Je, Dini Inapaswa Kujihusisha Katika Siasa?
Ulimwenguni pote, watu wengi wanaodai kumfuata Yesu Kristo wanajihusisha sana katika siasa. Wengine hujaribu kuendeleza imani zao za kidini na viwango vya maadili kwa kuwaunga mkono wanasiasa au vyama vya kisiasa. Nao wanasiasa mara nyingi hutumia masuala ya kimaadili au ya kijamii kuwavutia watu wa dini wawaunge mkono. Na ni kawaida kwa viongozi wa kidini kujaribu kujipatia vyeo vya kisiasa. Katika nchi fulani, huenda hata dini inayodai kuwa ya Kikristo ikawa na wadhifa wa pekee, na kuonwa kuwa dini ya taifa.
Una maoni gani? Je, wafuasi wa Yesu Kristo wanapaswa kujihusisha katika siasa? Tunaweza kupata jibu kwa kuchunguza mfano wa Yesu. Alisema hivi: “Nimewawekea kielelezo, ili mfanye kama nilivyowafanyia.” (Yohana 13:15) Yesu aliweka kielelezo gani kuhusu mambo ya kisiasa?
Je, Yesu alijihusisha katika siasa?
Hapana. Yesu hakujihusisha katika siasa za ulimwengu huu.
Yesu hakutafuta cheo cha kisiasa. Alikataa kuwa mtawala wa serikali za wanadamu wakati ambapo Shetani Ibilisi alisema atampa “falme zote za ulimwengu.” (Mathayo 4:8-10)a Pindi nyingine, watu waliotambua kwamba Yesu ana uwezo wa kuwa mtawala mzuri, walijaribu kumchochea akubali cheo cha kisiasa. Biblia inatuambia hivi: “Yesu akijua walitaka kuja kumkamata wamfanye awe mfalme, akaondoka tena akaenda mlimani akiwa peke yake.” (Yohana 6:15) Yesu hakukubali ombi la watu hao. Badala yake, alikataa kujihusisha katika siasa.
Yesu hakuunga mkono upande wowote katika masuala ya kisiasa. Kwa mfano, katika siku za Yesu, Wayahudi walichukia kuilipa serikali ya Roma kodi na waliona kodi hiyo kuwa mzigo usio wa haki. Walipojaribu kumhusisha Yesu aunge mkono suala hilo, Yesu hakujihusisha katika majadiliano ya kuonyesha ikiwa kodi hizo zilikuwa za haki au la. Aliwaambia hivi: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.” (Marko 12:13-17) Hakuunga mkono upande wowote katika suala la kisiasa lakini akaonyesha kwamba kodi zinazodaiwa na mamlaka ya serikali ya Roma, iliyowakilishwa na Kaisari, zilipaswa kulipwa. Wakati huohuo, alionyesha kwamba utii kwa mamlaka ya serikali una mipaka. Mtu hakupaswa kuipa serikali haki ya Mungu, inayotia ndani ujitoaji na ibada.—Mathayo 4:10; 22:37, 38.
Yesu aliunga mkono na kutangaza serikali ya mbinguni, Ufalme wa Mungu. (Luka 4:43) Hakujihusisha katika siasa kwa sababu alijua kwamba Ufalme wa Mungu ndio ungetimiza mapenzi ya Mungu duniani, na si serikali za wanadamu. (Mathayo 6:10) Alielewa kwamba Ufalme wa Mungu haungetenda kupitia serikali za wanadamu bali ungeziangamiza.—Danieli 2:44.
Je, Wakristo wa karne ya kwanza walijihusisha katika siasa?
Hapana. Wafuasi wa Yesu walitii amri yake ya kuepuka kuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Walifuata mfano wake na kuendelea kujitenga na siasa za ulimwengu. (Yohana 17:16; 18:36) Badala ya kujihusisha katika siasa, walifanya kazi ambayo Yesu aliwaamuru—kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme wa Mungu.—Mathayo 28:18-20; Matendo 10:42.
Wakristo wa karne ya kwanza walitambua kwamba walipaswa kumtii Mungu kwanza maishani mwao, lakini walitambua pia kwamba walipaswa kuheshimu mamlaka za serikali. (Matendo 5:29; 1 Petro 2:13, 17) Walitii sheria na kulipa kodi. (Waroma 13:1, 7) Ingawa hawakujihusisha katika siasa, walitumia maandalizi ya kisheria na huduma mbalimbali zilizotolewa na serikali.—Matendo 25:10, 11; Wafilipi 1:7.
Wakristo leo hawaungi mkono upande wowote
Biblia inaonyesha wazi kwamba Yesu na wafuasi wake wa mapema hawakujihusisha katika siasa. Kwa sababu hiyo, kwa kuwa wao ni Wakristo, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote hawaungi mkono upande wowote wa mambo ya kisiasa. Kama tu Wakristo wa karne ya kwanza, wanafanya kazi ambayo Yesu aliwaamuru—wanahubiri “hii habari njema ya Ufalme.”—Mathayo 24:14.
a Yesu alipopinga kishawishi hicho, hakusema kwamba Shetani hakuwa na mamlaka ya kumpa falme zote. Baadaye, alimwita Shetani kuwa “mtawala wa ulimwengu.”—Yohana 14:30