Onyesha Unawajali Watu Kikweli—Kwa Kuwauliza Maswali na Kuwasikiliza
1 Watu wengi hufurahia kutoa maoni, lakini wao huudhika wanapolazimika kumsikiliza mtu mwingine anayeongea mfululizo, na hawapendi kuulizwa maswali mengi. Kwa hiyo, wahudumu Wakristo wanahitaji kujifunza jinsi ya kutumia maswali vizuri ili wajue maoni ya watu.—Met. 20:5.
2 Maswali yetu yanapaswa kuwachochea watu wafikiri badala ya kuwaaibisha. Anapohubiri nyumba kwa nyumba, ndugu mmoja huwauliza wenye nyumba swali hili: “Je, unafikiri kwamba siku moja watu wote watatendeana kwa staha na heshima?” Ikitegemea jibu la mwenye nyumba yeye huuliza: “Unafikiri ni mabadiliko gani yanayohitajika ili watu waheshimiane?” au “Kwa nini unaamini hivyo?” Ndugu mwingine anapohubiri isivyo rasmi na katika sehemu za umma, yeye huwauliza hivi watu walio na watoto: “Kwa nini unafurahia kuwa mzazi?” Halafu anawauliza: “Ni mambo gani yanayokuhangaisha hasa?” Maswali hayo yanawapa watu fursa ya kutoa maoni bila kuwaaibisha. Kwa kuwa hali zinatofautiana, huenda ikatubidi kubadili maswali yetu, na jinsi tunavyoyatumia, ili yafae watu katika eneo letu.
3 Jinsi ya Kuwachochea Watu Wajieleze: Ikiwa watu wanataka kukuambia maoni yao, sikiliza kwa makini bila kuwakatiza. (Yak. 1:19) Washukuru kwa maoni yao. (Kol. 4:6) Unaweza kusema: “Asante sana. Nimefurahi kujua maoni yako.” Wapongeze ukiweza kufanya hivyo kwa moyo. Waulize maswali mengine ili ujue maoni yao na kwa nini wana maoni hayo. Jitahidi kuzungumzia mambo ambayo wenye nyumba wanakubali. Unapotaka kuwaonyesha andiko, unaweza kuuliza: “Je, umewahi kufikiria kile ambacho andiko hili linasema?” Usisisitize kutoa maoni yako wala usisababishe mabishano.—2 Tim. 2:24, 25.
4 Itikio la watu tunapowauliza maswali huenda likategemea jinsi tunavyosikiliza. Watu wanaweza kutambua kama tunapendezwa kwa moyo kujua maoni yao. Mwangalizi mmoja anayesafiri alisema hivi: “Watu huvutiwa sana unapowasikiliza kwa subira, na hilo huonyesha kwamba unawajali sana.” Kuwasikiliza wengine huonyesha kwamba tunawaheshimu, na huenda wakavutiwa kusikiliza habari njema tunayowahubiria.—Rom. 12:10.