-
Rafiki wa UwongoAmkeni!—2010 | Mei
-
-
Rafiki wa Uwongo
Umekuwa na “rafiki” ambaye mlifahamiana mlipokuwa vijana. Alikufanya ujihisi umekomaa na alikusaidia ukubaliwe na vijana wengine. Ulipohisi umefadhaika, ulimwendea ili upate “kitulizo.” Kwa kweli, umemtegemea chini ya hali nyingi.
Lakini baada ya muda ulitambua kwamba yeye si rafiki mzuri kama ulivyofikiri. Anataka kuwa nawe kila wakati, hata ikiwa hilo litamaanisha kwamba utafukuzwa unapoenda katika maeneo fulani. Na ingawa alikufanya ujihisi umekomaa, alidhuru afya yako. Zaidi ya hilo, ameiba sehemu fulani ya mshahara wako.
Hivi karibuni, umejaribu kuvunja uhusiano wenu, lakini yeye hataki ufanye hivyo. Kwa njia fulani, ni kama amekuwa bwana wako. Unajuta kukutana naye.
HUO ndio uhusiano uliopo kati ya watu wengi na sigara. Baada ya kuvuta sigara kwa miaka 50, mwanamke anayeitwa Earline anasema hivi: “Ilikuwa afadhali kuvuta sigara badala ya kushirikiana na mtu mwingine. Ilinisaidia kuliko rafiki yangu wa karibu, hata nyakati nyingine nilihisi kwamba sigara ndiye rafiki pekee niliyekuwa naye.” Hata hivyo, kama Earline alivyokuja kutambua, sigara ni rafiki wa uwongo na mkatili. Maneno yaliyotajwa hapo juu yanaweza kutumika kumhusu Earline. Tofauti ni kwamba alipojifunza eti kuvuta sigara ni vibaya machoni pa Mungu kwa sababu kunachafua miili ambayo ametupa, aliacha zoea hilo.—2 Wakorintho 7:1.
Mwanamume anayeitwa Frank pia aliamua kuacha kuvuta sigara ili ampendeze Mungu. Lakini siku moja hivi baada ya kumaliza sigara yake ya mwisho, alijikuta akitambaa ndani ya nyumba yake akitafuta vipande vilivyosalia vya sigara. “Hapo ndipo nilipofanya uamuzi,” akasema Frank. “Nilichukizwa kujikuta nimepiga magoti sakafuni huku nikitafuta-tafuta vipande vya sigara kwenye uchafu. Tangu wakati huo sijavuta sigara tena.”
Kwa nini ni vigumu kuacha kuvuta sigara? Wachunguzi wamegundua sababu kadhaa: (1) Vitu vinavyotengenezwa kutokana na tumbaku vinaweza kumfanya mtu awe mraibu kama tu ilivyo na kutumia dawa za kulevya. (2) Mtu anapovuta nikotini, inaingia ndani ya ubongo baada ya sekunde saba tu. (3) Mara nyingi kuvuta sigara huwa sehemu muhimu ya maisha ya mtu kwa kuwa anaivuta anapokula, anapokunywa, anapozungumza, anapotaka kuondoa mfadhaiko, na kadhalika.
Hata hivyo, kama Earline na Frank walivyoonyesha, inawezekana kuacha uraibu huo wenye kudhuru. Ikiwa wewe unavuta sigara lakini ungependa kuacha, huenda kusoma habari zifuatazo kukakusaidia kuanza maisha mapya.
-
-
Imarisha Azimio LakoAmkeni!—2010 | Mei
-
-
Imarisha Azimio Lako
“Jambo muhimu zaidi ambalo huwawezesha watu kuacha kabisa kuvuta sigara ni kujiwekea azimio imara.”—Kitabu “Stop Smoking Now!”
KWA ufupi, ukitaka kuacha kuvuta sigara, unapaswa kuazimia kabisa kuacha. Ni nini kitakachokuchochea kuacha? Fikiria jinsi utakavyofaidika ukiacha kuvuta sigara.
Utaokoa pesa. Kuvuta pakiti moja kwa siku kunaweza kugharimu maelfu ya dola kwa mwaka. “Sikutambua nilikuwa nikipoteza pesa nyingi kwa kutumia tumbaku.”—Gyanu, Nepal.
Utafurahia maisha zaidi. “Nilipoacha kuvuta sigara nilianza kufurahia maisha, nayo yanazidi kuwa bora kila wakati.” (Regina, Afrika Kusini) Watu wanapoacha kuvuta sigara, uwezo wao wa kunusa na kuonja unaboreka, na kwa kawaida wanakuwa na nguvu zaidi na sura yao inapendeza zaidi.
Afya yako inaweza kuwa nzuri zaidi. “Mara moja wanapoacha kuvuta sigara, wanaume na wanawake wa umri wote hupata faida kubwa za afya.”—Vituo vya Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza vya Marekani.
Utajiamini zaidi. “Niliacha kuvuta sigara kwa kuwa sikutaka kutawaliwa na tumbaku. Nilitaka kuudhibiti mwili wangu.”—Henning, Denmark.
Familia yako na marafiki watafaidika. “Kuvuta sigara . . . kunadhuru afya ya wale wanaokuzunguka. . . . Uchunguzi unaonyesha kwamba kila mwaka moshi wa sigara husababisha vifo vya maelfu ya watu ambao si wavutaji kutokana na kansa ya mapafu na magonjwa ya moyo.”—Sosaiti ya Kansa ya Marekani.
Utampendeza Muumba wako. “Wapendwa, . . . acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili.” (2 Wakorintho 7:1) “Mtoe miili yenu . . . [ikiwa] takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu.”—Waroma 12:1.
“Mara tu nilipoelewa kwamba Mungu anashutumu mambo yanayochafua mwili, niliamua kuacha kuvuta sigara.”—Sylvia, Hispania.
Hata hivyo, mara nyingi kuazimia tu hakutoshi. Huenda pia tukahitaji kusaidiwa na watu wengine, kutia ndani watu wa familia na marafiki. Wanaweza kufanya nini?
-
-
Tafuta MsaadaAmkeni!—2010 | Mei
-
-
Tafuta Msaada
“Mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake.”—Mhubiri 4:12.
TUNAPOTEGEMEZWA na wengine, tunaweza kumshinda adui, hata awe nani. Kwa hiyo, ukitaka kushinda zoea la kuvuta sigara, huenda likawa jambo la hekima kuwaomba msaada watu wa familia na marafiki—au mtu yeyote mwenye subira na anayeweza kukusaidia.
Watafute wale ambao wamefaulu kuacha zoea hilo kwa kuwa huenda zaidi ya kuelewa hisia zako, wanaweza kukusaidia. “Msaada wa watu wengine ulikuwa muhimu sana,” anasema Torben, Mkristo huko Denmark. Abraham, anayeishi India, anaandika hivi: “Upendo wa kweli nilioonyeshwa na familia yangu na Wakristo wenzangu ulinisaidia kuacha.” Lakini nyakati nyingine huenda hata msaada wa watu wa familia na marafiki usitoshe.
“Nilivuta sigara kwa miaka 27,” anasema mwanamume anayeitwa Bhagwandas, “lakini nilipojifunza kile ambacho Biblia inasema kuhusu mazoea machafu, niliamua kuacha. Kwa hiyo, nilijaribu kupunguza kiasi cha sigara nilichokuwa nikivuta. Nilibadili marafiki. Nilitafuta msaada wa wataalamu. Lakini sikufaulu. Usiku mmoja nilizungumza na Yehova Mungu katika sala na kumsihi anisaidie kuacha. Mwishowe, nilifaulu!”
Jambo lingine muhimu ni kujitayarisha kwa ajili ya magumu utakayokabili. Magumu hayo ni yapi? Habari inayofuata inaeleza.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
JE, UTUMIE DAWA?
Dawa zinazowasaidia watu waache kuvuta sigara, zinawaletea wafanyabiashara faida ya mabilioni ya dola. Kabla ya kuanza kutumia dawa hizo, fikiria maswali yafuatayo:
Zina faida gani? Inasemekana kuwa matibabu mengi yanamsaidia mtu aache kuvuta sigara kwa kupunguza athari zinazotokea baadaye. Hata hivyo, bado kuna mjadala kuhusu faida zake za kudumu.
Kuna hatari gani? Dawa fulani hutokeza matatizo mengine kama vile kichefuchefu, mshuko wa moyo, na kumfanya mtu awe na mawazo ya kujiua. Pia, kumbuka kwamba dawa zinazotumiwa badala ya nikotini huletea mtu matatizo ya afya. Kwa sababu hiyo, mtu anayetumia dawa hizo za badala anaendeleza uraibu huo.
Je, kuna njia nyingine? Katika uchunguzi mmoja, asilimia 88 ya watu waliofaulu kuacha kuvuta sigara walisema walifanya hivyo bila kutumia dawa zozote.
-
-
Jitayarishe kwa Ajili ya MagumuAmkeni!—2010 | Mei
-
-
Jitayarishe kwa Ajili ya Magumu
“Niliamua kuacha kuvuta sigara ili nisidhuru afya ya mtoto wetu aliyekuwa tu amezaliwa. Kwa hiyo, ndani ya nyumba niliweka ishara inayosema ‘Usivute Sigara.’ Saa moja tu baada ya kufanya hivyo, nilishambuliwa kwa ghafula na hamu ya kutumia nikotini na nikawasha sigara.”—Yoshimitsu, Japani.
KAMA kisa cha Yoshimitsu kinavyoonyesha, kuna magumu ya kuacha kuvuta sigara. Isitoshe, uchunguzi unaonyesha kwamba karibu asilimia 90 ya wale wanaojikwaa hurudia zoea lao. Kwa hiyo, ikiwa unajaribu kuacha, huenda tu ukafaulu ukijitayarisha. Ni magumu gani ambayo hutokea kwa ukawaida?
Hamu ya kutumia nikotini: Kwa kawaida hamu hiyo huwa kubwa zaidi siku tatu baada ya kuacha kuvuta sigara na hupungua baada ya majuma mawili hivi. Katika kipindi hicho, “tamaa hiyo huja kama mawimbi; haiji kila wakati,” anasema mtu mmoja aliyeacha kuvuta sigara. Hata miaka inapopita, huenda ukashikwa na tamaa ya kuvuta sigara. Ikikushika, usivute sigara mara moja. Subiri kwa dakika tano hivi, tamaa hiyo itakwisha.
Dalili nyingine: Mwanzoni, ni vigumu kuwa macho au kukaza fikira na huenda mtu akaongeza uzito kwa urahisi. Huenda pia akapatwa na maumivu ya viungo, akatokwa na jasho, akahisi anataka kujikunakuna, kukohoa, na hisia zake zikabadilika-badilika kama vile kutokuwa na subira, kukasirika kwa urahisi, au hata kushuka moyo. Hata hivyo, dalili nyingi huisha baada ya majuma manne hadi sita.
Wakati huo, kuna mambo fulani yanayoweza kukusaidia. Kwa mfano:
● Lala kwa muda mrefu zaidi.
● Kunywa maji mengi au maji ya matunda. Kula chakula chenye lishe.
● Fanya mazoezi ya kadiri.
● Vuta pumzi kabisa, na uwazie hewa safi ikijaa ndani ya mapafu yako.
Vichochezi: Huu ni utendaji au hisia zinazoweza kuchochea hamu ya kuvuta sigara. Kwa mfano, huenda kwa kawaida ulivuta sigara ulipokuwa ukinywa kinywaji fulani. Kwa hiyo, unapojaribu kuacha kuvuta sigara, epuka kunywa kinywaji hicho polepole. Bila shaka, baada ya muda utafurahia kunywa kinywaji hicho kwa utaratibu.
Hata hivyo, huenda hisia fulani zisiishe hata baada ya mwili wako kupoteza uraibu wa nikotini. “Miaka kumi na tisa baada ya kuacha kuvuta sigara,” anasema Torben, aliyetajwa mapema, “bado ninashikwa na hamu ninapokunywa kahawa.” Hata hivyo, muda unapopita mtu huacha kuhusianisha kuvuta sigara na utendaji fulani hususa.
Hata hivyo, mambo ni tofauti kileo kinapohusika. Kwa kweli, unapojaribu kuacha kuvuta sigara, huenda ukahitaji kuacha kutumia kileo na kuepuka maeneo ambako kinapatikana kwa sababu idadi kubwa ya watu ambao hurudia zoea la kuvuta sigara hufanya hivyo wanapokunywa kileo. Kwa nini?
● Hata kiasi kidogo cha kileo humfanya mtu afurahie nikotini.
● Mara nyingi mahali ambapo watu hunywa pamoja wao pia huvuta sigara.
● Kileo hudhoofisha uwezo wa kuamua mambo na kumfanya mtu atende kwa njia isiyo ya kawaida. Biblia inasema hivi: ‘Divai ndiyo huondoa kusudi jema.’—Hosea 4:11.
Marafiki: Uwe mteuzi. Kwa mfano, epuka watu wanaovuta sigara au wanaoweza kukupa sigara. Pia, waepuke watu wanaojaribu kuvuruga jitihada zako za kuacha kuvuta sigara, labda kwa kukudhihaki.
Hisia: Katika uchunguzi mmoja karibu asilimia 66 ya wale walioanza tena kuvuta sigara walifanya hivyo baada tu ya kufadhaika au kupandwa na hasira. Ukipatwa na hisia fulani inayokuchochea kuvuta sigara, jikengeushe fikira labda kwa kunywa maji, kutafuna chingamu, au kutembea. Jaribu kufikiria mambo yanayofaa, labda kwa kusali kwa Mungu au kusoma kurasa kadhaa za Biblia.—Zaburi 19:14.
Visingizio Unavyopaswa Kuepuka
● Nitavuta mara moja tu.
Ukweli: Kuvuta mara moja tu kunaweza kutosheleza asilimia 50 hivi ya vipokezi vya nikotini kwenye ubongo wako kwa saa tatu. Matokeo yatakuwa kwamba utaanza tena kuvuta sigara.
● Kuvuta sigara hunisaidia kutuliza mfadhaiko.
Ukweli: Uchunguzi unaonyesha kwamba nikotini huongeza kiwango cha homoni zinazomfanya mtu afadhaike. Hisia zozote zinazokudanganya kuwa mfadhaiko wako unapungua unapovuta sigara zinaweza kuwa zinasababishwa tu na athari za kuacha kuvuta sigara.
● Nimekuwa nikivuta sigara kwa muda mrefu sana siwezi kuacha.
Ukweli: Kukazia fikira mambo yasiyofaa huvunja moyo. Biblia inasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Kwa hiyo, usifikirie huwezi kuacha kuvuta sigara. Mtu yeyote ambaye kwa kweli anataka kuacha kuvuta sigara na anayefuata kanuni zinazofaa, kama zile zilizotajwa katika gazeti hili, anaweza kufanikiwa.
● Siwezi kukabiliana na athari zinazosababishwa na kuacha kuvuta sigara.
Ukweli: Ni kweli kwamba athari za kuacha kuvuta sigara zina nguvu, lakini zitapungua baada ya majuma machache tu. Kwa hiyo usife moyo! Ukishikwa na hamu ya kuvuta sigara baada ya miezi au miaka kadhaa, hiyo pia itakwisha, labda hata baada ya dakika chache, ikiwa hutavuta sigara.
● Nina tatizo la akili.
Ukweli: Ikiwa unatibiwa tatizo la akili, kama vile mshuko wa moyo au schizophrenia, mwombe daktari akusaidie uache kuvuta sigara. Bila shaka, atajitahidi kukusaidia labda hata atabadili matibabu yako ili yasiongeze ugonjwa wako au kuathiri dawa unazotumia.
● Ninapoanza tena kuvuta sigara mimi hujihisi bure.
Ukweli: Unapojikwaa na kuanza tena kuvuta sigara, kama watu wengi wanavyofanya wanapojaribu kuacha kuvuta, wewe si bure. Inuka na ujitahidi tena. Kuanguka hakumaanishi umeshindwa. Kukataa kuinuka ndiko kushindwa. Kwa hiyo, endelea kujitahidi. Mwishowe utafanikiwa.
Fikiria mfano wa Romualdo, aliyevuta sigara kwa miaka 26. Aliacha kuvuta sigara zaidi ya miaka 30 iliyopita. Anaandika hivi: “Niliacha kuhesabu mara ambazo nilijikwaa. Kila mara nilijihisi vibaya sana, kana kwamba singeweza kufaulu. Hata hivyo, nilipoazimia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu na kumwomba mara nyingi anisaidie, mwishowe nilifaulu kuacha kuvuta sigara kabisa.”
Katika habari ya mwisho ya mfululizo huu, tutachunguza mapendekezo mengine machache yanayofaa yanayoweza kukusaidia kuwa mwenye furaha unapoacha kuvuta sigara.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]
HATARI HATA ITUMIWE JINSI GANI
Tumbaku inatumiwa katika njia nyingi tofauti-tofauti. Tumbaku fulani huuzwa katika maduka yanayouza dawa na bidhaa zenye vyakula vya kuboresha afya. Hata hivyo, “tumbaku ni hatari hata itumiwe kwa njia gani,” linasema Shirika la Afya Ulimwenguni. Mtu anaweza kufa kutokana na magonjwa yanayosababishwa na tumbaku kama vile, kansa na magonjwa ya moyo. Akina mama waja-wazito wanaovuta sigara wanaweza kuwadhuru watoto wao walio tumboni. Watu hutumia tumbaku za aina gani?
Bidis: Sigara hizo ndogo zilizotengenezwa kwa mkono hutumiwa sana katika nchi za Asia. Mtu anapovuta bidis anapata lami, nikotini, na kaboni monoksidi nyingi zaidi kuliko sigara za kawaida.
Biri: Tumbaku za aina hii husokotwa kwa majani ya tumbaku au karatasi iliyotengenezwa kwa tumbaku. Kwa kulinganisha na asidi ya tumbaku iliyo kwenye sigara, tumbaku iliyo kwenye biri hufanya nikotini iingie kupitia mdomo hata ikiwa biri haijawashwa.
Kreteks, au sigara za karafuu: Kwa kawaida zinakuwa na asilimia 60 hivi ya tumbaku na asilimia 40 ya karafuu. Mtu anapozivuta anapata lami, nikotini, na kaboni monoksidi nyingi zaidi kuliko sigara za kawaida.
Viko: Kuvuta kiko na kuvuta sigara kuna hatari zilezile, kwa kuwa mazoea yote mawili yanaweza kutokeza kansa zilezile na magonjwa mengine.
Tumbaku zisizokuwa na moshi: Hilo linatia ndani kutafuna na kunusa tumbaku, na gutkha inayotumiwa Kusini-Mashariki ya Asia. Nikotini huingia kwenye damu kupitia mdomo. Ni hatari kutumia tumbaku hizo zisizokuwa na moshi kama tu tumbaku nyingine.
Tumbaku inayovutwa kupitia maji: Moshi wa tumbaku inayovutwa kwa njia hiyo hupitishwa kwenye maji kabla ya kuvutwa. Hata hivyo, mbinu hiyo haipunguzi kiasi cha sumu, kutia ndani zile zinazosababisha kansa, ambazo huingia kwenye mapafu.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
KUMSAIDIA MTU MWINGINE KUACHA
● Usiwe mchambuzi. Kumsifu mtu na kumpongeza huwa na matokeo mazuri kuliko kulalamika na kumzomea. Kusema “Nafikiri utafaulu ukijaribu tena” ni afadhali kuliko kusema “Ona sasa umeshindwa tena!”
● Uwe mwenye kusamehe. Jitahidi kutofunga kinyongo unapokasirikiwa na mtu anayejaribu kuacha kuvuta sigara. Tumia maneno yenye fadhili kama vile: “Najua ni vigumu, lakini pongezi kwa kujitahidi sana.” Usiseme: “Ulikuwa mtu mzuri zaidi ulipokuwa ukivuta sigara!”
● Uwe rafiki wa kweli. Biblia inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Naam, “nyakati zote” jaribu kuwa na subira na kumwonyesha upendo mtu anayejaribu kuacha, hata iwe ni saa ngapi au mtu awe anakabili hisia gani.
-
-
Unaweza Kufaulu!Amkeni!—2010 | Mei
-
-
Unaweza Kufaulu!
SASA ndio wakati wa kuwa ‘hodari na kutenda.’ (1 Mambo ya Nyakati 28:10) Unaweza kuchukua hatua gani ili ufanikiwe?
Jiwekee tarehe. Wizara ya Afya na Huduma za Jamii ya Marekani inapendekeza kwamba mara unapoamua kuacha, usijiwekee tarehe ambayo iko baada ya majuma mawili. Kwa njia hiyo hutapoteza tamaa ya kuacha. Tia alama kwenye kalenda tarehe unayotaka kufanya hivyo, waambie rafiki zako, na usibadili tarehe hiyo hata ikiwa hali zako zitabadilika.
Beba maandishi ya kukusaidia. Huenda yakawa na habari zifuatazo, au kitu kingine chochote kitakachokuchochea:
● Sababu zako za kuacha kuvuta sigara
● Namba za simu za watu ambao ungependa kuzungumza nao unapohisi umeanza kushawishika
● Maneno yenye kuchochea—labda hata mistari ya Biblia kama vile Wagalatia 5:22, 23—ambayo yatakusaidia kutimiza lengo lako
Beba maandishi hayo nyakati zote na uyasome mara kadhaa kwa siku. Hata utakapofaulu kuacha, endelea kusoma tena maandishi hayo unapojihisi kuwa unataka kuvuta sigara.
Acha mazoea pole kwa pole. Kabla ya tarehe hiyo ya kuacha kuvuta sigara kufika, anza kuepuka mazoea yoyote yanayohusiana na kuvuta sigara. Kwa mfano, ikiwa wewe huvuta sigara mara tu unapoamka kila siku, ahirisha kufanya hivyo kwa saa moja au zaidi. Ikiwa wewe huvuta sigara unapokula au mara baada ya kumaliza kula, acha zoea hilo. Epuka maeneo ambako watu wengine huvuta sigara. Na ujizoeze faraghani kusema kwa sauti: “Hapana. Nimeacha kuvuta sigara.” Kufanya mambo kama hayo kutakutayarisha kwa ajili ya siku utakayoacha kuvuta sigara. Pia, kufanya hivyo kutakukumbusha kwamba hivi karibuni utaacha kuvuta sigara.
Jitayarishe kuacha kuvuta. Tarehe yako ya kuacha kuvuta sigara inapokaribia, nunua vitu vya badala utakavyotumia: karoti, chingamu, karanga, na kadhalika. Wakumbushe watu wa familia na marafiki kuhusu tarehe uliyoweka ya kuacha kuvuta sigara na jinsi wanavyoweza kukuunga mkono. Kabla tu ya siku hiyo kufika, tupa visahani vyote vya kuwekea jivu, vifaa vya kuwasha sigara, na vitu vyovyote vinavyoweza kukushawishi uanze kuvuta—kama vile sigara zilizosalia nyumbani, garini, mfukoni, au kazini. Kwa kweli, ni vigumu zaidi kumwomba rafiki sigara au kuinunua, kuliko kuitoa tu ndani ya kabati! Pia, endelea kumwomba Mungu msaada, na ufanye hivyo kwa bidii baada ya kuvuta sigara ya mwisho.—Luka 11:13.
Watu wengi sana “wamevunja” uhusiano wao na yule aliyekuwa rafiki mwongo na mkatili anayeitwa sigara. Wewe pia unaweza kufanya hivyo. Utapata afya nzuri zaidi na utajihisi huru zaidi unapofaulu kuacha kuvuta sigara.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Beba maandishi ya kukusaidia kuacha kuvuta sigara nyakati zote na uyasome mara nyingi kila siku
-