-
Jinsi ya Kusitawisha Mazoea MazuriAmkeni!—2016 | Na. 4
-
-
HABARI KUU
Jinsi ya Kusitawisha Mazoea Mazuri
Saa ya Austin inapopiga kengele ya kumwamsha, yeye bado huwa na usingizi mwingi. Hata hivyo, huamka haraka, huvaa nguo za mazoezi alizotayarisha kabla ya kulala na kwenda kufanya mazoezi ambayo amekuwa akifanya tangu mwaka uliopita, mara tatu kila juma.
Laurie amegombana na mume wake. Akiwa amewaka hasira, Laurie anaenda jikoni, anachukua mfuko uliojaa peremende na kula peremende zote, kama ilivyo kawaida yake anapokasirika.
Austin na Laurie wana jambo gani linalofanana? Iwe wanajua au la, wote wanafanya mambo hayo kwa sababu wamezoea.
Namna gani wewe? Je, kuna mazoea fulani mazuri ambayo ungependa kusitawisha maishani? Huenda umepanga kufanya mazoezi kwa ukawaida, kulala vizuri, au kuwa karibu na watu unaowapenda.
Kwa upande mwingine, huenda ungependa kuacha mazoea mabaya, kama vile kuvuta sigara, kula vyakula visivyo na lishe, au kutumia muda mwingi kwenye Intaneti.
Ni wazi kwamba si rahisi kuacha mazoea mabaya. Kwa kweli, wengine wamesema kwamba mazoea mabaya ni kama kitanda chenye joto wakati wa baridi: ni rahisi kuingia lakini kutoka ni vigumu.
Hivyo, unawezaje kusitawisha mazoea mazuri na kuacha mazoea mabaya? Chunguza mapendekezo matatu yanayotegemea kanuni za Biblia katika gazeti hili.
-
-
1 Ona Mambo KihalisiAmkeni!—2016 | Na. 4
-
-
HABARI KUU | JINSI YA KUSITAWISHA MAZOEA MAZURI
1 Ona Mambo Kihalisi
Si rahisi kubadili mara moja kila kitu ambacho umezoea kufanya maishani. Huenda ukajiambia hivi, ‘Juma hili nitaacha kuvuta sigara, kutukana, kuchelewa kulala, nitaanza kufanya mazoezi, kula vyakula vyenye lishe, na kuwapigia simu bibi (nyanya) na babu.’ Hata hivyo, haiwezekani kufanya mambo hayo yote kwa wakati mmoja.
KANUNI YA BIBLIA: “Wenye kiasi wana hekima.”—Methali 11:2.
Mtu mwenye kiasi huona mambo kihalisi. Anatambua kwamba muda, nguvu na mali zake zina mipaka. Hivyo, badala ya kujaribu kubadili kila kitu mara moja, atajitahidi kufanya maendeleo hatua kwa hatua.
Haiwezekani kufanya mambo hayo yote kwa wakati mmoja!
MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA
Jitahidi kufanyia kazi zoea moja baada ya lingine. Hatua zifuatazo zinaweza kukusaidia:
Andika ‘orodha’ mbili, moja kuhusu mazoea mazuri ambayo ungependa kusitawisha na nyingine mazoea mabaya ambayo unataka kuacha. Andika mambo mengi katika kila orodha.
Panga mambo ambayo umeorodhesha ukitanguliza yaliyo muhimu zaidi.
Chagua jambo moja au mawili katika kila orodha na kuyafanyia kazi. Kisha chagua jambo moja au mawili yanayofuata katika kila orodha.
Ili ufaulu haraka, hakikisha kwamba mazoea mazuri yanachukua nafasi ya mazoea mabaya. Kwa mfano, ikiwa orodha yako ya mambo mabaya inatia ndani kutazama televisheni kwa muda mrefu na ile ya mambo mazuri inatia ndani kuwasiliana na wapendwa wako, huenda ukaamua: ‘Kuwasiliana na rafiki au mshiriki wa familia badala ya kutazama televisheni mara tu unapofika nyumbani kutoka kazini.’
-
-
2 Chunguza Mazingira YakoAmkeni!—2016 | Na. 4
-
-
HABARI KUU | JINSI YA KUSITAWISHA MAZOEA MAZURI
2 Chunguza Mazingira Yako
Umeazimia kuepuka vyakula visivyo na lishe, lakini unatamani sana vyakula hivyo.
Umeamua kuacha kuvuta sigara, lakini mara kwa mara rafiki yako anayejua kwamba unajitahidi kuacha zoea hilo anakupatia sigara.
Ulipanga kufanya mazoezi leo, hata hivyo, unahisi umechoka sana kiasi kwamba huwezi hata kuvaa mavazi ya mazoezi!
Je, umeona jambo moja la msingi linalokaziwa katika mifano hiyo mitatu? Mara nyingi, mifano halisi inaonyesha kwamba mazingira, yaani, hali tunazokabili na watu tunaoshirikiana nao wanaweza kuathiri jitihada zetu za kuacha mazoea mabaya.
KANUNI YA BIBLIA: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” —Methali 22:3.
Biblia inatushauri kufikiria matokeo. Kufanya hivyo kunaweza kutusaidia kuwa na tahadhari na kuepuka hali ambazo zitavuruga malengo yetu na kutufanya tuwe na mazoea mazuri. (2 Timotheo 2:22) Kwa ufupi, ni jambo la hekima kuchunguza mazingira yetu.
Azimia kuepuka mambo yasiyofaa na rahisisha mazingira ya kufanya mambo yanayofaa
MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA
Azimia kuepuka mambo yasiyofaa. Kwa mfano, ikiwa unataka kuacha kula vyakula visivyo na lishe, basi usinunue wala kuhifadhi vyakula hivyo. Kwa njia hiyo utaweza kushinda kishawishi hicho kwa urahisi.
Rahisisha mazingira ya kufanya mambo yanayofaa. Kwa mfano, ikiwa umepanga kufanya mazoezi asubuhi baada ya kuamka, weka mavazi ya mazoezi karibu na kitanda chako kabla ya kulala. Ukifaulu kuanza, itakuwa rahisi kuendelea na zoea hilo.
Chagua marafiki kwa uangalifu. Tuna mwelekeo wa kuwaiga watu tunaoshirikiana nao. (1 Wakorintho 15:33) Kwa hiyo, epuka kushirikiana na watu ambao watakushawishi urudie mazoea mabaya, na ushirikiane na wale watakaokusaidia kusitawisha mazoea mazuri.
-
-
3 Usikate TamaaAmkeni!—2016 | Na. 4
-
-
HABARI KUU | JINSI YA KUSITAWISHA MAZOEA MAZURI
3 Usikate Tamaa
Inasemekana kwamba mtu anaweza kuzoea tabia mpya kwa siku 21. Hata hivyo, utafiti unaonyesha kwamba huenda baadhi ya watu wakatumia muda mfupi kuzoea jambo fulani ilhali wengine wakatumia muda mrefu. Je, hilo linapaswa kukuvunja moyo?
Hebu fikiria hali hii: Tuseme kwamba unataka kusitawisha mazoea ya kufanya mazoezi mara tatu kwa juma.
Juma la kwanza, unafaulu kufikia lengo lako.
Juma la pili, unakosa kufanya mazoezi kwa siku moja.
Juma la tatu, unafaulu tena.
Juma la nne, unashindwa kufanya mazoezi hata kwa siku moja.
Juma la tano, unafaulu tena, na kuanzia hapo unatimiza lengo lako kila juma.
Imechukua majuma matano kuzoea hali hiyo mpya. Huenda huo ukaonekana kuwa muda mrefu, hata hivyo, mara tu unapofikia lengo lako unafurahi kwamba ulisitawisha zoea zuri.
KANUNI YA BIBLIA: “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.”—Methali 24:16.
Biblia inatutia moyo tusikate tamaa. Haijalishi tutashindwa mara ngapi lakini jambo la maana ni kufikia malengo yetu.
Haijalishi tutashindwa mara ngapi lakini jambo la maana ni kufikia malengo yetu
MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA
Kumbuka kwamba kuteleza si kuanguka. Tarajia kupata vizuizi unapojitahidi kufikia malengo yako.
Kumbuka wakati ulipofikia malengo yako. Kwa mfano, ikiwa unajaribu kuboresha njia ya kuwasiliana na watoto wako, jiulize hivi: ‘Ni wakati gani nilipotaka kuwafokea watoto wangu lakini nikajizuia kufanya hivyo? Nilifanya nini? Ninawezaje kufanya hivyo tena?’ Maswali kama hayo yanaweza kukusaidia uimarishe azimio lako la kutaka kufanikiwa badala ya kukazia fikira makosa.
Je, ungependa kujua jinsi ambavyo kanuni za Biblia zinaweza kukusaidia kushughulikia mambo mengine maishani kama vile, mahangaiko, kuwa na maisha ya familia yenye furaha na jinsi ya kuwa na furaha ya kweli? Zungumza na Mashahidi wa Yehova, au tembelea tovuti yetu ya jw.org/sw.
-