Sanduku La Swali
◼ Kwa kuwa sasa tuna kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, funzo la Biblia nyumbani lapaswa kuongozwa kwa muda gani?
Huduma ya Ufalme Yetu ya Septemba 1993 ilipendekeza kwamba funzo la Biblia nyumbani liendelezwe kwa watu wapya wenye kupendezwa hadi vitabu viwili vimalizwe kusomwa. Kwa kuwa sasa tuna kitabu Ujuzi, yaonekana yafaa kufanya marekebisho katika utaratibu huu, kama ionyeshwavyo kwenye kurasa 13 na 14 za toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 1996.
Kitabu Ujuzi kimetayarishwa ili kusaidia watu “waliokuwa wamekusudiwa [“waliokuwa na mwelekeo ufaao kwa ajili ya,” NW] uzima wa milele” wajifunze yale wanayohitaji kujua ili wajitoe wakfu kwa Yehova na kubatizwa. (Mdo. 13:48) Kwa hiyo, baada ya kumaliza kusoma kichapo hiki kipya, si lazima kujifunza kitabu cha pili na mwanafunzi huyohuyo. Wanafunzi wako wa Biblia waanzapo kuikubali kweli, unaweza kuwatia moyo hatua kwa hatua wajenge ujuzi wao kwa kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova na vilevile kusoma Biblia na vichapo vingine vya Kikristo.
Ikiwa unafahamu kabisa maswali yaliyo kwenye kurasa 175 hadi 218 ya kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu, yaweza kuwa msaada. Ijapokuwa hupaswi kurejezea maswali haya au kuyapitia na mwanafunzi wa Biblia, huenda ikawa vizuri kukazia mambo yaliyo kwenye kitabu Ujuzi yatakayomsaidia mwanafunzi aonyeshe uelewevu ufaao kwa kweli za msingi za Biblia wakati wazee wapitiapo maswali ya wataka kubatizwa.
Hakuna uhitaji wa kuongezea habari ya ziada kwa kitabu Ujuzi, kuleta habari ya nje au hoja za ziada ili kuunga mkono mafundisho ya Biblia au kupinga mafundisho ya uwongo. Kufanya hivyo kutarefusha tu kipindi cha funzo. Badala ya hivyo, yatumainiwa kwamba kitabu hiki chaweza kumalizwa kusomwa haraka, labda kwa miezi sita hivi. Hili hukazia uhitaji wetu wa kujifunza habari hiyo kikamili mapema ili kwamba tuweze kuitoa waziwazi na kwa usahihi. Mwanafunzi apaswa pia kuhimizwa ajifunze mapema, aangalie maandiko yaliyowekwa bila kunukuliwa, na kujitahidi kufahamu waziwazi kile ambacho kitabu hicho kinafundisha katika kila sura.
Mnara wa Mlinzi limekazia uhitaji wa Mashahidi wa Yehova kuongoza idadi kubwa zaidi ya mafunzo ya Biblia yenye matokeo kwa kipindi kifupi zaidi cha wakati. (Ona Isaya 60:22.) Matumizi yenye matokeo ya kitabu Ujuzi yaweza kusaidia wapya wapate ujuzi uongozao kwenye uhai udumuo milele na kutenda kupatana nao.—Yn. 17:3.