Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ijwyp makala 106
  • Ninawezaje Kuwa na Uhusiano Mzuri na Mwalimu Wangu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ninawezaje Kuwa na Uhusiano Mzuri na Mwalimu Wangu?
  • Vijana Huuliza
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwalimu mkali
  • Mambo ya kufanya
  • Jinsi ya kuzungumza na mwalimu wako
  • Ninaweza Kufanya Nini ili Nielewane na Mwalimu Wangu?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Kwa Nini Tunahitaji Walimu?
    Amkeni!—2002
  • Alifanikiwa Kuliko Alivyotarajia
    Amkeni!—2003
  • Kwa Nini Mtu Huchagua Kuwa Mwalimu?
    Amkeni!—2002
Pata Habari Zaidi
Vijana Huuliza
ijwyp makala 106
Mwalimu akimrekebisha msichana mbele ya darasa.

VIJANA HUULIZA

Ninawezaje Kuwa na Uhusiano Mzuri na Mwalimu Wangu?

  • Mwalimu mkali

  • Mambo ya kufanya

  • Jinsi ya kuzungumza na mwalimu wako

  • Vijana wenzako wanasema nini

Mwalimu mkali

Karibu kila mwanafunzi huona kwamba kuna mwalimu mmoja ambaye hatendi kwa haki, anadai mengi, au ni mkali tu.

  • Luis mwenye umri wa miaka 21 anasema hivi: “Tulikuwa na mwalimu ambaye kila mara alitumia matusi na kuwatendea wanafunzi wake kwa njia isiyo na heshima. Alijua angestaafu baada ya muda mfupi, hivyo huenda alikuwa na uhakika kwamba hawezi kufutwa kazi.”

  • Melanie mwenye umri wa miaka 25, anakumbuka mwalimu wake akimtendea vibaya kuliko alivyowatendea wanafunzi wengine. Anasema: “Sababu yake ya kunitendea hivyo ni kwamba sikuwa wa dini inayojulikana sana. Aliniambia alikuwa akinitayarisha kutendewa hivyo nitakapokuwa mtu mzima.”

Hata ikiwa mwalimu wako ni mkali, bado unaweza kufanya mambo fulani ili ufurahie shule. Jaribu mapendekezo yafuatayo.

Mambo ya kufanya

  • Badilika kulingana na hali. Kila mwalimu anatazamia mambo tofauti kutoka kwa wanafunzi wake. Jaribu kuelewa mwalimu wako anatarajia nini kutoka kwako, kisha ujitahidi kutimiza hilo.

    Kanuni ya Biblia: “Mtu mwenye hekima husikiliza na kujifunza zaidi.”—Methali 1:5.

    “Niligundua kwamba nilihitaji kuelewa mapendezi ya mwalimu wangu, hivyo nilifanya yote niwezayo ili kufanya kazi alizonipa kulingana na maelekezo yake. Kufanya hivyo kumefanya iwe rahisi kuelewana naye.”—Christopher.

  • Onyesha heshima. Zungumza na walimu wako kwa fadhili. Usibishane nao hata ikiwa unahisi kwamba wamekukosea heshima. Kumbuka kwamba wanakuona kuwa mwanafunzi wao, si mtu mzima mwenzao.

    Kanuni ya Biblia: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yaliyokolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.”—Wakolosai 4:6.

    “Kwa kawaida walimu hawaheshimiwi na wanafunzi, hivyo ukijitahidi kuwaheshimu walimu, watakutendea kwa heshima pia.”—Ciara.

  • Elewa hali zao. Walimu ni wanadamu pia. Wao pia wanakabili matatizo na changamoto nyingi, kama watu wengine. Hivyo, usifikie mkataa kwamba ‘Mwalimu wangu ni mkali’ au ‘Mwalimu wangu ananichukia.’

    Kanuni ya Biblia: ‘Kwa maana sisi sote hufanya makosa.’—Yakobo 3:2, maelezo ya chini.

    “Walimu wana kazi ngumu sana. Si jambo rahisi kuhakikisha wanafunzi wote wanadumisha tabia nzuri na kuwafundisha. Sikuzote nilijiambia ninapaswa kurahisisha kazi ya mwalimu na hivyo kumpunguzia mkazo.”—Alexis.

  • Zungumza na wazazi wako. Wazazi wako wanaunga mkono jitihada zako. Wangependa ufanye vizuri shuleni, na ushauri wao unaweza kukusaidia kushughulika na mwalimu anayetaka mengi kutoka kwako.

    Kanuni ya Biblia: “Mipango huvunjika watu wasiposhauriana.”—Methali 15:22.

    “Wazazi wana uzoefu mwingi zaidi wa kutatua matatizo kuliko vijana. Hivyo sikiliza ushauri wao. Huenda unaweza kukusaidia kufanikiwa.”—Olivia.

Jinsi ya kuzungumza na mwalimu wako

Katika visa fulani, huenda ukahitaji kuzungumza na mwalimu wako kuhusu changamoto unayokabili kwa sababu yake. Ikiwa wewe hupendi mabishano, usiwe na wasiwasi. Hayo ni mazungumzo, na utashangaa jinsi yatakavyokuwa rahisi na yenye matokeo mazuri.

Kanuni ya Biblia: ‘Fuatilia mambo yanayoleta amani.’—Waroma 14:19.

“Ikiwa inaonekana kwamba mwalimu wako ni mkali anaposhughulika na wewe, muulize ikiwa umefanya jambo lililomkasirisha. Jibu lake linaweza kukusaidia kujua mambo unayohitaji kufanya ili kuboresha hali.”—Juliana.

“Huenda ikafaa kuzungumza na mwalimu wako kuhusu hali hiyo kwa utulivu na mkiwa peke yenu kabla au baada ya vipindi vya darasani. Huenda akawa na usawaziko na akaheshimu jinsi ulivyoshughulikia hali hiyo.”—Benjamin.

SIMULIZI HALISI

“Nilikuwa nikipata alama za chini shuleni, na mwalimu wangu hakunisaidia kwa njia yoyote ile. Nilitaka kuacha shule kwa sababu alifanya maisha yangu yawe magumu zaidi.

“Niliamua kuomba ushauri kutoka kwa mwalimu mwingine. Aliniambia hivi: ‘Mwalimu huyo hakufahamu, na wewe pia humfahamu. Unahitaji kumwambia changamoto unazokabili. Kufanya hivyo kunaweza kuwasaidia wanafunzi wengine wanaoogopa kuzungumza naye.’

“Sikutaka kufuata ushauri huo! Hata hivyo, nilifikiria mambo aliyoniambia, na kwa kweli hakuwa amekosea. Ikiwa nilitaka hali zibadilike, nilipaswa kuchukua hatua ya kwanza.

“Basi siku iliyofuata, nilimwendea mwalimu wangu na kwa heshima nikamwambia kwamba ninathamini sana mambo anayotufundisha na ningependa kujifunza mengi zaidi kutoka kwake. Lakini nikamwambia kwamba ninakabili changamoto na sikujua jambo la kufanya. Mwalimu huyo alinipa mapendekezo na hata akasema alikuwa tayari kunisaidia baada ya masomo au kupitia barua pepe.

“Nilishangaa sana! Mazungumzo hayo yaliniwezesha kuboresha uhusiano wangu na mwalimu wangu na kufanya maisha yangu shuleni yasiwe na mkazo kama zamani.”—Maria.

Maria akiongea na mwalimu wake baada ya darasa.

Dokezo: Ikiwa huna uhusiano mzuri na mwalimu wako, ona changamoto hiyo kuwa mazoezi ya kuwa mtu mzima. Katie mwenye umri wa miaka 22, anasema hivi: “Hata baada ya kuhitimu, utakutana na watu wenye mamlaka ambao hawatashughulika nawe kwa fadhili. Ikiwa utafaulu kushughulika na mwalimu ambaye huna uhusiano mzuri naye, basi utaweza kushughulika na watu wasio na fadhili wakati ujao.”

Vijana wenzako wanasema nini

Jayza.

“Kuna pindi ambazo mwalimu alinikasirisha. Hata hivyo, mama yangu alinisaidia kufikiria maoni ya mwalimu. Kufanya hivyo kulinisaidia kuwa mwenye usawaziko kuelekea mambo niliyotarajia kutoka kwa walimu wangu.”—Jayza.

Victor.

“Si lazima umpende mtu ili uheshimu cheo chake. Walimu wanastahili kuheshimiwa. Hivyo, hata kama mwalimu ni mkali, ukimwonyesha heshima utaweza kuboresha hali kwa kiasi kikubwa sana. Kufanya hivyo kunaweza hata kumfanya mwalimu abadili jinsi anavyokutendea.”—Victor.

Julia.

“Ukiwa mwenye fadhili na mpole—hata kama mwalimu wako haonyeshi sifa hizo—utaonyesha kwamba wewe ni mnyenyekevu na mwenye heshima. Huenda mwalimu akakuheshimu zaidi na akaanza kukutendea kwa fadhili.”—Julia.

Muhtasari: Ninawezaje kuwa na uhusiano mzuri na mwalimu wangu?

  • Badilika kulingana na hali. Jaribu kuelewa mwalimu wako anatarajia nini kutoka kwako, kisha ujitahidi kutimiza hilo.

  • Onyesha heshima. Kumbuka kwamba wewe ni mwanafunzi, hivyo zungumza kwa fadhili na usibishane na mwalimu wako.

  • Elewa hali zao. Kazi ya ualimu ina mkazo mkubwa sana. Jitahidi kuwa na subira nao.

  • Zungumza na wazazi wako. Wana uzoefu mwingi zaidi wa kushughulika na watu.

  • Zungumza na mwalimu wako. Kwa utulivu na bila mabishano yoyote, mwombe mwalimu wako msaada. Mweleze wazi kwamba ungependa kushirikiana naye.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki