Yehova Awalinda Watu Wake Katika Hangari
HANGARI, iliyoko katikati ya Ulaya, mara nyingi imepata misukosuko ya historia. Watu wayo wameteseka sana, kujapokuwa kutolewa kwao wakfu kwa Bikira Mariamu na kulazimishwa kuwa Wakristo kwa jina katika mwaka wa 1001 na Stephen, mfalme wao wa kwanza.
Kwa muda wa karne zilizopita Hangari ilidhoofishwa na mapigano mengi ya kindani yaliyowezesha mataifa mengine yaishinde kwa kurudia-rudia. Wakazi wa vijiji vizima waliuawa katika mapigano hayo, baadaye mahali pao pakichukuliwa na wageni. Hivyo, wakazi walikuja kuwa mchanganyiko wa watu kutoka mataifa mengi. Kusema kidini, karibu sehemu mbili kwa tatu za wakazi wa nchi hiyo waliendelea kuwa Wakatoliki, ingawa yale Mapinduzi Makubwa yalienea baadaye katika maeneo mengine.
Mwanzo wa Kiasi
Mbegu za kweli ya Biblia zilipandwa mara ya kwanza katika Hangari mwaka wa 1908. Hilo lilifanywa na mwanamke aliyekuwa amejifunza kweli kutoka kwa Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Kwa sababu ya kuhubiri kwake, wengi walianza kupendezwa na habari njema. Muda mfupi baadaye wanaume wawili waliorudi Hangari kutoka United States walieneza habari njema wakati wote wakiwa makolpota (wahubiri wa wakati wote). Kweli ilienea polepole lakini kwa hakika, na matbaa ya kupigia chapa ikafunguliwa katika Kolozsvár.
Ripoti ya kwanza yenye kutegemeka ilipatikana katika 1922, wakati Wanafunzi wa Biblia 67 kutoka majiji kumi walipohudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kazi yao ya kutoa ushahidi ilikuwa na matokeo ya mara moja, ikitokeza upinzani wakati makasisi walipokuwa na uvutano juu ya serikali na vyombo vya habari waizuie kazi ya kuhubiri.
Mashambulio Yaongezeka
Katika 1928, padri Mkatoliki Zoltán Nyisztor alitoa kikaratasi chenye kichwa Millennialist Bible Students. Ndani yacho alidai hivi kuhusu Wanafunzi wa Biblia: “Wao ni wabaya zaidi ya wabolshevisti wekundu [wakomunisti] wanaoshambulia kwa silaha, kwani hawa huongoza vibaya wale wasio na hatia kwa kutumia Biblia kuyaficha madhumuni yao ya kweli. Polisi wa Serikali ya Kifalme ya Hangari wanatazama utendaji wao kwa bidii.”
Wakati huo ndugu mwenye bidii aliyeitwa Josef Kiss aliyazuru makutaniko. Polisi walimfuata kisiri. Katika 1931 alikuwamo nyumbani mwa ndugu mmoja wakati polisi walipomvamia ghafula na kumwamuru aondoke mara hiyo. Ndugu Kiss alipoanza kukusanya vitu vyake, polisi mmoja alimpiga kwa tako la bunduki yake akamtisha hivi: “Harakisha, ama utachomwa kisu!” Ndugu Kiss akatabasamu na kusema: “Basi nitakwenda nyumbani upesi zaidi,” akirejezea tumaini lake la kimbingu akiwa Mkristo aliyepakwa kwa roho.
Askari-jeshi walimfuata Ndugu Kiss hadi kwenye gari-moshi. Alitazamiwa kuwasili kwenye kutaniko la Debrecen katika Juni 20, 1931, lakini hakutokea kamwe. Akina ndugu walikata maneno kwamba maadui wake walimwua, kwamba kwa kweli “alikuwa ameenda nyumbani” kwenye thawabu yake ya kimbingu. Ingawa kazi yake ilikuwa imekomeshwa, wenye mamlaka hawakuweza kamwe kuizima nuru ya kweli.
Mara nyingi ustadi ulitumiwa ili kutoa ushahidi. Kwa kielelezo, katika miaka ya katikati ya 1930 ndugu mmoja alikufa katika Tiszakarád. Wakati huo maziko yaliweza kufanywa tu kwa ruhusa ya maofisa. Akina ndugu waliruhusiwa dakika moja tu kwa sala na dakika moja tu kwa wimbo. Polisi, waliohudhuria maziko hayo wakiwa na bunduki na singe, walipaswa watekeleze hilo. Watu wengi wa mji huo walikuja kwa sababu walikuwa na udadisi juu ya jinsi maziko hayo yangeongozwa.
Ndugu mmoja alisimama kando ya sanduku ya maiti akasali kwa muda wa nusu saa lakini kwa njia ambayo watu walisema hawakuwa kamwe wamesikia jambo kama hilo. “Hata kama mapadri sita wangaliongoza maziko hayo,” wakasema, “yasingekuwa yenye kugusa moyo jinsi hiyo.” Halafu ndugu mwenye sauti nzuri akaanza kuongoza wimbo, lakini polisi mmoja akamwamuru akae kimya. Polisi walikiri baadaye kwamba, ingawa hawakuhisi kustareheka, hawakuweza kuikatiza sala.
Mashambulio yalipoendelea, Lajos Szabó, kasisi mmoja wa Reformed Church, aliandika yafuatayo katika broshua yake ya 1935 Antichrist by the River Tisza: “Lilikuwa wazo la akili nyingi kuwalisha watu na ubolsheviki [ukomunisti] kwa jina la dini . . . Maksi alichukua sura ya Kristo . . . Mpinga Kristo alikuwa hapa akiwa na vazi lake jekundu pamoja na Mashahidi wa Yehova.”
Miaka Mingi Chini ya Marufuku
Katika 1939 kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku kabisa. Kazi hiyo iliitwa utendaji “dhidi ya dini na dhidi ya jamii.” Waadventisti, Wabaptisti, Waevanjeli, na Wapresbiteri walitoa vikaratasi dhidi ya Mashahidi. Lakini Yehova hakuwaacha watu wake, nao walitunzwa na Mashahidi katika nchi nyinginezo. Kwa kuongezea, watu wa Mungu katika Hangari walikuwa na maono mengi ya kuimarisha imani.
Kwa kielelezo, ndugu mmoja alipoleta mfuko unaobebwa mgongoni uliojaa magazeti yetu kutoka Chekoslovakia, ofisa wa forodha aliuliza hivi: “Ni nini kilichomo mfukoni mwako?” Ndugu huyo alijibu hivi kwa unyoofu: “Minara ya Mlinzi.” Kisha ofisa huyo akafanya ishara kwa mkono wake kana kwamba kuonyesha kwamba ndugu huyo alikuwa mwenye wazimu, akamwacha aende zake. Hivyo, chakula cha kiroho kiliwasili kwa usalama katika Hangari.
Lakini, ndugu waliendelea kusumbuliwa. Ndugu wengi zaidi na zaidi walikamatwa na kuwekwa kifungoni kwa vipindi tofauti-tofauti vya wakati. Halafu kikosi cha pekee cha upelelezi kikapewa mgawo wa kuwasaka Mashahidi wa Yehova. Katika 1942, wanaume, wanawake, na watoto walikusanywa na kuingizwa katika mazizi ya farasi na katika shule tupu za Kiyahudi. Baada ya miezi miwili ya kuteswa, walijaribiwa na kuhukumiwa. Baadhi yao walihukumiwa kifungo cha maisha; wengine walipewa kifungo cha miaka 2 hadi 15 gerezani. Ndugu watatu—Dénes Faluvégi, András Bartha, na János Konrád—walihukumiwa kifo kwa kunyongwa, lakini baadaye kifungo hicho kikabadilishwa kuwa kifungo cha maisha. Halafu, ndugu 160 walipelekwa kwenye kambi ya kifo katika Bor. Baada ya kuvuka mpaka, waliambiwa kwamba wasingerudi kamwe wakiwa hai. Kati ya wale Wayahudi 6,000 waliohamishiwa kwenye kambi hiyo, ni 83 tu walioendelea kuwa hai. Hata hivyo, Mashahidi wote walirudi ila wanne.
Baadhi ya Mashahidi wa Yehova walifia imani yao. Kuelekea mwisho wa Vita ya Ulimwengu 2, Wanazi waliwaua ndugu kadhaa. Bertalan Szabó, János Zsondor, na Antal Hónis walipigwa risasi wakafa, na Lajos Deli akanyongwa.—Mathayo 24:9.
Badiliko Zuri Ni la Muda Tu
Baada ya vita ya ulimwengu ya pili, hali ilibadilika tena. Serikali ya muungano iliahidi kutekeleza haki za kibinadamu. Ndugu waliorudi kutoka katika kambi walianza kuhubiri mara moja na kupanga makutaniko kitengenezo. Walihisi kwamba Yehova alikuwa amewapa uhuru ili waweze kulisifu jina lake kuu, si ili wajaribu kukusanya mali za kimwili. Kufikia mwisho wa 1945, kulikuwa wahubiri wa Ufalme wenye kutenda 590. Katika 1947 nyumba kubwa ilinunuliwa ili itumiwe kuwa ofisi ya tawi ya Watch Tower Society, na mkusanyiko wa kwanza wa kitaifa ukafanywa katika jumba la michezo. Hudhurio lilikuwa watu 1,200, na hata reli ya serikali ya Hangari ikapunguza nauli kwa asilimia 50 kwa wale waliokuwa wakisafiri kwenda kwenye mkusanyiko huo.
Hata hivyo, uhuru haukudumu muda mrefu. Upesi, Chama cha Kikomunisti kilianza kutawala, na serikali ikabadilika. Ongezeko la watu wa Yehova lilionwa na serikali hiyo mpya, kwani walikuwa wameongezeka kutoka wahubiri 1,253 katika 1947 hadi 2,307 katika 1950. Katika mwaka huo maofisa wa serikali walianza kuwekea vizuizi kazi ya kuhubiri. Vibali vya kuhubiri vilihitajiwa, lakini serikali ilikataa kuvitoa, na wale walioviomba wakapigwa na Askari wa Serikali. Makala za magazeti ya habari ziliwashutumu Mashahidi daima kuwa ‘mawakili wa mabeberu.’ Kwa ajabu, kabla ya Ukomunisti kuanza kutawala, Mashahidi walikuwa wamepelekwa kwenye kambi za kifungo wakishtakiwa kuwa ‘Wakomunisti wenye kuwaunga mkono Wayahudi.’
Hofu Kuu Yaanza
Katika Novemba 13, 1950, mwangalizi wa tawi na mtafsiri (wawili kati ya wale waliokuwa wamehukumiwa kifo) walikamatwa, pamoja na mwangalizi wa mzunguko wa kwanza. Walipelekwa kwenye lile gereza lenye sifa mbaya la chini ya ardhi kwenye barabara iitwayo 60 Andrássy Street katika Budapest, ili “walainishwe.” Kesi yao ilianza katika Februari 2 mwaka uliofuata. Mwangalizi wa tawi alihukumiwa miaka kumi kifungoni, mtafsiri akahukumiwa miaka tisa, na mwangalizi wa mzunguko miaka minane. Wote watatu walinyang’anywa mali zao. Wakati wa kesi hiyo, waangalizi wa kutaniko wanne zaidi walihukumiwa vifungo vya gerezani kutoka miaka mitano hadi sita kwa mashtaka ya kujaribu kuipindua serikali.
Ndugu hao waliwekwa katika gereza lenye ulinzi mkali, ambapo hawakuweza kupokea barua, vifurushi, wala wageni. Familia zao hazikupata habari zao. Majina yao hayakuweza hata kutajwa na walinzi. Ili kuwatambulisha, kila mmoja alivaa kibandiko cha mbao kilichoangikwa shingoni pake chenye nambari juu yacho. Hata kulikuwa ishara ukutani iliyosomwa hivi: “Msiwalinde wafungwa tu; bali wachukieni pia.”
Mashahidi walifanya kazi kichinichini, lakini kazi ya kuhubiri haikusimama. Mashahidi wengine waliendelea katika mahali pa wale waliofungwa gerezani. Baadaye wale waliochukua mahali pao walikamatwa. Kufikia mwaka 1953, ndugu zaidi ya 500 walikuwa wamejaribiwa na kuhukumiwa kifungo cha gerezani, lakini habari njema hazikuweza kufungwa kwa minyororo. Ni ndugu wachache tu walioamini zile ahadi za walinzi zenye kushawishi wakaridhiana.
Mataraja Maangavu
Katika vuli ya 1956, watu walianza kuasi dhidi ya serikali. Jeshi la Sovieti lilikomesha uasi huo, na Chama cha Kikomunisti kikapata utawala tena.
Mashahidi wote waliokuwa wamefungwa gerezani walikuwa wamewekwa huru, lakini ndugu wachache waliojulikana sana wakarudishwa gerezani kuendelea na vifungo vyao, ingawa wapya hawakuhukumiwa. Mwishoni, katika 1964, hali ikaanza kuwa afadhali. Wenye mamlaka hawakufanya lolote tena kuyakatiza maziko na karamu za harusi. Makusanyiko ya mzunguko yalifanywa misituni. Ingawa baadhi yayo yalikatizwa, hakuna Mashahidi wengine zaidi waliopelekwa gerezani.
Katika 1978 ndugu waangalizi waliruhusiwa wahudhurie mkusanyiko katika Vienna. Pia katika mwaka huo, wenye mamlaka waliahidi kuwapa Mashahidi wa Yehova utambuzi wa kisheria, lakini miaka kumi mingine ikapita kabla ya hilo kutukia kikweli. Katika 1986 mkusanyiko wa wilaya wa kwanza ulifanywa, kwenye Youth Park ya Msitu wa Kamara, wenye mamlaka wakijua juu yao. Hata ishara ikawekwa, ikisema kwamba huo ulikuwa “Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova. Mwaka uliofuata Mkusanyiko “Tumaini Katika Yehova” ulifanywa, na katika 1988 akina ndugu wakafurahia Mkusanyiko “Haki ya Kimungu.”
Huru Hatimaye!
Juni 27, 1989, ilikuwa siku nzuri ajabu, kwani ndio wakati akina ndugu walipopokea hati inayotambua rasmi Shirika la Kidini la Mashahidi wa Yehova katika Hangari. Katika Julai jumba liitwalo Budapest Sports Hall lenye fahari lilikuwa na hudhurio la watu 9,477 kwenye “Ujitoaji Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya. Jumba lilo hilo lilitumiwa kwa ajili ya “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko wa Wilaya katika 1990, na mikusanyiko ilifanywa pia katika majiji mengine makubwa matatu katika Hangari.
Kwa kuwa marufuku ilikuwa imeondolewa kabisa sasa, iliwezekana kupangia mkusanyiko wa kimataifa wa kwanza. Ijapokuwa halihewa mbaya, mkusanyiko ulifanywa huko Népstadion katika Budapest, ambako 40,601 walikutana kufurahia uchangamfu wa upendo wa kidugu. Washiriki wa Baraza Linaloongoza walihudhuria na kuimarisha imani ya akina ndugu kwa hotuba zao, na vitabu na broshua mpya zenye picha za rangi kamili zikatolewa kwenye mkusanyiko huo.
Lile Linalotukia Leo
Sasa chapa za Kihangari za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zinachapishwa wakati uleule na zile za Kiingereza na kwa namna ileile yenye uzuri. Katika 1992, Kitabu-Mwaka kilianza kuchapishwa katika Kihangari. Idadi ya wahubiri wa habari njema iliongezeka upesi kutoka 6,352 katika 1971 hadi 13,136 katika Januari 1993.
Leo, Mashahidi wa Yehova katika Hangari hufurahia uhuru wa dini na kuhubiri kwa uhuru kutoka nyumba kwa nyumba. Kuna makutaniko 205, na watu 27,844 walihudhuria Ukumbusho katika Aprili 17, 1992. Mpaka Majumba ya Ufalme ya kutosha yapatikane, makutaniko yanaendelea kukutana katika shule, majumba ya kitamaduni, makao matupu ya kijeshi, na hata katika ofisi zilizoachwa tupu za Chama cha Kikomunisti. Kufikia 1992, makutaniko kumi yalikuwa yameweka wakfu Majumba ya Ufalme yao yenyewe, na majumba mengine yanaendelea kujengwa.
Muda wote wa mabadiliko na mapinduzi, akina ndugu wameendelea kwa uaminifu kwenye upande wa Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo, na wameendelea kuhubiri. Misukosuko ya nyakati haikuwaangamiza, kwani Yehova amewalinda watu wake katika Hangari.—Mithali 18:10.
[Ramani page 9]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Vienna
AUSTRIA
Budapest
Debrecen
HANGARI
ROMANIA
[Picha katika ukurasa wa 10]
Watu wa Yehova wakiwa wamekusanyika katika Budapest a wamekusanyika katika Budapest