Tangaza Ujumbe wa Ufalme
1 “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu kwa ajili ya hili nilitumwa.” (Luka 4:43) Yesu alijulisha habari kuu ya huduma yake, yaani, Ufalme wa Mungu. Ujumbe tunaotangaza leo unakazia pia Ufalme huo, kama ilivyotabiriwa kwenye Mathayo 24:14: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” Watu wanahitaji kusikia kweli zipi kuhusu Ufalme wa Mungu?
2 Ufalme wa Mungu unatawala sasa kutoka mbinguni na hivi karibuni utaondoa tawala zote za binadamu. Tayari Ibilisi ameondolewa mbinguni, na mfumo mwovu wa mambo uliopo sasa umeingia siku zake za mwisho. (Ufu. 12:10, 12) Mfumo mwovu wa Shetani utaharibiwa kabisa, lakini Ufalme wa Mungu hautaondoshwa kamwe. Utabaki milele.—Dan. 2:44; Ebr. 12:28.
3 Ufalme utatosheleza tamaa zinazofaa za wanadamu wote watiifu. Utakomesha mateso yote yanayosababishwa na vita, uhalifu, ukandamizaji na umaskini. (Zab. 46:8, 9; 72:12-14) Kutakuwako na chakula kingi kwa watu wote. (Zab. 72:16; Isa. 25:6) Magonjwa na kutojiweza vitakuwa mambo ya kale, yasiyokumbukwa tena. (Isa. 33:24; 35:5, 6) Huku wanadamu wakiendelea kufikia ukamilifu, dunia itageuzwa iwe paradiso, na watu watakaa pamoja kwa upatano.—Isa. 11:6-9.
4 Twaonyesha kwamba twataka kuwa raia wa Ufalme wa Mungu katika njia tunayoishi sasa. Ujumbe wa Ufalme wapaswa kuongoza maisha yetu yote, kutia ndani miradi na mambo tunayotanguliza. Kwa mfano, ijapokuwa tuna wajibu wa kuandalia familia yetu vitu vya kimwili, hatuwezi kuruhusu mahangaiko ya kimwili yasonge masilahi ya Ufalme. (Mt. 13:22; 1 Tim. 5:8) Badala yake, twapaswa kutii onyo hili la upole la Yesu: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi [mahitaji muhimu ya maisha] mtaongezewa.”—Mt. 6:33.
5 Ni jambo la muhimu kwa watu kusikia na kutenda kulingana na ujumbe wa Ufalme wakati ungalipo. Na tuwasaidie wafanye hivyo kwa “kutumia ushawishi kuhusu ufalme wa Mungu.”—Mdo. 19:8.