Iga Imani Yao
1 Mtume Paulo alifafanua imani kuwa “hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana.” Aliongezea kwamba “pasipo imani haiwezekani kumpendeza [Mungu].” (Ebr. 11:1, 6) Paulo alitusihi tudhihirishe imani, tuwe nayo kwa wingi, na tuifuatie.—2 Kor. 4:13; Kol. 2:7; 2 Tim. 2:22.
2 Kuna vielelezo vingi vyenye kutokeza vya imani vilivyosimuliwa katika Biblia. Katika Waebrania sura 11, Paulo atoa orodha ndefu ya mashahidi walioonyesha imani isiyovunjika. Orodha hii yatia ndani Abeli, aliyekuwa wa kwanza kufia imani. Noa anaorodheshwa kwa sababu kwa imani yake alionyesha hofu ya kimungu iliyohitajiwa kuokoa watu wa nyumba yake. Abrahamu anapongezwa kwa imani yake na utii wake. Musa anasifiwa kwa sababu kwa imani yake aliendelea akiwa imara kana kwamba alikuwa akimwona Yule asiyeonekana. Orodha ya vielelezo hivyo ilikuwa ndefu mno hivi kwamba Paulo alisema wakati ungekosekana ikiwa angeendelea kueleza vyote hivyo. Tunashukuru kama nini kwamba twaweza kuimarisha imani yetu kupitia “mwenendo [wao] mtakatifu na utauwa”!—2 Pet. 3:11.
3 Katika karne ya kwanza, Yesu alitokeza swali hili: “Atakapokuja Mwana wa Adamu, je! ataiona imani duniani?” (Luka 18:8) Basi, je, tuna vielelezo halisi vya imani miongoni mwetu leo? Je, twaona wanaume na wanawake, vijana kwa wazee, wanaoonyesha imani isiyotikisika katika Yehova kama walivyokuwa wakifanya watumishi wa Mungu katika nyakati za Biblia?
4 Vielelezo vya Imani vya Siku ya Kisasa: Vielelezo vyenye kutokeza vya imani vyapatikana miongoni mwetu! Imani ya waangalizi wenye kuongoza miongoni mwetu vyastahili kuigwa. (Ebr. 13:7) Lakini si hawa tu walio vielelezo bora vya imani. Kuna waaminifu-washikamanifu wanaoshirikiana na kila kutaniko walio na rekodi ndefu ya utumishi mwaminifu kwa Yehova, mara nyingi ukifanywa chini ya hali ngumu sana.
5 Lazima tuvutiwe na dada zetu waaminifu ambao, kwa miaka mingi, wamevumilia upinzani kutoka kwa waume zao wenye kupinga. Imewalazimu wazazi wasio na wenzi kukabili magumu ya kulea watoto wakiwa peke yao. Kuna wajane wazee-wazee miongoni mwetu wasiokosa utendaji wa kutaniko kamwe hata ingawa huenda wasiwe na familia ya kuwatia moyo. (Linganisha Luka 2:37.) Twastaajabia imani ya wale wanaovumilia matatizo ya kudumu ya afya. Wengi huendelea kutumikia kwa uaminifu-mshikamanifu hata kama wana mapungufu yanayowazuia wasipate mapendeleo ya ziada ya utumishi. Kuna Mashahidi wachanga ambao wamedhihirisha imani kwa moyo mkuu wajapopata upinzani shuleni. Ujitoaji-kimungu wetu huendelea kuwa na nguvu tunapoona mapainia waaminifu ambao huvumilia mwaka baada ya mwaka wanapokabili matatizo yasiyoelezeka. Kama Paulo, wakati ungekosekana ikiwa tungejaribu kusimulia mambo yote yaliyoonwa ya utumishi wa Ufalme na matendo ya imani yatimizwayo na ndugu na dada hawa!
6 Vielelezo hivi vya waaminifu hutupa faraja na kitia-moyo. (1 The. 3:7, 8) Twafanya vema kuiga imani yao kwa sababu “watendao uaminifu ndio furaha yake [Yehova].”—Mit. 12:22.