Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ijwbq makala 193
  • Biblia Inasema Nini Kumhusu Danieli?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Biblia Inasema Nini Kumhusu Danieli?
  • Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jibu la Biblia
  • Danieli Alikuwa Nani?
  • Kitabu cha Danieli Chashtakiwa
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
  • Kitabu Cha Biblia Namba 27—Danieli
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Danieli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Jinsi Kitabu Cha Danieli Kinavyokuhusu
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
Pata Habari Zaidi
Maswali ya Biblia Yajibiwa
ijwbq makala 193
Nabii Danieli anasali akiwa kwenye shimo la simba.

Biblia Inasema Nini Kumhusu Danieli?

Jibu la Biblia

Danieli alikuwa nabii Myahudi aliyeishi katika karne ya saba na ya sita K.W.K. Mungu alimwezesha kueleza maana ya ndoto, pia alimpa maono kuhusu matukio ya wakati ujao, na alimwongoza kwa roho kuandika kitabu cha Biblia kinachoitwa kwa jina lake, yaani, kitabu cha Danieli.​—Danieli 1:17; 2:19.

Danieli Alikuwa Nani?

Danieli alilelewa katika ufalme wa Yuda. Jiji la Yerusalemu na hekalu la Wayahudi lilikuwa sehemu ya ufalme huo. Mwaka wa 617 K.W.K., mfalme Nebukadneza wa Babiloni, alivamia Yerusalemu na kuwateka “viongozi wa nchi” akawapeleka uhamishoni Babiloni. (2 Wafalme 24:15; Danieli 1:1) Danieli, ambaye huenda wakati huo alikuwa tineja, alitekwa pia.

Danieli na vijana wengine wanapelekwa na walinzi wa mfalme kwenye makao ya mfalme wa Babiloni.

Daneli na vijana wengine (kutia ndani Shadraki, Meshaki na Abednego) walipelekwa kwenye makao ya mfalme wa Babiloni ili kupata mafunzo ya pekee kwa ajili ya kumtumikia mfalme. Ingawa walishinikizwa kukana imani yao, Danieli na rafiki zake watatu walibaki washikamanifu kwa Mungu wao, Yehova. (Danieli 1:3-8) Baada ya kupata mafunzo kwa miaka mitatu, Mfalme Nebukadneza aliwasifu kwa sababu ya hekima na ujuzi wao, na akasema kwamba “walikuwa bora mara kumi kuliko makuhani wote wachawi na watu waliofanya mazingaombwe katika milki yake yote.” Alimchagua Danieli na rafiki zake kutumikia katika makao ya mfalme.​—Danieli 1:18-20.

Miongo mingi baadaye, Danieli alipokuwa na umri wa miaka 90 hivi, aliitwa kwenye makao ya mfalme. Mwanamume aliyeitwa Belshaza, ambaye alikuwa akitawala Babiloni wakati huo, alimwomba Danieli amweleze maana ya maandishi yaliyokuwa yametokea ghafula ukutani. Kwa mwongozo wa Mungu, Danieli alieleza kwamba milki ya Babiloni ingeshindwa na milki ya Wamedi na Waajemi. Jiji la Babiloni lilitekwa usiku huohuo.​—Danieli 5:1, 13-31.

Danieli anaeleza maana ya maandishi yaliyo kwenye ukuta.

Chini ya utawala wa Wamedi na Waajemi, Danieli aliteuliwa kuwa ofisa mkuu na Mfalme Dario alitaka kumuongezea madaraka zaidi. (Danieli 6:1-3) Maofisa wenye wivu walipanga njama ili Danieli auawe kwa kutupwa ndani ya shimo la simba. (Danieli 6:4-23) Danieli alipokaribia mwisho wa maisha yake, malaika alimtokea na mara mbili alimwita Danieli “mtu mwenye thamani sana.”​—Danieli 10:11, 19.

Jionee matukio hayo katika drama ya Biblia iliyo na sehemu mbili yenye kichwa, Danieli Alionyesha Imani Maisha Yake Yote.

Historia inafunua nini kuhusu kitabu cha Biblia cha Danieli?

Danieli aliandika: Nebukadneza alitengeneza sanamu kubwa, akawaagiza watu wake waiabudu sanamu hiyo, na akawatupa kwenye tanuru lenye moto wale waliokataa kufanya hivyo.​—Danieli 3:1-6.

Kile ambacho historia inafunua: Kitabu Encyclopædia Britannica kinasema kwamba Nebukadneza alianzisha miradi mikubwa ya ujenzi huko Babiloni “si kujitukuza yeye mwenyewe tu bali pia kuiheshimu miungu. Alidai kwamba ‘yeye ndiye aliyewashawishi watu kuiabudu miungu mikuu.’”

Maandishi ya kale ya Babiloni yanataja mara kadhaa visa vya kuwaua watu kwa kuwatupa kwenye tanuru lenye moto, kutia ndani visa ambavyo maagizo kama hayo yalitolewa na watawala. Hati moja ya zamani inayoaminiwa kuwa ya kipindi cha Nebukadneza, inaeleza kuhusu adhabu waliyopewa maofisa walioshtakiwa kwamba wamekufuru miungu ya Babiloni. Hati hiyo inasema: “Waangamize, wachome, waunguze. . . katika jiko la mpishi . . . moshi mwingi na upae, wateketeze kwa moto mkali.”a

Danieli aliandika: Mfalme Nebukadneza alijivuna kwa kiburi kwa sababu ya miradi yake ya ujenzi. —Danieli 4:29, 30.

Tofali lililochimbuliwa huko Babiloni, lenye jina la Nebukadneza

Kile ambacho historia inafunua: “Mambo ambayo Nebukadneza aliandika kujihusu yanaonyesha kwamba . . . alijiona kuwa mfalme mkuu, mwadilifu, na mwenye nguvu.b Kwa mfano, jengo moja lina maandishi haya yenye majivuno ya Nebukadneza: “Nimejenga kwa lami na tofali ukuta imara usioweza kusogezwa kwani uko kama mlima . . . Nimeimarisha ngome ya Esagila na ya Babiloni ili watu waukumbuke utawala wangu milele.”c Mengi kati ya matofali yaliyochimbuliwa katika Babiloni yana jina la Nebukadneza.

Danieli aliandika: Mfalme Belshaza alimpa Danieli nafasi ya kuwa “mtawala wa tatu katika ufalme” wa Babiloni.​—Danieli 5:1, 13-16.

Bamba hili la mwaka wa 550 K.W.K. linamtaja Mfalme Nabonido na Belshaza, mwana wake

Kile ambacho historia inafunua: Mwanamume anayeitwa Nabonido alikuwa mtawala katika kipindi kinachozungumziwa kwenye Danieli sura ya 5. Hata hivyo, ingawa Nabonido alikuwa mtawala, alitumia muda mwingi wa utawala wake huko Arabia na si Babiloni. Ni nani aliyetawala Babiloni katika vipindi ambavyo Nabonido hakuwepo? Katika kitabu chake, Nabonidus and Belshazzar, mwanahistoria Raymond Philip Dougherty anaeleza hivi: “Hati moja ya kale inasema kwamba Nabonido alimkabidhi utawala mwana wake wa kwanza wa kiume, yaani, Belshaza. Belshaza alifanya shughuli zote za kifalme kwa niaba ya mfalme ambaye hakuwepo, yaani, baba yake.” Kwa sababu Nabonido na Belshaza tayari walikuwa na vyeo viwili vya juu zaidi katika ufalme, Belshaza alitaka kumpa Danieli cheo cha tatu.

a Kitabu Journal of Biblical Literature, Buku la 128, Namba 2, ukurasa 279, 284.

b Kitabu Babylon​—City of Wonders, cha Irving Finkel na Michael Seymour, ukurasa 17.

c Kitabu Archæology and the Bible, cha George Barton, ukurasa 479.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki