Broshua—Vifaa Vyenye Thamani kwa Huduma
1 Fundi mwenye ustadi hubeba vifaa mbalimbali, kila moja ikiwa imebuniwa kwa kazi hususa. Tukiwa wapiga-mbiu wa Ufalme, tuna broshua mbalimbali za kutusaidia tutimize mahitaji ya kiroho ya watu tunaohubiria kwa ustadi. (Mit. 22:29) Katika mlango mmoja huenda ukakuta mtu aliyeshuka moyo, ilhali mtu mwingine anajiuliza ikiwa kuna kusudi la kuishi. Twaweza kutumiaje broshua zetu tuwasaidie watu hawa?
2 Unapotoa broshua “Je! Kweli Mungu Anatujali?,” unaweza kusema jambo kama hili:
◼ “Watu fulani ambao wanaona kuteseka na ukosefu wa haki katika ulimwengu huelekea kuweka lawama yote kwa Mungu. Wao husababu kwamba kwa kuwa Mungu ni mweza yote, angekomesha kuteseka kwetu ikiwa kweli anatujali. Wewe wahisije kuhusu hilo? [Ruhusu itikio.] Zaburi 72:12-14 huonyesha kwamba Mungu anatujali kwelikweli. Kuteseka na ukosefu wa haki si kosa lake. Yeye ameahidi kwamba watenda mabaya wataondolewa karibuni. Broshua hii, Je! Kweli Mungu Anatujali?, yaonyesha atakalofanya na jinsi tuwezavyo kunufaika.” Unaweza kuendeleza mazungumzo na maelezo yaliyo kwenye ukurasa wa 27, fungu la 22.
3 Ikiwa unatumia broshua “Kusudi la Uhai,” huenda ukataka kuanza kwa njia hii:
◼ “Hatimaye, karibu kila mtu hujiuliza juu ya kusudi la uhai. Je! ni kuishi tu kwa miaka 70 au 80 kisha mtu afe? Au kuna maana zaidi ya uhai? Wewe wafikirije? [Ruhusu itikio.] Hapa kwenye Zaburi 37:29, twaona kusudi lenye kupendeza la Mungu kwa mwanadamu na dunia.” Baada ya kusoma andiko hilo, fungua kielezi kilicho kwenye ukurasa wa 31, na ueleze zaidi kuhusu jinsi itakavyokuwa kuishi katika Paradiso.
4 Broshua “Tazama!” yaweza kutolewa kwa kuonyesha kielezi cha jalada lote zima na kuuliza:
◼ “Unafikiri itahitaji nini kufanya dunia ionekane hivi? [Ruhusu itikio.] Kila mtu katika picha hii ana makao na kazi ya kufurahisha. Pana amani na chakula tele, na dunia haina uchafuzi. Hata wajaribu jinsi gani, binadamu hawawezi kutokeza ulimwengu kama huo. Hata hivyo, Biblia yatuhakikishia kwamba Mungu ‘atafanya vitu vyote kuwa vipya.’ [Fungua ukurasa wa 30, na usome Ufunuo 21:3, 4.] Broshua hii yaweza kukusaidia ujifunze unalohitaji kufanya ili uishi katika ulimwengu huo mpya.” Kisha, fungua ukurasa wa 3, na uonyeshe jinsi ya kuongoza funzo la Biblia.
5 Unaweza kutumia mfikio huu ukiwa na broshua “Maisha Duniani”:
◼ “Watu wengi hufikiri watahitaji kwenda mbinguni ili wafurahie uhai wa milele, lakini wafikirije kuhusu kuishi milele duniani? [Ruhusu itikio.] Biblia yatuhakikishia kwamba uhai wa milele wawezekana, nayo yaeleza jinsi twaweza kufikia mradi huo.” Soma Yohana 17:3. Kisha mwonyeshe mwenye nyumba kielezi cha 49 na uulize: “Ungeonaje kuishi katika ulimwengu kama huu?” Mtolee broshua, na upange ziara ya kurudia.
6 Broshua hizi zatoa masomo ya wakati ufaao, zajibu maswali ya watu, na zatoa faraja. Kwa kutumia vifaa hivi kwa ustadi, twaweza kusaidia watu wenye mioyo minyoofu ‘wapate kujua yaliyo kweli.’—1 Tim. 2:4.