-
Je, Biblia Ina Faida Leo?Amkeni!—2015 | Februari
-
-
HABARI KUU
Je, Biblia Ina Faida Leo?
‘Kwa mara ya kwanza maishani mwangu, nilipata furaha.’
HILTON alipenda mchezo wa ndondi. Akiwa na umri wa miaka saba alikuwa akipigana na watu si tu kwenye jukwaa la ndondi bali pia mitaani. Alipojiunga na shule ya upili (sekondari) yeye na rafiki zake walizurura wakitafuta mtu wa kumpiga. Anasimulia hivi: “Nilikuwa mwizi, nilicheza kamari, niliwanyanyasa wanawake, nilitazama ponografia, na kuwatukana wazazi wangu. Tabia yangu iliharibika hivi kwamba wazazi wangu walifikiri nisingeweza kubadilika. Baada ya kumaliza shule ya upili, niliondoka nyumbani.”
Aliporudi nyumbani baada ya miaka 12, wazazi wake hawakuamini macho yao! Hilton alikuwa mtulivu, mpole, na mwenye heshima. Ni nini kilichomfanya abadilike? Alipokuwa mbali na nyumbani, alitafakari sana kuhusu maisha yake. Pia, alianza kuichunguza Biblia ili imsaidie kubadilisha mwenendo wake. Anasema hivi: “Nilitumia mambo niliyojifunza katika Biblia. Mambo hayo yalitia ndani kuuvua utu wangu wa zamani na kutii amri inayopatikana kwenye andiko la Waefeso 6:2, 3 linalosema kwamba ninapaswa kuwatii wazazi wangu. Kwa mara ya kwanza maishani mwangu, nilipata furaha ya kweli na kuwafurahisha wazazi wangu.”
Simulizi la Hilton linaonyesha jinsi Biblia ilivyo na nguvu ya kumbadili mtu na jinsi viwango vyake vilivyo na faida. (Waebrania 4:12) Acheni tuchunguze baadhi ya viwango hivyo, kama vile: unyoofu, kujizuia, uaminifu, na upendo—na tuone jinsi vinavyoweza kuboresha maisha yetu.
-
-
Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—UnyoofuAmkeni!—2015 | Februari
-
-
HABARI KUU | JE, BIBLIA INA FAIDA LEO?
Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Unyoofu
KANUNI YA BIBLIA: “Ni nani atakayekuwa mgeni katika hema lako [Mungu]? . . . Yeye anayetembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wake.”—Zaburi 15:1, 2.
FAIDA: Watu wengi huvutiwa na sifa ya unyoofu na uaminifu. Lakini wanatendaje wanapojua kwamba watafaidika kwa kutenda kwa njia ambayo si ya unyoofu na ikiwa hakuna yeyote atakayewakamata? Jambo hilo litategemea hali ya mtu ya moyoni.
Raquel, mwanamke ambaye kazi yake ilihusisha kununua bidhaa mbalimbali za kampuni, alisema hivi: “Wauzaji fulani walijaribu kunihonga. Waliniahidi kwamba iwapo ningenunua bidhaa zao, wangenipa kisiri baadhi ya pesa za ziada zilizokusudiwa kwenda kwenye kampuni niliyofanyia kazi. Lakini nilikumbuka ushauri wa Biblia kuhusu umuhimu wa unyoofu na nikakataa pesa hizo. Msimamizi wangu alipojua jambo hilo, aliendelea kuniamini zaidi.”
Ikiwa Raquel angekubali kupokea rushwa hiyo, huenda angefaidika kifedha kwa muda mfupi tu. Lakini hali ingekuwaje ikiwa mwajiri wake angegundua jambo hilo? Je, Raquel angefutwa kazi? Je, angefaulu kupata kazi nyingine wakati ujao? Jambo muhimu kwake lilikuwa kudumisha dhamiri njema na heshima yake. Andiko la Methali 22:1 linasema: “Ni afadhali kuchagua jina badala ya utajiri mwingi; kibali ni bora kuliko hata fedha na dhahabu.”
Jessie aliaminiwa na mwajiri wake kwa sababu ya kuwa mfanyakazi mnyoofu
Jessie pia alikuwa mnyoofu na mwaminifu, na aliaminiwa sana na mwajiri wake. Alifaidikaje? Mwajiri wake alimteua kuwa msimamizi na akampa uhuru wa kujipangia shughuli zake za kazi. Jambo hilo lilimsaidia apate muda zaidi wa kuwa pamoja na mke na watoto wake na hata muda kwa ajili ya mambo ya ibada.
Waajiri wengine hutafuta wafanyakazi miongoni mwa mashirika yanayojulikana kuwa na watu wenye sifa ya unyoofu. Kwa mfano, meneja mmoja wa kampuni nchini Filipino aliandika barua kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini humo akiomba Mashahidi wajaze maombi ya kazi katika kampuni yake. Alisema hivi: Wao ni “wachapakazi, ni wanyoofu, na waaminifu.” Bila shaka, utukufu na sifa zimwendee Yehova Mungu, ambaye anatufundisha ‘tuchukie yaliyo mabaya’ na ‘kupenda yaliyo mema.’—Amosi 5:15.
-
-
Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—KujizuiaAmkeni!—2015 | Februari
-
-
HABARI KUU | JE, BIBLIA INA FAIDA LEO?
Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Kujizuia
KANUNI YA BIBLIA: “Mtu mjinga huiachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima huituliza mpaka mwisho.”—Methali 29:11.
“Nahisi kwamba nilinusurika kifo!”
FAIDA: Ikiwa ungeorodhesha faida zinazotokana na kuwa na sifa ya kujizuia, bila shaka ungehitaji rundo la karatasi! Kwa ufupi, sifa hii hutulinda kiafya. Biblia husema hivi: “Moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.” Pia inasema, “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.” (Methali 14:30; 17:22) Utafiti umeonyesha kwamba watu wakali na wanaopenda kukasirika ovyoovyo wanaweza kupata matatizo ya afya na hasa ugonjwa wa moyo. Kwa kweli, kuwa na sifa ya kujizuia kuna faida nyingi.
Cassius, ambaye ana umri wa miaka 30 hivi anasema: “Nilipenda mabishano na nilikasirika upesi, na mara kwa mara pia nilipenda kupigana. Sikujiheshimu. Lakini nilipoanza kufuata kanuni za Biblia mambo yalibadilika. Nilijifunza jinsi ya kudhibiti hasira, kuwa mnyenyekevu, na hata kuwasamehe wengine. Nisingefanya hivyo, leo hii ningekuwa gerezani. Kusema kweli, nahisi kwamba nilinusurika kifo!”
Cassius alijifunza kudhibiti hasira na kuwasamehe wengine
-
-
Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—UaminifuAmkeni!—2015 | Februari
-
-
HABARI KUU | JE, BIBLIA INA FAIDA LEO?
Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Uaminifu
KANUNI YA BIBLIA: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi.”—Waebrania 13:4.
FAIDA: Watu wengine wanasema kwamba maneno hayo yamepitwa na wakati. Hata hivyo, wamekosea sana! Ukosefu wa uaminifu una madhara makubwa leo, sawa tu na ilivyokuwa Biblia ilipoandikwa.—Methali 6:34, 35.
Jessie, mwanamume aliyefunga ndoa na aliye na watoto wawili, alisema hivi: “Uaminifu katika ndoa umechangia kwa kiasi kikubwa furaha na uhusiano mzuri nilio nao pamoja na mke wangu. Kuaminiana ni jambo muhimu sana katika ndoa. Ukosefu wa uaminifu husababisha kutokuaminiana.” Vilevile watoto huathiriwa sana mume na mke wanapokosa uaminifu katika ndoa yao!
Ligayaa alihatarisha ndoa yake. Anasema hivi: “Nilianza kushirikiana na watu wasiofaa. Nikaanza kwenda kwenye vilabu vya usiku na pia kufanya uzinzi.” Je, maisha hayo yalimletea furaha? La hasha! Kila siku alikorofishana na mume wake, na hakuwa na furaha. Anaongezea kusema hivi: “Nilipotafakari kuhusu matatizo niliyojiletea, nilitambua kwamba wazazi wangu hawakuwa wamekosea walipokuwa wakiniambia, ‘Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.’”—1 Wakorintho 15:33.
Ligaya anaendelea kusema: “Kabla mambo hayajaharibika kabisa, niliamua kuacha njia zangu mbaya, na nikaanza kujifunza Biblia. Wakati huu niliamua kufuata mambo niliyokuwa nikijifunza.” Ikawaje? Ligaya aliokoa ndoa yake, na mume wake akaanza kumheshimu na kumtendea kwa fadhili. Anamalizia kwa kusema hivi: “Biblia ilibadili maisha yangu, na sijuti kwamba niliacha njia zangu mbaya na marafiki niliokuwa nao.”
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
-
-
Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—UpendoAmkeni!—2015 | Februari
-
-
HABARI KUU | JE, BIBLIA INA FAIDA LEO?
Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Upendo
KANUNI YA BIBLIA: “Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:14.
FAIDA: Upendo unaotajwa mara nyingi katika Biblia si ule wa kimahaba au kimapenzi. Bali, Biblia huzungumzia zaidi kuhusu upendo unaoongozwa na kanuni, wenye sifa kama vile huruma, kusamehe, unyenyekevu, fadhili, upole, na subira. (Mika 6:8; Wakolosai 3:12, 13) Tofauti na hisia za kimahaba ambazo mara nyingi hufifia kadiri muda unavyopita, upendo huo huendelea kukua daima dawamu.
Brenda, mwanamke ambaye amekuwa katika ndoa kwa karibu miaka 30, anasema hivi: “Upendo kati ya watu waliofunga ndoa karibuni hauwezi kulinganishwa na kina cha upendo ambacho mume na mke huonyeshana kadiri muda unavyopita.”
Sam, mume ambaye amekuwa katika ndoa kwa zaidi ya miaka 12, anasema hivi: “Sikuzote mimi na mke wangu tumefurahia na hata kushangazwa na jinsi mashauri ya Biblia yalivyo rahisi kueleweka, na jinsi ambavyo kuyatumia huleta matokeo mazuri. Unapoyatumia, mambo yanakuwa shwari. Hata ingawa ningependa kusema kwamba nafuata mashauri ya Biblia nyakati zote, kuna wakati ambapo ninashindwa kufanya hivyo. Kwa mfano, ninapokuwa katika hali ya kuudhika upesi, kutaka kufanya nipendavyo, au ninapokuwa nimechoka. Nyakati kama hizo mimi humwomba Yehova anisaidie kushinda hisia zozote zisizofaa. Kisha ninamkumbatia mke wangu, na baada ya muda mfupi, hali inakuwa shwari kana kwamba hakuna jambo lolote baya lililotendeka!”
“Hekima huonyeshwa kwa matendo yake”
Yesu Kristo alisema “hekima huonyeshwa kwa matendo yake.” (Mathayo 11:19) Kwa msingi wa maneno hayo, ni Biblia pekee yenye hekima ya kweli. Imethibitika kwamba viwango na mafundisho yake huwanufaisha watu sikuzote. Viwango na mafundisho yake huwanufaisha watu wa nchi na tamaduni zote. Biblia inaelezea kwa kina kuhusu tabia za asili za wanadamu na hilo halishangazi kwa sababu Mtungaji wa Biblia ni Muumba wetu—Yehova Mungu. Hata hivyo, kufuata mafundisho ya Biblia kutatuthibitishia kwamba yeye ndiye chanzo cha viwango hivyo. Kwa hiyo, Biblia inatualika tufuate na kutumia viwango na mafundisho ya Yehova inaposema “onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.” (Zaburi 34:8) Je, utakubali mwaliko huo?
-