyoosha mambo.” (Waebrania 9:10) Sheria ilipowaongoza mabaki ya Waisraeli kumpokea Yesu akiwa Mesiya, au Kristo, ikawa imetimiza kusudi lake. Hivyo, Paulo alitangaza hivi: “Kristo ndiye mwisho wa Sheria.”—Waroma 10:4; Wagalatia 3:19-25; 4:4, 5.
2. Ni nani waliokuwa chini ya Sheria, nao walifunguliwa lini kutoka katika Sheria hiyo?
2 Je, yamaanisha kuwa hatuna wajibu wa kuifuata Sheria leo? Kwa hakika, idadi kubwa mno ya wanadamu haikuwahi kuwa chini ya Sheria, kama alivyoeleza mtunga-zaburi: “[Yehova] humhubiri Yakobo neno lake, na Israeli amri zake na hukumu zake. Hakulitendea taifa lolote mambo kama hayo, wala hukumu zake hawakuzijua.” (Zaburi 147:19, 20) Mungu alipoanzisha agano jipya kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, hata taifa la Israeli halikuwajibika kuitii Sheria. (Wagalatia 3:13; Waefeso 2:15; Wakolosai 2:13, 14, 16) Iwapo, basi, si lazima kufuata Sheria, Yehova hutaka nini kutoka kwa wale wanaotamani kumtumikia leo?
Yale Atakayo Yehova
3, 4. (a) Kwa ujumla, Yehova hutaka nini kutoka kwetu leo? (b) Kwa nini tuzifuate hatua za Yesu kwa ukaribu?
3 Katika mwaka wa mwisho wa huduma ya Yesu, mitume wake Petro, Yakobo, na Yohana waliandamana naye kwenye mlima mrefu, labda kilima kilichoko kwenye Mlima Hermoni. Huko waliona ono la unabii juu ya Yesu akiwa katika utukufu mkuu nao wakasikia sauti ya Mungu mwenyewe ikitangaza: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye mimi nimemkubali; msikilizeni yeye.” (Mathayo 17:1-5) Kwa ujumla, Yehova hutaka haya kutoka kwetu—kumsikiliza Mwana wake na kufuata kielelezo na mafundisho yake. (Mathayo 16:24) Hivyo, mtume Petro aliandika hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia kigezo ili nyinyi mfuate hatua zake kwa ukaribu.”—1 Petro 2:21.
4 Kwa nini tufuate hatua za Yesu kwa ukaribu? Kwa sababu tunapomwiga yeye, twamwiga Yehova Mungu. Yesu alimjua Baba kwa undani, kwa kuwa aliishi naye mbinguni kwa mabilioni ya miaka kabla ya kuja duniani. (Mithali 8:22-31; Yohana 8:23; 17:5; Wakolosai 1:15-17) Alipokuwa duniani, Yesu alimwakilisha Baba yake kwa uaminifu-mshikamanifu. Alieleza hivi: “Kama vile Baba alivyonifundisha nasema mambo haya.” Kwa kweli, Yesu alimwiga Yehova kikamili hivi kwamba angeweza kusema: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yohana 8:28; 14:9.
5. Wakristo wako chini ya sheria gani, na sheria hiyo ilianza kutenda lini?
5 Kumsikiliza na kumwiga Yesu kwahusisha nini? Je, kwamaanisha kuwa chini ya sheria? Paulo aliandika hivi: “Mimi mwenyewe siko chini ya sheria.” Alikuwa akirejezea “agano la zamani,” agano la Sheria lililofanywa na Israeli. Paulo alikiri kwamba yupo “chini ya sheria kuelekea Kristo.” (1 Wakorintho 9:20, 21; 2 Wakorintho 3:14) Agano la Sheria la zamani lilipokoma, “agano jipya” likaanza kutenda likiwa na “sheria [yake] ya Kristo” ambayo watumishi wote wa Yehova leo huwajibika kuitii.—Luka 22:20; Wagalatia 6:2; Waebrania 8:7-13.
6. “Sheria ya Kristo” yaweza kufafanuliwaje, nasi twaitiije?
6 Yehova hakuongoza kuandikwa kwa “sheria ya Kristo” katika mkusanyo maalum, akiipanga kwa sehemu mbalimbali, kama agano la Sheria la zamani. Hii sheria mpya kwa wafuasi wa Kristo haihusishi orodha ndefu ya mambo ya kufanya na ya kuepuka. Hata hivyo, Yehova alihifadhi katika Neno lake masimulizi manne yenye mambo mengi juu ya maisha na mafundisho ya Mwana wake. Na zaidi, Mungu aliwapulizia baadhi ya wafuasi wa mapema wa Yesu waandae maagizo yaliyoandikwa yahusuyo tabia ya kibinafsi, mambo ya kutaniko, mwenendo katika familia, na mambo mengine. (1 Wakorintho 6:18; 14:26-35; Waefeso 5:21-33; Waebrania 10:24, 25) Tunapopatanisha maisha yetu na kielelezo na mafundisho ya Yesu Kristo na kutii ushauri wa waandikaji wa Biblia waliopuliziwa wa karne ya kwanza, basi twaitii “sheria ya Kristo.” Yehova hutaka hayo kutoka kwa watumishi wake leo.
Umuhimu wa Upendo
7. Yesu alikaziaje kiini cha sheria yake wakati wa Sikukuu ya Kupitwa ya mwisho akiwa na mitume wake?
7 Ingawa upendo ulikuwa muhimu chini ya Sheria, huo hasa ndio kiini, au kitovu, cha sheria ya Kristo. Yesu alikazia uhakika huo alipokutana pamoja na mitume wake kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 33 W.K. Kwa mujibu wa muhtasari wa mtume Yohana kuhusu yaliyotendeka usiku huo, Yesu alirejezea upendo mara 28 katika maneno yake ya kutoka moyoni. Hilo liliwakazia mitume wake kiini, au maana, ya sheria yake. Kwa kufaa, Yohana alianzisha mazungumzo ya matukio ya jioni hiyo kwa kusema hivi: “Kwa sababu alijua kabla ya msherehekeo wa sikukuu ya kupitwa kwamba saa yake ilikuwa imekuja ya kuhama kutoka katika ulimwengu huu kwenda kwa Baba, Yesu, akiisha kuwa amependa walio wake mwenyewe waliokuwa ulimwenguni, aliwapenda hadi mwisho.”—Yohana 13:1.
8. (a) Ni nini kionyeshacho kwamba kulikuwepo bishano lenye kuendelea miongoni mwa mitume? (b) Yesu aliwafundishaje mitume wake unyenyekevu?
8 Yesu aliwapenda mitume wake, hata ingawa alikuwa amejaribu bila mafanikio dhahiri kuwasaidia washinde tamaa yao kubwa ya kupata mamlaka na cheo. Miezi kadhaa kabla ya kuwasili kwao Yerusalemu, “wa[li]bishania miongoni mwao wenyewe nani aliye mkubwa zaidi.” Na punde kabla ya kuingia jijini kwa ajili ya Sikukuu ya Kupitwa, bishano juu ya cheo likazuka tena. (Marko 9:33-37; 10:35-45) Kionyeshacho kwamba hilo lilikuwa tatizo lenye kuendelea ni kile kilichotendeka muda mfupi baada ya mitume kuingia katika chumba cha juu ili kula Sikukuu ya Kupitwa, ambayo ingekuwa ya mwisho wakiwa pamoja. Wakati huo hakuna aliyejitolea kuhudumia wengine kwa kunawisha miguu yao kulingana na desturi ya ukaribishaji. Yesu mwenyewe akawaosha miguu yao ili kuwafundisha unyenyekevu.—Yohana 13:2-15; 1 Timotheo 5:9, 10.
9. Yesu alishughulikiaje hali iliyotokea baada ya Sikukuu ya Kupitwa ya mwisho?
9 Licha ya fundisho hilo, ona lililotokea mara nyingine tena baada ya kushika Sikukuu ya Kupitwa na Yesu kuanzisha Ukumbusho wa kifo chake kilichokuwa karibu. Masimulizi ya Gospeli ya Luka yasema hivi: “Kukatokea pia bishano kali miongoni mwao juu ya ni yupi kati yao aliyeonekana kuwa mkubwa zaidi ya wote.” Badala ya kuwakasirikia na kuwakemea mitume, Yesu aliwashauri kwa fadhili juu ya uhitaji wa kuwa tofauti na watawala wa ulimwengu wanaong’ang’ania mamlaka. (Luka 22:24-27) Ndipo akaandaa kinachoweza kuitwa kiini cha sheria ya Kristo, akisema: “Mimi ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi, kwamba nyinyi pia mpendane.”—Yohana 13:34.
10. Yesu aliwapa wanafunzi wake amri gani, nayo ilihusisha nini?
10 Baadaye jioni hiyo, Yesu alionyesha jinsi upendo kama wa Kristo inavyopaswa kuwa. Alisema: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile mimi nimewapenda nyinyi. Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” (Yohana 15:12, 13) Je, Yesu alimaanisha kwamba wafuasi wake wapaswa kuwa tayari kufa kwa niaba ya waamini wenzao ikihitajika? Yohana, aliyeshuhudia pindi hiyo, alielewa hivyo, kwa kuwa aliandika hivi baadaye: “Kwa hili tumekuja kujua upendo, kwa sababu huyo [Yesu Kristo] alitoa nafsi yake kwa ajili yetu; na sisi tuko chini ya wajibu kutoa nafsi zetu kwa ajili ya ndugu zetu.”—1 Yohana 3:16.
11. (a) Twatimizaje sheria ya Kristo? (b) Yesu alitoa kielelezo gani?
11 Hivyo basi, twatimiza sheria ya Kristo kwa kufanya mengi zaidi ya kuwafundisha wengine kumhusu. Twapaswa pia kuishi na kutenda kama Yesu. Ni kweli kwamba katika hotuba zake Yesu alitumia maneno mazuri, yaliyoteuliwa vyema. Ingawa hivyo, alifundisha kwa kielelezo pia. Hata ingawa Yesu alikuwa kiumbe wa roho mwenye nguvu mbinguni, alitwaa nafasi ya kutumikia masilahi ya Baba yake duniani na kuonyesha jinsi tupaswavyo kuishi. Alikuwa mnyenyekevu, mwenye fadhili, naye aliwafikiria wengine, akiwasaidia wale waliolemewa na mizigo na kuonewa. (Mathayo 11:28-30; 20:28; Wafilipi 2:5-8; 1 Yohana 3:8) Pia Yesu aliwasihi wafuasi wake wapendane, kama alivyowapenda.
12. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba sheria ya Kristo haipunguzi uhitaji wa kumpenda Yehova?
12 Upendo kwa Yehova—amri kuu ya Sheria—una mahali gani katika sheria ya Kristo? (Mathayo 22:37, 38; Wagalatia 6:2) Mahali pa pili? Sivyo kamwe! Upendo kwa Yehova na kwa Wakristo wenzetu hauwezi kutenganishwa hata kidogo. Mtu hawezi kumpenda Yehova kikweli pasipo pia kumpenda ndugu yake, kwa kuwa mtume Yohana alisema hivi: “Ikiwa yeyote atoa taarifa: ‘Mimi nampenda Mungu,’ na bado anachukia ndugu yake, yeye ni mwongo. Kwa maana yeye ambaye hapendi ndugu yake, ambaye ameona, hawezi kuwa anapenda Mungu, ambaye hajaona.”—1 Yohana 4:20; linganisha 1 Yohana 3:17, 18.
13. Ni nini iliyokuwa athari ya utii wa wanafunzi kwa amri mpya ya Yesu?
13 Yesu alipowapa wanafunzi wake amri mpya ya kupendana kama alivyowapenda, alifafanua athari yake. “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu,” akasema, “mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Kwa maoni ya Tertullian, aliyeishi zaidi ya miaka mia moja baada ya kifo cha Yesu, upendo wa kidugu wa Wakristo wa mapema ulikuwa na athari hiyo hasa. Tertullian aliwanukuu watu wasio Wakristo wakisema kuhusu wafuasi wa Kristo: ‘Ona jinsi wanavyopendana na jinsi walivyo tayari kufiliana.’ Huenda tukajiuliza, ‘Je, naonyesha Wakristo wenzangu upendo kama huo hivi kwamba wathibitisha kuwa mimi ni mmoja wa wanafunzi wa Yesu?’
Jinsi Tunavyothibitisha Upendo Wetu
14, 15. Ni nini kiwezacho kufanya iwe vigumu kuitii sheria ya Kristo, lakini ni nini kiwezacho kutusaidia kufanya hivyo?
14 Ni muhimu kwa watumishi wa Yehova kuonyesha upendo kama wa Kristo. Lakini je, wewe huona ni vigumu kuwapenda Wakristo wenzako wenye tabia za ubinafsi? Naam, kama ambavyo tumeona, hata mitume walibishana na kujaribu kuendeleza masilahi yao wenyewe. (Mathayo 20:20-24) Wagalatia pia walibishana miongoni mwao. Baada ya kutaja kwamba upendo kwa jirani unatimiza Sheria, Paulo aliwaonya: “Lakini, ikiwa mnafuliza kuumana na kunyafuana, jihadharini kwamba msipate kuangamizana mtu na mwenzake.” Baada ya kutofautisha kazi za mwili na matunda ya roho ya Mungu, Paulo aliongeza shauri hili: “Acheni sisi tusiwe wenye majisifu ya bure, wenye kuchochea shindano juu ya mtu na mwenzake, tukihusudiana.” Kisha mtume akasihi hivi: “Endeleeni kuchukuliana mizigo yenye kulemea, na hivyo kutimiza sheria ya Kristo.”—Wagalatia 5:14–6:2.
15 Je, Yehova anataka mengi mno kutoka kwetu kwa kututaka tuitii sheria ya Kristo? Ingawa yaweza kuwa vigumu kuwaonyesha fadhili wale ambao wametutupia maneno makali na kutudhuru kihisia-moyo, twawajibika ‘kuwa waigaji wa Mungu, tukiwa watoto wapendwa, na kuendelea kutembea katika upendo.’ (Waefeso 5:1, 2) Twahitaji kuendelea kutazama kielelezo cha Mungu, ‘anayependekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.’ (Waroma 5:8) Tukichukua hatua ya kwanza kuwasaidia wengine, pamoja na wale waliotudhulumu, twaweza kupata ridhaa ya kujua kwamba tunamwiga Mungu na kuitii sheria ya Kristo.
16. Twathibitishaje upendo wetu kwa Mungu na Kristo?
16 Twapaswa kukumbuka kuwa twathibitisha upendo wetu kwa matendo yetu, bali si kwa yale tusemayo tu. Siku moja hata Yesu aliona ugumu kukubali sehemu fulani ya mapenzi ya Mungu kwa sababu ya mambo yaliyohusika. “Baba, ikiwa wataka, ondoa kikombe hiki kutoka kwangu,” Yesu akasali. Lakini mara akaongeza hivi: “Hata hivyo, acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Yesu alifanya mapenzi ya Mungu licha ya mateso yote yaliyompata. (Waebrania 5:7, 8) Utii ni ithibati ya upendo wetu nao huonyesha kwamba twaitambua njia ya Mungu kuwa ndiyo bora zaidi. “Maana hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha,” Biblia yasema, “kwamba tushike amri zake.” (1 Yohana 5:3) Yesu naye aliwaambia mitume wake: “Ikiwa mwanipenda, mtashika amri zangu.”—Yohana 14:15.
17. Yesu aliwapa wafuasi wake amri gani ya pekee, nasi twajuaje kwamba inatuhusu leo?
17 Mbali na kuwaamuru wafuasi wake wapendane, Kristo aliwapa amri gani nyingine ya pekee? Aliwaamuru wafanye kazi ya kuhubiri aliyokuwa amewazoeza. Petro alisema hivi: “Alituagiza sisi tuwahubiri watu na kutoa ushahidi kamili.” (Matendo 10:42) Yesu alikuwa ameamuru kihususa: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Yesu alionyesha kuwa maagizo hayo yangehusu pia wafuasi wake leo, “wakati wa mwisho,” kwa maana alisema: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Danieli 12:4; Mathayo 24:14) Bila shaka, ni mapenzi ya Mungu tuhubiri. Ingawa hivyo, huenda wengine wakaona kwamba Mungu anataka mengi mno kutoka kwetu kwa kututaka tufanye kazi hii. Lakini ndivyo ilivyo kweli?
Sababu Huenda Ikaonekana Kuwa Ngumu
18. Twapaswa kukumbuka nini tunapoteseka kwa kufanya atakayo Yehova?
18 Kama ambavyo tumeona, Yehova amewataka watu wafuate matakwa mbalimbali kwa muda wote katika historia. Wametakiwa kutimiza matakwa mbalimbali, nao wamejaribiwa kwa njia mbalimbali vilevile. Mwana wa Mungu alikabili majaribu magumu zaidi, hatimaye akauawa kikatili zaidi kwa sababu alifanya aliyotaka Mungu. Lakini tutesekapo kwa kufanya atakayo Yehova kutoka kwetu, twapaswa kukumbuka kwamba siye anayeleta majaribu hayo. (Yohana 15:18-20; Yakobo 1:13-15) Uasi wa Shetani ulianzisha dhambi, kuteseka, na kifo, naye ndiye amesababisha hali ambazo mara nyingi zimefanya iwe vigumu kwa watumishi wa Yehova kufanya atakayo kutoka kwao.—Ayubu 1:6-19; 2:1-8.
19. Kwa nini ni pendeleo kufanya yale Mungu atakayo kutoka kwetu kupitia Mwana wake?
19 Katika wakati huu wa mwisho, Yehova amewaamuru watumishi wake, kupitia Mwana wake, watangaze duniani kote kwamba suluhisho pekee la kuteseka kwa mwanadamu ni utawala wa Ufalme. Serikali hii ya Mungu itaondoa matatizo yote duniani—vita, uhalifu, umaskini, uzee, ugonjwa, kifo. Pia Ufalme huo utaleta paradiso tukufu ya kidunia, ambamo hata wafu watafufuliwa. (Mathayo 6:9, 10; Luka 23:43; Matendo 24:15; Ufunuo 21:3, 4) Ni pendeleo lililoje kutangaza habari njema ya mambo hayo! Kwa wazi basi, yale atakayo Yehova kutoka kwetu si magumu. Twakabili upinzani, ingawa ni Shetani Ibilisi na ulimwengu wake wanaousababisha.
20. Twaweza kuushindaje ugumu wowote usababishwao na Ibilisi?
20 Twaweza kuyashindaje magumu yoyote yaletwayo na Shetani? Kwa kuzingatia maneno haya: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” (Mithali 27:11) Yesu alimpa Yehova jibu la kukabiliana na dhihaka za Shetani kwa kuacha maisha salama ya mbinguni ili kufanya mapenzi ya Baba yake duniani. (Isaya 53:12; Waebrania 10:7) Akiwa mwanadamu, Yesu alivumilia kila jaribu lililomkabili, hata kifo kwenye mti wa mateso. Tukimfuata akiwa Kielelezo chetu, sisi pia twaweza kuvumilia mateso na kufanya yale atakayo Yehova kutoka kwetu.—Waebrania 12:1-3.
21. Wewe wauonaje upendo ulioonyeshwa na Yehova na Mwana wake?
21 Mungu na Mwana wake wametuonyesha upendo ulioje! Kwa sababu ya dhabihu ya Yesu, wanadamu watiifu wanatarajia kuishi milele Paradisoni. Basi tusiruhusu lolote lidhoofishe tumaini letu. Badala yake, sisi mmoja-mmoja na tuzingatie yale ambayo Yesu alifanya yawezekane, kama Paulo, aliyesema: ‘Mwana wa Mungu alinipenda mimi na kujikabidhi mwenyewe kwa ajili yangu.’ (Wagalatia 2:20) Na tuonyeshe shukrani ya kutoka moyoni kwa Mungu wetu mwenye upendo, Yehova, asiyetaka mengi mno kutoka kwetu.
Ungejibuje?
◻ Yehova hutaka nini kutoka kwetu leo?
◻ Katika jioni ya mwisho akiwa na mitume wake, Kristo alikaziaje umuhimu wa upendo?
◻ Twaweza kuthibitishaje kwamba twampenda Mungu?
◻ Kwa nini ni pendeleo kufanya yale Yehova atakayo kutoka kwetu?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Yesu alifundisha jambo gani kwa kuosha miguu ya mitume wake?
[Picha katika ukurasa wa 25]
Licha ya upinzani, ni pendeleo zuri kuhubiri habari njema