Usafi Humheshimu Mungu
1 Sheria ya Kimusa ilikuwa na matakwa imara kuhakikisha usafi. Hayo yaliweka Israeli kando wakiwa watu waliotakwa wajiweke safi kimwili na kiroho. (Law. 11:35, 36; 15:1-11; Isa. 52:11) Hali hiyo ya usafi ilimletea Mungu heshima na ilichangia afya ya taifa.
2 Leo vilevile, usafi ni ishara ya kuwatambulisha watu wa Yehova. Lakini ingawa huo huwatambulisha watu wa Yehova wakiwa kikundi, je, ni hivyo kwa kila mmoja wetu? Kadiri ambavyo sisi twahangaikia unadhifu na usafi wa kibinafsi huonyesha kadiri tunavyothamini matakwa ya Yehova.
3 Namna gani sura ya nyumba yetu? Je! hiyo hufanya wengine wauone vibaya ujumbe wa Ufalme tulio nao? Je! yawezekana kwamba wengine huenda wakatilia shaka weupe wetu wa moyo tukisema juu ya kugeuza dunia iwe paradiso huku nyumba yetu ni chafu na uwanja wa nje umejaa nyasi au magugu yasiyokatwa? Nyumba yetu ikionekana kuwa shaghalabaghala au kuna uvundo wenye kuchukiza kwa sababu ya tabia ziwezazo kudhuru afya, je, yaweza kusemwa kwamba tumesitawisha “mazoea na mifano ya usafi itakayopatana na ulimwengu mpya chini ya Ufalme wa Mungu”?—om-SW uku. 130-1.
4 Namna gani gari tunalotumia katika utumishi wa shambani? Je! ni safi ifaavyo, ndani na nje, hivi kwamba sura yalo hailetei sifa mbaya kazi yetu ya kuhubiri? Namna gani mavazi yetu, mfuko wetu, na mapambo ya kibinafsi? Je! ni nadhifu na yenye kupendeza, ambayo hayaudhi? Yafaa kwamba tujiweke wenyewe na mavazi yetu safi kwa kuoga na kufua nguo kwa ukawaida.—w89-SW 6/1 kur. 16-19.
5 Namna gani ikiwa ndugu amekuwa mlegevu hivi kwamba usafi wake wa kibinafsi au mazingira yake yameletea kutaniko suto? Labda yeye ahitaji tu msaada wenye upendo kwa sababu ya umri au ugonjwa fulani. Ikiwa ni hivyo, lingekuwa jambo la fadhili kumsaidia. Huenda mtu akawa na tatizo hilo na hata asitambue; onyo lenye upole la fadhili, laweza kumchochea arekebishe hali hiyo. Watu mmoja-mmoja wanaoweka kielelezo kibaya daima kuhusiana na jambo hilo wasingestahili kupata mapendeleo yenye kutokeza kutanikoni. Bila shaka, wazee wapaswa wawe waangalifu wasije wakaweka viwango au mapendezi yao ya kibinafsi.
6 Wale wenye kupendezwa karibuni wanaalikwa kufurahia karamu za kiroho kwenye Jumba la Ufalme letu. Kwa kawaida, sisi huwa na hamu ya kuwaalika kwa sababu jumba ni lenye kuvutia sana na ni nadhifu. Lakini, jitihada inatakikana ili kuliweka likiwa hivyo. Tazama kotekote katika jumba lenu. Je! viti, sakafu, na kuta ni safi? Je! vyoo husafishwa kabisa kwa kawaida? Tunapozoea kuona mkeka uliochafuka au kuta zenye rangi inayoambuka, huenda upesi tukazoea hilo. Hata hivyo, huenda wageni wanaokuja kwa mara ya kwanza wakapata maoni yasiyofaa. Twapaswa kufanya kadiri tuwezavyo kudumisha jumba lenye kuvutia na la kupendeza, tukifanya sehemu yetu wakati unapofika wa kusafisha au kufanyiza upya.
7 Bila kusema neno, twaweza kumtukuza Mungu kwa sura yetu ya kibinafsi na unadhifu wa nyumba zetu, magari yetu, na Majumba ya Ufalme yetu. Kielelezo chema hakitatoa sababu yoyote ya kukwaza bali kitatoa ushuhuda kwamba ibada yetu ni safi na ya unyoofu.—1 Kor. 10:31, 32; Yak. 1:27.