Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wp21 Na. 3 kur. 9-11
  • Je, Kuwa Mtu Mwema Kutakuhakikishia Maisha Bora ya Wakati Ujao?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Kuwa Mtu Mwema Kutakuhakikishia Maisha Bora ya Wakati Ujao?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NJIA INAYOFUATWA NA WATU WENGI
  • MATOKEO NI NINI?
  • Kila Mtu Anatamani Kuwa na Maisha Bora ya Wakati Ujao
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
  • Jinsi ya Kuwa na Maisha Bora ya Wakati Ujao
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
  • Utangulizi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
  • “Wapole Wataimiliki Dunia”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2018
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
wp21 Na. 3 kur. 9-11
Mwanamke kwenye basi akimpisha bibi aketi kwenye kiti.

Je, Kuwa Mtu Mwema Kutakuhakikishia Maisha Bora ya Wakati Ujao?

Kwa karne nyingi, watu wengi wamehisi kwamba wakiwa watu wema na wenye maadili mazuri watakuwa na maisha bora ya wakati ujao. Kwa mfano, watu wa Mashariki waliheshimu sana maneno haya ambayo mwanafalsafa na mwalimu aliyeitwa Confucius (551-479 K.W.K.) alisema: “Jambo ambalo hutaki wengine wakutendee, usiwatendee.”a

NJIA INAYOFUATWA NA WATU WENGI

Bado watu wengi waamini kwamba kuwa na tabia njema ndiyo siri ya kupata mafanikio ya wakati ujao. Wanajitahidi kuwa na heshima, tabia nzuri, kutambua wajibu wao katika jamii, na kudumisha dhamiri njema. Linh, mwanamke anayeishi Vietnam anasema: “Sikuzote niliamini kwamba ikiwa ningekuwa msema kweli na mnyoofu, ningepata baraka.”

Mwanamke huyohuyo akiwapatia chakula watu maskini na wasio na makazi.

Baadhi ya watu wanajitahidi kufanya mema kwa sababu ya imani zao za kidini. Mwanamume anayeitwa Hsu-Yun, anayeishi Taiwan, anasema, “Nilifundishwa kwamba matendo ya mtu anapokuwa hai yanaamua ikiwa atapata raha milele au atateseka motoni milele atakapokufa.”

MATOKEO NI NINI?

Mwishowe mwanamke huyo, amehuzunika na kuchoka, akiwa amembeba mtoto wake.

Ni kweli kwamba tunapata faida nyingi kwa kuwatendea wengine mema. Hata hivyo, watu wengi ambao kwa unyoofu wanajitahidi kuwatendea wengine mema, wanatambua kwamba mara nyingi hawapati matokeo waliyotarajia. Shiu Ping, mwanamke anayeishi Hong Kong anasema: “Nimejionea mwenyewe kwamba si wakati wote wale wanaowatendea wengine mema wanapata maisha bora kama walivyotarajia. Nilijitahidi sana kuitunza familia yangu na kufanya mambo mazuri. Lakini, ndoa yangu ilivunjika na mume wangu alitutelekeza mimi na mtoto wangu.”

Watu wengi wamejionea kwamba, si kila mara dini zinawasaidia watu kuwa wema. Etsuko, mwanamke kutoka Japani anasema hivi; “Nilijiunga na shirika fulani la dini, na kisha nikawa msimamizi wa shughuli za vijana. Nilishangazwa kuona washiriki wa dini yangu wakiwa na maadili mabaya, wakigombania vyeo, na kutumia vibaya pesa za kanisa.”

“Nilijitahidi sana kuitunza familia yangu na kufanya mambo mazuri. Lakini ndoa yangu ilivunjika na mume wangu alitutelekeza mimi na mtoto wangu.”​—SHIU PING, HONG KONG

Baadhi ya watu wamevunjika moyo kwa sababu wamepatwa na mambo mabaya licha ya kushika dini na kutenda mema. Hivyo ndivyo Van, mwanamke kutoka Vietnam, alivyohisi. Anasema hivi; “Kila siku nilinunua matunda, maua, na chakula na kuvitoa sadaka kwa mababu waliokufa nikitumaini kwamba nitapata baraka. Licha ya kufanya mema na kufuata desturi za kidini kwa miaka mingi, mume wangu alipatwa na ugonjwa mbaya sana. Kisha binti yangu aliyekuwa akisoma nje ya nchi akafa akiwa na umri wa miaka 20 tu.”

KWA NINI KUWA MTU MWEMA TU HAKUTOSHI

Ni muhimu kuwa mtu mwema lakini hilo halikuhakikishii kwamba utakuwa na maisha bora ya wakati ujao. Kwa nini? Fikiria mambo ambayo Maandiko Matakatifu yanasema.

SI KILA MTU ANAYEFANYA MEMA

“Mtenda dhambi mmoja tu anaweza kuharibu mambo mengi mazuri.”​—MHUBIRI 9:18.

Hata ikiwa unajitahidi kuwa mtu mwema, watu wenye ubinafsi wanaweza kukudhuru. Kwa mfano, wakati wa janga hili la corona, unaweza kufuata ushauri wa wenye mamlaka kwa kudumisha umbali unaofaa na wengine. Lakini vipi ikiwa wengine watakataa kutii maagizo hayo? Matendo yao yanaweza kuhatarisha afya ya wale wanaojitahidi kufuata maagizo hayo.

INAWEZEKANA WATU WASIWE NA MAONI SAHIHI KUHUSU JAMBO JEMA NA BAYA

“Kuna njia inayoonekana kuwa sawa machoni pa mtu, lakini mwishowe inaongoza kwenye kifo.”​—METHALI 14:12.

Historia imejaa mifano ya watu ambao walifuata njia fulani wakiamini kabisa ilikuwa sahihi, lakini baadaye waligundua kwamba haikuwa sahihi. Hata ikiwa mtu alifanya uamuzi fulani kwa nia njema, anaweza kupata matokeo mabaya kwa sababu ya maamuzi mabaya aliyofanya.

MAISHA HAYATABIRIKI

“Hamjui jinsi maisha yenu yatakavyokuwa kesho.”​—YAKOBO 4:14.

Hata mtu mwema anaweza kufa ghafla tu bila kutarajia. Kwa mfano, wakati wa janga hili la corona (COVID-19), watu wengi waliojitolea kuwasaidia wengine walipoteza uhai wao. Au, fikiria mfano wa Liting, mwanamke kutoka China ambaye baba yake alikufa katika aksidenti ya gari. Anasema hivi: “Sikuelewa kwa nini mtu mwema hivyo afe. Baba yangu alikuwa mnyenyekevu, mnyoofu sana, na alifanya kazi kwa bidii. Ni yeye peke yake aliyekufa kwenye aksidenti hiyo.”

Ikiwa kuwa mtu mwema hakutuhakikishii maisha bora ya wakati ujao, ni nini kinachoweza kutupatia uhakika huo? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji mwongozo wenye kutegemeka kabisa—chanzo cha habari kinachoweza kutupa majibu ya maswali yetu na kutuelekeza kwenye maisha bora ya wakati ujao. Tunaweza kupata wapi mwongozo huo?

a Kwa maelezo zaidi kuhusu mambo ambayo Confucius alifundisha, tazama sura ya 7, fungu la 31-35, la kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova na ambacho kinapatikana mtandaoni kwenye www.jw.org/sw.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki