Jumatatu, Julai 14
Akaenda nje akalia kwa uchungu.—Mt. 26:75.
Mtume Petro alipambana na udhaifu wake mbalimbali. Fikiria mifano michache. Yesu alipoeleza jinsi ambavyo angeteseka na kufa ili kutimiza unabii wa Biblia, Petro alimkemea. (Marko 8:31-33) Petro na wale mitume wengine walibishana tena na tena kuhusu yule aliyekuwa mkuu zaidi kati yao. (Marko 9:33, 34) Usiku wa mwisho kabla ya kifo cha Yesu, Petro alimshambulia mwanamume fulani na kumkata sikio. (Yoh. 18:10) Usiku huohuo Petro alilemewa na woga na mara tatu akakana kwamba hamjui Yesu, rafiki yake. (Marko 14:66-72) Baada ya hapo Petro alilia kwa uchungu. Yesu hakumwacha mtume huyo aliyekuwa amevunjika moyo sana. Baada ya Yesu kufufuliwa, alimpa Petro fursa ya kuonyesha kwamba bado anampenda. Yesu alimwalika Petro awe mchungaji mnyenyekevu wa kondoo wake. (Yoh. 21:15-17) Petro aliitikia kwa njia nzuri. Alikuwa huko Yerusalemu siku ya Pentekoste na alikuwa miongoni mwa Wakristo wa kwanza kutiwa mafuta kwa roho takatifu. w23.09 22 ¶6-7
Jumanne, Julai 15
Chunga kondoo wangu wadogo.—Yoh. 21:16.
Petro aliwahimiza hivi wazee wenzake: “Lichungeni kundi la Mungu.” (1 Pet. 5:1-4) Ikiwa wewe ni mzee wa kutaniko, tunajua kwamba unawapenda ndugu na dada zako, na unataka kuwachunga kiroho. Hata hivyo, huenda nyakati nyingine ukahisi kwamba una shughuli nyingi sana au una uchovu mwingi sana hivi kwamba huwezi kutimiza mgawo huo. Unaweza kufanya nini? Mmiminie Yehova mahangaiko yako. Petro aliandika hivi: “Yeyote akihudumu, na afanye hivyo kama anayetegemea nguvu ambazo Mungu hutoa.” (1 Pet. 4:11) Huenda ndugu na dada zako wanakabili matatizo ambayo hayawezi kusuluhishwa kabisa katika mfumo huu wa mambo. Lakini kumbuka kwamba “mchungaji mkuu,” Yesu Kristo, anaweza kuwasaidia kwa njia nzuri zaidi kuliko unavyoweza. Anaweza kufanya hivyo leo na katika ulimwengu mpya. Mungu anataka wazee wawapende na kuwachunga ndugu zao na wawe “vielelezo kwa kundi.” w23.09 29-30 ¶13-14
Jumatano, Julai 16
Yehova anajua kwamba kufikiri kwa watu wenye hekima ni ubatili.—1 Kor. 3:20.
Ni lazima tuepuke kutumia njia ya kufikiri ya wanadamu. Ikiwa tutaona mambo kulingana na maoni ya wanadamu, huenda tukampuuza Yehova na viwango vyake. (1 Kor. 3:19) Mara nyingi, “hekima ya ulimwengu huu” huchochea tamaa za mwili. Baadhi ya Wakristo huko Pergamamu na Thiatira waliwaiga watu waliowazunguka ambao walikuwa na maadili mapotovu na waliabudu sanamu. Yesu aliyapatia makutaniko hayo mawili shauri kali kwa sababu ya kuvumilia uasherati. (Ufu. 2:14, 20) Leo, tunashawishiwa kukubali maoni yasiyofaa. Huenda watu wa familia yetu na marafiki wakajaribu kutusadikisha kwamba tuna msimamo mkali sana na kwamba hatupaswi kufuata sheria za Yehova. Kwa mfano, huenda wakadai kwamba si jambo muhimu kuendelea kuwa safi kiadili na viwango vya maadili vya Biblia vimepitwa na wakati. Nyakati nyingine, huenda tukafikiri kwamba mwongozo ambao Yehova anatupatia hautoshi. Hata huenda tukashawishiwa ‘kupita mambo yaliyoandikwa.’—1 Kor. 4:6. w23.07 16 ¶10-11