Mungu alipotawala, viumbe wote waliishi kwa amani na umoja
Kwa Nini Tunahitaji Ufalme wa Mungu?
Mwanzoni mwa historia ya wanadamu, Muumba wetu, ambaye jina lake ni Yehova, ndiye alikuwa Mtawala pekee. Alitawala kwa upendo. Aliwatayarishia wanadamu makao maridadi ya kuishi, yaani, bustani ya Edeni. Pia, aliwapatia chakula kingi. Isitoshe, Yehova aliwapatia wanadamu kazi nzuri sana. (Mwanzo 1:28, 29; 2:8, 15) Wanadamu wangeendelea kufurahia amani ikiwa wangemruhusu Mungu aendelee kuwatawala kwa upendo.
Wanadamu wa kwanza walimkataa Mungu kuwa Mtawala wao
Biblia inaonyesha kwamba malaika mwasi, ambaye baadaye aliitwa Shetani Ibilisi, alitilia shaka haki ya Mungu ya kutawala. Alidai kwamba wanadamu watakuwa na furaha wakikataa kutawaliwa na Mungu na wakiacha kufuata mwongozo wake. Kwa kusikitisha, wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walimsikiliza Shetani nao wakamwasi Mungu.—Mwanzo 3:1-6; Ufunuo 12:9.
Kwa kuwa Adamu na Hawa walimkataa Mungu kuwa Mtawala wao, walifukuzwa kutoka katika Paradiso na kupoteza tumaini la kuishi milele wakiwa na afya kamilifu. (Mwanzo 3:17-19) Uamuzi wao uliathiri watoto wao wote. Biblia inasema kwamba kwa sababu ya dhambi ambayo Adamu alifanya, “dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” (Waroma 5:12) Dhambi ilikuwa na matokeo mengine mabaya: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu mwenzake kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Hilo linamaanisha kwamba wanadamu wanapojitawala, lazima matatizo yatokee.
MWANZO WA UTAWALA WA WANADAMU
Nimrodi alimwasi Yehova
Mtawala wa kwanza wa wanadamu anayetajwa katika Biblia aliitwa Nimrodi. Aliasi utawala wa Yehova. Tangu siku za Nimrodi, watu wenye mamlaka wametumia mamlaka yao vibaya kuwaumiza wengine. Miaka 3,000 hivi iliyopita, Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Nikaona machozi ya wanaokandamizwa, na hakukuwa na mtu yeyote wa kuwafariji. Na wale waliowakandamiza walikuwa na nguvu.”—Mhubiri 4:1.
Mambo hayajabadilika leo. Mwaka 2009, chapisho moja la Umoja wa Mataifa lilisema kwamba utawala mbaya umeonekana kuwa chanzo cha mambo maovu yanayoendelea duniani leo.
MUDA WA KUCHUKUA HATUA UMEKARIBIA!
Ulimwengu unahitaji watawala bora na utawala mzuri. Muumba wetu ametuahidi jambo hilo!
Hata serikali bora za wanadamu zimeshindwa kusuluhisha matatizo makubwa ya wanadamu
Mungu ameusimamisha Ufalme au utawala ambao utaondoa serikali zote za wanadamu, “nao pekee utasimama milele.” (Danieli 2:44) Huo ndio Ufalme ambao mamilioni ya watu wamekuwa wakiomba uje. (Mathayo 6:9, 10) Lakini Mungu amemchagua mtawala wa serikali Yake. Mtawala huyo amewahi kuwa mwanadamu. Mungu amemchagua nani?