Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Agosti kur. 26-30
  • Ingawa Nilikuwa Mwenye Haya, Nilikuja Kuwa Mmishonari

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ingawa Nilikuwa Mwenye Haya, Nilikuja Kuwa Mmishonari
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NAANZA UTUMISHI WA WAKATI WOTE
  • NAANZA KUJIWEKEA LENGO LA KUWA MMISHONARI
  • KUTUMIKIA KATIKA NCHI YENYE VITA
  • CHANGAMOTO MPYA
  • KUKABILIANA NA MAJARIBU YA KIBINAFSI
  • NINATHAMINI UTEGEMEZO WA YEHOVA
  • Kitu Chenye Thamani Kuliko Kazi
    Amkeni!—2011
  • Kampeni ya Pekee Nchini Bulgaria Yafanikiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Nimeandaliwa Tumaini Linalonitegemeza
    Amkeni!—2000
  • Je! Wewe Huona Sura ya Nje-Nje Tu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Agosti kur. 26-30
Marianne Wertholz.

SIMULIZI LA MAISHA

Ingawa Nilikuwa Mwenye Haya, Nilikuja Kuwa Mmishonari

LIMESIMULIWA NA MARIANNE WERTHOLZ

NILIPOKUWA mtoto, nilikuwa mwenye haya na niliwaogopa watu. Lakini baada ya muda, Yehova alinisaidia kuwa mmishonari aliyependezwa na watu. Jinsi gani? Mwanzoni, kupitia msaada wa baba yangu. Kisha, kupitia mfano bora wa dada mmoja tineja. Na mwishowe, kupitia maneno yenye fadhili na subira ya mume wangu. Acheni niwaeleze zaidi kuhusu maisha yangu.

Nilizaliwa mwaka wa 1951 katika jiji la Vienna, Austria, katika familia ya Kikatoliki. Nilikuwa mwenye haya, lakini niliamini kwamba kuna Mungu na nilisali mara nyingi. Nilipokuwa na umri wa miaka tisa, baba yangu alianza kujifunza na Mashahidi wa Yehova; kisha baadaye kidogo mama yangu pia alianza kujifunza.

Pamoja na dada yangu, Elisabeth (kushoto)

Baada ya muda mfupi, tukaanza kushirikiana na kutaniko la Döbling jijini Vienna. Tulifanya mambo mengi pamoja tukiwa familia. Tulisoma na kujifunza Biblia, tulihudhuria mikutano ya kutaniko, na tulijitolea kufanya kazi katika makusanyiko. Tangu nilipokuwa mtoto mdogo, baba yangu alinisaidia kusitawisha upendo wenye kina kumwelekea Yehova. Kwa kweli, baba yangu alikuwa akisali sikuzote kwamba mimi na dada yangu tuwe mapainia. Lakini kwa wakati huo, hilo halikuwa lengo langu.

NAANZA UTUMISHI WA WAKATI WOTE

Nilibatizwa mwaka wa 1965, nikiwa na umri wa miaka 14. Hata hivyo, ilikuwa vigumu kwangu kuzungumza na watu nisiowajua katika huduma. Pia, nilipambana na hisia za kujiona sifai na nilitamani sana nikubaliwe na vijana wengine. Hivyo, muda mfupi tu baada ya kubatizwa, nilianza kushirikiana na watu ambao hawakuwa wakimtumikia Yehova. Ingawa nilifurahia ushirika wao, dhamiri yangu ilinisumbua kwa kuwa nilitumia muda mwingi na watu ambao hawakuwa Mashahidi. Lakini haikuwa rahisi kwangu kuacha kushirikiana nao. Ni nini kilichonisaidia?

Marianne na Dorothée.

Nilijifunza mengi kutoka kwa Dorothée (kushoto)

Katika kipindi hicho, msichana mwenye umri wa miaka 16 alihamia kutanikoni kwetu. Bidii yake kwa ajili ya huduma ya nyumba kwa nyumba ilinivutia sana. Nilikuwa na umri mkubwa kidogo kuliko yeye, lakini sikuhubiri kwa ukawaida. Nilijiambia hivi: ‘Wazazi wangu ni Mashahidi, lakini katika familia yao, Dorothée tu ndiye aliyekuwa Shahidi. Anaishi na mama yake ambaye ni mgonjwa, na bado sikuzote anashiriki katika huduma!’ Mfano wake ulinichochea kufanya mengi zaidi kwa ajili ya Yehova. Muda mfupi baadaye, Dorothée akawa mwandamani wangu katika upainia. Kwanza, tulikuwa mapainia wasaidizi, ambao wakati huo waliitwa mapainia wa likizo, na baadaye, tulitumikia pamoja tukiwa mapainia wa kawaida. Dorothée aliniambukiza shauku yake. Alinisaidia kuanzisha funzo langu la kwanza la Biblia. Baada ya muda, ilikuwa rahisi zaidi kwangu kuzungumza na watu katika huduma ya nyumba kwa nyumba, barabarani, na sehemu nyingine.

Katika mwaka wangu wa kwanza wa upainia wa kawaida, ndugu kutoka Austria aliyeitwa Heinz alihamia kutanikoni kwetu. Alijifunza kweli nchini Kanada alipokuwa akimtembelea ndugu yake, ambaye alikuwa Shahidi. Heinz alikuwa amepewa mgawo wa upainia wa pekee katika kutaniko letu jijini Vienna. Nilimpenda tangu siku ya kwanza nilipomwona. Lakini alitaka kuwa mmishonari, nami sikuwa na lengo hilo kabisa. Hivyo, mwanzoni nilimficha hisia zangu. Hata hivyo, baadaye, mimi na Heinz tulianzisha urafiki wa kimapenzi, tukafunga ndoa, na kwa pamoja tukaanza kufanya upainia nchini Austria.

NAANZA KUJIWEKEA LENGO LA KUWA MMISHONARI

Mara nyingi Heinz aliniambia kuhusu tamaa yake ya kuwa mmishonari. Ingawa hakunishinikiza, alinichochea kwa kuniuliza maswali kama vile, “Kwa kuwa hatuna watoto, je, tunaweza kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova?” Kwa sababu nilikuwa mwenye haya, niliogopa kuwa mmishonari. Ni kweli nilifanya upainia, lakini wazo la kuwa mmishonari lilinilemea. Hata hivyo, kwa subira Heinz aliendelea kuzungumzia kuhusu lengo hilo. Pia, alinitia moyo nikazie fikira zaidi kuwajali watu kuliko kuwa na wasiwasi kuhusu hali yangu. Ushauri wake ulinisaidia sana.

Heinz akiongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi katika kutaniko dogo la Kiyugoslavia jijini Salzburg, Austria, mwaka wa 1974

Hatua kwa hatua, nilikuza tamaa ya kuwa mmishonari, kwa hiyo tulijaza ombi la kuhudhuria Shule ya Gileadi. Hata hivyo, mtumishi wa ofisi ya tawi alipendekeza kwamba kwanza niboreshe Kiingereza changu. Baada ya kujitahidi kuboresha Kiingereza changu kwa miaka mitatu, tulishangaa tulipopewa mgawo wa kutumikia katika kutaniko la Kiyugoslavia jijini Salzburg, Austria. Tulitumikia huko kwa miaka saba, kutia ndani mwaka mmoja katika kazi ya kuzungukia makutaniko. Lugha ya Kiserbia-Kikroatia ilikuwa ngumu, hata hivyo tulikuwa na mafunzo mengi ya Biblia.

Kisha katika mwaka wa 1979, tuliombwa kwenda “likizo” nchini Bulgaria. Kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku katika nchi hiyo. Hivyo, hatukuhubiri tulipokuwa kwenye “likizo” hiyo. Lakini tuliingiza kwa siri nchini humo nakala ndogo za machapisho kwa ajili ya dada watano walioishi katika mji mkuu, Sofia. Niliogopa sana, lakini Yehova alinisaidia kutimiza mgawo huo wenye kusisimua. Kuona ujasiri wa akina dada hao na shangwe waliyokuwa nayo licha ya hatari ya kufungwa gerezani, kulinipa ujasiri wa kufanya yote niwezayo ili kutimiza jambo lolote ambalo tengenezo la Yehova lingeniomba nifanye.

Wakati huo, tulijaza tena ombi la kuhudhuria Shule ya Gileadi, na wakati huu tulialikwa. Tulifikiri kwamba tungehudhuria shule hiyo nchini Marekani kwa lugha ya Kiingereza. Lakini Novemba 1981, tengenezo letu lilianza kuwa na madarasa ya Shule ya Gileadi katika ofisi ya tawi ya Wiesbaden, Ujerumani. Hivyo, tuliweza kuhudhuria shule hiyo katika Kijerumani, ambayo ilikuwa rahisi zaidi kwangu kuelewa. Tungepewa mgawo wapi?

KUTUMIKIA KATIKA NCHI YENYE VITA

Tulipewa mgawo wa kutumikia nchini Kenya! Hata hivyo, ofisi ya tawi ya Kenya ilituomba ikiwa tuko tayari kutumikia katika nchi ya jirani ya Uganda. Zaidi ya miaka kumi mapema, serikali ya Uganda ilikuwa imepinduliwa katika mapinduzi ya kijeshi yaliyoongozwa na Jenerali Idi Amin. Katika miaka iliyofuata, utawala wake wa kidikteta ulisababisha vifo vya maelfu ya watu na mateso kwa mamilioni ya watu. Kisha, mwaka wa 1979, serikali ya Uganda ilipinduliwa kwa mara nyingine tena. Kwa kweli, kwa kiasi fulani niliogopa kuhamia katika nchi yenye vita. Lakini Shule ya Gileadi ilitusaidia kumtumaini Yehova. Hivyo, tukakubali mgawo huo.

Hali ya usalama nchini Uganda haikuwa nzuri. Heinz alifafanua hivi hali hiyo katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2010: “Huduma nyingi, . . . kama vile maji na mawasiliano zilikuwa zimezorota. . . . Milio ya risasi na unyang’anyi yalikuwa mambo ya kawaida, hasa wakati wa usiku. . . . Kila mtu alikaa nyumbani akitumaini—na mara nyingi kusali—kwamba usiku utapita salama.” Licha ya changamoto hizo, ndugu wenyeji waliendelea vizuri sana kiroho!

Tukitayarisha mlo pamoja na familia ya Waiswa

Mwaka wa 1982, mimi na Heinz tuliwasili Kampala, mji mkuu wa Uganda. Katika miezi mitano ya kwanza, tulikaa nyumbani kwa Sam na Christina Waiswa pamoja na watoto wao watano na watu wao wa ukoo wanne. Mara nyingi, familia ya Ndugu na Dada Waiswa ilikula mlo mmoja tu kwa siku, hivyo ukarimu wao ulikuwa wa pekee sana. Tulipokuwa tukiishi pamoja na familia ya Waiswa, mimi na Heinz tulijifunza mambo mengi ambayo yalitusaidia katika utumishi wa umishonari. Kwa mfano, tulijifunza jinsi ya kutunza maji kwa kutumia lita chache tu tulipooga, kisha kutumia maji hayo chooni. Katika mwaka wa 1983, mimi na Heinz tulipata nyumba yetu wenyewe katika eneo ambalo lilikuwa na usalama wa kadiri katika jiji la Kampala.

Mimi na Heinz tulifurahia sana huduma. Ninakumbuka kwamba katika mwezi mmoja tuliwaachia watu magazeti zaidi ya 4,000! Lakini jambo bora zaidi lilikuwa kuona jinsi watu walivyoitikia kweli. Walimheshimu Mungu na walitaka kuzungumzia Biblia. Kwa kawaida, kila mmoja wetu aliongoza mafunzo ya Biblia 10 hadi 15. Na tulijifunza mambo mengi kutoka kwa wanafunzi wetu. Kwa mfano, tulithamini mtazamo wao mzuri, kwa kuwa ingawa walihitaji kutembea kila juma ili kuhudhuria mikutano, hawakulalamika na sikuzote walitabasamu.

Mwaka wa 1985 na 1986, kulikuwa na vita vingine viwili nchini Uganda. Mara nyingi tuliwaona watoto waliobeba silaha wakitumiwa kama wanajeshi kulinda vizuizi barabarani. Wakati huo, tulisali tupate utambuzi na moyo mtulivu tulipokuwa tukitafuta watu wanaopendezwa katika huduma. Na Yehova alijibu sala yetu. Mara nyingi woga wetu uliisha mara tu tulipokutana na mtu aliyeitikia vizuri ujumbe wa Ufalme.

Mimi na Heinz pamoja na Tatjana (katikati)

Tulifurahia pia kuwahubiria watu kutoka nchi nyingine. Kwa mfano, tulikutana na kujifunza na Murat na Dilbar Ibatullin, wenzi wa ndoa kutoka Tatarstan (Urusi ya Kati). Murat alikuwa daktari. Wenzi hao walikubali kweli na bado wanaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Baadaye, nilikuwa na pendeleo la kukutana na Tatjana Vileyska, mwanamke kutoka Ukrainia aliyekuwa anafikiria kujiua. Baada ya Tatjana kubatizwa, alirudi Ukrainia na baadaye alitumikia akiwa mtafsiri wa machapisho yetu.a

CHANGAMOTO MPYA

Mwaka wa 1991, mimi na Heinz tulipokuwa likizo nchini Austria, ofisi ya tawi ilitujulisha kuhusu mgawo wetu mpya: Bulgaria. Baada ya kuanguka kwa ukomunisti Ulaya Mashariki, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilitambuliwa kisheria nchini Bulgaria. Kama nilivyotaja awali, mimi na Heinz tuliingiza machapisho kisiri kulipokuwa na marufuku nchini humo. Lakini sasa tulikuwa tunatumwa kwenda kuhubiri huko.

Tuliagizwa tusirudi tena Uganda. Hivyo, hatukurudi katika nyumba yetu ya umishonari ili kuchukua vitu vyetu au kuwaaga rafiki zetu, tulienda katika Betheli ya Ujerumani, tukapewa gari, na kusafiri kwenda Bulgaria. Tulipewa mgawo wa kushirikiana na kikundi cha wahubiri 20 katika jiji la Sofia.

Tulikabili changamoto kadhaa mpya nchini Bulgaria. Kwanza, hatukuijua lugha. Kwa kuongezea, machapisho pekee yaliyopatikana katika Kibulgaria yalikuwa kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Na haikuwa rahisi kwetu kuanzisha mafunzo ya Biblia. Licha ya changamoto hizo, kikundi chetu kidogo lakini chenye bidii cha Mashahidi kilikuwa kinafanya maendeleo. Kanisa la Othodoksi liliona jambo hilo, na hapo ndipo matatizo yalipoanza.

Mwaka wa 1994, usajili wa Mashahidi ulifutwa na tukaanza kutendewa kama dhehebu lililopigwa marufuku. Baadhi ya akina ndugu walikamatwa. Vyombo vya habari vilisambaza uwongo mbaya sana kutuhusu, vikidai kwamba Mashahidi wa Yehova waliua watoto na kuwashawishi Mashahidi wengine kujiua. Haikuwa rahisi kwa mimi na Heinz kuhubiri. Mara nyingi tulikutana na watu wakali waliotukemea, waliotuitia polisi, na hata kuturushia vitu. Ilikuwa vigumu sana kuingiza machapisho nchini, na kukodisha mahali kwa ajili ya mikutano. Polisi hata walikatisha kusanyiko moja. Mimi na Heinz hatukuwa tumezoea chuki ya aina hiyo. Hali hiyo ilikuwa tofauti kabisa na watu wenye urafiki na waliokuwa tayari kujifunza Biblia nchini Uganda! Ni nini kilichotusaidia kukabiliana na badiliko hilo?

Tulipata shangwe kwa kushirikiana na ndugu na dada zetu. Walifurahi kwamba walipata kweli na walithamini msaada tuliowapatia. Wote walishirikiana kwa ukaribu na kusaidiana. Tulijifunza kwamba tunaweza kuwa na furaha katika mgawo wowote ikiwa tutaendelea kuwapenda watu.

Marianne na Heinz Wertholz.

Tukiwa katika ofisi ya tawi ya Bulgaria, mwaka wa 2007

Hata hivyo, baada ya muda mambo yakawa mazuri zaidi. Mashahidi wa Yehova walisajiliwa tena mwaka wa 1998, na baada ya muda mfupi machapisho mengi yalipatikana katika Kibulgaria. Kisha mwaka wa 2004, ofisi mpya ya tawi iliwekwa wakfu. Leo, kuna makutaniko 57 nchini Bulgaria, na wahubiri 2,953. Katika mwaka wa utumishi uliopita, jumla ya watu 6,475 walihudhuria Ukumbusho. Ingawa wakati mmoja kulikuwa na dada watano tu katika jiji la Sofia, sasa kuna makutaniko tisa! Kwa kweli tumejionea ‘mdogo akiwa elfu.’—Isa. 60:22.

KUKABILIANA NA MAJARIBU YA KIBINAFSI

Nimekuwa na matatizo mengi ya kiafya maishani. Katika miaka hiyo, nimepatwa na kansa mbalimbali, kutia ndani iliyokuwa kichwani. Nilipata tiba ya mionzi na kufanyiwa upasuaji kwa saa 12 nchini India ili kuondoa sehemu kubwa ya kansa hiyo. Baada ya kupata nafuu katika ofisi ya tawi ya India, tulirudi katika mgawo wetu nchini Bulgaria.

Wakati huo, Heinz alianza kuugua ugonjwa wa kurithi unaowapata watu wachache unaoitwa Huntington. Ilikuwa vigumu kwake kutembea, kuzungumza, na kudhibiti misuli yake. Kadiri ugonjwa huo ulivyozidi kuwa mbaya, alihitaji kutegemea msaada wangu zaidi na zaidi. Nyakati fulani, nililemewa na uchovu na wasiwasi kuhusu jinsi hali itakavyokuwa. Hata hivyo, ndugu kijana anayeitwa Bobi alikuwa na kawaida ya kumwalika Heinz ili wahubiri pamoja. Bobi hakuona aibu kwamba Heinz hakuzungumza vizuri au alishindwa kudhibiti mikono na miguu yake. Sikuzote niliweza kumtegemea Bobi niliposhindwa kumsaidia Heinz. Ingawa mimi na Heinz tuliahirisha kupata watoto katika mfumo huu, tulihisi kwamba Yehova alitupatia Bobi kuwa mwana wetu!—Marko 10:​29, 30.

Heinz aliugua pia kansa. Kwa kusikitisha, mume wangu mpendwa alikufa mwaka wa 2015. Ninamkosa sana mume wangu, sikuzote yeye ndiye aliyekuwa ananisaidia nilipokuwa na wasiwasi; ilikuwa vigumu kwangu kuamini kwamba amekufa. Lakini anaendelea kuishi katika kumbukumbu langu! (Luka 20:38) Mara nyingi ninapokuwa katika shughuli zangu, ninakumbuka vizuri maneno yake yenye fadhili na ushauri wake mzuri. Ninathamini sana kwamba tuliweza kumtumikia Yehova pamoja kwa uaminifu kwa miaka mingi.

NINATHAMINI UTEGEMEZO WA YEHOVA

Kwa hakika, Yehova amenitegemeza katika majaribu yangu yote. Pia, alinisaidia kushinda hali yangu ya kuwa mwenye haya na nikawa mmishonari anayewapenda watu. (2 Tim. 1:7) Ninamshukuru Yehova kwamba mimi na dada yangu wa kimwili tuko katika utumishi wa wakati wote. Leo, yeye na mume wake wanazungukia makutaniko yanayozungumza Kiserbia yaliyo barani Ulaya. Sala alizotoa baba yangu miaka mingi iliyopita zilijibiwa!

Kusoma Biblia kunanipatia amani moyoni. Katika nyakati ngumu, nimejifunza kusali “kwa bidii zaidi,” kama Yesu alivyofanya. (Luka 22:44) Njia moja ambayo sala zangu zimejibiwa ni kupitia fadhili na upendo ninaoonyeshwa na ndugu na dada katika kutaniko langu la Nadezhda, Sofia. Wananialika nitumie wakati pamoja nao na mara nyingi wananiambia kwamba wananithamini, jambo ambalo linanipatia shangwe nyingi.

Mara nyingi ninatafakari kuhusu ufufuo. Ninawazia kuwaona wazazi wangu wakiwa wamesimama mbele ya nyumba yetu, wakiwa vijana kama siku waliyofunga ndoa. Ninamwona dada yangu akitayarisha mlo. Ninamwona Heinz akiwa amesimama kando ya farasi wake. Ninapowazia mambo hayo, hisia zisizofaa zinatoweka na moyo wangu unajaa shukrani kumwelekea Yehova.

Ninapotafakari kuhusu maisha yangu na kutazamia wakati ujao, ninakubaliana kwa moyo wote na maneno haya ya Daudi kwenye Zaburi 27:​13, 14: “Ningekuwa wapi ikiwa singekuwa na imani kwamba nitauona wema wa Yehova katika nchi ya walio hai? Mtumaini Yehova; uwe jasiri na uwe na moyo mkuu. Naam, mtumaini Yehova.”

a Tazama simulizi la maisha la Tatjana Vileyska katika gazeti la Amkeni! la Desemba 22, 2000, uku. 20-24.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki