Yehova Ni Mungu Anayenionyesha Fadhili-upendo
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JOHN ANDRONIKOS
Ulikuwa mwaka wa 1956. Siku tisa tu baada ya kufunga ndoa nilikuwa nimesimama mbele ya mahakama ya rufani huko Komotiní, kaskazini mwa Ugiriki. Nilitumainia kwamba kifungo cha miezi 12 nilichokuwa nimehukumiwa kwa sababu ya kuhubiri Ufalme wa Mungu kingebatilishwa. Uamuzi wa mahakama ya rufani—kufungwa gerezani miezi sita—ulivunja matumaini hayo na kuwa mwanzo tu wa mfululizo wa kesi. Hata hivyo, katika hayo yote Yehova alithibitika kuwa Mungu anayenionyesha fadhili-upendo.
NILIPOZALIWA Oktoba 1, 1931, familia yetu ilikuwa ikiishi katika jiji la Kaválla, lililoitwa Neapolisi la Makedonia, ambalo lilitembelewa na mtume Paulo wakati wa safari yake ya pili ya umishonari. Mama alipata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova nilipokuwa mwenye umri wa miaka mitano, na ingawa alikuwa na elimu ya chini, alijitahidi awezavyo kunikazia kikiki upendo na hofu kwa Mungu. Baba yangu hakupendelea mabadiliko kabisa, naye alishikilia kwa dhati mapokeo ya Kanisa Othodoksi la Kigiriki. Hakupendezwa kabisa na kweli ya Biblia naye alimpinga mama yangu, mara nyingi akitumia jeuri.
Hivyo, nikakulia katika nyumba iliyogawanyika, ambapo Baba alimpiga na kumdhulumu Mama na hata akatuacha. Tangu nilipokuwa mtoto, Mama alitupeleka mimi na dada yangu mdogo kwenye mikutano ya Kikristo. Lakini nilipofikia umri wa miaka 15, tamaa za ujana na roho ya kutaka kuwa huru ikanikengeusha nisishirikiane na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, mama yangu mwaminifu alijitahidi sana, akalia mara nyingi katika jitihada za kunisaidia.
Kwa sababu ya umaskini na maisha mabaya niliyokuwa nikiishi, nikawa mgonjwa sana na kulazimika kulala kitandani kwa zaidi ya miezi mitatu. Wakati huo ndipo ndugu mmoja mnyenyekevu sana, aliyemsaidia mama yangu kujifunza kweli, alitambua kwamba nilimpenda Mungu kikweli. Aliona kwamba ningeweza kusaidiwa kupata nafuu kiroho. Wengine walimwambia: “Unapoteza wakati wako kujaribu kumsaidia John; hatapendezwa tena na mambo ya kiroho.” Lakini subira ya ndugu huyo na uvumilivu wake katika kunisaidia zikawa na matokeo. Katika Agosti 15, 1952, nikiwa na umri wa miaka 21, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji.
Nafungwa Gerezani Baada tu ya Kufunga Ndoa
Miaka mitatu baadaye nilijuana na Martha, dada wa kiroho aliyekuwa na sifa zenye kutokeza, na muda si muda tukachumbiana. Nilishangaa sana siku moja Martha aliponiambia: “Leo ninapanga kuhubiri mlango hadi mlango. Je, unataka kuandamana nami?” Sikuwa nimewahi kuhubiri mlango hadi mlango, kwa kuwa sanasana nilihubiri kivivi hivi. Wakati huo kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku nchini Ugiriki, na tulilazimika kuendelea kuhubiri kisiri. Matokeo yakawa kwamba watu walikamatwa kwa wingi, kukawa na kesi nyingi mahakamani, na hukumu kali za kufungwa gerezani zikatolewa. Hata hivyo, singeweza kukataa kuandamana na mchumba wangu!
Nilimwoa Martha mwaka wa 1956. Wakati huo, siku tisa baada ya ndoa yetu, ndipo nilipohukumiwa na mahakama ya rufani ya Komotiní kifungo cha miezi sita gerezani. Jambo hilo lilinikumbusha swali ambalo hapo awali nilikuwa nimemwuliza dada mmoja Mkristo, rafiki ya mama yangu: “Ninaweza kuonyeshaje kwamba mimi ni Shahidi wa kweli wa Yehova? Sijapata kuwa na fursa ya kuthibitisha imani yangu.” Dada huyo alipokuja kuniona gerezani, alinikumbusha swali hilo na kusema: “Sasa unaweza kumwonyesha Yehova kadiri unavyompenda. Huu ni mgawo wako.”
Nilipojua kwamba wakili wangu alikuwa akijaribu kukusanya pesa ili anitoe gerezani kwa dhamana, nilimwambia kwamba nilipendelea kumaliza kifungo changu. Nilifurahi kama nini mwishoni mwa kifungo hicho cha miezi sita kuona watu wawili niliofungwa nao wakikubali kweli! Katika miaka iliyofuata, nilihusika katika kesi nyingi mahakamani kwa ajili ya habari njema.
Maamuzi Ambayo Hatujapata Kujutia
Katika mwaka wa 1959, miaka kadhaa baada ya kuachiliwa, nilikuwa nikitumikia nikiwa mtumishi wa kutaniko, au mwangalizi-msimamizi, na kualikwa kuhudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme, ambayo ni mtaala wa kuzoeza wazee wa kutaniko. Lakini wakati huohuo nikapewa kazi ya kudumu kwenye hospitali moja ya umma, kazi ambayo ingenipa mimi na familia yangu usalama wa kifedha kwa muda wa maisha yetu yote. Nichague gani? Nilikuwa tayari nimefanya kazi katika hospitali hiyo kwa muda wa miezi mitatu, na mkurugenzi alipendezwa sana na kazi yangu, lakini mwaliko wa kuhudhuria shule ulipofika, hangeniruhusu hata kuchukua likizo bila malipo. Baada ya kusali kuhusu tatizo hilo, niliamua kutanguliza masilahi ya Ufalme na kukataa kazi hiyo niliyopewa.—Mathayo 6:33.
Karibu wakati huohuo, mwangalizi wa wilaya na wa mzunguko walikuja kutumikia kutaniko letu. Tulilazimika kufanya mikutano yetu kisiri katika nyumba za watu binafsi kwa sababu ya upinzani mkali wa makasisi wa Kanisa Othodoksi la Kigiriki na wenye mamlaka. Baada ya mojawapo ya mikutano hiyo, mwangalizi wa wilaya alinikaribia na kuniuliza kama nilikuwa nimefikiria kuchukua utumishi wa wakati wote. Dokezo lake lilinigusa moyo kwa kuwa nilikuwa nikitamani kufanya hivyo tangu nilipobatizwa. Nikajibu: “Nataka sana.” Hata hivyo, nilikuwa na daraka la ziada la kumlea binti yangu. Huyo ndugu akaniambia: “Mtumaini Yehova, naye atakusaidia utimize miradi yako.” Hivyo, bila kuyapuuza madaraka ya familia yetu, mimi na mke wangu tuliweza kurekebisha hali yetu hivi kwamba katika Desemba 1960, nilianza kutumikia katika sehemu za mashariki ya Makedonia nikiwa painia wa pekee—mmojawapo wa mapainia wa pekee watano tu nchini.
Ofisi ya tawi katika Athene iliniomba nitumikie nikiwa mwangalizi anayesafiri baada ya kuwa painia wa pekee kwa mwaka mmoja. Niliporudi nyumbani baada ya kuzoezwa kwa mwezi mmoja kufanya utumishi huo, na nikiwa bado namsimulia Martha mambo niliyoona, mkurugenzi wa mgodi mkubwa wa madini ya manganizi alituzuru na kuniomba niwe meneja wa idara ya kusafisha madini, akinipa mkataba mzuri wa kufanya kazi hiyo kwa miaka mitano na nipewe nyumba nzuri na gari. Alitaka nimjibu baada ya siku mbili. Bila kusita hata kidogo nilisali kwa Yehova kwa mara nyingine: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isaya 6:8) Mke wangu alikubaliana nami kabisa. Kwa kumtumaini Mungu, tulianza kazi ya kusafiri, na kwa fadhili-upendo wake, Yehova hakutukatisha tamaa.
Kutumikia Katika Hali za Aina Zote
Ingawa kulikuwa na matatizo ya kiuchumi, tuliendelea mbele naye Yehova akatuandalia yale tuliyohitaji. Mwanzoni, nilitumia pikipiki ndogo kuyazuru makutaniko, nikisafiri umbali uliofikia kilometa 500. Nilikuwa na matatizo mara nyingi, na kupata aksidenti kadhaa. Nikiwa njiani kurudi kutoka katika kutaniko moja wakati wa majira ya baridi kali, injini ilizimika nilipokuwa nikivuka mto uliokuwa umefurika, nikalowa maji hadi kwenye magoti. Kisha gurudumu moja la pikipiki likapata pancha. Mpita njia mmoja aliyekuwa na pampu akanisaidia, na hivyo nikaweza kufika kwenye kijiji kilichokuwa karibu ambako nilirekebisha gurudumu hilo. Hatimaye nilifika nyumbani saa tisa usiku, nikiwa naona baridi nyingi na nimechoka sana.
Katika pindi nyingine, nilipokuwa nikisafiri kutoka kutaniko moja kwenda jingine, pikipiki hiyo iliteleza, ikaniangukia kwenye goti. Hivyo, suruali yangu ikararuka na kulowa damu. Sikuwa na suruali nyingine, kwa hiyo, jioni hiyo nilitoa hotuba nikiwa nimevalia suruali ya ndugu mwingine, ambayo ilikuwa kubwa sana kwangu. Hata hivyo, hakuna tatizo ambalo lingezima tamaa yangu ya kumtumikia Yehova na ndugu zangu.
Katika aksidenti nyingine, nilijeruhiwa vibaya, nikavunjika mkono na meno ya mbele. Wakati huo ndipo nilipotembelewa na dada yangu asiye Shahidi ambaye alikuwa akiishi Marekani. Nilipata kitulizo kilichoje aliponisaidia kununua gari! Ndugu katika ofisi ya tawi ya Athene waliniandikia barua yenye kutia moyo waliposikia juu ya aksidenti yangu, na kati ya mambo waliyoandika, walitia ndani maneno ya Waroma 8:28, ambayo kwa sehemu yasema: “Mungu hufanya kazi zake zote zishirikiane pamoja kwa ajili ya mema ya wale wampendao Mungu.” Uhakikisho huo umethibitika tena na tena kuwa kweli maishani mwangu!
Mshangao Wenye Kupendeza
Katika mwaka wa 1963, nilikuwa nikihubiri na painia wa pekee katika kijiji ambako watu hawakuwa wenye kuitikia. Tuliamua kuhubiri tukiwa mmoja-mmoja, kila mmoja akihubiri sehemu moja ya barabara. Kwenye nyumba moja, nilibisha mlango na mara hiyohiyo mwanamke akanivuta ndani himahima na kufunga mlango nyuma yangu. Nilishangaa sana, nikijiuliza ni nini kinachoendelea. Muda mfupi baadaye, alimwita yule painia wa pekee kwa hima pia aingie ndani ya nyumba. Ndipo huyo mwanamke akatuambia: “Nyamazeni! Hata msiondoke mahali mlipo!” Baada ya muda, tukasikia sauti zenye uhasama nje. Watu walikuwa wakitutafuta. Hali ilipotulia, huyo mwanamke akatuambia: “Nilifanya hivi ili kuwalinda nyinyi. Ninawastahi kwa kuwa ninaamini kwamba nyinyi ni Wakristo wa kweli.” Tulimshukuru sana na kuondoka, tukimwachia fasihi nyingi.
Miaka kumi na minne baadaye, nilipokuwa nikihudhuria mkusanyiko wa wilaya nchini Ugiriki, mwanamke mmoja alinikaribia na kusema: “Ndugu, wanikumbuka? Mimi ndiye yule mwanamke aliyewaficha ili wapinzani wasiwaone mlipokuja kijijini mwetu kutoa ushahidi.” Alikuwa amehamia Ujerumani, akajifunza Biblia, na kushirikiana na watu wa Yehova. Sasa familia yake yote ilikuwa katika kweli.
Kwa kweli, katika miaka hiyo yote, tumebarikiwa kwa ‘barua nyingi za pendekezo.’ (2 Wakorintho 3:1) Baadhi ya watu ambao tulikuwa na pendeleo la kuwasaidia wapate ujuzi wa kweli ya Biblia sasa wanatumikia wakiwa wazee, watumishi wa huduma, na mapainia. Inasisimua kama nini kuona wahubiri kadhaa katika mizunguko niliyotumikia katika miaka ya mapema ya 1960 wakiongezeka na kufikia zaidi ya waabudu 10,000 wa Yehova! Sifa zote zinamwendea Mungu mwenye fadhili-upendo, ambaye hututumia kwa njia yake mwenyewe.
“Alipo Mgonjwa Kitandani”
Wakati wa miaka tuliyotumikia katika kazi ya kusafiri, Martha alikuwa msaidizi mwenye kutokeza na mwenye furaha sikuzote. Hata hivyo, katika Oktoba 1976, akawa mgonjwa sana na kufanyiwa upasuaji wenye maumivu makali. Upasuaji huo ulimwacha amepooza na mwenye kutumia kiti cha magurudumu. Tungeweza kukabilianaje na gharama na msononeko wa kihisia-moyo? Tulimtumaini Yehova kwa mara nyingine na kuona upendo na ukarimu wake. Nilipoondoka kutumikia huko Makedonia, Martha alikaa kwa nyumba ya ndugu jijini Athene ili apate tiba ya maungo. Alikuwa akinipigia simu na kusema maneno haya yenye kutia moyo: “Mimi ni mzima. Wewe endelea tu, nami nitakapojimudu tena, nitaandamana nawe katika kiti changu cha magurudumu.” Na hivyo ndivyo alivyofanya. Ndugu zetu wapendwa kutoka Betheli walituandikia barua nyingi zenye kututia moyo. Martha alikumbushwa tena na tena maneno yaliyo kwenye Zaburi 41:3: “BWANA atamtegemeza alipo mgonjwa kitandani. Katika ugonjwa wake umemtandikia.”
Kwa sababu ya matatizo hayo mabaya ya afya, iliamuliwa katika mwaka wa 1986 kwamba ingefaa nitumikie nikiwa painia wa pekee jijini Kaválla, ambako tunaishi karibu na familia ya binti yetu mpendwa. Mwezi wa Machi uliopita, mpendwa wangu Martha alikufa, mwaminifu hadi mwisho. Kabla hajafa, ndugu walipomwuliza: “U hali gani?” yeye kwa kawaida alikuwa akiwajibu: “Kwa kuwa niko karibu na Yehova, mimi ni mzima!” Tulipotayarisha mikutano au kupokea mialiko yenye kuvutia ya kwenda kutumikia katika maeneo ambako watu huitikia zaidi, Martha alikuwa akisema: “John, acha twende tukatumikie mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi.” Alikuwa na roho yenye bidii daima.
Miaka kadhaa iliyopita, mimi pia nilikabiliana na tatizo baya la afya. Katika Machi 1994, ilipatikana kwamba nina ugonjwa wa moyo wenye kuhatarisha uhai, ikawa lazima nifanyiwe upasuaji. Kwa mara nyingine tena, nilipata utegemezo wa Yehova wenye upendo katika kipindi hicho cha hatari. Sitasahau kamwe sala ambayo mwangalizi mmoja wa mzunguko alitoa kando ya kitanda changu nilipotoka katika chumba cha wagonjwa mahututi, na vilevile sherehe ya Ukumbusho niliyoongoza humohumo ndani ya chumba changu cha hospitali pamoja na wagonjwa wanne walioonyesha kupendezwa na kweli kwa kadiri fulani.
Yehova Amekuwa Msaidizi Wetu
Wakati huyoyoma, na mwili wetu hudhoofika, lakini roho yetu hufanywa upya kupitia funzo na utumishi. (2 Wakorintho 4:16) Sasa ni miaka 39 tangu niliposema “Mimi hapa, nitume mimi.” Yamekuwa maisha kamili, yenye furaha, na yenye kuthawabisha. Ndiyo, wakati mwingine mimi hujiona kuwa “maskini na mhitaji,” lakini naweza kumwambia Yehova hivi nikiwa na uhakika: “[Wewe] ndiwe msaada wangu na mwokozi wangu.” (Zaburi 40:17) Kwa kweli amekuwa Mungu anionyeshaye fadhili-upendo.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Nikiwa na Martha mwaka wa 1956
[Picha katika ukurasa wa 26]
Bandari ya Kaválla
[Picha katika ukurasa wa 26]
Nikiwa na Martha mwaka wa 1997