Huduma Yetu Inatimiza Nini?
1 Kulingana na Neno la Mungu, Wakristo wanasonga mbele kwa shangwe katika utumishi wa Yehova, kana kwamba wanashiriki katika maandamano ya ushindi. (2 Kor. 2:14-16) Tunapowahubiria watu kumhusu Mungu, huduma yetu huwa kama uvumba unaompendeza Yehova. Baadhi ya watu huvutiwa na utamu wa habari njema, wengine nao huikataa. Hata hivyo, ijapokuwa wengi wanakataa habari njema, hilo halimaanishi kwamba kazi yetu ni ya bure. Fikiria yale ambayo huduma yetu inatimiza.
2 Tunamtukuza Yehova: Shetani anadai kwamba watu wanamtumikia Yehova ili wanufaike. (Ayu. 1:9-11) Huduma ya Kikristo inatupa fursa ya kuonyesha kwamba tunamtumikia Mungu kwa unyoofu wa moyo. Wahubiri wengi wanaendelea kutii amri ya kuhubiri na kufanya wanafunzi licha ya kwamba wana matatizo ya kibinafsi au watu wengi wanakataa kusikiliza. Ushikamanifu na uvumilivu wao hufanya moyo wa Yehova ushangilie!—Met. 27:11.
3 Isitoshe, huduma yetu inahusiana na kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Yehova amesema hivi kuhusu kuharibiwa kwa ulimwengu wa Shetani: “Mataifa watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Eze. 39:7) Ili watu wa mataifa wajue hilo, ni lazima watumishi wa Mungu waendelee kutangaza jina na kusudi lake “kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.”—Ufu. 14:6, 7.
4 Msingi wa Hukumu: Zaidi ya hayo, kazi ya kuhubiri habari njema ni msingi wa hukumu. Mtume Paulo alisema kwamba Kristo Yesu atawalipiza kisasi “wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” (2 The. 1:8, 9) Watu watahukumiwa kupatana na jinsi wanavyotenda wanapohubiriwa habari njema. Watumishi wa Mungu wana wajibu mzito sana! Ili tuepuke hatia ya damu, hatuna budi kutangaza ujumbe wa Ufalme wenye kuokoa uhai.—Mdo. 20:26, 27.
5 Rehema ya Yehova inadhihirishwa katika jitihada zetu za kuwasaidia watu wapate kibali chake. (1 Tim. 2:3, 4) Kwa sababu tunajua kwamba maisha ya watu yanabadilika-badilika, tunawatembelea tena na tena na kuwasihi wamtafute Yehova maadamu kuna wakati. Kwa kufanya hivyo, tunaiga “huruma nyororo za Mungu wetu,” ambaye “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—Luka 1:78; 2 Pet. 3:9.
6 Tunajinufaisha Wenyewe: Kuwa na shughuli nyingi katika utumishi wa Yehova ni ulinzi kwetu. Hilo linatusaidia “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova” na kuepuka kutiwa unajisi na ulimwengu huu mwovu. (2 Pet. 3:11-14; Tito 2:11, 12) Kwa hiyo, tuendelee ‘kuwa imara na thabiti, sikuzote tukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, tukijua kwamba kazi yetu si ya bure.’—1 Kor. 15:58.
[Maswali ya Funzo]
1. Yehova anaionaje huduma yetu, na je, watu wanaikubali?
2. Huduma yetu inatupa fursa gani?
3. Kwa nini ni muhimu kuendelea kutangaza jina na kusudi la Mungu?
4. Kazi ya kuhubiri ni msingi wa hukumu kwa njia gani?
5. Rehema ya Mungu inadhihirishwaje katika huduma yetu?
6. Tunanufaikaje kwa kuwa na shughuli nyingi katika utumishi wa Yehova?