-
UtatuKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
mngalifurahi kwa sababu naenda kwa Baba, kwa maana Baba ni mkuu kuliko mimi.”
1 Kor. 11:3, UV: “Nataka mjue ya kuwa kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa na mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu.” (Kwa wazi, basi, Kristo si Mungu, na Mungu ana cheo kikuu kuliko Kristo. Kumbuka kwamba maneno hayo yaliandikwa karibu mwaka wa 55 W.K., miaka 22 hivi baada ya Yesu kurudi mbinguni. Kwa hiyo ukweli unaoelezwa hapa unahusu uhusiano uliopo kati ya Mungu na Kristo mbinguni.)
1 Kor. 15:27, 28, UV: “[Mungu] alivitiisha vitu vyote chini ya miguu yake [ya Yesu]. Lakini atakaposema, Vyote vimetiishwa, ni dhahiri ya kuwa yeye aliyemtiishia vitu vyote hayumo. Basi, vitu vyote vikiisha kutiishwa chini yake, ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika wote.”
Neno la Kiebrania Shad·daiʹ na neno la Kigiriki Pan·to·kraʹtor yote mawili hutafsiriwa “Mweza-Yote.” Maneno yote mawili ya lugha za kwanza yanatumiwa tena na tena kumhusu Yehova, Baba. (Kut. 6:3; Ufu. 19:6) Kati ya maneno hayo, hakuna kamwe linalotumiwa kumhusu Mwana wala roho takatifu.
Je, Biblia hufundisha kwamba kila mmoja wa wale wanaosemwa kuwa sehemu ya Utatu ni Mungu?
Yesu alisema hivi katika sala: “Baba, . . . uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yoh. 17:1-3, UV; italiki zimeongezwa.) (Tafsiri nyingi hapa hutumia maneno “Mungu wa pekee wa kweli” kumhusu Baba. NAJ husema: “ambaye pekee ni Mungu wa kweli.” Hawezi kuwa “Mungu wa pekee wa kweli,” “ambaye pekee ni Mungu wa kweli,” ikiwa kuna wengine wawili ambao ni Mungu kwa kiwango kilekile kama yeye, sivyo? Wengine wowote wanaoitwa “miungu” lazima wawe wa uwongo au mrudisho tu wa utukufu wa Mungu wa kweli.)
1 Kor. 8:5, 6, UV: “Ijapokuwa wako waitwao miungu, ama mbinguni ama duniani, kama vile walivyoko miungu mingi na mabwana wengi; lakini kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake, nasi tunaishi kwake; yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo, ambaye kwake vitu vyote vimekuwapo, na sisi kwa yeye huyo.” (Andiko humwonyesha Baba kuwa ‘Mungu mmoja’ wa Wakristo na akiwa katika daraja tofauti na Yesu Kristo.)
1 Pet. 1:3, UV: “Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.” (Tena na tena, hata baada ya Yesu kupanda mbinguni, Maandiko yanamwita Baba “Mungu” wa Yesu Kristo. Katika andiko la Yohana 20:17, baada ya Yesu kufufuliwa, yeye mwenyewe alimwita Baba kuwa “Mungu wangu.” Baadaye, akiwa mbinguni, kama ilivyoandikwa katika Ufunuo 3:12, tena alitumia maneno hayohayo. Lakini hakuna mahali popote kamwe katika Biblia ambapo inasemekana Baba anamwita Mwana “Mungu wangu,” wala Baba au Mwana hawaiiti roho takatifu “Mungu wangu.”)
Ili kupata maelezo kuhusu maandiko ambayo watu fulani hutumia wakijaribu kuthibitisha kwamba Kristo ni Mungu, ona ukurasa wa 430-434, chini ya kichwa “Yesu Kristo.”
Katika Theological Investigations, Karl Rahner, S.J., hukubali hivi: “Neno Θεός [Mungu] halitumiwi kamwe kuhusu Roho,” na: neno “ὁ θεός [kihalisi, yule Mungu] halitumiwi kamwe katika Agano Jipya kusema kuhusu [roho takatifu].”—(Baltimore, Md.; 1961), kilichotafsiriwa kutoka Kijerumani, Buku la 1, uku. 138, 143.
Kati ya maandiko yanayotumiwa na Wana-Utatu ili kuunga mkono imani yao, je, lolote lina msingi imara kwa fundisho hilo?
Mtu ambaye kwa kweli anatafuta kujua kweli kumhusu Mungu hatachunguza Biblia akitumaini kupata andiko ambalo atalielewa kuwa linafaa yale ambayo tayari anaamini. Yeye hutaka kujua mambo ambayo Neno la Mungu lenyewe husema. Huenda akaona maandiko fulani anayohisi yanaweza kueleweka kwa njia kadhaa, lakini hayo yanapolinganishwa na maandiko mengine ya Biblia kuhusu habari hizohizo, maana yake itakuwa wazi. Kumbuka mapema kwamba maandiko mengi yanayotumiwa “kuthibitisha” Utatu kwa kweli yanataja watu wawili tu, wala si watatu; kwa hiyo hata ikiwa maelezo ya Wana-Utatu kuhusu maandiko hayo yangekuwa sahihi, hayo hayangethibitisha kwamba Biblia hufundisha Utatu. Fikiria mambo yafuatayo:
(Isipokuwa imeonyeshwa vingine, maandiko yote yaliyonukuliwa katika sehemu inayofuata yanatoka katika UV.)
Maandiko ambayo jina linalomhusu Yehova linatumiwa kumhusu Yesu Kristo au linadaiwa kwamba linamhusu Yesu
Alfa na Omega: Majina hayo ni ya nani? (1) Katika andiko la Ufunuo 1:8, inasemwa mwenyewe ni Mungu, Mweza-Yote. Katika mstari wa 11 kulingana na ZSB, majina hayo yanatumika kumhusu yule ambaye maelezo yanayofuata yanaonyesha kuwa ni Yesu Kristo. Lakini wasomi wanatambua kwamba mtajo wa majina Alfa na Omega katika mstari wa 11 ni wa uwongo, na kwa hiyo majina hayo katika mstari huo hayapatikani katika UV, BHN, NAJ, VB. (2) Tafsiri nyingi za Ufunuo katika Kiebrania zinatambua kwamba yule anayesimuliwa katika mstari wa 8 ni Yehova, na kwa hiyo zinarudisha jina la Mungu hapo. Ona NW, chapa ya Marejeo ya 1984. (3) Andiko la Ufunuo 21:6, 7 huonyesha kwamba Wakristo ambao wanapata ushindi kiroho watakuwa ‘wana’ wa yule anayeitwa Alfa na Omega. Hilo halisemwi kamwe kuhusu uhusiano kati ya Wakristo watiwa-mafuta na Yesu Kristo. Yesu aliwaita ‘ndugu’ zake. (Ebr. 2:11; Mt. 12:50; 25:40) Lakini hao ‘ndugu’ za Yesu wanaitwa “wana wa Mungu.” (Gal. 3:26; 4:6) (4) Katika andiko la Ufunuo 22:12, BHN hutia ndani jina Yesu, kwa hiyo mtajo wa Alfa na Omega katika mstari wa 13 huonekana kana kwamba unamhusu yeye. Lakini katika Kigiriki, jina Yesu halionekani katika mstari huo, na tafsiri nyingine hazilitii ndani. (5) Katika andiko la Ufunuo 22:13, Alfa na Omega pia anasemwa kuwa “wa kwanza na wa mwisho,” maneno yanayotumiwa kumhusu Yesu katika Ufunuo 1:17, 18. Vivyo hivyo, neno “mtume” linatumiwa kumhusu Yesu Kristo na pia baadhi ya wafuasi wake. Lakini je, hilo linathibitisha kwamba wao ni mtu yuleyule au wana cheo kinacholingana? (Ebr. 3:1) Kwa hiyo uthibitisho unaonyesha kwamba majina “Alfa na Omega” yanamhusu Mungu Mweza-Yote, ambaye ni Baba, wala si Mwana.
Mwokozi: Tena na tena, Maandiko yanamwita Mungu kuwa Mwokozi. Katika Isaya 43:11 Mungu hata husema: “Zaidi yangu mimi hapana mwokozi.” Kwa kuwa Yesu pia anaitwa Mwokozi, je, Mungu na Yesu ni mtu mmoja? Sivyo kabisa. Tito 1:3, 4 husema kuhusu “Mwokozi wetu Mungu,” na kisha kuhusu wote wawili “Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Mwokozi wetu.” Kwa hiyo, hao watu wawili ni waokozi. Andiko la Yuda 25 linaonyesha uhusiano huo, likisema, “Mungu pekee, Mwokozi wetu kwa Yesu Kristo Bwana wetu.” (Italiki zimeongezwa.) (Ona pia Matendo 13:23.) Katika andiko la Waamuzi 3:9, neno lilelile la Kiebrania (moh·shiʹa, lililotafsiriwa “mwokozi” au “mkombozi”) linalotumiwa katika Isaya 43:11 limetumiwa kumhusu Othnieli, mwamuzi katika Israeli, lakini je, hilo lilimfanya Othnieli awe Yehova? Kusoma Isaya 43:1-12 kunaonyesha kwamba mstari wa 11 humaanisha kwamba Yehova pekee Ndiye aliyeandaa wokovu, au ukombozi, kwa ajili ya Israeli; wokovu huo haukuja kutoka kwa yeyote kati ya miungu ya mataifa jirani.
Mungu: Katika andiko la Isaya 43:10 Yehova anasema: “Kabla yangu hakuumbwa Mungu awaye yote, wala baada yangu mimi hatakuwapo mwingine.” Je, hilo linamaanisha kwamba, kwa sababu katika unabii Yesu Kristo anaitwa “Mungu mwenye nguvu” katika Isaya 9:6, ni lazima Yesu awe Yehova? Tena, muktadha unajibu, Hapana! Hakuna lolote la mataifa yenye kuabudu sanamu yaliyofanyiza mungu kabla ya Yehova, kwa sababu hakuna yeyote aliyekuwako kabla ya Yehova. Wala hawangeweza kufanyiza mungu yeyote halisi wakati ujao, ambaye angeweza kutoa unabii. (Isa. 46:9, 10) Lakini hilo halimaanishi kwamba Yehova hakufanyiza kamwe yeyote ambaye kwa kufaa anatajwa kuwa mungu. (Zab. 82:1, 6; Yoh. 1, 1, NW) Katika andiko la Isaya 10:21 Yehova anaitwa “Mungu, aliye mwenye nguvu” kama vile Yesu anavyoitwa katika Isaya 9:6; lakini ni Yehova pekee anayeitwa “Mungu Mwenyezi.”—Mwa. 17:1.
Ikiwa jina fulani au fungu fulani la maneno linapatikana zaidi ya mahali pamoja katika Maandiko, isiamuliwe haraka-haraka kamwe kwamba ni lazima sikuzote maneno hayo yanamaanisha mtu yuleyule. Kutoa sababu kwa njia hiyo kunaweza kumfanya mtu aamue kwamba Nebukadneza alikuwa Yesu Kristo, kwa sababu wote wawili waliitwa “mfalme wa wafalme” (Dan. 2:37; Ufu. 17:14) na kwamba wanafunzi wa Yesu kwa hakika walikuwa ni Yesu Kristo, kwa sababu hao na pia Yesu waliitwa “nuru ya ulimwengu.” (Mt. 5:14; Yoh. 8:12) Sikuzote tunapaswa kuchunguza muktadha na maandiko mengine katika Biblia ambapo maneno hayohayo hupatikana.
Mafungu kutoka Maandiko ya Kiebrania ambayo yanamhusu Yehova lakini ambayo waandikaji wa Biblia walioongozwa na roho waliyatumia kumhusu Yesu Kristo
Kwa nini andiko la Yohana 1:23 linanukuu Isaya 40:3 na kulitumia kuhusu yale ambayo Yohana Mbatizaji alifanya katika kumtayarishia Yesu Kristo njia, hali andiko la Isaya 40:3 kwa wazi linazungumzia kutayarisha njia mbele za Yehova? Kwa sababu Yesu alimwakilisha Baba yake. Alikuja katika jina la Baba yake naye alihakikishiwa kwamba sikuzote Baba yake alikuwa pamoja naye kwa sababu alifanya mambo yaliyompendeza Baba yake.—Yoh. 5:43; 8:29.
Kwa nini andiko la Waebrania 1:10-12 linanukuu Zaburi 102:25-27 na kuyatumia kumhusu Mwana, hali zaburi hiyo husema kwamba yalielekezwa kwa Mungu? Kwa sababu Mungu alifanya kazi za uumbaji zinazosimuliwa humo na mtunga-zaburi kupitia Mwana. (Ona Wakolosai 1:15, 16; Methali 8:22, 27-30.) Kumbuka kwamba katika Waebrania 1:5b nukuu limetolewa katika 2 Samweli 7:14 na kutumiwa kumhusu Mwana wa Mungu. Ingawa andiko hilo lilimhusu kwanza Sulemani, linapotumiwa baadaye kumhusu Yesu Kristo halimaanishi kwamba Sulemani na Yesu ni mtu mmoja. Yesu ni “mkubwa kuliko Sulemani” naye anafanya kazi iliyofananishwa mapema na ile ya Sulemani.—Luka 11:31.
Maandiko yanayotaja Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu pamoja
Andiko la Mathayo 28:19 na la 2 Wakorintho 13:14 ni mifano ya maandiko hayo. Hakuna moja la maandiko hayo linalosema kwamba Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu wanalingana au wote ni wa milele au kwamba wote ni Mungu. Uthibitisho wa Kimaandiko ambao tayari umetolewa katika ukurasa wa 370-374 unapinga kutia mawazo hayo katika maandiko hayo.
Kichapo Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature cha McClintock na Strong, ingawa kinaunga mkono fundisho la Utatu, kinakubali hivi kuhusu Mathayo 28:18-20: “Hata hivyo, andiko hili likichukuliwa peke yake, halingethibitisha kabisa utu wa wale watu wanaotajwa, wala usawa wala uungu wao.” (chapa ya 1981, Buku la 10, uku. 552) Kuhusu maandiko mengine ambayo pia hutaja hao watatu pamoja, Cyclopedia hii inakubali kwamba, yakichukuliwa peke yake, “hayatoshi” kuthibitisha Utatu. (Linganisha na 1 Timotheo 5:21, ambapo Mungu na Kristo na malaika hutajwa pamoja.)
Maandiko ambamo wingi wa majina hutumiwa kumhusu Mungu katika Maandiko ya Kiebrania
Katika Mwanzo 1:1 jina “Mungu” linatafsiriwa kutoka ’Elo·himʹ, ambalo ni jina la wingi katika Kiebrania. Wana-Utatu huelewa hilo kuwa linamaanisha Utatu. Wao pia husema kwamba andiko la Kumbukumbu la Torati 6:4 linamaanisha watu walio katika Utatu ni mtu mmoja linaposema “BWANA, Mungu [kutoka ’Elo·himʹ] wetu, BWANA ndiye mmoja.”
Wingi wa jina lililotumiwa hapa katika Kiebrania ni wingi wa fahari au utukufu. (Ona NAB, St. Joseph Edition, Bible Dictionary, uku. 330; pia, New Catholic Encyclopedia, 1967, Buku la 5, uku. 287.) Neno hilo halitoi wazo lolote la wingi wa watu katika mungu mmoja. Vivyo hivyo, katika Waamuzi 16:23 wakati Dagoni mungu wa uwongo anapotajwa, jina ’elo·himʹ linatumiwa; kitenzi kinachofuata ni cha umoja, kuonyesha kwamba jina hilo ni la mungu huyo mmoja tu. Katika Mwanzo 42:30, Yosefu anaitwa “bwana” (’adho·nehʹ, wingi wa utukufu) wa Misri.
Lugha ya Kigiriki haina ‘wingi wa fahari au utukufu.’ Kwa hiyo, katika Mwanzo 1:1 watafsiri wa Septuajinti walitumia ho The·osʹ (jina Mungu, katika umoja) kuwa jina linalolingana na ’Elo·himʹ. Katika Marko 12:29, ambapo Yesu anatoa jibu akinukuu Kumbukumbu la Torati 6:4, jina la Kigiriki ho The·osʹ katika umoja limetumiwa vilevile.
Katika Kumbukumbu la Torati 6:4, maandishi ya Kiebrania yana zile Herufi Nne mara mbili, na hivyo yanafaa yaseme hivi: “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.” (NW) Taifa la Israeli, lililoambiwa maneno hayo, halikuamini Utatu. Wababiloni na Wamisri waliabudu miungu ya utatu-utatu, lakini Waisraeli waliambiwa wazi kwamba Yehova ni tofauti.
Maandiko ambayo mtu anaweza kuyaelewa kwa njia kadhaa, ikitegemea tafsiri ya Biblia anayotumia
Ikiwa fungu linaweza kutafsiriwa kisarufi kwa njia zaidi ya moja, tafsiri sahihi ni gani? Ni ile inayopatana na sehemu nyingine za Biblia. Mtu akipuuza sehemu nyingine za Biblia na kutegemeza imani yake juu ya tafsiri anayoipenda zaidi ya mstari fulani, basi yale anayoamini kwa kweli huonyesha, si Neno la Mungu, bali mawazo yake mwenyewe na labda yale ya mwanadamu mwingine asiyekamilika.
UV husema hivi: “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu.” (BHN, VB, NAJ, ZSB hutumia maneno yanayokaribia kufanana na hayo.) Hata hivyo, NW husema hivi: “Hapo mwanzo Neno alikuwako, na Neno alikuwa pamoja na Mungu, na Neno alikuwa mungu. Hapo mwanzo huyo alikuwa pamoja na Mungu.”
Ni tafsiri gani ya Yohana 1:1, 2 inayopatana na mistari inayofuata? Andiko la Yohana 1:18 linasema: “Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wowote.” Mstari wa 14 unasema waziwazi kwamba “Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake.” Pia, mstari wa 1 na 2 husema kwamba hapo Mwanzo yeye alikuwako “kwa Mungu.” Je, mtu anaweza kuwa kwa mtu fulani na wakati huohuo awe ndiye mtu huyo? Katika Yohana 17:3, Yesu anamwita Baba “Mungu wa pekee wa kweli”; kwa hiyo, Yesu akiwa “mungu” huonyesha tu sifa za kimungu za Baba yake.—Ebr. 1:3.
Je, tafsiri “mungu” inapatana na kanuni za sarufi ya Kigiriki? Vitabu fulani vya marejeo hudai kwa nguvu kwamba maandishi ya Kigiriki lazima yatafsiriwe, “Neno alikuwa Mungu.” Lakini si wote wanaokubali hivyo. Katika makala yake “Qualitative Anarthrous Predicate Nouns: Mark 15:39 and John 1:1,” Philip B. Harner alisema kwamba vifungu kama kile katika Yohana 1:1, vyenye “maneno yasiyo na kibainishi yanayotangulia kitenzi, kwa msingi vinaonyesha sifa. Vinaonyesha kwamba logos ni kama theos.” Yeye anapendekeza hivi: “Labda kifungu hicho kinaweza kutafsiriwa, ‘Neno alikuwa kama Mungu.’” (Journal of Biblical Literature, 1973, uku. 85, 87) Kwa hiyo, ni jambo muhimu kwamba katika andiko hilo, katika sentensi ya Kigiriki, jina la pili the·os halina kibainishi (ho) na limewekwa kabla ya kitenzi. Kwa kupendeza, watafsiri wanaoshikilia kwamba andiko la Yohana 1:1 litafsiriwe “Neno alikuwa Mungu,” hawasiti kutumia kibainishi kisicho dhahiri wanapotafsiri mafungu mengine yenye maneno ya jina la umoja lisilo na kibainishi linalotukia kabla ya kitenzi. Kwa hiyo, katika andiko la Yohana 6:70, UV na ZSB zote humwita Yuda Iskariote “shetani” na katika Yohana 9:17 zinamwita Yesu “nabii.”
John L. McKenzie, S.J., anasema hivi katika Dictionary of the Bible: “Andiko la Yohana 1:1 linapaswa kutafsiriwa kabisa ‘neno alikuwa pamoja na Mungu [= Baba], na neno alikuwa wa kimungu.’”—(Mabano ni yake. Kilichapishwa kwa idhini ya haki ya uchapishaji ya Kikatoliki.)—(New York, 1965), uku. 317.
Kupatana na yaliyo juu, AT husema hivi: “Neno alikuwa wa kimungu”; Mo, “Logos alikuwa wa kimungu”; NTIV, “neno alikuwa mungu.” Katika tafsiri yake ya Kijerumani Ludwig Thimme anatafsiri hivi: “Neno alikuwa Mungu wa namna fulani.” Kumwita Neno (aliyekuja kuwa Yesu Kristo) “mungu” kunapatana na matumizi ya neno hilo katika sehemu nyingine za Maandiko. Kwa mfano, katika Zaburi 82:1-6 waamuzi wanadamu katika Israeli waliitwa “miungu” (Kiebrania, ’elo·himʹ; Kigiriki, the·oiʹ, katika Yohana 10:34) kwa sababu walikuwa wawakilishi wa Yehova nao walipaswa kusema sheria yake.
Ona pia nyongeza ya NW, chapa ya Marejeo ya 1984, uku. 1579.
UV husema hivi: “Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Yeye Ibrahimu asijakuwako, mimi niko [Kigiriki, e·goʹ ei·miʹ].” (ZSB, BHN zote zinasema “mimi niko,” na hata nyingine, kama VB, husema “Ndimi Niliye,” kwa kutumia herufi kubwa ili kutoa wazo la jina. Kwa hiyo zinajaribu kuhusisha maneno hayo na andiko la Kutoka 3:14, ambapo, kulingana na tafsiri yao, Mungu anajiita “MIMI NIKO.”) Hata hivyo, katika NW sehemu hiyo ya mwisho ya Yohana 8:58 husema: “Kabla ya Abrahamu kuwako, mimi nimekuwako.” (Wazo hilohilo linatolewa na maneno katika AT, Mo, CBW, na SE.)
Ni tafsiri gani inayokubaliana na mistari mingine iliyo karibu? Swali la Wayahudi (mstari wa 57) ambalo Yesu alikuwa akijibu lilihusu umri, si utambulisho. Kupatana na akili, jibu la Yesu lilishughulika na umri wake, muda wa kuwako kwake. Jambo linalopasa kuzingatiwa ni kwamba neno e·goʹ ei·miʹ halitumiwi kamwe kuwa jina la roho takatifu.
Kichapo A Grammar of the Greek New Testament in the Light of Historical Research, cha A. T. Robertson kinasema hivi: “Sawa na vitenzi vingine, mara nyingine kitenzi [ei·miʹ] hurejelea kuwako, kama ilivyo katika neno [e·goʹ ei·miʹ] (Yoh. 8:58).”—Nashville, Tenn.; 1934, uku. 394.
Ona pia nyongeza ya NW, chapa ya Marejeo ya 1984, uku. 1582, 1583.
UV husema hivi: “Jitunzeni nafsi zenu, na lile kundi lote nalo, ambalo Roho Mtakatifu amewaweka ninyi kuwa waangalizi ndani yake, mpate kulilisha kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe.” (ZSB, VB zinatumia maneno kama hayo.) Hata hivyo, katika NW sehemu ya mwisho ya mstari huo husema hivi: “damu ya Mwana wake mwenyewe.” (NAJ, BHN hutumia maneno kama hayo. Ijapokuwa chapa ya 1953 ya RS husema “kwa damu yake mwenyewe,” chapa ya 1971 husema “kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.”)
Ni tafsiri gani inayokubaliana na andiko la 1 Yohana 1:7, linalosema: “Damu yake Yesu, Mwana wake [wa Mungu], yatusafisha dhambi yote”? (Ona pia Ufunuo 1:4-6.) Kama ilivyoandikwa katika Yohana 3:16, je, Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee, au je, yeye mwenyewe alikuja akiwa mwanadamu, ili tupate uzima? Damu iliyomwagwa si ya Mungu bali ni ya Mwana wake.
Ona pia nyongeza ya NW, chapa ya Marejeo ya 1984, uku. 1580.
UV husema hivi: “Ambao mababu ni wao, na katika hawa alitoka Kristo kwa jinsi ya mwili. Ndiye aliye juu ya mambo yote, Mungu, mwenye kuhimidiwa milele. Amina.” (ZSB, VB husema sawa na hivyo.) Hata hivyo, katika NW sehemu ya mwisho ya mstari huo husema hivi: “ambao Kristo alitoka kwao kulingana na mwili: Mungu, aliye juu ya wote, abarikiwe milele. Amina.” (BHN hutumia maneno yanayofanana na NW.)
Je, mstari huo unasema kwamba Kristo yuko “juu ya mambo yote” na kwa hiyo yeye ni Mungu? Au je, unaonyesha kwamba Mungu na Kristo ni watu mbalimbali na kusema kwamba Mungu yuko “juu ya mambo yote”? Ni tafsiri gani ya Waroma 9:5 inayokubaliana na Waroma 15:5, 6, ambayo kwanza humtofautisha Mungu na Kristo Yesu, kisha humsihi msomaji “kumtukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo”? (Ona pia 2 Wakorintho 1:3 na Waefeso 1:3.) Fikiria yanayofuata katika Waroma sura ya 9. Mstari wa 6-13 huonyesha kwamba kutimizwa kwa kusudi la Mungu hakutegemei urithi kulingana na mwili bali mapenzi ya Mungu. Mstari wa 14-18 hutaja ujumbe wa Mungu kwa Farao, kama ulivyoandikwa katika Kutoka 9:16, ili kukazia kwamba Mungu yuko juu ya wote. Katika mstari wa 19-24 ukuu wa Mungu unaonyeshwa zaidi kwa kutumia mfano wa mfinyanzi na vyombo vya udongo anavyotengeneza. Basi, maneno haya yanafaa kama nini katika mstari wa 5: “Mungu, aliye juu ya wote, abarikiwe milele. Amina”!—NW.
The New International Dictionary of New Testament Theology hueleza hivi: “Andiko la Waroma 9:5 hubishaniwa. . . . Ingekuwa rahisi, na ingewezekana kabisa kisarufi kuyatumia maneno hayo kumhusu Kristo. Ndipo mstari huo ungesema hivi, ‘Kristo aliye Mungu juu ya wote, abarikiwe milele. Amina.’ Hata hivyo, Kristo hangelinganishwa kabisa na Mungu, bali angesimuliwa tu kuwa wa kimungu, kwa maana neno hili theos halina kibainishi. . . . Maelezo yanayofaa zaidi ni kwamba maneno hayo ni sifa inayoelekezwa kwa Mungu.”—(Grand Rapids, Mich.; 1976), kilichotafsiriwa kutoka Kijerumani, Buku la 2, uku. 80.
Ona pia nyongeza ya NW, chapa ya Marejeo ya 1984, uku. 1580, 1581.
UV husema hivi: “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho.” (VB inasema sawa na hivyo. BHN husema hivi: “hakufikiri kwamba kule kuwa sawa na Mungu ni kitu cha kung’ang’ania kwa nguvu.”) Hata hivyo, katika NW sehemu ya mwisho ya fungu hilo husema hivi: “ambaye, ingawa alikuwa katika umbo la Mungu, hakufikiria kufanya unyakuzi [Kigiriki, har·pag·monʹ], yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu.”)
Ni wazo gani linalokubaliana na muktadha? Mstari wa 5 huwashauri Wakristo wamwige Kristo katika jambo linalozungumziwa hapa. Je, wangesihiwa wafikirie kwamba wana haki ya “kung’ang’ania kwa nguvu” ili “kuwa sawa na Mungu”? Bila shaka sivyo! Hata hivyo, wanaweza kumwiga yule ambaye “hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu.” (NW) (Linganisha na Mwanzo 3:5.) Tafsiri hiyo inakubaliana pia na Yesu Kristo mwenyewe, aliyesema: “Baba ni mkuu kuliko mimi.”—Yoh. 14:28.
The Expositor’s Greek Testament husema: “Hatuoni fungu lolote ambapo neno [har·paʹzo] au maneno mengine yoyote yanayotokana nalo [kutia ndani har·pag·monʹ] lina maana ya ‘kuhifadhi,’ ‘kutunza’. Nyakati zote linaonekana kumaanisha ‘kupokonya,’ ‘kunyakua kwa nguvu’. Kwa hiyo hairuhusiki kuacha maana hii ya kweli ‘kukamata’ na kuingia katika ile iliyo tofauti kabisa, ‘kushikamana.’”—(Grand Rapids, Mich.; 1967), kilichohaririwa na W. Robertson Nicoll, Buku la 3, uku. 436, 437.
UV husema hivi: “Katika yeye [Kristo] unakaa utimilifu wote wa Mungu [Kigiriki, the·oʹte·tos], kwa jinsi ya kimwili.” (Wazo kama hilo linatolewa na tafsiri zilizo katika ZSB, VB, BHN.) Hata hivyo, NW husema hivi: “Ni katika yeye kwamba ujazo wote wa sifa ya Mungu hukaa kimwili.” (NAJ husema “ukamilifu wote wa kimungu,” badala ya “utimilifu wa Mungu.” Linganisha na 2 Petro 1:4.)
Ni wazi kwamba si kila mtu anayetoa tafsiri ileile ya Wakolosai 2:9. Lakini ni jambo gani linalokubaliana na sehemu nyingine za barua hiyo iliyoongozwa na roho ambayo Wakolosai waliandikiwa? Je, Kristo alikuwa na jambo fulani ndani yake mwenyewe lililo lake kwa sababu yeye ni Mungu, sehemu ya Utatu? Au je, “ujazo” unaokaa ndani yake ni kitu ambacho kilikuja kuwa chake kwa sababu ya uamuzi wa mtu mwingine? Andiko la Wakolosai 1:19 (UV, VB) linasema kwamba utimilifu wote hukaa katika Kristo kwa sababu “Mungu ametaka” iwe hivyo. BHN husema kwamba “Mungu alipenda.”
Fikiria mistari inayotangulia andiko la Wakolosai 2:9: Katika mstari wa 8, wasomaji wanaonywa wasipotoshwe na wale wanaotetea falsafa na mapokeo ya wanadamu. Pia wanaambiwa kwamba ndani ya Kristo “hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika” nao wanasihiwa ‘waenende katika yeye’ na kuwa ‘wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; wamefanywa imara kwa imani.’ (Mstari wa 3, 6, 7) “Utimilifu” wenye thamani unakaa ndani yake, wala si ndani ya waanzilishi au walimu wa falsafa ya wanadamu. Je, katika andiko hilo mtume Paulo alikuwa akisema kwamba “utimilifu” uliokuwa ndani ya Kristo ulimfanya Kristo awe Mungu mwenyewe? Sivyo kulingana na Wakolosai 3:1, ambapo Kristo husemwa kuwa “ameketi mkono wa kuume wa Mungu.”—Ona UV, BHN, VB, NAJ, ZSB.
Kulingana na Greek-English Lexicon, ya Liddell na Scott, neno the·oʹtes (jina linalotokeza the·oʹte·tos) humaanisha “uungu, asili ya kimungu.” (Oxford, 1968, uku. 792) Kwa kweli “uungu,” au kuwa wa “asili ya kimungu,” hakumfanyi Yesu Mwana wa Mungu awe sawa na awe wa umilele kama Baba, kama vile ambavyo wanadamu wote kushiriki “ubinadamu” au “asili ya kibinadamu” hakumaanishi kwamba wanalingana na wote ni wa umri mmoja.
UV husema hivi: “Tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo wetu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu.” (Maneno kama hayo yanapatikana katika ZSB, VB, BHN, NAJ.) Hata hivyo, NW husema hivi: “tukilingojea tumaini la furaha na kufunuliwa kwenye utukufu kwa Mungu mkuu na kwa Mwokozi wetu, Kristo Yesu.”
Ni tafsiri gani inayokubaliana na Tito 1:4, linalosema “Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Mwokozi wetu”? Ijapokuwa Maandiko pia humwita Mungu kuwa Mwokozi, andiko hili linaonyesha tofauti iliyo wazi kati ya yeye na Kristo Yesu, yule ambaye Mungu huandaa wokovu kupitia yeye.
Wengine hudai kwamba andiko la Tito 2:13 huonyesha kwamba Kristo ni Mungu na pia Mwokozi. Kwa kupendeza, UV, BHN, VB, ZSB hutafsiri Tito 2:13 kwa njia ambayo huenda ikaeleweka kwamba inaruhusu maoni hayo, lakini hazifuati kanuni ileile zinapotafsiri 2 Wathesalonike 1:12. Henry Alford, katika The Greek Testament, asema hivi: “Maoni yangu ni kwamba [tafsiri inayotofautisha waziwazi Mungu na Kristo, katika Tito 2:13] hutosheleza matakwa yote ya kisarufi ya sentensi hiyo: kwamba kulingana na muundo na pia muktadha inaelekea zaidi kuwa hivyo, na inakubaliana zaidi na njia ya kuandika ya Mtume.”—(Boston, 1877), Buku la 3, uku. 421.
Ona pia nyongeza ya NW, chapa ya Marejeo ya 1984, uku. 1581, 1582.
NAJ husema hivi: “Lakini kuhusu Mwana, anasema; ‘Kiti chako cha enzi, Wewe Mungu, kitadumu milele na milele.” (UV, ZSB, VB, BHN zina tafsiri zinazofanana na hiyo.) Hata hivyo, NW husema hivi: “Lakini kumhusu Mwana: ‘Mungu ni kiti chako cha ufalme milele na milele.’”
Ni tafsiri gani inayopatana na mistari iliyo karibu? Mistari inayotangulia husema kwamba Mungu ndiye anayesema, si kwamba yeye ndiye anayeambiwa; na mstari unaofuata unatumia maneno “Mungu, Mungu wako,” kuonyesha kwamba yeye anayeambiwa siye Mungu Aliye Juu Zaidi bali ni mwabudu wa Mungu huyo. Andiko la Waebrania 1:8 linanukuu Zaburi 45:6, ambalo hapo mwanzo lilielekezwa kwa mfalme wa kibinadamu wa Israeli. Kwa wazi, mwandikaji wa Biblia wa Zaburi hiyo hakufikiri kwamba mfalme huyo wa kibinadamu alikuwa ni Mungu Mweza-Yote. Badala yake, Zaburi 45:6, katika BHN, husema “Kiti chako cha enzi chadumu milele kama cha Mungu.” Sulemani, ambaye labda ndiye mfalme ambaye hapo kwanza alizungumziwa katika Zaburi 45, alisemwa kuwa ameketi “juu ya kiti cha ufalme cha Yehova.” (1 Nya. 29:23, NW) Kupatana na uhakika wa kwamba Mungu ndiye “kiti cha ufalme,” au Chanzo na Mtegemezaji wa ufalme wa Kristo, Danieli 7:13, 14 na Luka 1:32 huonyesha kwamba Mungu humpa yeye mamlaka hiyo.
Andiko la Waebrania 1:8, 9 linanukuu Zaburi 45:6, 7, ambayo msomi wa Biblia B. F. Westcott anasema hivi kuihusu: “Septuajinti inakubali tafsiri mbili: neno [ho the·osʹ] linaweza kuchukuliwa kuwa linamaanisha mtu anayeambiwa katika visa vyote viwili (kiti chako cha enzi, Mungu, . . . kwa hiyo MUNGU, Mungu wako . . . ) au linaweza kuchukuliwa kuwa mtu anayesema (au mtu anayezungumziwa) katika kisa cha kwanza (Mungu ni kiti Chako cha enzi, au Kiti chako cha enzi ni Mungu . . . ), na katika usawa na [ho the·osʹ sou] katika kisa cha pili (Kwa hiyo Mungu, hata Mungu Wako . . . ). . . . Haiwezekani kabisa kwamba neno [’Elo·himʹ] katika maandishi ya kwanza linaweza kuelekezwa kwa mfalme. Basi ukweli ni kinyume cha ile imani kwamba neno [ho the·osʹ] linamaanisha yule anayezungumziwa katika Septuajinti. Kwa ujumla inaonekana inafaa zaidi kufuata katika fungu la kwanza tafsiri hii: Mungu ni kiti Chako cha ufalme (au, kiti Chako cha ufalme ni Mungu), yaani ‘Mungu, Mwamba imara, ndiye msingi wa kiti chako.’”—The Epistle to the Hebrews (London, 1889), uku. 25, 26.
UV husema hivi: “Kwa maana wako watatu washuhudiao [mbinguni, Baba, na Neno, na Roho Mtakatifu, na watatu hawa ni umoja. Kisha wako watatu washuhudiao duniani], Roho, na maji, na damu; na watatu hawa hupatana kwa habari moja.” (ZSB, VB (5:7, 8) pia zina fungu hilo la Utatu.) Hata hivyo, NW haina maneno “mbinguni, Baba, na Neno, na Roho Mtakatifu, na watatu hawa ni umoja. Kisha wako watatu washuhudiao duniani.” (BHN, NAJ pia hazina fungu hilo la Utatu.)
Kuhusu fungu hilo la Utatu, mchambuzi wa maandishi F. H. A. Scrivener aliandika: “Hatusiti kutangaza usadikisho wetu kwamba maneno hayo yanayobishaniwa hayakuandikwa na Mtakatifu Yohana: kwamba hapo kwanza yaliingizwa katika nakala za Kilatini katika Afrika kutoka pembeni, ambapo yalikuwa yamewekwa kama nyongeza isiyo ya kweli katika mstari wa 8: kwamba kutoka Kilatini yaliingia kisiri katika vitabu viwili au vitatu vya Kigiriki vya baadaye, na kisha katika maandishi ya Kigiriki yaliyochapwa, mahali ambapo hayakuwa na haki ya kuwapo.”—A Plain Introduction to the Criticism of the New Testament (Cambridge, 1883, chapa ya tatu), uku. 654.
Ona pia nyongeza ya NW, chapa ya Marejeo ya 1984, uku. 1580.
Maandiko mengine ambayo Wana-Utatu husema yana habari zinazounga mkono fundisho lao
Ona kwamba andiko la kwanza kati ya hayo humtaja Mwana peke yake; lingine humtaja Baba na pia Mwana; hakuna linalomtaja Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu na kusema kwamba wao ni Mungu mmoja.
Kutokana na yale aliyosema katika andiko hili, je, Yesu alimaanisha kwamba angejifufua mwenyewe kutoka kwa wafu? Je, hilo linamaanisha kwamba Yesu ni Mungu, kwa sababu andiko la Matendo 2:32 linasema, “Yesu huyo Mungu alimfufua”? Sivyo hata kidogo. Maoni hayo yangepingana na andiko la Wagalatia 1:1, linalosema kwamba Baba ndiye aliyemfufua Yesu, wala si Mwana. Akitumia maneno kama hayo, Yesu ananukuliwa katika andiko la Luka 8:48 akimwambia hivi mwanamke mmoja: “Imani yako imekuponya.” Je, mwanamke huyo alijiponya mwenyewe? Sivyo; ni nguvu kutoka kwa Mungu ndizo zilizomponya kwa sababu alikuwa na imani. (Luka 8:46; Mdo. 10:38) Vivyo hivyo, kwa utii wake mkamilifu akiwa mwanadamu, Yesu aliandaa msingi wa kiadili kwa ajili ya Baba kumfufua kutoka kwa wafu, hivyo akimkiri Yesu kuwa Mwana wa Mungu. Kwa sababu Yesu aliishi maisha ya uaminifu, ingeweza kusemwa kwa kufaa kwamba Yesu mwenyewe alikuwa na daraka kwa ajili ya kufufuliwa kwake.
A. T. Robertson anasema katika Word Pictures in the New Testament: “Kumbuka andiko la [Yohana] 2:19 ambapo Yesu alisema: ‘Nami katika siku tatu nitalisimamisha.’ Yeye hakumaanisha kwamba atajifufua mwenyewe kutoka kwa wafu bila kumtegemea Baba akiwa mfufuaji. (Rom. 8:11).”—(New York, 1932), Buku la 5, uku. 183.
Wakati aliposema, “Mimi na Baba tu umoja,” je, Yesu alimaanisha kwamba wanalingana? Wana-Utatu fulani husema kwamba alimaanisha hivyo. Lakini katika andiko la Yohana 17:21, 22, Yesu alisali hivi kuhusu wafuasi wake: “Wote wawe na umoja,” na kuongezea, “ili wawe na umoja kama sisi tulivyo umoja.” Alitumia neno lilelile la Kigiriki (hen) kwa ajili ya “umoja” katika visa hivyo vyote. Kwa wazi, wanafunzi wa Yesu hawawi wote sehemu ya Utatu. Bali wanakuwa na umoja wa kusudi pamoja na Baba na Mwana, umoja uleule unaomuunganisha Mungu na Kristo.
Wale wanaoshikilia fundisho la Utatu wanajiweka katika hali gani?
Wanajiweka katika hatari kubwa. Uthibitisho unaonyesha waziwazi kwamba fundisho la Utatu halipatikani katika Biblia, wala halipatani na yale ambayo Biblia hufundisha. (Ona kurasa zilizotangulia.) Fundisho hilo linapotosha kabisa ukweli kumhusu Mungu wa kweli. Yesu Kristo alisema: “Saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Yoh. 4:23, 24, UV) Kwa hiyo Yesu alionyesha wazi kwamba wale ambao ibada yao si ‘katika kweli,’ ambayo haipatani na kweli iliyoandikwa katika Neno la Mungu mwenyewe, wao si ‘waabudu halisi.’ Yesu aliwaambia hivi viongozi wa kidini Wayahudi wa karne ya kwanza: “Mkalitangua neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu. Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.” (Mt. 15:6-9, UV) Jambo hilo linawahusu vivyo hivyo washiriki wa Jumuiya ya Wakristo leo ambao huunga mkono mapokeo ya wanadamu badala ya kweli zilizo wazi za Biblia.
Kuhusu Utatu, ile Imani ya Athanasia (katika Kiingereza) husema kwamba washiriki wake “hawawezi kufahamika.” Walimu wa fundisho hilo mara nyingi husema kwamba ni “fumbo.” Kwa wazi Mungu huyo wa Utatu si yule ambaye Yesu alimaanisha aliposema: “Sisi tunaabudu tukijuacho.” (Yoh. 4:22, UV) Je, wewe kweli unamjua Mungu unayemwabudu?
Kila mmoja wetu anakabiliwa na maswali mazito: Je, tunaipenda kweli kwa moyo mnyoofu? Je, kweli tunataka uhusiano unaokubaliwa pamoja na Mungu? Si kila mtu anayeipenda kweli kwa moyo mnyoofu. Wengi wanatanguliza kupata kibali cha watu wao wa ukoo na washiriki wao badala ya kupenda kweli na kumpenda Mungu. (2 The. 2:9-12; Yoh. 5:39-44) Lakini, kama Yesu alivyosema katika sala kwa Baba yake wa mbinguni: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yoh. 17:3, NW) Na andiko la Zaburi 144:15 husema kikweli hivi: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—NW.
Mtu Akisema—
‘Unaamini Utatu?’
Unaweza kujibu hivi: ‘Watu wengi sana huamini fundisho hilo leo. Lakini unajua kwamba Yesu na wanafunzi wake hawakufundisha Utatu? Kwa hiyo, sisi tunamwabudu Yule ambaye Yesu alisema tumwabudu.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Yesu alipokuwa akifundisha, hii ndiyo amri aliyosema ni kuu kuliko zote . . . (Marko 12:28-30).’ (2) ‘Yesu hakudai kamwe kwamba yeye ni sawa na Mungu. Alisema . . . (Yoh. 14:28).’ (3) ‘Basi, fundisho la Utatu lilitoka wapi? Ona yale ambayo ensaiklopedia mashuhuri zinasema kuhusu jambo hilo. (Ona ukurasa wa 367, 368.)’
Au unaweza kusema: ‘Hapana, mimi siamini fundisho hilo. Kumbuka kwamba kuna maandiko ya Biblia ambayo siwezi kuyapatanisha kamwe na fundisho hilo. Moja la maandiko hayo ni hili. (Mt. 24:36) Labda unaweza kunieleza.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Ikiwa Mwana analingana na Baba, kwa nini Baba anajua mambo fulani ambayo Mwana hajui?’ Wakijibu kwamba hali ilikuwa hivyo tu kuhusu hali yake ya kibinadamu, ndipo uliza hivi: (2) ‘Lakini kwa nini roho takatifu haijui?’ (Mtu huyo akionyesha kuipenda kweli kwa moyo mnyoofu, mwonyeshe yale ambayo Maandiko yanasema kumhusu Mungu. [Zab. 83:18; Yoh. 4:23, 24])
Pia unaweza kusema: ‘Sisi tunamwamini Yesu Kristo lakini hatuamini Utatu. Kwa nini? Kwa sababu tunaamini yale ambayo mtume Petro aliamini kumhusu Kristo. Ona yale aliyosema . . . (Mt. 16:15-17).’
Pendekezo lingine: ‘Nimeona kwamba watu wanaposema kuhusu Utatu, wana maoni mbalimbali kuhusu fundisho hilo. Labda ninaweza kulijibu swali lako vizuri zaidi nikijua unachomaanisha.’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Asante kwa maelezo hayo. Lakini mambo ninayoamini ni yale tu ambayo Biblia hufundisha. Je, umewahi kuona neno “Utatu” katika Biblia? . . . (Rejelea konkodansi katika Biblia yako.) Lakini je, Kristo anatajwa katika Biblia? . . . Ndiyo, nasi tunamwamini. Ona hapa katika konkodansi chini ya “Kristo” kwamba mojawapo ya marejeo ni andiko la Mathayo 16:16. (Lisome.) Hilo ndilo ninaloamini.’
Au unaweza kujibu hivi: (ikiwa mtu anataja kihususa andiko la Yohana 1:1): ‘Naujua mstari huo. Tafsiri fulani za Biblia husema kwamba Yesu ni “Mungu,” na nyingine husema kwamba yeye ni “mungu.” Kwa nini hivyo?’ (1) ‘Je, labda ni kwa sababu mstari unaofuata unasema kwamba yeye alikuwa “pamoja na Mungu”?’ (2) ‘Je, labda pia ni kwa sababu ya yale yanayopatikana hapa katika Yohana 1:18?’ (3) ‘Je, umewahi kujiuliza ikiwa Yesu mwenyewe humwabudu mwingine akiwa Mungu? (Yoh. 20:17)’
‘Je, unaamini kwamba Kristo ni mungu?’
Unaweza kujibu hivi: ‘Ndiyo, bila shaka naamini. Lakini labda maoni yangu ni tofauti na yako unaposema “Kristo ni mungu.”’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Kwa nini nasema hivyo? Katika andiko la Isaya 9:6 Yesu Kristo anaitwa “Mungu Mwenye Nguvu,” lakini Baba yake peke yake ndiye anayeitwa Mungu Mweza-Yote katika Biblia.’ (2) ‘Na ona kwamba katika Yohana 17:3 Yesu anamwita Baba yake kuwa “Mungu wa pekee wa kweli.” Kwa hiyo, Yesu ni mrudisho tu wa utukufu wa Mungu wa kweli.’ (3) ‘Tunapaswa kufanya nini ili tumpendeze Mungu? (Yoh. 4:23, 24)’
-
-
UumbajiKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Uumbaji
Maana: Uumbaji, kama unavyoelezwa katika Biblia, humaanisha kwamba Mungu Mweza-Yote aliubuni na kuutokeza ulimwengu, kutia ndani watu wengine wa kiroho na aina zote za msingi za viumbe vilivyo duniani.
Katika ulimwengu huu wa kisasa, wa kisayansi, je, ni jambo linalopatana na akili kuamini uumbaji?
“Sheria za asili za ulimwengu ni sahihi sana hivi kwamba si vigumu kutengeneza vyombo vya angani viruke mpaka mwezini na tunaweza kupima kwa usahihi safari yake hata kwa sehemu ya sekunde. Lazima sheria hizo ziliwekwa na mtu fulani.”—Akasema Wernher von Braun, aliyehusika sana katika kuwatuma wanaanga wa Marekani mwezini.
Ulimwengu unaoonekana: Ikiwa ungepata saa iliyo sahihi, je, ungekata shauri kwamba ilijitokeza yenyewe kutokana na mavumbi yaliyopulizwa pamoja? Kwa wazi, ilitengenezwa na mtu mwenye akili. Kuna “saa” iliyo ya ajabu hata zaidi. Sayari zilizo katika mfumo wetu wa jua, pia nyota zilizo ulimwenguni, husafiri kwa mwendo sahihi kuliko saa nyingi zilizobuniwa na kutengenezwa na mwanadamu. Galaksi iliyo na mfumo wetu wa jua ina nyota zaidi ya bilioni 100, na wataalamu wa nyota hukadiria kwamba kuna bilioni 100 za galaksi kama hizo ulimwenguni. Ikiwa saa hubuniwa na mtu mwenye akili, je, ulimwengu ulio mkubwa zaidi na mgumu kufahamika haukuhitaji kubuniwa na mtu mwenye akili hata zaidi? Biblia humtaja Mbuni wake kuwa “Mungu wa kweli, Yehova, Muumba wa mbingu na Mkuu anayezitandaza.”—Isa. 42:5; 40:26; Zab. 19:1.
Dunia: Unapovuka jangwa lenye ukame, ikiwa ungefika mahali penye nyumba nzuri sana, iliyo na vifaa mbalimbali na chakula tele, je, ungeamini kwamba ilijitokeza yenyewe baada ya mlipuko fulani? Hapana; ungetambua kwamba mtu fulani mwenye hekima aliijenga. Wanasayansi bado hawajapata uhai katika sayari yoyote ya mfumo wetu wa jua isipokuwa katika dunia hii; uthibitisho uliopo huonyesha kwamba sayari nyingine hazina uhai. Kitabu The Earth kinasema dunia hii ni “ajabu ya ulimwengu, sayari isiyo na kifani.” (New York, 1963, Arthur Beiser, uku. 10) Iko umbali unaofaa kabisa kutoka kwenye jua kwa ajili ya uhai wa kibinadamu, na inasonga kwa mwendo unaofaa kabisa ili isitoke kwenye mzingo wake. Hali ya hewa, ya aina inayopatikana duniani tu, imefanyizwa kwa mchanganyiko unaofaa wa gesi ili kuendeleza uhai. Kwa kustaajabisha, nuru kutoka kwenye jua, kaboni-dioksidi kutoka kwenye hewa, na maji na madini kutoka kwenye udongo wenye rutuba huungana ili kuzalisha chakula kwa ajili ya wakaaji wa dunia. Je, yote hayo yalitokea kwa sababu ya mlipuko fulani angani ambao haukuongozwa na mtu? Jarida Science News hukubali hivi: “Inaonekana kwamba hali hususa na sahihi kama hizo hazingaliweza kutokea zenyewe tu.” (Agosti 24 na 31, 1974, uku. 124) Uamuzi huu wa Biblia unapatana na akili: “Bila shaka, kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.”—Ebr. 3:4.
Ubongo wa binadamu: Kompyuta za kisasa zimetengenezwa baada ya uchunguzi na ufundi mkubwa. ‘Hazikutokea zenyewe tu.’ Namna gani ubongo wa binadamu? Tofauti na ubongo wa mnyama yeyote, ubongo wa mtoto mchanga wa binadamu huongezeka ukubwa mara tatu katika mwaka wake wa kwanza. Jinsi unavyotenda kazi bado ni fumbo kubwa kwa wanasayansi. Wanadamu wana uwezo wa asili wa kujifunza lugha ngumu, kufurahia uzuri, kutunga muziki, kutafakari chanzo na maana ya uhai. Robert White, daktari anayepasua ubongo, alisema: “Sina la kusema ila kukubali kwamba kuna Akili Iliyo Kubwa Zaidi, iliyobuni na kusitawisha uhusiano wa ajabu kati ya akili na ubongo—jambo ambalo mwanadamu hawezi kabisa kulielewa.” (The Reader’s Digest, Septemba 1978, uku. 99) Jambo hilo la ajabu huanza kwa chembe ndogo iliyotungwa katika tumbo la uzazi. Akiwa na ufahamu huo wa ajabu, Daudi mwandikaji wa Biblia alimwambia Yehova: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha. Kazi zako ni za ajabu, kama vile nafsi yangu inavyojua vema.”—Zab. 139:14.
Chembe hai: Chembe hai ndogo mara nyingine hutajwa kuwa namna “rahisi” ya uhai. Lakini mnyama mwenye chembe moja anaweza kukamata chakula, kukimeng’enya, kuondoa taka mwilini, kujijengea nyumba na kujamiiana. Kila chembe ya mwili wa binadamu imefananishwa na jiji lenye kuta, lenye serikali kuu ya kudumisha utaratibu, kiwanda cha kutokeza nishati, viwanda vya kutengeneza protini, mfumo tata wa usafirishaji, na walinzi wa kusimamia kinachoruhusiwa kuingia. Na mwili mmoja wa binadamu umefanyizwa kwa chembe zipatazo trilioni 100. Jinsi yanavyofaa maneno ya Zaburi 104:24: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima”!
Je, wazo la kwamba Mungu alitumia mageuzi ili kufanyiza aina mbalimbali za vitu vilivyo hai linapatana na Biblia?
Mwanzo 1:11, 12 husema kwamba majani na miti vilifanywa vizae kila kimoja “kulingana na aina yake.” Mistari 21, 24, 25 huongeza kwamba Mungu aliumba viumbe vya baharini, viumbe vinavyoruka na wanyama wa nchi kavu, vyote “kulingana na aina yake.” Kwa hiyo, haiwezekani kwamba aina moja ya msingi ingegeuka au kubadilika kuwa aina nyingine.
Katika andiko la Mwanzo 1:26, Mungu alisema hivi kumhusu mwanadamu: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu.” Kwa hiyo mwanadamu alipaswa kuwa na sifa kama za Mungu, wala si tabia zilizositawi kutokana na mnyama. Andiko la Mwanzo 2:7 laongeza hivi: “Na Yehova Mungu akamfanya mtu [si kutokana na kiumbe fulani kilichotangulia kuishi bali] kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai.” Hapa hakuna dokezo la mageuzi, bali, badala yake hilo ni simulizi la uumbaji mpya.
Je, Mungu aliumba mamilioni yote ya namna mbalimbali za viumbe vilivyo duniani leo?
Mwanzo sura ya 1 husema kwamba Mungu aliumba kila kiumbe “kulingana na aina yake.” (Mwa. 1:12, 21, 24, 25) Wakati wa matayarisho kwa ajili ya Gharika ya duniani pote katika siku za Noa, Mungu aliagiza kwamba viumbe vya kila “aina” ya mnyama wa nchi kavu na kiumbe kinachoruka, viingizwe katika safina. (Mwa. 7:2, 3, 14) Kila “aina” inaweza kutokeza viumbe vya aina nyingi mbalimbali. Kwa hiyo, inasemekana kwamba kuna aina mbalimbali za mbwa zaidi ya 400 na aina mbalimbali za farasi zaidi ya 250. Namna zote za wanyama tofauti wanaoweza kuzaana ni “aina” moja tu kulingana na Mwanzo. Vivyo hivyo, namna zote za wanadamu—wa Mashariki, Waafrika, Weupe, wale walio warefu kama vile Wadinka wa Sudan wenye kimo cha futi saba na wale walio wafupi kama Mbilikimo wenye kimo cha futi nne na inchi nne—hutokana na wale watu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa.—Mwa. 1:27, 28; 3:20.
Kwa nini viumbe hai hufanana?
‘Mungu aliviumba vitu vyote.’ (Efe. 3:9) Kwa hiyo kila kitu kilibuniwa na Mbuni Mkuu yuleyule.
“Vitu vyote vilikuja kuwako kupitia kwake [Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, aliyekuwa Yesu Kristo alipokuwa duniani], na bila yeye hakuna hata kitu kimoja kilichokuja kuwako.” (Yoh. 1:3) Kwa hiyo, kulikuwa na Stadi mmoja tu wa Kazi ambaye Yehova alimtumia kutimiza kazi zake za uumbaji.—Met. 8:22, 30, 31.
-