Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ijwyp makala 114
  • Nifanye Nini Ikiwa Sitamani Kuendelea Kuishi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nifanye Nini Ikiwa Sitamani Kuendelea Kuishi?
  • Vijana Huuliza
  • Habari Zinazolingana
  • Ninataka Kufa—Je, Biblia Inaweza Kunisaidia Ikiwa Nina Mawazo ya Kujiua?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Afadhali Nijiue?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Ninaweza Kukabilianaje na Kushuka Moyo?
    Vijana Huuliza
  • Kwa Nini Nisijiue?
    Amkeni!—2008
Pata Habari Zaidi
Vijana Huuliza
ijwyp makala 114
Msichana aliyeshuka moyo akitazama nje dirishani mvua inaponyesha.

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Sitamani Kuendelea Kuishi?

“Miaka michache iliyopita nilikuwa na mahangaiko mengi na nilihisi kana kwamba ninapambana na moto kila siku. Nilipopitia hali hiyo nilitamani kujiua mwenyewe. Kusema kweli sikutaka kufa. Nilitaka tu mahangaiko hayo yaishe.”​—Jonathan miaka 17.

Katika utafiti fulani uliowahusisha wanafunzi 14,000 wa sekondari, iligunduliwa kwamba mwanafunzi 1 kati ya 5 alipata mawazo ya kujiua katika miezi 12 iliyotangulia.a Ikiwa unahisi maisha yamekuchosha, unaweza kufanya nini?

  • Subiri. Amua kwamba hutatenda haraka unapopata hisia hizo. Ikiwa unahisi matatizo unayokabiliana nayo yanakulemea, bado kuna mambo kadhaa unayoweza kufanya ili kukabiliana na matatizo hayo.

Msichana anayetafuta njia ya kutokea.

Huenda ukahisi kwamba matatizo yako hayana suluhisho lakini kuwa na hisia fulani hakumaanishi kwamba hali iko hivyo kihalisi. Kuna njia ambazo unaweza ukatumia ili kukabiliana na hali yako. Ukipata msaada unaofaa, huenda ukapata suluhisho haraka kuliko unavyofikiri.

  • Kanuni ya Biblia: “Tunakandamizwa katika kila njia, lakini hatubanwi kupita kiasi cha kushindwa kusonga; tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa.”​—2 Wakorintho 4:8.

    Pendekezo: Ikiwa unalemewa na mawazo ya kujiua au hayaishi, tafuta msaada labda kwa kupiga simu kwenye kituo cha kutoa msaada au kwenye idara ya hospitali inayoshughulikia hali za dharura. Utapata wataalamu wanaoweza kukusaidia na kwa kweli wanataka kufanya hivyo.

  • Zungumza na mtu. Kuna watu ambao wanakujali na wako tayari kukusaidia. Watu hao wanatia ndani marafiki zako au watu wa familia ambao hawawezi kujua unapitia hali gani usipowaeleza.

Msichana akivaa miwani.

Baadhi ya watu wanahitaji miwani ili kuona vizuri. Vivyo hivyo, rafiki anaweza kukusaidia kuona matatizo yako kwa njia tofauti na hivyo kukuchochea utake tena kuendelea kuishi.

  • Kanuni ya Biblia: “Rafiki wa kweli . . . amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”​—Methali 17:17.

    Pendekezo: Ili kuanzisha mazungumzo unaweza kusema: “Kuna jambo fulani limekuwa likinihangaisha kwa muda. Je, ninaweza kukueleza?” Au unaweza kusema: “Nina matatizo fulani ambayo nahisi siwezi kuyatatua mwenyewe. Je, unaweza kunisaidia?”

  • Mwone daktari. Matatizo ya afya kama vile kuwa na wasiwasi au mfadhaiko unaopita kiasi au kushuka moyo yanaweza kumfanya mtu apoteze hamu ya kuendelea kuishi. Habari njema ni kwamba magonjwa hayo yana tiba.

Msichana ambaye ni mgonjwa ameduwaa. Hali chakula kilicho mbele yake.

Unapopata mafua unapoteza hamu ya kula, vivyo hivyo, unaposhuka moyo unapoteza hamu ya kuishi. Hata hivyo, magonjwa yote mawili yana tiba.

  • Kanuni ya Biblia: “Watu wenye afya hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji.”​—Mathayo 9:12.

    Pendekezo: Lala vya kutosha, fanya mazoezi, na ule chakula chenye lishe. Afya yako inaweza kuathiri hisia zako.

  • Sali. Biblia inasema hivi kumhusu Muumba wetu: “Ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” (1 Yohana 3:20) Kwa nini usisali kwake leo? Tumia jina lake Yehova na uzungumze kutoka moyoni mwako.

Msichana akiwa amelemewa na mzigo mkubwa aliobeba.

Matatizo mengine ni mazito sana ukiyabeba mwenyewe. Lakini Yehova, Muumba wako, yuko tayari kukusaidia.

  • Kanuni ya Biblia: “Mjulisheni Mungu maombi yenu; na amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.”​—Wafilipi 4:6, 7.

    Pendekezo: Zaidi ya kumwambia Yehova kuhusu matatizo yako, fikiria angalau jambo moja zuri maishani mwako leo na umshukuru. (Wakolosai 3:15) Kuonyesha shukrani kunaweza kukusaidia kukazia fikira mambo mazuri maishani mwako.

Ikiwa unahisi kwamba hutamani kuendelea kuishi, omba msaada. Jonathan aliyetajwa hapo mwanzoni alifanya hivyo. Anasema hivi: “Nilizungumza mara nyingi pamoja na wazazi wangu na pia nilipata usaidizi wa daktari. Sasa, ninahisi vizuri zaidi. Ingawa wakati mwingine ninakabiliana na huzuni, sipati tena mawazo ya kujiua.”

a Utafiti huo ulifanywa mwaka 2019 na Vituo vya Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza vya Marekani.

Vijana wenzako wanasema nini

Alexandra.

“Afya ya kiakili ni muhimu kama ilivyo afya ya kimwili. Tofauti ni kwamba unaweza kuona mtu anapovunjika mkono au mguu lakini huwezi kuona mtu anapovunjika moyo. Ikiwa unataabika moyoni usiogope kusema. Ni vizuri kuomba msaada.”​—Alexandra.

Ian.

“Miaka kadhaa iliyopita, wazazi wangu walinisaidia kuelewa kwamba kila tatizo maishani linaweza kutatuliwa au mtu anaweza kulivumilia. Kuzungumza na wazazi wangu kulinisaidia sana kuona matatizo yangu kwa njia nzuri zaidi.”​—Ian.

Mistari ya Biblia inayoweza kukusaidia

Unaweza kutengeneza orodha ya mistari ya Biblia inayoweza kukusaidia unapovunjika moyo. Hii ni mifano michache.

Zaburi 34:18: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; huwaokoa waliopondeka roho.”

Maana: Yehova anawajali sana watu wanaohisi kwamba wamelemewa na matatizo yao. Anataka kuwasaidia.

Zaburi 46:1: “Mungu ni kimbilio letu na nguvu zetu, msaada unaopatikana kwa urahisi nyakati za taabu.”

Maana: Unaweza kusali kwa Yehova wakati wowote unapohisi umelemewa na mahangaiko au wasiwasi. Yuko tayari kukusaidia uvumilie hali hiyo.

Zaburi 94:18, 19: “Niliposema: ‘Mguu wangu unateleza,’ upendo wako mshikamanifu, Ee Yehova, uliendelea kunitegemeza. Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.”

Maana: Mungu anaweza kukupatia faraja unayohitaji kupitia Neno lake, Biblia. Usiruhusu siku ipite bila kulisoma Neno lake!

Zaburi 139:23, 24: “Nichunguze kabisa, Ee Mungu, . . . uyajue mawazo yangu yanayonihangaisha. Angalia ikiwa kuna njia yoyote yenye madhara ndani yangu, uniongoze katika njia ya milele.”

Maana: Yehova anakujua vizuri zaidi kuliko unavyojijua wewe mwenyewe. Anaweza kukusaidia kurekebisha njia yoyote mbaya ya kufikiri ili uwe na furaha tena maishani.

Isaya 41:10: “Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia.”

Maana: Yehova anaweza kutupatia nguvu ya kuvumilia hali yoyote ngumu tunayokabili.

Pitio: Nifanye nini ikiwa sitamani kuendelea kuishi?

  • Subiri. Amua kwamba hutatenda haraka unapopata hisia hizo. Kuna mambo kadhaa unayoweza kufanya ili kukabiliana na matatizo hayo.

  • Zungumza na mtu. Marafiki wako au watu wa familia hawawezi kujua unapitia hali gani usipowaeleza.

  • Mwone daktari. Mawazo ya kujiua yanaweza kuwa dalili ya ugonjwa wa kushuka moyo na ugonjwa huo una tiba.

  • Zungumza na Mungu kupitia sala. Anakujua vizuri zaidi kuliko unavyojijua wewe mwenyewe, na anataka kukusaidia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki