Wazazi—Fundisheni Watoto Wenu Mazoea Mazuri
1 Mazoea mazuri hayarithiwi, wala hayajitokezi yenyewe. Zaidi ya hilo, kufundisha watoto mazoea mazuri huchukua muda. “Kufundisha” humaanisha “kuelimisha hatua kwa hatua” au “kuzoeza taratibu.” Wazazi wanahitaji kufanya hivyo kwa ukawaida ili ‘waendelee kuwalea [watoto wao] katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.’—Efe. 6:4.
2 Anza Utotoni: Uwezo wa watoto wachanga zaidi wa kujifunza na kufanya mambo mapya ni wa ajabu. Ijapokuwa mara nyingi watu wazima huona vigumu kujifunza lugha mpya, watoto ambao hawajafikia umri wa kwenda shuleni wanaweza kujifunza lugha mbili au tatu wakati uleule. Usifikiri kamwe kwamba mtoto wako ni mchanga mno kuweza kusitawisha mazoea mazuri. Mafunzo ya kweli za Biblia yakianza mapema na kuendelezwa, mtoto atakapokuwa na umri wa miaka kadhaa, akili yake itajaa ujuzi utakaomfanya awe “mwenye hekima kwa ajili ya wokovu.”—2 Tim. 3:15.
3 Fanya Utumishi wa Shambani Uwe Zoea Lako: Zoea zuri ambalo mtoto atafunzwa anapoendelea kukua ni lile la kuhubiri kwa ukawaida habari njema za Ufalme wa Mungu. Wazazi wengi huanza kwa kwenda pamoja na watoto wao wakiwa wangali wachanga katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Wazazi wanaposhiriki kwa ukawaida katika kazi ya kutoa ushahidi wanawasaidia watoto wao wasitawishe uthamini na bidii kwa ajili ya huduma. Wazazi wanaweza kuonyesha watoto jinsi ya kutoa ushahidi katika kila sehemu ya utumishi wa shambani.
4 Pia kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi husaidia watoto. Huwafundisha mazoea mazuri ya kujifunza na jinsi ya kusoma kwa uelewevu. Wanajifunza kuzungumza juu ya Biblia, kufanya ziara za kurudia, na kuongoza mafunzo ya Biblia. Mazoezi hayo huenda yakawachochea kufanya upainia na kufikia mapendeleo ya pekee ya utumishi. Wanabetheli wengi na mishonari wengi wanakumbuka vizuri siku zao za awali katika shule hiyo nao huiona kuwa uandalizi uliowasaidia wasitawishe mazoea mazuri.
5 Sisi ni kama udongo mikononi mwa Mfinyanzi Mkuu, Yehova. (Isa. 64:8) Udongo unapokuwa mwororo, ndipo inapokuwa rahisi kuufinyanga. Kadiri unavyokauka, ndivyo unavyokuwa mgumu. Ndivyo ilivyo na watu. Wanapokuwa wangali wachanga, wananyumbulika kwa urahisi sana—wanapokuwa wachanga zaidi, matokeo yanakuwa bora zaidi. Miaka yao ya mapema ni miaka ya kukua, wakati ambapo kufinyangwa kutakuwa na matokeo mazuri au mabaya. Ukiwa mzazi anayejali, anza mapema kufundisha watoto wako mazoea mazuri katika huduma ya Kikristo.