Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w14 6/15 kur. 8-11
  • Wasaidie Waamini Wenzako Waliotalikiana—Jinsi Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wasaidie Waamini Wenzako Waliotalikiana—Jinsi Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KULEMEWA NA HISIA ZINAZOBADILIKA
  • PAMBANO LA KUPATA TENA USAWAZIKO
  • HISIA ZA UPWEKE NA ZA KUTOPENDWA ZINAPOANZA
  • Kusonga Mbele Baada ya Talaka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Jinsi Talaka Inavyowaathiri Watoto
    Msaada kwa Ajili ya Familia
  • Talaka Matokeo Yayo Mabaya
    Amkeni!—1992
  • Mambo Manne Unayopaswa Kujua Kuhusu Talaka
    Amkeni!—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
w14 6/15 kur. 8-11

Unawezaje Kuwasaidia Waamini Wenzako Waliotalikiana?

Mwanamke akimtia moyo dada mkristo aliyetalikiana

Inaelekea kwamba unamjua mtu au watu kadhaa waliotalikiana na wenzi wao kwa sababu wengi wanatalikiana. Kwa mfano, utafiti uliofanywa nchini Poland ulionyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa wenzi wenye umri wa miaka 30 waliooana kwa miaka mitatu hadi sita kutalikiana, na si watu wenye umri huo tu wanaotalikiana.

Kwa kweli, Taasisi ya Sera za Familia nchini Hispania inaripoti hivi: “Takwimu zinaonyesha kwamba [katika Ulaya] nusu ya idadi ya watu wanaofunga ndoa watatalikiana.” Ndivyo ilivyo katika nchi nyingine zilizoendelea.

KULEMEWA NA HISIA ZINAZOBADILIKA

Ni nini kinachosababisha hali hiyo ya kawaida? Mshauri mmoja wa ndoa mwenye uzoefu kutoka Ulaya Mashariki alisema hivi: “Wenzi wanaotalikiana huwa tayari hawana uhusiano mzuri na wameachana, jambo linalosababisha maumivu makali ya kihisia.” Aliongezea hivi: ‘Mara nyingi watu waliotalikiana huwa na hisia kali zenye nguvu kama vile hasira, majuto, kuvunjika moyo, kukata tamaa, na aibu.’ Nyakati nyingine hisia hizo humfanya mtu atake kujiua. Mshauri huyo aliendelea kusema hivi: “Watu wanapotalikiana kwa njia rasmi kortini, kipindi kingine cha hisia huanza. Kwa sababu ya kuhisi kwamba ametengwa na hafai, huenda mtu aliyetalikiana na mwenzi wake akajiuliza hivi: ‘Sasa kwa kuwa nimetalikiana na mwenzi wangu, mimi ni nani hasa? Nina kusudi gani maishani?’”

Akikumbuka jinsi alivyohisi miaka kadhaa iliyopita, Ewa anasema hivi: “Baada ya kutalikiana na mume wangu, niliaibika sana hasa majirani na wafanyakazi wenzangu waliponiita ‘mtalikiwa.’ Nilikasirika sana. Kwa kuwa nilibaki na watoto wawili wadogo, nililazimika kuwa mama na baba.”a Adam, aliyetumika kwa miaka 12 akiwa mzee wa kutaniko mwenye kuheshimika, anasema hivi: “Ninahisi sifai hata kidogo. Nyakati nyingine ninakasirika sana na kushawishika kujitenga na watu wote.”

PAMBANO LA KUPATA TENA USAWAZIKO

Kwa sababu ya kulemewa na mahangaiko kuhusu wakati wao ujao, wengine wangali wanapambana ili kupata tena usawaziko, miaka mingi baada ya talaka. Huenda wakafikiri kwamba wengine hawapendezwi nao. Zaidi ya hilo, mwandishi mmoja wa masuala ya talaka anasema kwamba wanapaswa “kubadilika na kujifunza kukabiliana na matatizo wakiwa peke yao.”

Stanisław anakumbuka hivi: “Tulipotalikiana, aliyekuwa mke wangu alinizuia kuwatembelea binti zangu wawili wadogo. Nilihisi kwamba hakuna aliyenijali tena na hata Yehova alikuwa ameniacha. Nilitamani kufa. Baada ya muda, nilitambua kwamba nilikosea katika kufikiri kwangu.” Wanda, mwanamke aliyetalikiwa, alihangaikia pia wakati wake ujao. Anasema hivi: “Nilikuwa na hakika kwamba baada ya muda, watu, kutia ndani waamini wenzangu, hawatanijali wala kuwajali hata kidogo watoto wangu. Hata hivyo, sasa ninaona jinsi akina ndugu walivyotujali na kunisaidia nilipokuwa nikijitahidi kuwalea watoto wangu ili wawe waabudu wa Yehova.”

Maelezo hayo yanaonyesha kwamba watu fulani hulemewa na hisia zisizofaa baada ya talaka. Huenda wakajiona hawafai na kufikiri hawana thamani wala hawastahili ufikirio. Na huenda pia wakaanza kuwachambua-chambua wale walio karibu nao. Hivyo, wanaweza kufikiri kwamba kutaniko haliwajali na halina huruma. Hata hivyo, visa kama vya Stanisław na Wanda vinaonyesha kwamba waliotalikiana huenda wakatambua baadaye kuwa ndugu na dada zao wanawajali kikweli. Kwa kweli, Wakristo wenzao wamekuwa wakiwajali kwa njia ya pekee, hata ikiwa mwanzoni hawakutambua hilo.

HISIA ZA UPWEKE NA ZA KUTOPENDWA ZINAPOANZA

Kumbuka kwamba hata tukijitahidi kadiri gani, huenda waamini wenzetu waliotalikiana wakahisi upweke mara kwa mara. Hasa akina dada waliotalikiana na wenzi wao wanaweza kuhisi kwamba ni watu wachache tu wanaowajali. Alicja anakiri hivi: “Miaka minane imepita tangu nilipotalikiana na mume wangu. Lakini nyakati nyingine bado ninahisi kwamba sifai. Nyakati hizo, mimi hujitenga na watu, hulia sana na kujihurumia.”

Ingawa ni kawaida kwa mtu aliyetalikiana na mwenzi wake kuhisi hivyo, Biblia hutushauri tusijitenge na wengine. Mtu asiyefuata shauri hilo huenda akakataa “hekima yote inayotumika.” (Met. 18:1) Hata hivyo, mtu anayehisi upweke anapaswa kuelewa kwamba ni hekima inayotumika kuepuka kutafuta tena na tena mashauri au faraja kutoka kwa mtu wa jinsia tofauti. Kwa njia hiyo, hawatashawishiwa kusitawisha hisia zisizofaa za kimahaba.

Waamini wenzetu waliotalikiana wanaweza kulemewa na hisia mbalimbali, kama vile mahangaiko kuhusu wakati ujao na hisia za upweke au kutopendwa. Tukitambua kwamba ni kawaida kwa wale waliotalikiana kuhisi hivyo na ni vigumu kushinda hisia hizo, tunapaswa kumwiga Yehova kwa kuwategemeza kwa ushikamanifu ndugu na dada hao. (Zab. 55:22; 1 Pet. 5:​6, 7) Tunaweza kuwa na hakika kwamba watathamini sana msaada wowote tunaowapa. Kwa kweli, watasaidiwa na marafiki wa kweli kutanikoni.​—Met. 17:17; 18:24.

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

Maoni Yaliyosawazika Kuhusu Talaka

Watumishi wa Yehova huichukulia ndoa kwa uzito sana kwa sababu maoni yetu yanategemea Maandiko. Kwa mfano, katika andiko la Malaki 2:16, tunasoma maneno haya ya Mungu yaliyo wazi: ‘Ninachukia talaka.’ Msingi pekee wa Kimaandiko wa talaka ni uasherati. Kwa hiyo, ni kosa zito kwa mtu kufikiria kumtaliki mwenzi wake kwa msingi usio wa kimaandiko, huku akipanga kufunga ndoa na mtu mwingine.​—Mwa. 2:22-24; Kum. 5:21; Mt. 19:4-6, 9.

Hata hivyo, talaka inapotokea, labda baada ya mwenzi wa Mkristo kukosa uaminifu, ndugu na dada kutanikoni humtegemeza mwenzi asiye na hatia. Wanamwiga Yehova kwa kufanya yote wanayoweza ili kuwasaidia waadilifu hao ambao ‘wamepondwa roho’ kwa muda.​—Zab. 34:15, 18; Isa. 41:10.

UNAWEZA KUWASAIDIAJE?

Je, unaweza kutoa msaada unaohitajiwa sana? Unaweza kufanya nini ili kumsaidia mtu aliye na hisia zilizotajwa? Fikiria kile ambacho Biblia inasema, na uone jinsi ambavyo Wakristo washikamanifu wamesaidia.

Uwe msikilizaji mwenye utambuzi. (Met. 16:20, 23)

Inaeleweka kwamba baada ya talaka, huenda mtu akakataa kuzungumzia mambo yaliyosababisha talaka. Na ukweli ni kwamba huenda kusema kwa hasira kuhusu kilichotokea hakutasaidia wala kupunguza mahangaiko. (Met. 12:25; Rom. 12:15) Michał, ambaye alimsaidia Adam aliyetajwa hapo juu, anakubali kwamba unaweza kumsikiliza kwa utambuzi na huruma bila kuwa mdadisi: “Nimejaribu kumsaidia Adam kuelewa kwamba anapolemewa na hisia zisizofaa, anaweza kuniambia jambo ambalo hakukusudia na baadaye kuhisi kwamba hakupaswa kufanya hivyo.” Hivyo, Michał alimweleza waziwazi kwamba hakuhitaji kujua habari zote. Lakini alimsikiliza akiwa rafiki wa kweli. Tunaweza kuwatia moyo sana kabla au baada ya mikutano ya Kikristo kwa kuuliza hivi: “Unaendeleaje? Bila shaka unakabili hali ngumu sana. Niko tayari kukusaidia.”

Pendezwa nao kibinafsi. (Flp. 2:4)

Mirosław anakumbuka hivi: “Mimi na mke wangu tumetenga wakati wa kumsaidia dada aliyetalikiana na mume wake. Kwa mfano, tulirekebisha mlango wake. Tulitumia pia gari letu kumpeleka kumwona daktari.” Hayo yanaweza kuonekana kuwa mambo madogo lakini yalimsaidia sana. Dada aliyesaidiwa na wenzi hao alipata usawaziko hatua kwa hatua. Zaidi ya hilo, baadaye alianza kufanya upainia, na binti yake mwenye umri wa miaka 11 akabatizwa.

Famila ikionyesha upendezi wa kibinafsi kwa dada mkristo aliyetalikiwa

Mhakikishie aliyetalikiana na mwenzi wake kwamba Yehova anaelewa hali yake.

Ikiwa mtu anajiona hafai, unaweza kumhakikishia kwamba Mungu anamthamini kila mmoja wa watumishi wake. Bila shaka, sisi “ni bora kuliko shomoro wengi,” yaani, sisi ni wa pekee na wenye thamani machoni pa Mungu. (Mt. 10:29-31) “Yehova ndiye mchunguzaji wa mioyo” na hivyo anaweza kuelewa hali ya wale waliotalikiana. Hatamwacha yeyote kati ya watumishi wake waaminifu. (Met. 17:3; Zab. 145:18; Ebr. 13:5) Kwa hiyo, unapomwonyesha aliyetalikiwa kwamba unamjali, mhakikishie kwamba Mungu anathamini upendo wake kwa ajili ya kweli na jitihada zake za kutegemeza ibada ya kweli.​—Flp. 2:29.

Mtie moyo aliyetalikiana na mwenzi wake akae karibu na kutaniko.

Baadhi ya Wakristo hushindwa kuhudhuria mikutano wanapolemewa na hisia mbalimbali. Lakini mikutano hiyo hutuimarisha na kututia moyo. Inakusudiwa ‘kutujenga.’ (1 Kor. 14:26; Zab. 122:1) Wazee husaidia sana wanapochukua hatua ya kwanza ili kutoa kitia-moyo. Wanda, aliyetajwa awali, anasema hivi: “Bado tunakumbuka jinsi walivyotutunza kwa upendo.”

Mtie moyo aliyetalikiana na mwenzi wake aimarishe uhusiano wake na Mungu kwa kusali, kujifunza kibinafsi, na kutafakari. (Yak. 4:8)

Hata ingawa Yehova ni mweza yote na anaishi mbinguni, yeye humkazia uangalifu ‘anayeteseka na kujuta rohoni na kutetemeka kwa ajili ya neno Lake.’ Mhakikishie jambo hilo aliyetalikiana na mwenzi wake, na ukazie jinsi kila mmoja wetu anavyonufaika kwa kuendelea kumkaribia Mungu kupitia sala na funzo la kibinafsi.​—Isa. 66:2.

Jitolee kuhubiri au kutayarisha mkutano pamoja naye.

Ndugu wawili wakristo wakihubiri pamoja

Kufanya hivyo kutamsaidia Mkristo aliyetalikiana na mwenzi wake kuendelea na maisha kwa ujasiri. Marta, ambaye amemtegemeza dada mwenye bidii aliyevunjika moyo baada ya talaka, anasema hivi: “Tunahubiri pamoja kwa ukawaida. Tunapata shangwe tunapotimiza miradi tuliyojiwekea. Nyakati nyingine tunatayarisha mikutano pamoja, kisha tunapika chakula kitamu.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki