Msaidie Mwanafunzi Athamini Sifa za Yehova Zisizo na Kifani
1 Katika huduma yetu tunafanya mengi zaidi ya kuwafundisha watu kweli za msingi za Biblia. Tunawasaidia watu kumjua Yehova kama mtu halisi na kuwasaidia wathamini sifa zake zisizo na kifani. Watu wanyoofu wanapojifunza kweli kumhusu Mungu, kweli hiyo huwaathiri sana ikiwasukuma kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yao ‘ili watembee kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili.’—Kol. 1:9, 10; 3:9, 10.
2 Kitabu Chetu Kipya cha Kufundishia: Kuanzia mwanzo, kitabu Biblia Inafundisha kinakazia sifa za Yehova. Katika sura ya kwanza tu kinajibu maswali kama: Je, kweli Mungu anakujali?, Mungu ana utu wa aina gani?, na Je, tunaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu? Sura hiyo pia inakazia utakatifu wa Yehova (fu. 10), haki na huruma zake (fu. 11), upendo wake (fu. 13), nguvu zake (fu. 16), rehema zake, neema, kuwa tayari kusamehe, uvumilivu na uaminifu (fu. 19). Fungu la 20 linamalizia habari hiyo kwa kusema hivi: “Unapozidi kujifunza kumhusu Yehova, atakuwa halisi zaidi kwako nawe utampenda na kumkaribia zaidi.”
3 Tunaweza kutumiaje kitabu Biblia Inafundisha kuwasaidia wanafunzi wa Biblia kumkaribia Yehova? Baada ya kuchunguza fungu linaloonyesha moja ya sifa za Yehova, tunaweza kumwuliza mwanafunzi, “Sifa hii inakufundisha nini kumhusu Yehova?” au “Sifa hii inakusaidiaje kuona jinsi Yehova anavyokupenda wewe binafsi?” Mara kwa mara tunapowauliza wanafunzi maswali kama hayo, tunawazoeza kutafakari wakati wanapojifunza na kuwasaidia kuthamini zaidi sifa zisizo na kifani za Yehova.
4 Tumia Sanduku la Pitio: Mwishoni mwa kila sura mwombe mwanafunzi atoe maelezo yake mwenyewe kuhusu kila hoja kwenye sanduku “Mambo ambayo Biblia Inafundisha.” Kazia maandiko yaliyoonyeshwa. Ili ujue yaliyo moyoni mwa mwanafunzi unaweza kumwuliza hivi, “Unapofikiria hoja hii, unahisije kuhusu kile ambacho Biblia inafundisha?” Kwa kufanya hivyo hutakuwa unakazia mambo makuu ya sura tu bali pia utajua kile ambacho mwanafunzi anaamini. Hilo litamsaidia mwanafunzi aanze kujenga uhusiano pamoja na Yehova.