MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA
Methali 17:17—“Rafiki Hupenda Sikuzote”
“Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote, naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”—Methali 17:17, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.
“Rafiki hupenda sikuzote; Na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Methali 17:17,Union Version.
Maana ya Methali 17:17
Rafiki wa kweli wanategemeka na wanaaminika. Kama ndugu waliozaliwa pamoja walivyo karibu, rafiki wa kweli ni washikamanifu na wenye kujali, hasa katika nyakati ngumu.
“Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote.” Usemi huu unaweza pia kumaanisha “rafiki hupenda daima.” Neno la Kiebrania linalotumiwa kurejelea “upendo” katika muktadha huu lina maana kubwa zaidi kuliko tu hisia kumwelekea mtu fulani. Huu ni upendo usio na ubinafsi ambao unaonyeshwa kupitia matendo. (1 Wakorintho 13:4-7) Marafiki wanaopendana kwa njia hiyo wanaendelea kuwa washikamanifu hata uhusiano wao unapojaribiwa. Wanapokosa kuelewana au wanapokuwa na mkazo kwa sababu ya matatizo ya maisha, bado wanaendelea kuwa marafiki. Isitoshe, wanasameheana kwa hiari. (Methali 10:12) Rafiki wa kweli pia hamwonei wivu rafiki yake mambo yanapomwendea vizuri. Badala yake, anashangilia pamoja na rafiki yake.—Waroma 12:15.
“Rafiki wa kweli . . . ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.” Methali hii inatumia maneno hayo kwa sababu ndugu waliozaliwa pamoja wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu sana. Hivyo, tunapofanya yote tuwezayo kumsaidia rafiki yetu anayepitia wakati mgumu, tunamtendea kama vile ambavyo ndugu au dada yake wa kimwili angemtendea. Isitoshe, majaribu hayawezi kudhoofisha urafiki wa aina hiyo. Badala yake, unaimarika kwa sababu wanapokabili matatizo, wanazidi kupendana na kuheshimiana.
Muktadha wa Methali 17:17
Kitabu cha Methali kina misemo mingi yenye hekima inayomchochea msemaji kufikiri. Mfalme Sulemani aliandika sehemu kubwa ya kitabu hiki cha Biblia. Njia yake ya kuandika ilitumika sana katika mashairi ya Kiebrania ambayo badala ya kutumia vina vyenye silabi zinazofanana au vyenye sauti ya namna moja, yalitumia mawazo yanayolingana au yanayokinzana. Mstari au mshororo mmoja ungekazia habari za mstari uliotangulia au ungekuwa na habari zinazokinzana. Methali 17:17 ni ushairi ambao hutumia mawazo yanayolingana. Sehemu ya pili ya mstari huo inatoa habari zinazotilia mkazo sehemu ya kwanza ya mstari. Kwa upande mwingine, Methali 18:24 ni ushairi ambao hutumia maneno yanayokinzana. “Kuna marafiki walio tayari kuangamizana, lakini kuna rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu kuliko ndugu.”
Alipokuwa akiandika Methali 17:17, huenda Sulemani alikuwa akifikiria urafiki wa karibu uliokuwa kati ya baba yake, Daudi, na Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli. (1 Samweli 13:16; 18:1; 19:1-3; 20:30-34, 41, 42; 23:16-18) Daudi na Yonathani hawakuwa watu wa ukoo mmoja lakini walikuwa na uhusiano wa karibu kuliko ndugu. Yonathani hata alihatarisha uhai wake ili kumlinda Daudi.a
Methali 17:17 Katika Biblia Nyingine
“Rafiki wa kweli ni rafiki sikuzote, ndugu huzaliwa asaidie wakati wa taabu.”—Biblia Habari Njema.
“Rafiki hupenda wakati wote naye ndugu amezaliwa kwa ajili ya wakati wa shida.”—Neno: Biblia Takatifu.
Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Methali.
a Ona makala “Wakashikamana na Kuwa Marafiki wa Karibu Sana.”