GAZETI la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1913, lilirudia maneno yaliyojulikana sana wakati lilipomnukuu mwandishi wa habari Mmarekani Herbert Kaufman aliyesema hivi: “‘Kutowezekana’ sasa ni neno ambalo limepitwa na wakati . . . Karibu kila ndoto ya zamani imekuwa halisi leo.” Mwaka 1913 ulipoanza watu walikuwa na matumaini maangavu kuhusu wakati wao ujao.
Sababu moja ya matumaini hayo maangavu ilikuwa ni maendeleo ya tekinolojia. Kwa mfano, nchini Marekani, Kampuni ya Ford Motor ilifungua kiwanda kipya katika jiji la Highland Park, Michigan. Ghafla bei ya magari ilishuka sana hivi kwamba mamilioni ya watu wangeweza kununua gari. Nini kilichosababisha kushuka kwa bei ya magari? Kiwanda hicho kilikuwa na mitambo iliyotengeneza gari hatua kwa hatua. Maendeleo hayo yaliiwezesha Kampuni ya Ford kutengeneza gari lake maarufu aina ya Model T katika kipindi ambacho gari hizo zilihitajika, na hivyo bei ya magari ikashuka.
Watu wa Yehova pia walikuwa na matarajio maangavu lakini kwa sababu tofauti. Miaka mingi kabla ya mwaka 1914, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamehubiri kwamba mwaka 1914 ungekuwa mwaka muhimu katika historia ya wanadamu, na walikuwa na matarajio makubwa. Utendaji wao wa moyo wote ulionyesha kwamba hawakuwa wakipunguza bidii kadiri mwaka huo ulivyokuwa ukikaribia.
Kadi: Safari ya Pasta Russell Kuzunguka Nchi Mbalimbali
Mnamo Juni 1913 mfululizo wa makusanyiko ulianza kwa kusanyiko la siku moja katika Jiji la Kansas, Missouri, Marekani. Katika wiki nne zilizofuata, treni iliyokodiwa ilibeba kikundi chenye shangwe cha ndugu na dada zaidi ya 200 wakipita magharibi mwa Marekani na Kanada. Katika kila kusanyiko, wageni walipewa nafasi ya kuomba habari zaidi. Maelfu walifanya hivyo, na wale waliopendezwa, baadaye walitembelewa na Wanafunzi wa Biblia.
Mnamo 1913 wafanyakazi wa makao makuu Brooklyn walikuwa na kazi kubwa ya kutengeneza sinema ya “Photo-Drama of Creation.” Hiyo ilikuwa programu ya saa nane ya hotuba za Biblia zilizorekodiwa na muziki ulioambatanishwa na picha za rangi na sinema. Wanafunzi wa Biblia walitarajia kwamba “Photo-Drama” ingetumiwa kufikia mamilioni ya watu wanaopendezwa. Ingawa kwa wakati huo kulikuwa na watangazaji watendaji 5,100 hivi wa habari njema, kusudi lao lilikuwa kwamba sinema hiyo “ionyeshwe kwa mapana na marefu duniani kote kwa kadiri iwezekanavyo.”
Ni nini kingetokea mwaka wa 1914? “Photo-Drama” ingekuwa na matokeo gani? Ni nini kingetokea hatimaye baada ya Nyakati za Mataifa kuisha? Wanafunzi wa Biblia walisubiri kwa hamu majibu ya maswali hayo, huku wakimtegemea Yehova kwa ukamili.
Vita Kubwa ambayo baadaye ilikuja kuitwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu ilifutilia mbali matarajio ya watu. Maendeleo ya teknolojia hayakutoa suluhisho la matatizo ambayo watu walikabili. Mwaka uliofuata ulikuwa na mabadiliko makubwa kwa Wanafunzi wa Biblia—na kwa ulimwengu mzima.