Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wp16 Na. 6 kur. 4-7
  • Ukweli Kuhusu Wale Wanaoishi Mbinguni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ukweli Kuhusu Wale Wanaoishi Mbinguni
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2016
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YEHOVA NDIYE MKUU ZAIDI
  • YESU ANAISHI MBINGUNI
  • MALAIKA WANAMTUMIKIA MUNGU
  • SHETANI HUPOTOSHA MAMILIONI YA WATU
  • WALE WANAOTOKA DUNIANI
  • MAMBO AMBAYO WALE WALIO MBINGUNI WATAFANYA
  • Maono Kuhusu Makao ya Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Rafiki Yetu Bora Zaidi Yuko Katika Makao ya Roho
    Amkeni!—1996
  • Malaika—Jinsi Wanavyohusika Katika Maisha Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Malaika—“Roho kwa Ajili ya Utumishi wa Watu Wote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2016
wp16 Na. 6 kur. 4-7
Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Yehova, na wakiwa wamezungukwa na malaika

HABARI KUU | UKWELI KUHUSU MAONO YA MBINGUNI

Maono Kuhusu Wale Wanaoishi Mbinguni

Biblia inataja maono yenye kustaajabisha ambayo yanatusaidia kuelewa jinsi makao ya kiroho yalivyo. Tunakutia moyo uchunguze kwa makini maono hayo. Ingawa baadhi ya mambo katika maono hayo si halisi, yatakusaidia kuwajua wale wanaoishi mbinguni na jinsi wanavyohusika maishani mwako.

YEHOVA NDIYE MKUU ZAIDI

“Kiti cha ufalme kilikuwa mahali pake mbinguni, na kuna yule aliyeketi juu ya kile kiti cha ufalme. Na yule aliyeketi, kuonekana kwake ni kama jiwe la yaspi na jiwe jekundu la thamani, na upinde wa mvua ambao kuonekana kwake ni kama zumaridi unakizunguka kile kiti cha ufalme.”​—Ufunuo 4:2, 3.

“Naye alikuwa na mwangaza kuzunguka pande zote. Kulikuwa na kitu kinachoonekana kama upinde ambao hutokea katika wingu kubwa katika siku ya mvua. Hivyo ndivyo ulivyokuwa mwangaza uliozunguka pande zote. Kulikuwa ni kuonekana kwa mfano wa utukufu wa Yehova.”​—Ezekieli 1:27, 28.

Maono hayo ya mtume Yohana na nabii Ezekieli yanaonyesha utukufu wa Mungu Mkuu Zaidi, Yehova, na tunaweza kuyaelewa kwa sababu yanataja vitu tunavyojua, kama vile, mawe ya thamani yenye kung’aa, upinde wa mvua na ukuu wa kiti cha enzi. Maono hayo yanaonyesha kwamba makao ya Yehova yanavutia na ni matulivu sana.

Ufafanuzi huo kumhusu Mungu unapatana na maneno haya ya mtunga zaburi: “Kwa maana Yehova ni mkuu na wa kusifiwa sana. Ni mwenye kuogopesha kuliko miungu mingine yote. Kwa maana miungu yote ya vikundi vya watu ni miungu isiyo na thamani; lakini Yehova, amezifanya mbingu. Utukufu na fahari ziko mbele zake; nguvu na uzuri zipo katika patakatifu pake.”—Zaburi 96:4-6.

Licha ya kwamba Yehova ni Mkuu Zaidi, anatualika tumkaribie kupitia sala na anatuhakikishia kwamba atatusikiliza. (Zaburi 65:2) Mungu anatupenda na kutujali sana hivi kwamba mtume Yohana aliandika hivi kwa unyofu: “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.

YESU ANAISHI MBINGUNI

“[Mwanafunzi Mkristo Stefano], akiwa amejaa roho takatifu, akakaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu, naye akasema: ‘Tazameni! Ninaziona mbingu zimefunguka na Mwana wa binadamu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.’”—Matendo 7:55, 56.

Kabla ya ono hilo, Yesu alikuwa ameuawa kutokana na uchochezi wa viongozi Wayahudi ambao sasa Stefano alikuwa akizungumza nao. Ono hilo lilithibitisha kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa na kupewa cheo cha juu. Mtume Paulo alieleza hivi: ‘[Yehova] alimfufua [Yesu] kutoka kwa wafu na kumketisha kwenye mkono wake wa kuume katika mahali pa kimbingu, juu zaidi kuliko kila serikali na mamlaka na nguvu na utawala na kila jina linalotajwa, si katika mfumo huu wa mambo tu, bali pia katika ule ujao.’—Waefeso 1:20, 21.

Zaidi ya kueleza kuhusu cheo chake cha juu, Maandiko yanaonyesha kwamba, kama alivyo Yehova, Yesu anawajali sana wanadamu. Alipokuwa duniani, Yesu aliwaponya wagonjwa, walemavu, na kufufua wafu. Pia, alionyesha kwamba anampenda sana Mungu na wanadamu kwa kutoa uhai wake uwe dhabihu. (Waefeso 2:4, 5) Hivi karibuni, Yesu, akiwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu, atatumia mamlaka yake kuwaletea wanadamu watiifu hapa duniani baraka nyingi.

MALAIKA WANAMTUMIKIA MUNGU

Nabii Danieli alisema hivi: “Nikaendelea kutazama mpaka viti vya ufalme vikawekwa na Mzee wa Siku [Yehova] akaketi. . . . Kulikuwa na maelfu elfu walioendelea kumtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake.”—Danieli 7:9, 10.

Katika ono hilo, Danieli aliona maelfu ya malaika wakiwa mbinguni. Bila shaka, hilo lilikuwa ono lenye kustaajabisha sana! Malaika ni viumbe wa kiroho wenye utukufu, nguvu, na akili nyingi. Malaika hao wanatia ndani maserafi na makerubi. Biblia inawataja malaika zaidi ya mara 250.

Malaika si wanadamu walioishi duniani zamani. Mungu aliwaumba malaika muda mrefu kabla ya kuwaumba wanadamu. Dunia ilipoumbwa, malaika walipaaza sauti na kushangilia.—Ayubu 38:4-7.

Malaika waaminifu wanamtumikia Mungu kwa kushiriki katika kazi muhimu inayofanywa duniani, yaani, kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Katika maono, mtume Yohana aliona jinsi malaika wanavyoshiriki katika kazi ya kuhubiri, na aliandika hivi: “Nami nikamwona malaika mwingine akiruka katikati ya mbingu, naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufunuo 14:6) Ingawa siku hizi malaika hawazungumzi na wanadamu kama zamani, wao huwaongoza wahubiri wa habari njema kuwahubiria watu wanyofu.

SHETANI HUPOTOSHA MAMILIONI YA WATU

“Na vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli [Yesu Kristo] na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa, naye joka mkubwa na malaika zake wakapigana lakini hakushinda, wala mahali hapakupatikana mbinguni kwa ajili yao tena. Kwa hiyo yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.”—Ufunuo 12:7-9.

Kuna wakati ambapo mbinguni hakukuwa na amani. Mwanzoni kabisa mwa historia ya wanadamu, malaika mmoja alitamani kuabudiwa na hivyo akamwasi Yehova na kuwa Shetani, jina linalomaanisha “Mpinzani.” Baadaye, malaika wengine waliasi pia nao wakawa roho waovu. Ni waovu sana, nao humpinga Yehova na wamewapotosha watu wengi wasifuate mwongozo wenye upendo wa Yehova.

Shetani na roho wake ni waovu na wakatili. Wao ni adui za wanadamu, nao husababisha mateso mengi duniani. Kwa mfano, Shetani aliwaua watumishi na mifugo ya mwanamume mwaminifu Ayubu. Kisha, akawaua watoto wote kumi wa Ayubu kwa kuleta “upepo mkubwa” ambao ulivunja nyumba walimokuwa. Mwishowe, Shetani alimpiga Ayubu kwa “majipu hatari kuanzia wayo wa mguu wake mpaka kwenye utosi wa kichwa chake.”—Ayubu 1:7-19; 2:7.

Hata hivyo, hivi karibuni Shetani ataharibiwa. Tangu alipotupwa duniani, anajua kwamba “ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Ni habari njema kujua kwamba Shetani ataangamizwa!

WALE WANAOTOKA DUNIANI

‘Wewe [Yesu] ulimnunulia Mungu watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa, nawe ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’—Ufunuo 5:9, 10.

Kama vile Yesu alivyofufuliwa na kwenda mbinguni, wengine pia wanaenda mbinguni. Yesu aliwaambia hivi mitume wake waaminifu: “Ninaenda kuwatayarishia ninyi mahali. Pia, . . . nitakuja tena nami nitawapokea ninyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo mimi, ninyi pia muwe hapo.”—Yohana 14:2, 3.

Wanadamu wanaoenda mbinguni wanaenda huko kwa kusudi fulani. Wakiwa pamoja na Yesu, watafanyiza Ufalme ambao hatimaye utaitawala dunia yote na kuwaletea baraka wanadamu. Huo ndio Ufalme ambao Yesu aliwaambia wanafunzi wake wasali kuuhusu katika sala ya mfano aliposema hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.

Yesu akiwa na baadhi ya wale waliofufuliwa na kwenda kuishi mbinguni

MAMBO AMBAYO WALE WALIO MBINGUNI WATAFANYA

Mtume Yohana alisema hivi: “Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, . . . naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’”—Ufunuo 21:3, 4.

Maono hayo ya kinabii yanahusu wakati ambao Ufalme wa Mungu, utakaofanyizwa na Yesu na wale waliofufuliwa kutoka duniani, utaangamiza utawala wa Shetani na kuifanya dunia iwe paradiso. Mambo ambayo yamewasababishia wanadamu maumivu mengi na huzuni hayatakuwapo tena. Hata kifo kitaondolewa.

Namna gani mabilioni ya watu waliokufa ambao hawana tumaini la kwenda kuishi mbinguni? Wakati ujao, watafufuliwa wakiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani.—Luka 23:43.

USIWAOGOPE ROHO WAOVU

Mamilioni ya watu ni kama wafungwa katika zoea la uwasiliani roho nao huwaogopa sana roho waovu. Wanatumia hirizi na uchawi ili kujilinda. Hupaswi kufanya mambo hayo. Biblia inatufariji kwa kutuhakikishia hivi: “Kwa maana, kwa habari ya Yehova, macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Ukimtumaini Mungu wa kweli, Yehova, atakulinda kwa kuwa ana nguvu kuliko Shetani.

Ili kupata ulinzi wa Yehova, unahitaji kujifunza mambo yanayompendeza na kisha utende mambo hayo. Kwa mfano, katika karne ya kwanza, Wakristo katika jiji la Efeso walivichoma vitabu vyao vyote vya uchawi. (Matendo 19:19, 20) Vivyo hivyo, ili Mungu akulinde unapaswa kuharibu vitu vyote vinavyohusiana na uwasiliani roho kama vile hirizi, na vitabu vya uchawi.

Biblia inasema hivi: “Jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” (Yakobo 4:7) Ukijitiisha kwa Mungu na kumtumikia, unaweza kuwa na uhakika kwamba Shetani na roho wake waovu hawatakushinda.

Maono hayo yanatuthibitishia kwamba Yehova Mungu, Mwana wake Yesu Kristo, malaika waaminifu, na wale walionunuliwa kutoka duniani, wanatujali sana na kuhangaikia hali yetu. Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu mambo watakayofanya, tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova au tembelea tovuti ya, www.jw.org/sw na upakue kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki