Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w20 Mei kur. 20-25
  • Je, Unathamini Zawadi Zinazotoka kwa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Unathamini Zawadi Zinazotoka kwa Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SAYARI YETU YA PEKEE
  • UBONGO WETU WA PEKEE
  • BIBLIA​—ZAWADI YA PEKEE
  • Jinsi Ulivyo Kiumbe cha Kipekee!
    Je, Kuna Muumba Anayekujali?
  • Ubongo Wako Hufanyaje Kazi?
    Amkeni!—1999
  • Uumbaji Unamfunua Mungu Aliye Hai
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Sayari Yenye Uhai Tele
    Uhai—Ulitokana na Muumba?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
w20 Mei kur. 20-25

MAKALA YA 21

Je, Unathamini Zawadi Zinazotoka kwa Mungu?

“Jinsi ulivyotenda mambo mengi sana, Ee Yehova Mungu wangu, kazi zako zinazostaajabisha na mawazo yako kutuelekea.”—ZAB. 40:5.

WIMBO 5 Kazi za Mungu za Ajabu

MUHTASARIa

1-2. Kulingana na Zaburi 40:5, Yehova ametupatia zawadi gani, na kwa nini tutazungumza kuzihusu?

YEHOVA ni Mungu mkarimu. Fikiria baadhi ya zawadi ambazo ametupatia: dunia, makao yetu maridadi na ya pekee; ubongo wetu ulioumbwa kwa njia yenye kustaajabisha; na Biblia, Neno lake lenye thamani. Kwa sababu Yehova ametupatia zawadi hizo tatu, tuna mahali pa kuishi, tunaweza kufikiri na kuwasiliana na wengine, na tumepata majibu ya maswali muhimu zaidi tunayoweza kuuliza.—Soma Zaburi 40:5.

2 Katika makala hii, tutazungumzia kwa ufupi zawadi hizo tatu. Kadiri tunavyotafakari kuzihusu, ndivyo tutakavyozithamini zaidi na ndivyo tamaa yetu ya kumpendeza Yehova, Muumba wetu mwenye upendo, itakavyozidi kuongezeka. (Ufu. 4:11) Pia, tutaweza kujadiliana kwa njia nzuri zaidi na wale ambao wamepotoshwa na fundisho la uwongo la mageuzi.

SAYARI YETU YA PEKEE

3. Kwa nini dunia ni ya pekee?

3 Hekima ya Mungu inaonekana waziwazi kupitia jinsi alivyoiumba dunia, makao yetu.(Rom. 1:20; Ebr. 3:4) Kuna sayari nyingine zinazozunguka jua, lakini dunia ni ya pekee kwa sababu ina hali zote zinazofaa ili kuendeleza uhai wa wanadamu.

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba dunia ni bora kuliko mashua iliyotengenezwa na mwanadamu?

4 Kwa njia fulani, dunia ni kama mashua inayoelea kwenye bahari kubwa sana ya anga. Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya dunia yetu na mashua iliyojaa watu ambayo imetengenezwa na mwanadamu. Kwa mfano, watu walio kwenye mashua halisi wangeweza kuendelea kuishi humo kwa muda mrefu kadiri gani, ikiwa wangelazimika kuzalisha hewa safi ya oksijeni, chakula, na maji, na ikiwa wangeacha takataka zote ndani ya mashua? Punde si punde wote wangekufa. Tofauti na mashua hiyo, dunia inategemeza mabilioni ya viumbe hai. Dunia inatokeza hewa safi ya oksijeni, chakula, na maji tunayohitaji, na hatupungukiwi na vitu hivyo muhimu sana. Takataka zinazozalishwa hazitupwi nje ya dunia; ingawa hivyo dunia inaendelea kubaki ikiwa maridadi na mahali salama kwa ajili ya viumbe. Hilo linawezekanaje? Yehova aliiumba dunia ikiwa na uwezo wa kubadili vitu vilivyotumika viweze kutumiwa tena kwa njia nyingine yenye manufaa. Tutachunguza kwa ufupi jinsi hekima ya Yehova inavyoonekana kupitia mzunguko wa oksijeni na mzunguko wa maji.

5. Mzunguko wa oksijeni ni nini, nao unathibitisha nini?

5 Oksijeni ni hewa inayoendeleza uhai ambayo hutumiwa na baadhi ya viumbe hai, kutia ndani sisi wanadamu. Imekadiriwa kwamba kwa mwaka mmoja viumbe hai hupumua tani bilioni mia moja za hewa ya oksijeni. Viumbe haohao hutoa hewa chafu inayoitwa kaboni-dioksidi. Hata hivyo, viumbe hai hawawezi kumaliza hewa yote ya oksijeni, na anga hewa haitawahi kulemewa na hewa “chafu” ya kaboni-dioksidi. Kwa nini? Kwa sababu Yehova aliumba pia viumbe hai wengine—kuanzia miti mikubwa mpaka mwani mdogo sana—ambao huvuta hewa ya kaboni-dioksidi na kutoa hewa ya oksijeni. Kwa njia halisi kabisa, mzunguko wa oksijeni unathibitisha maneno ya andiko la Matendo 17:24, 25 linalosema: “Mungu . . . huwapa watu wote uhai na pumzi.”

6. Mzunguko wa maji ni nini, nao unathibitisha nini? (Tazama pia sanduku “Zawadi ya Yehova ya Mzunguko wa Maji.”)

6 Kuna maji duniani kwa sababu Mungu aliiweka sayari yetu umbali unaofaa kabisa kutoka kwenye jua. Ikiwa dunia ingesogea kidogo tu karibu na jua, maji yote yangekauka, na dunia ingekuwa kame na yenye joto jingi na bila uhai wowote. Ikiwa dunia ingesogea mbali kidogo tu na jua, maji yote yangeganda, na dunia ingebadilika na kuwa mwamba mkubwa wa barafu. Kwa kuwa Yehova aliiweka dunia mahali panapofaa kabisa, mzunguko wa maji unaweza kuendelea kutegemeza uhai. Jua hufanya maji ya baharini na ya nchi kavu yawe mvuke, kisha mvuke huo hufanyiza mawingu. Kila mwaka, kiasi cha maji ambacho jua hugeuza na kuwa mvuke kinazidi kiasi cha maji kilichomo katika maziwa yote duniani. Kiasi hicho cha maji huendelea kukaa kwenye anga hewa kwa siku kumi hivi kabla ya kunyesha kama mvua au theluji. Hatimaye maji hayo hurudi baharini na kwenye maziwa au sehemu nyingine, na mzunguko huo unajirudia tena. Mzunguko huo wenye utaratibu na usiokoma unathibitisha kwamba Yehova ni mwenye hekima na mwenye nguvu.—Ayu. 36:27, 28; Mhu. 1:7.

Zawadi ya Yehova ya Mzunguko wa Maji

Mkusanyo wa picha: Mzunguko wa maji. 1. Joto kutoka kwenye jua linasababisha mvuke upande kutoka baharini na kufanyiza wingu. 2. Mvua inanyesha duniani kutoka katika wingu. 3. Maji yakirudi baharini.
  • Mkulima akitazama angani huku mvua ikinyesha.

    MATUNDA, MBOGA, NA MAUA

    Mvua hufanya mimea ikue, na kutupatia chakula. Pia, mimea mingi hutokeza maua yanayotufurahisha

  • Mpiga-picha akipiga picha maporomoko ya maji na milima.

    MANDHARI MARIDADI NA YENYE KUFURAHISHA

    Mito, maziwa, na maporomoko ya maji hurembesha dunia na kutuletea furaha

  • Mwanamume akiyakausha maji ya baharini ili kukusanya chumvi.

    FAIDA NYINGINE

    Mzunguko wa maji una faida nyingine. Kwa mfano, chumvi hutokezwa wakati maji yenye chumvi ya bahari yanapovukizwa angani na kuwa mvuke

  • Mwanamke akinywa maji kutoka kwenye glasi.

    MATUMIZI YA KILA SIKU

    Tunakunywa maji na kuyatumia kutengeneza vinywaji vingine, kama vile maji ya ndimu, kahawa, na chai. Pia tunatumia maji kupikia, kufanya usafi, na kuogea

7. Taja baadhi ya njia tunazoweza kuonyesha kwamba tunathamini zawadi inayotajwa kwenye Zaburi 115:16.

7 Ni nini kinachoweza kutusaidia tuithamini zaidi sayari yetu yenye kustaajabisha na vitu vyote vyema vilivyomo? (Soma Zaburi 115:16.) Njia moja ni kwa kutafakari kuhusu vitu ambavyo Yehova ameumba. Jambo hilo litatuchochea tumshukuru Yehova kila siku kwa vitu vyema anavyotupatia. Na tunaonyesha kwamba tunaithamini dunia kwa kudumisha mazingira tunayoishi yakiwa safi kadiri iwezekanavyo.

UBONGO WETU WA PEKEE

8. Kwa nini tunaweza kusema kwamba ubongo wetu umeumbwa kwa njia yenye kustaajabisha sana?

8 Ubongo wetu umeumbwa kwa njia yenye kustaajabisha sana. Ulipokuwa katika tumbo la mama yako, ubongo wako uliendelea kukua kwa kufuata utaratibu fulani uliopangwa, na maelfu ya chembe mpya za ubongo zilifanyizwa kila dakika! Watafiti wanakadiria kwamba ubongo wa mtu mzima una karibu chembe za pekee bilioni 100 zinazoitwa nuroni. Chembe hizo zimeunganishwa kwa ustadi sana na kutokeza ubongo wetu wenye uzito wa kilogramu 1.5. Fikiria mambo haya machache kuhusu uwezo wenye kustaajabisha wa ubongo.

9. Ni nini kinachokuthibitishia kwamba uwezo wetu wa kuzungumza ni zawadi kutoka kwa Mungu?

9 Uwezo wetu wa kuzungumza ni muujiza. Fikiria kidogo kuhusu kile ambacho hufanyika tunapozungumza. Kila unapotamka neno moja, ubongo wako huwasilisha habari kwenye misuli 100 hivi iliyo kwenye ulimi, koo, midomo, taya, na kifua ili iweze kusonga vizuri. Misuli hiyo yote inapaswa kusonga kwa usahihi kabisa ili maneno yaweze kueleweka. Kuhusu uwezo wa kuzungumza lugha mbalimbali, utafiti mmoja uliochapishwa mwaka wa 2019 ulionyesha kwamba watoto waliozaliwa hivi karibuni wanaweza kutambua na kuitikia kulingana na maneno wanayosikia. Utafiti huo unaunga mkono mambo ambayo watafiti wengi wanaamini, kwamba tunazaliwa tukiwa na uwezo wa kutambua na kujifunza lugha. Kwa hakika, uwezo wetu wa kuzungumza ni zawadi kutoka kwa Mungu.—Kut. 4:11.

10. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini zawadi tuliyopewa na Mungu ya kuzungumza?

10 Njia moja tunayoweza kuonyesha kwamba tunathamini zawadi yetu ya kuzungumza ni kwa kuwafafanulia wale wanaoamini mageuzi sababu inayotufanya tuamini kwamba Mungu aliumba vitu vyote. (Zab. 9:1; 1 Pet. 3:15) Wale wanaounga mkono fundisho hilo wangependa tuamini kwamba dunia na uhai wote uliomo ulijitokeza wenyewe tu. Kwa kutumia Biblia na baadhi ya hoja tulizozungumzia katika makala hii, tunaweza kumtetea Baba yetu wa mbinguni na kuwafafanulia wale walio tayari kusikiliza sababu inayotufanya tusadiki kwamba Yehova ndiye Muumba wa mbingu na dunia.—Zab. 102:25; Isa. 40:25, 26.

11. Taja sababu moja inayoonyesha kwamba ubongo wetu unastaajabisha.

11 Uwezo wetu wa kukumbuka unastaajabisha. Miaka mingi iliyopita, mwandishi mmoja alikadiria kwamba ubongo wa mwanadamu una uwezo wa kukumbuka habari zinazoweza kujaa kwenye vitabu milioni 20. Hata hivyo, sasa inasemekana kwamba uwezo wetu wa kukumbuka ni mkubwa zaidi ya huo. Wanadamu wana uwezo gani wa pekee?

12. Uwezo wetu wa kujifunza kuhusu maadili unatutofautishaje na wanyama?

12 Kati ya viumbe wote walio duniani, ni wanadamu peke yao walio na uwezo wa kujifunza kuhusu maadili kwa kukumbuka na kuchanganua matukio yaliyopita. Kwa sababu hiyo, tunaweza kujifunza viwango bora zaidi na kubadili maisha yetu na pia njia yetu ya kufikiri. (1 Kor. 6:9-11; Kol. 3:9, 10) Isitoshe, tunaweza kuzoeza dhamiri zetu kutambua tofauti kati ya yaliyo sawa na yasiyo sawa. (Ebr. 5:14) Tunaweza kujifunza kuonyesha upendo, huruma, na rehema. Na tunaweza kujifunza kumwiga Yehova katika kuonyesha haki.

13. Kulingana na andiko la Zaburi 77:11, 12, tunapaswa kuitumiaje zawadi yetu ya kukumbuka?

13 Njia moja tunayoweza kuthibitisha kwamba tunathamini zawadi ya kumbukumbu ni kwa kuchagua kukumbuka pindi zote ambazo Yehova alitusaidia na kutufariji wakati uliopita. Jambo hilo litaimarisha uhakika wetu kwamba atatusaidia pia wakati ujao. (Soma Zaburi 77:11, 12; 78:4, 7) Njia nyingine ni kwa kukumbuka mambo mazuri ambayo wengine wanatufanyia na kuthamini mambo wanayotufanyia. Watafiti wamegundua kwamba ni rahisi zaidi kwa watu wanaoonyesha uthamini kuwa na furaha. Pia, ni vizuri tumwige Yehova inapohusu mambo anayochagua kusahau. Kwa mfano, Yehova ana kumbukumbu kamilifu, lakini yeye huchagua kusamehe na kusahau makosa tunayofanya, ikiwa tunatubu. (Zab. 25:7; 130:3, 4) Yehova anataka sisi pia tufanye vivyo hivyo wengine wanapotuomba msamaha kwa sababu ya makosa yao yaliyotuumiza.—Mt. 6:14; Luka 17:3, 4.

Mkusanyo wa picha: 1. Dada akitumia kadi zenye maneno na kitabu ili kujifunza Kihindi. 2. Dada huyo anamhubiria mwanamke wa Kihindi sokoni, akitumia broshua ‘Habari Njema.’.

Tunaonyesha kwamba tunaithamini zawadi ya ubongo wetu kwa kuutumia kumheshimu Yehova (Tazama fungu la 14)b

14. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaithamini zawadi yenye kustaajabisha ya ubongo wetu?

14 Tunaweza kuonyesha kwamba tunaithamini zawadi yenye kustaajabisha ya ubongo wetu kwa kuutumia kumheshimu Yule aliyetupatia. Wengine wamechagua kutumia ubongo wao kuendeleza tamaa zao wenyewe za kichoyo, yaani, kujiwekea viwango vyao vya lililo jema na lililo kosa. Lakini kwa kuwa Yehova ndiye aliyetuumba, ni wazi kwamba viwango vyake ndivyo bora zaidi kuliko viwango vyovyote tunavyoweza kujiwekea. (Rom. 12:1, 2) Tunapoishi kulingana na viwango vyake, maisha yetu yanakuwa na amani. (Isa. 48:17, 18) Na tunapata kusudi halisi la maisha, yaani, kumletea heshima Muumba na Baba yetu na kumfanya atuonee fahari.—Met. 27:11.

BIBLIA​—ZAWADI YA PEKEE

15. Zawadi ya Biblia inaonyeshaje kwamba Yehova anawapenda wanadamu?

15 Biblia ni zawadi yenye upendo kutoka kwa Mungu. Baba yetu wa mbinguni alitumia roho yake takatifu kuwaongoza wanadamu waiandike kwa sababu anatupenda sana. Kwa kutumia Biblia, Yehova anatujibu maswali muhimu sana tunayoweza kujiuliza, kama vile: Tulitoka wapi? Kusudi la maisha ni nini? Maisha yatakuwaje wakati ujao? Yehova anataka watoto wake wote wapate majibu ya maswali hayo, hivyo aliwachochea watu mbalimbali waitafsiri Biblia katika lugha nyingi. Leo, Biblia ikiwa nzima au kwa sehemu inapatikana katika lugha zaidi ya 3,000! Biblia ndicho kitabu kilichotafsiriwa na kusambazwa zaidi katika historia. Hata iwe watu wanaishi wapi au wanazungumza lugha gani, wengi wana fursa ya kusoma ujumbe wa Biblia katika lugha yao ya mama.—Tazama sanduku “Kuifanya Biblia Ipatikane Katika Lugha za Afrika.”

Kuifanya Biblia Ipatikane Katika Lugha za Afrika

Kufikia mwaka wa 1800, nakala zilizochapishwa za Biblia ikiwa nzima au kwa sehemu zilipatikana katika lugha 70 hivi, lakini ni lugha chache kati ya hizo zilizozungumzwa Afrika. Wakati huo, lugha za Kibantu za Afrika hazikuwa zimeandikwa. Mambo yalibadilika wakati watu kama William Boyce kutoka Uingereza walipofika Afrika na kuishi pamoja na watu waliozungumza lugha ambazo hazikuandikwa. Boyce alisaidia kuanzisha mfumo wa kuandika lugha ya Xhosa, na yeye pamoja na watu wengine walitafsiri Injili ya Luka katika lugha hiyo ya Xhosa. Injili hiyo iliyochapishwa mwaka wa 1833 ina jina la Mungu katika mistari yote iliyo na jina la Mungu kwenye Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya sasa. Pia, Boyce alivumbua sheria tata za kisarufi zinazotumiwa na lugha ya Xhosa na kundi lote la lugha za Kibantu. Jambo hilo liliwafungulia njia watafsiri, nao wakaanza kutafsiri Biblia katika lugha nyingine nyingi za Afrika. Leo, Biblia ikiwa nzima au kwa sehemu inapatikana katika lugha zaidi ya 1,000 za Afrika. Ni wazi kwamba Yehova anataka watu kutoka kila taifa wapate zawadi hiyo!—Mdo. 10:35.

Akina dada na ndugu mmoja wakiwa wameshika ‘Tafsiri ya Ulimwengu Mpya’ iliyotoka tu kutolewa katika lugha ya Xhosa.

Katika mwaka wa 2019, Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa katika lugha ya Xhosa ambayo ni mojawapo ya lugha zaidi ya 180 ambazo tafsiri hiyo inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu

16. Kama andiko la Mathayo 28:19, 20 linavyoonyesha, tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaithamini Biblia?

16 Tunaweza kuonyesha kwamba tunaithamini Biblia kwa kuisoma kila siku, kwa kutafakari kuhusu mafundisho yake, na kwa kufanya yote tuwezayo ili kutumia mambo tunayojifunza. Pia, tunaonyesha shukrani zetu kwa Mungu kwa kujitahidi kabisa kuwapa watu wengi kadiri iwezekanavyo ujumbe wa Biblia.—Zab. 1:1-3; Mt. 24:14; soma Mathayo 28:19, 20.

17. Tumezungumzia zawadi za aina gani katika makala hii, na tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

17 Kufikia sasa tumezungumzia zawadi zinazotoka kwa Mungu kama vile dunia, makao yetu; ubongo wetu ulioumbwa kwa njia yenye kustaajabisha; na Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu. Lakini kuna zawadi nyingine ambazo Yehova ametupatia ambazo hatuwezi kuziona kwa macho yetu. Katika makala inayofuata tutazungumzia hazina hizo tusizoweza kuona kwa macho yetu.

TUNAWEZA KUONYESHAJE KWAMBA TUNATHAMINI . . .

  • dunia?

  • ubongo wetu?

  • Biblia?

WIMBO 12 Mungu Mkuu, Yehova

a Makala hii itaimarisha uthamini wetu kwa Yehova na kwa zawadi tatu ambazo ametupatia. Pia, itatusaidia kujadiliana na wale wanaotilia shaka kuwepo kwa Mungu.

b MAELEZO YA PICHA : Dada anajifunza lugha ya kigeni ili awafundishe wahamiaji kweli za Neno la Mungu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki