Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 2/06 kur. 3-4
  • Waonyeshe Wengine “Nuru ya Ulimwengu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Waonyeshe Wengine “Nuru ya Ulimwengu”
  • Huduma ya Ufalme—2006
  • Habari Zinazolingana
  • Tangazeni Kotekote Sifa Bora za Yehova
    Huduma ya Ufalme—2007
  • Wanatakwa—Mapainia-Wasaidizi 2,500
    Huduma Yetu ya Ufalme—1997
  • ‘Lihubiri Neno la Mungu Kikamili’
    Huduma Yetu ya Ufalme—2002
  • Je, Wewe Utafanya Upainia Msaidizi?
    Huduma ya Ufalme—2013
Pata Habari Zaidi
Huduma ya Ufalme—2006
km 2/06 kur. 3-4

Waonyeshe Wengine “Nuru ya Ulimwengu”

1 Kupitia nabii Isaya, Yehova alitabiri hivi: “Watu waliokuwa wakitembea katika giza wameona nuru kuu. Kwa habari ya wale wanaokaa katika nchi yenye kivuli kizito, nuru imewaangazia.” (Isa. 9:2) Hiyo “nuru kuu” ilionekana katika mwenendo wa Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. Kazi aliyofanya alipokuwa hapa duniani na baraka zilizotokana na dhabihu yake ziliwachochea wale waliokuwa katika giza la kiroho. Nuru kama hiyo ndiyo watu wanahitaji katika nyakati hizi zenye giza. Mlo wa Jioni wa Bwana hutupa nafasi ya pekee ya kuwaonyesha wengine “nuru ya ulimwengu.” (Yoh. 8:12) Mwaka uliopita, mamilioni ya watu walionyesha imani ya kadiri fulani kwa kujiunga nasi kutii amri ya Yesu inayosema: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Maadhimisho ya ukumbusho ya mwaka huu yanapokaribia, tunaweza kushiriki jinsi gani katika kuwaonyesha wengine nuru kuu ambayo Yehova ametoa?—Flp. 2:15.

2 Sitawisha Uthamini wa Moyoni: Majira ya Ukumbusho ni wakati mzuri wa kutafakari kuhusu upendo mkubwa ambao Yehova na Yesu walionyesha kwa kuwatolea wanadamu dhabihu ya fidia. (Yoh. 3:16; 2 Kor. 5:14, 15) Bila shaka kufanya hivyo kutaongeza uthamini wetu wa kutoka moyoni kwa ajili ya tukio hili takatifu. Watu wote wa Mungu wangependa kutenga wakati wa kusoma na kutafakari usomaji wa pekee wa Biblia kwa ajili ya Ukumbusho, kama unavyoonyeshwa katika kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Kufikiria sifa za Yehova zisizo na kifani, ambazo zimeonekana wazi kwa kututolea fidia, hutufanya tujivunie yeye kuwa Mungu wetu. Kutafakari yale ambayo fidia inamaanisha kwa ajili yetu binafsi kunaongeza upendo wetu wa kutoka moyoni kumwelekea Mungu na Mwana wake na kutuchochea tujitahidi kadiri tuwezavyo kufanya mapenzi ya Mungu.—Gal. 2:20.

3 Tukiongeza uthamini wetu kwa uandalizi wa Yehova wa wokovu, msisimuko wetu kwa ajili ya Ukumbusho utawachochea wanafunzi wa Biblia, marudio, watu wa ukoo, majirani, wanafunzi wenzetu, wafanyakazi wenzetu, na wengine ambao tunakaribisha kwenye tukio hilo la pekee. (Luka 6:45) Kwa hiyo, fanya jitihada ya pekee kuwakaribisha watu hao wote kwa kuwapa mwaliko wa Ukumbusho uliochapishwa ili wasisahau. Ili wasimsahau mtu yeyote, wengi wameona kuwa inafaa kuandika orodha ya watu wanaowakaribisha kwa ukawaida kwenye Ukumbusho. Nao huongeza majina kwenye orodha hiyo kila mwaka. Tunapofanya hivyo kwa mpango na kujitahidi kuwaalika wote wanaopendezwa tutakuwa tukionyesha shukrani zetu kwa Yehova Mungu “kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.”—2 Kor. 9:15.

4 Kuongeza Utendaji Wetu Katika Huduma: Je, unaweza kuongeza utendaji wako katika huduma mwezi wa Machi na Aprili? Bila shaka utapata baraka za Yehova unapojitahidi kuwahubiria wengine “habari njema yenye utukufu juu ya Kristo.” Yehova, ambaye ndiye Chanzo cha nuru yote ya kiroho, ameamuru hivi: “Nuru na iangaze kutoka katika giza.” (2 Kor. 4:4-6) Inapofaa, wazee watapanga mikutano ya utumishi wa shambani nyakati za ziada na mahali mbalimbali. Watajitahidi pia kuwasaidia wahubiri wanaotaka kuhubiri kwa muda mrefu. Hiyo inaweza kutia ndani kuhubiri barabarani mapema asubuhi au kupanga kuhubiri maeneo ya biashara na kuhubiri kwa simu alasiri au jioni. Ili uongeze utendaji wako katika huduma, jiwekee mradi wa saa unaofaa, na ujitahidi sana kuutimiza. Kwa wengi, kumtolea Yehova kilicho bora kunatia ndani pendeleo la kuwa mapainia-wasaidizi.—Kol. 3:23, 24.

5 Je, Unaweza Kuwa Painia-Msaidizi? Miaka saba sasa imepita tangu takwa la saa kwa ajili ya mapainia-wasaidizi lipunguzwe. Badiliko hilo limewawezesha wengi kufurahia baraka za utumishi wa upainia msaidizi. Je, umejaribu utumishi huo? Wengine huhakikisha kwamba wamefanya upainia msaidizi kila mwaka. Katika makutaniko mengi wahubiri wengi hufanya utumishi huo pamoja. Hilo huwa jambo kuu katika utendaji wa kutaniko mwaka huo. Je, unaweza kutenga wakati ili ufurahie upainia msaidizi katika majira ya Ukumbusho? Huenda Aprili ukawa mwezi mzuri kwa wengine kwani una miisho-juma mitano.

6 Je, kutaniko lenu litakuwa na ziara ya mwangalizi wa mzunguko mwezi wa Machi au Aprili? Basi una nafasi ya pekee. Kama ilivyotangazwa awali, wakati wa mwaka wa utumishi wa 2006, wote ambao ni mapainia-wasaidizi mwezi ambao mwangalizi wa mzunguko anazuru wataalikwa wahudhurie sehemu ya kwanza ya mkutano unaofanywa pamoja na mapainia. Bila shaka habari yenye kuimarisha kiroho inayotolewa kwenye mkutano huo itawasaidia mapainia wengi wasaidizi wafikie mradi wa kuwa mapainia wa kawaida. Isitoshe, mwezi wa Machi tutafurahia kuwasaidia watu wapate nuru ya kiroho kwa kutumia kitabu kipya cha kujifunza chenye kichwa Biblia Inafundisha Nini Hasa? Kwa nini usijiwekee mradi wa kuanzisha funzo la Biblia ukitumia kitabu hicho kipya?

7 Unapofikiria takwa la saa 50 kwa ajili ya mapainia-wasaidizi, amua ni ratiba gani itakayokuwezesha kuangaza nuru ya kweli kwa kutumia saa 12 hivi kila juma. Zungumza na wengine ambao tayari wamefaulu kulitimiza. Zungumza pia na wahubiri wengine. Kwa kufanya hivyo, huenda ukawatia moyo wajiunge nawe. Kwa kuwa na mpango mzuri, wahubiri waliobatizwa, vijana kwa wazee, wameona kwamba si vigumu kutimiza mradi huo mzuri. Sali kuhusu jambo hilo. Kisha, fanya mipango yako, na ufurahie upainia msaidizi!—Mal. 3:10.

8 Familia nyingi zimeona kwamba wote wanaposhirikiana inawezekana kwa angalau mmoja wao kutimiza mradi huo. Familia moja iliamua kwamba washiriki wote watano waliobatizwa wangekuwa mapainia-wasaidizi. Watoto wawili ambao hawakuwa wamebatizwa walifanya jitihada ya pekee kuongeza utumishi wao. Familia hiyo ilinufaikaje kwa kuongeza utendaji wao? Waliandika hivi: “Ulikuwa mwezi wenye kupendeza sana, na tulihisi kwamba vifungo vya familia yetu viliimarika. Tunamshukuru Yehova kwa baraka nzuri ajabu!”

9 Je, utendaji wetu wa pekee mwezi wa Machi na Aprili utatuchochea na kufanya tumkaribie zaidi Baba yetu wa mbinguni? Tutafaulu ikiwa tutajitahidi kuongeza upendo wetu kwa Mungu na Mwana wake na pia kuongeza utendaji wetu katika huduma. Azimio letu na liwe kama la mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Nitamsifu sana Yehova kwa kinywa changu, na katikati ya watu wengi nitamsifu.” (Zab. 109:30) Yehova atabariki utendaji wetu wa bidii katika majira haya ya Ukumbusho. Kwa hiyo na tuangaze nuru kuu ili wengine wengi watoke gizani na ‘kuwa na nuru ya uzima.’—Yoh. 8:12.

[Maswali ya Funzo]

1. Ni nuru gani kuu iliyotabiriwa katika Neno la Mungu, na ni tukio gani la pekee ambalo husaidia kuwaonyesha wengine nuru hiyo?

2. Tunawezaje kuongeza uthamini wetu wa kutoka moyoni kwa ajili ya dhabihu ya fidia, na kufanya hivyo kutakuwa na matokeo gani?

3. Tunaweza kuonyeshaje uthamini wetu kwa ajili ya Ukumbusho?

4. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuongeza utendaji wetu katika huduma mwezi wa Machi na Aprili?

5. Wengi wananufaikaje kutokana na kupunguzwa kwa takwa la saa kwa ajili ya mapainia-wasaidizi?

6. Ni maandalizi gani yenye kusisimua ambayo yametolewa?

7, 8. (a) Ni nini kinachoweza kutusaidia kupanga ratiba ya kufanya upainia msaidizi? (b) Ushirikiano wa familia unaweza kusaidiaje, na familia yote hunufaikaje?

9. Tunaweza kuangazaje nuru yetu katika majira haya ya Ukumbusho?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki