Kueneza Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
1 Yehova ndiye ‘afundishaye wanadamu ujuzi.’ (Zab. 94:10, NW) Yeye hututumia sisi kueneza ujuzi uokoao uhai unaohusu yeye kwa wale wasiojua jinsi ya kumtumikia kwa njia inayokubalika. Kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele ni chombo kizuri cha kufundisha ambacho kupitia hicho watu wenye mioyo ya haki wanaweza kupata uelewevu sahihi wa Mungu kutokana na Neno lake lililoandikwa, Biblia. (1 Tim. 2:3, 4) Uelezaji wa kweli ulio wazi na wenye kusababu kuzuri wa kitabu Ujuzi utasaidia watu waelewe yale ambayo Yehova anataka kuwafundisha. Mwezi huu twataka kuhusisha watu katika mazungumzo ambayo yatawafanya watake kusoma kitabu hiki. Hapa pana madokezo kadhaa. Badala ya kujaribu kuyakariri, jaribu kueleza mawazo ya msingi kwa maneno yako mwenyewe na njia ya kawaida ya kuzungumza.
2 Kwa kuwa watu wengi wamepoteza mpendwa katika kifo, unaweza kueleza tumaini la ufufuo kwa kusema jambo kama hili kwanza:
◼ “Wengi wetu tumepoteza mpendwa katika kifo. Je, umepata kujiuliza kama utamwona mtu huyo tena? [Ruhusu itikio.] Kifo hakikuwa sehemu ya kusudi la Mungu la awali kwa mwanadamu. Yesu alithibitisha kwamba wapendwa wetu wanaweza kukombolewa kutoka kifo. [Soma Yohana 11:11, 25, 44.] Hata ingawa jambo hili lilitendeka karne nyingi zilizopita, laonyesha yale ambayo Mungu ameahidi kutufanyia. [Fungua kitabu Ujuzi kwenye picha katika ukurasa 85 na usome maelezo yayo. Kisha onyesha picha iliyo kwenye ukurasa 86 na utoe maelezo juu yayo.] Ikiwa ungependa kusoma zaidi kuhusu tumaini hili lenye kufariji la ufufuo, ningependa kukuachia kitabu hiki.”
3 Baada ya mazungumzo ya kwanza juu ya tumaini la ufufuo, unaweza kuanza mazungumzo yenu yafuatayo na mtu huyohuyo kwa njia hii:
◼ “Huenda ukakumbuka nikisema kwamba kifo hakikuwa sehemu ya kusudi la Mungu la awali kwa mwanadamu. Ikiwa hilo ni kweli, kwa nini sisi huzeeka na kufa? Kasa wengine huishi kwa zaidi ya miaka 100, na kuna miti ambayo imekuwa ikiishi kwa maelfu ya miaka. Kwa nini wanadamu huishi miaka 70 au 80 tu? [Ruhusu itikio.] Tunakufa kwa sababu watu wa kwanza wawili walikosa kumtii Mungu.” Soma Warumi 5:12. Fungua ukurasa 53 katika kitabu Ujuzi na usome kichwa cha sura hiyo. Chunguzeni mafungu matatu ya kwanza, ukionyesha majibu ya maswali yaliyochapwa. Fanya mpango wa kurudi baadaye ili kuzungumzia sehemu iliyobaki ya sura. Tia moyo mtu huyo amalize kuisoma kabla ya wewe kurudi.
4 Ukiongea na mtu anayeonekana kuwa wa kidini, unaweza kusema hivi:
◼ “Kwa kweli kuna mamia ya dini tofauti-tofauti leo. Hizo hufundisha aina zote za itikadi zenye kupingana. Watu fulani husema kwamba dini zote ni nzuri na haidhuru tunaamini nini. Maoni yako ni nini? [Ruhusu itikio.] Yesu alifundisha dini ya kweli na kuonyesha kwamba aina nyingine za ibada hazikubaliwi na Mungu. [Soma Mathayo 7:21-23.] Tukitaka kumpendeza Mungu, lazima tumwabudu kupatana na mapenzi yake.” Fungua kitabu Ujuzi kwenye sura ya 5, soma kichwa, na ukazie baadhi ya vichwa vidogo. Eleza kwamba habari hii itamsaidia mtu kujifunza jinsi ya kumpendeza Mungu. Toa kitabu na utoe wonyesho wa njia ya kujifunza.
5 Watu ambao wamevurugika kwa sababu kuna dini nyingi sana wanaweza kuthamini jibu la swali hili kwenye ziara yako ya kurudia:
◼ “Leo kukiwa na dini nyingi sana, twaweza kujuaje ni ipi ya kweli? Ungeamuaje ni ipi iliyo sawa? [Ruhusu itikio.] Yesu alituambia jinsi ya kutambua wafuasi wake wa kweli.” Soma Yohana 13:35. Chunguza mafungu 18 na 19 katika sura ya 5 ya kitabu Ujuzi. Kazia kwamba kwa kutumia miongozo hii ya Kimaandiko na utaratibu wa kuchuja dini, mtu anaweza kutambua dini ya kweli. Simulia jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyojulikana ulimwenguni pote kwa upendo wao halisi na viwango vyao vya juu vya adili. Eleza jinsi funzo la Biblia, kwa kutumia kitabu Ujuzi, litakavyotambulisha waziwazi aina ya ibada ambayo Mungu hukubali.
6 Ukimkuta mzazi, mfikio huu waweza kuwa na matokeo:
◼ “Kila siku twasikia ripoti juu ya mwenendo mtukutu wa vijana wanaoonekana hawana viwango vya adili. Watu wazima wengine wanataka kulaumu mfumo wa shule kwa kutofundisha watoto tofauti kati ya mema na mabaya. Unafikiri ni nani anayepaswa kuandaa mazoezi haya? [Ruhusu itikio.] Sikiliza yale ambayo Biblia yasema kuhusu swali hili. [Soma Waefeso 6:4.] Andiko hilo latuambia kwamba kufundisha watoto kidogo-kidogo viwango vya adili ni daraka la wazazi.” Fungua kitabu Ujuzi ukurasa 145, soma fungu la 16, na utoe maelezo juu ya picha zilizo kwenye ukurasa 147. Eleza kwamba kitabu hicho kimekusudiwa familia nzima kujifunza. Ukitumia mafungu 17 na 18 kwenye ukurasa 146, onyesha jinsi tunavyoweza kuongoza funzo hilo na familia.
7 Ikiwa ulianzisha funzo na mzazi aliye na wasiwasi ulipozuru mara ya kwanza, unaweza kuliendeleza katika ziara ya kurudia kwa kusema:
◼ “Ulimwengu wa leo huweka vishawishi vingi mbele za wachanga wetu. Jambo hilo hufanya iwe vigumu sana kwao kuwa wenye kumhofu Mungu wanapokua. Labda unakumbuka kwamba katika mazungumzo yetu ya mwisho, tuliteua kanuni mbili. Tukiwa wazazi wa kimungu, twahitaji kuweka vielelezo vyema kwa watoto wetu, na twapaswa kuandaa wonyesho daima wa upendo kwao. Kuna jambo jingine ambalo Biblia husema watoto wanahitaji kutoka kwa wazazi wao.” Soma Mithali 1:8. Fungua ukurasa 148 katika kitabu Ujuzi na uendeleze funzo, ukishughulikia mafungu 19-23. Sema utarudi tena ili kujifunza na familia nzima, kuanzia sura ya 1.