Kujulisha Jina la Mungu
1 Ulihisije ulipojua jina la Mungu kwa mara ya kwanza? Wengi huitikia kama mwanamke mmoja aliyesema: “Nilipoona jina la Mungu kwa mara ya kwanza katika Biblia, nililia. Niliguswa moyo sana nilipotambua kwamba ninaweza kulijua na kulitumia jina la Mungu.” Kwa mwanamke huyo, kulijua jina la Mungu kulikuwa hatua muhimu ya kupata kumjua Yehova kibinafsi na kusitawisha uhusiano naye.
2 Kwa Nini Tulijulishe? Kujua jina la Mungu kunatia ndani kujua sifa zake, makusudi na matendo yake. Ni lazima pia tujue jina lake ili tuokolewe. “Kila mtu aitiaye jina la Yehova ataokolewa,” akaandika mtume Paulo. Lakini “watamwitiaje,” akauliza Paulo, wasipojifunza kwanza kumhusu Yehova na kumwamini? Kwa hiyo ni muhimu Wakristo wawajulishe wengine jina la Mungu na umuhimu wa jina hilo. (Rom. 10:13, 14) Hata hivyo, kuna sababu kubwa hata zaidi ya kulijulisha jina la Mungu.
3 Katika miaka ya 1920, watu wa Mungu walitambua kutokana na Maandiko suala la ulimwengu la kutetewa kwa enzi kuu ya Mungu na kutakaswa kwa jina lake. Kabla Yehova hajaharibu waovu na kuliondolea jina lake lawama, ni lazima kweli kumhusu ‘ijulikane katika dunia yote.’ (Isa. 12:4, 5; Eze. 38:23) Kwa hiyo, sababu yetu kuu ya kuhubiri ni kumsifu Yehova hadharani na kulitakasa jina lake mbele ya wanadamu wote. (Ebr. 13:15) Upendo wetu kwa Mungu na jirani utatuchochea tushiriki kikamili kazi iliyoagizwa na Mungu.
4 “Watu kwa Ajili ya Jina Lake”: Tulianza kutumia jina Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1931. (Isa. 43:10) Tangu wakati huo, watu wa Mungu wamelijulisha jina la Mungu kwa kadiri ya kwamba kitabu Wapiga-Mbiu chasema hivi kwenye ukurasa wa 124: “Kimataifa, yeyote ambaye hutumia sana jina Yehova anatambuliwa haraka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.” Je, wewe unatambuliwa vivyo hivyo? Shukrani kwa ajili ya wema wa Yehova zinapaswa kutuchochea ‘tulihimidi jina lake,’ na kuongea kumhusu kila pindi inayofaa.—Zab. 20:7; 145:1, 2, 7.
5 Tukiwa “watu kwa ajili ya jina lake,” ni lazima tutii kanuni zake. (Mdo. 15:14; 2 Tim. 2:19) Mara nyingi jambo ambalo watu huona kwanza kuhusu Mashahidi wa Yehova ni mwenendo wao mzuri. (1 Pet. 2:12) Hatungetaka kamwe kuchafua jina la Mungu kwa kuvunja kanuni zake au kutotanguliza ibada yake maishani mwetu. (Law. 22:31, 32; Mal. 1:6-8, 12-14) Badala yake, mwenendo wetu na uonyeshe kwamba tunathamini pendeleo la kuitwa kwa jina la Mungu.
6 Leo, tunaona tangazo hili la Yehova likitimizwa: “Tokea maawio ya jua hata machweo yake jina langu ni kuu katika Mataifa.” (Mal. 1:11) Na tuendelee kujulisha ukweli kumhusu Yehova na ‘tulihimidi jina lake takatifu milele na milele.’—Zab. 145:21.
[Maswali ya Funzo]
1. Watu huhisije wanapojifunza jina la Mungu?
2. Kwa nini ni muhimu tuwafundishe wengine kumhusu Yehova?
3. Sababu yetu kuu ya kuhubiri ni ipi?
4. Mashahidi wa Yehova wametambuliwaje kwa jina lake?
5. Mwenendo wetu unahusianaje na jina la Mungu?
6. Tunaweza kufurahia pendeleo gani sasa na hata milele?