-
Maria (Mama ya Yesu)Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Unaweza kujibu hivi: ‘Maandiko Matakatifu yanasema waziwazi kwamba mama ya Yesu Kristo alikuwa bikira, nasi tunaamini hivyo. Mungu alikuwa Baba yake (Yesu). Mtoto aliyezaliwa alikuwa kweli Mwana wa Mungu, kama malaika alivyomwambia Maria. (Luka 1:35)’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Lakini umewahi kujiuliza kwa nini ilikuwa muhimu kwamba Yesu azaliwe kwa njia hiyo? . . . Ni kwa njia hiyo tu fidia inayofaa ingeweza kutolewa, fidia ambayo ingefanya iwezekane kwetu kufunguliwa kutoka katika dhambi na kifo.—1 Tim. 2:5, 6; kisha unaweza kusoma pia Yoh. 3:16.’
Au unaweza kusema: ‘Ndiyo, tunamwamini. Tunaamini kila jambo ambalo Maandiko Matakatifu yanasema kumhusu, nayo yanasema waziwazi kwamba alikuwa bikira alipomzaa Yesu. Pia mambo mengine ambayo Maandiko yanatuambia kumhusu Maria na yale tunayoweza kujifunza kutoka kwake yananichangamsha moyo sana. (Tumia habari kwenye ukurasa wa 181.)’
‘Ninyi hammwamini Bikira Maria’
Unaweza kujibu hivi: ‘Nimetambua kwamba kuna watu ambao hawaamini kwamba yule aliyemzaa Mwana wa Mungu alikuwa bikira. Lakini sisi tunaamini alikuwa bikira. (Fungua kimoja cha vitabu vyetu kwenye sehemu inayozungumzia jambo hilo na umwonyeshe mwenye nyumba.)’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Je, kuna jambo lolote zaidi linalohitajiwa ikiwa tunataka kupata wokovu? . . . Ona yale ambayo Yesu alimwambia Baba yake katika sala. (Yoh. 17:3)’
-
-
MisaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Misa
Maana: Kama inavyoelezwa na Kundi Takatifu la Ibada za Kanisa Katoliki, Misa ni “—Dhabihu ambayo katika hiyo Dhabihu ya Msalaba inadumishwa;—Ukumbusho wa kifo na ufufuo wa Bwana, aliyesema ‘fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu’ (Luka 22:19);—Karamu takatifu ambapo, kupitia ushirika wa Mwili na Damu ya Bwana, Watu wa Mungu hushiriki faida za Dhabihu ya Pasaka, hufanya upya Agano Jipya ambalo Mungu amefanya pamoja na wanadamu mara moja kwa wakati wote kupitia Damu ya Kristo, na katika imani na tumaini hutangulia kuonyesha na kutarajia karamu ya mwisho katika ufalme wa Baba, wakitangaza kifo cha Bwana ‘hata ajapo.’” (Eucharisticum Mysterium, Mei 25, 1967) Hiyo ndiyo njia ya Kanisa Katoliki ya kufanya kile wanachoelewa kwamba Yesu Kristo alifanya katika Mlo wa Jioni wa Bwana.
Je, mkate na divai vinabadilishwa hakika na kuwa mwili na damu ya Kristo?
Katika “Ungamo Zito la Imani” Juni 30, 1968, Papa Paulo wa Sita alitangaza hivi: “Tunaamini kwamba kama vile mkate na divai vilivyotakaswa na Bwana katika Mlo wa Jioni wa Bwana vilibadilishwa vikawa Mwili Wake na Damu Yake ambavyo vilipasa kutolewa kwa ajili yetu juu ya msalaba, vivyo hivyo mkate na divai vinavyotakaswa na padri vinabadilishwa na kuwa Mwili na Damu ya Kristo aliyetawazwa kwa utukufu mbinguni, na Sisi tunaamini kwamba kuwapo kwa kifumbo kwa Bwana, chini ya kuonekana kwa vitu hivyo vinavyoonekana kwa hisia zetu kuwa ni vilevile baadaye kama kabla ya Utakaso, ni kuwapo ambako ni kwa kweli na halisi. . . . Kwa kufaa, Kanisa linaliita badiliko hilo la kifumbo kuwa kubadilika kwa mkate na divai kuwa mwili na damu halisi ya Kristo.” (Official Catholic Teachings—Christ Our Lord, Wilmington, N.C.; 1978, Amanda G. Watlington, uku. 411) Je, Maandiko Matakatifu yanakubaliana na imani hiyo?
Yesu alimaanisha nini aliposema, “Huu ndio mwili wangu,” “Hii ndiyo damu yangu”?
Mt. 26:26-29, UV: “Nao walipokuwa wakila Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akisema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu. Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Nyweni nyote katika hiki, kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi. Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.”
Kuhusu maneno “huu ndio mwili wangu” na “hii ndiyo damu yangu,” kumbuka mambo haya yafuatayo: Mo husema hivi, “huu unamaanisha mwili wangu,” “hii inamaanisha damu yangu.” (Italiki zimeongezwa.) NW husema vivyo hivyo. LEF hutafsiri maneno hayo hivi, “huu unawakilisha mwili wangu,” “hii inawakilisha damu yangu.” (Italiki zimeongezwa.) Tafsiri hizo zinapatana na yale yanayosemwa katika muktadha, katika mstari wa 29, katika chapa mbalimbali za Kikatoliki. VB husema hivi: “Sitakunywa tena mazao haya ya mzabibu, mpaka siku ile nitakapokunywa yale mapya, pamoja nanyi, katika ufalme wa Babangu.” (Italiki zimeongezwa.) UV, ZSB, BHN pia huonyesha Yesu akielekeza kwenye kile kilichokuwa katika kikombe kama “uzao huu wa mzabibu,” “matunda ya mizabibu,” “divai ya zabibu,” na hiyo ilikuwa baada ya Yesu kusema, “Hii ndiyo damu yangu.”
Fikiria maneno “huu ndio mwili wangu” na “hii ndiyo damu yangu” kwa kukumbuka maneno mengine yaliyo wazi yanayotumiwa katika Maandiko. Yesu pia alisema, “Mimi ndimi nuru ya ulimwengu,” “Mimi ndimi mlango wa kondoo,” “Mimi ndimi mzabibu wa kweli.” (Yoh. 8:12; 10:7; 15:1, UV) Je, lolote kati ya maneno hayo lilimaanisha kubadilika kimuujiza?
Katika andiko la 1 Wakorintho 11:25 (UV), mtume Paulo aliandika kuhusu Mlo wa Jioni wa Bwana na kutoa mawazo hayohayo kwa kutumia maneno tofauti kidogo. Badala ya kumnukuu Yesu akisema hivi kuhusu kikombe, “Nyweni nyote katika hiki . . . kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano,” alitumia maneno haya: “Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu.” Hakika hilo halikumaanisha kwamba kikombe hicho kilibadilishwa kimuujiza na kuwa agano jipya. Je, si jambo linalopatana na akili zaidi kukata shauri kwamba kilichokuwa katika kikombe kiliwakilisha damu ya Yesu ambayo ilihalalisha agano jipya?
Yesu alimaanisha nini aliposema maneno yaliyo katika Yohana 6:53-57?
“Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi.”—Yoh. 6:53-57, UV.
Je, ieleweke kwamba hayo yanamaanisha walipaswa kula kihalisi mwili wa Yesu na kunywa damu yake? Ikiwa ingekuwa hivyo, Yesu angekuwa akiunga mkono kuvunjwa kwa Sheria ambayo Mungu alikuwa amewapa Waisraeli kupitia Musa. Sheria hiyo ilikataza kula aina yoyote ya damu. (Law. 17:10-12) Kinyume cha kuunga mkono jambo kama hilo, Yesu alipinga kabisa kuvunjwa kwa takwa lolote la Sheria hiyo. (Mt. 5:17-19) Kwa hiyo jambo ambalo Yesu alikuwa nalo akilini lazima lilikuwa kula na kunywa kwa maana ya mfano, yaani, kuwa na imani katika dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu.—Linganisha na Yohana 3:16; 4:14; 6:35, 40.
Je, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wafanye ukumbusho wa kifo chake tu, au pia wafanye kawaida ya ibada ambayo kwa hakika ingefanya upya dhabihu yake?
Kulingana na kichapo The Documents of Vatican II: “Katika Mlo wa Jioni wa Bwana, katika usiku ambao Yeye alisalitiwa, Mwokozi wetu alianzisha Dhabihu ya Ekaristi ya Mwili na Damu Yake. Yeye alifanya hivyo ili adumishe dhabihu ya Msalaba . . . ”—(New York, 1966), kilichohaririwa na W. M. Abbott, S.J., uku. 154; italiki zimeongezwa.
The Catholic Encyclopedia inasema hivi: “Kanisa linakusudia Misa ionwe kuwa ‘dhabihu ya kweli na halisi’ . . . Hata hivyo, chanzo kikuu cha fundisho letu ni mapokeo, ambayo tangu nyakati za zamani zaidi yanatangaza thamani ya uombezi ya Dhabihu ya Misa.”—(1913), Buku la 10, uku. 6, 17.
Yesu mwenyewe alisema: “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” (Luka 22:19; 1 Kor. 11:24, UV) Katika Luka 22:19, BHN na ZSB husema hivi: “Fanyeni hivi kwa kunikumbuka.” Yesu hakusema kwamba jambo alilofanya katika Mlo wa Jioni wa Bwana lilikuwa dhabihu yake mwenyewe wala hakusema kwamba wanafunzi wake walipaswa kufanya upya dhabihu yake.
Ebr. 9:25-28, UV: “Wala si kwamba ajitoe mara nyingi, kama vile kuhani mkuu [Myahudi] aingiavyo katika patakatifu kila mwaka kwa damu isiyo yake; kama ni hivyo ingalimpasa kuteswa mara nyingi tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu; lakini sasa, mara moja tu, . . . amefunuliwa, azitangue dhambi kwa dhabihu ya nafsi yake. Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu; kadhalika Kristo naye, akiisha kutolewa sadaka mara moja.” (Italiki zimeongezwa.)
Je, yote hayo ni “fumbo lisiloweza kufahamika”?
Biblia inasema kuhusu mafumbo ya Mungu, au siri takatifu. Lakini hakuna moja la mafumbo hayo linalopingana na kweli za Kimaandiko zilizoandikwa waziwazi. Kuhusu wale waliotanguliza mapokeo yao badala ya Maandiko, Yesu alisema: “Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.”—Mt. 15:7-9, UV.
Je, Yesu alikusudia ukumbusho huo ufanywe labda kila siku au kila juma?
Kichapo Basic Catechism kinasema: “Kazi za Pekee za Wakristo Wakatoliki” hutia ndani “kushiriki Misa kila Jumapili na sikukuu ya amri.” (Boston, 1980, uku. 21) “Kwa hakika waamini wanatiwa moyo kushiriki Misa na kupokea Komunyo mara kwa mara, hata kila siku.”—The Teaching of Christ—A Catholic Catechism for Adults, Chapa Iliyofupishwa (Huntington, Ind.; 1979), uku. 281.
Je, marejeo yote katika Maandiko kuhusu “kuumega mkate” yanaonyesha kwamba kifo cha Kristo kilikuwa kikikumbukwa? (Mdo. 2:42, 46; 20:7, UV) Yesu ‘aliimega mikate’ walipokuwa wakila chakula hata kabla ya Mlo wa Jioni wa Bwana. (Marko 6:41; 8:6) Mkate uliotumiwa na Wayahudi wakati huo haukuwa ule ambao watu wengi wanaujua leo. Wakati wa kuula, mara nyingi waliumega au kukata kipande.
Yesu hakutaja waziwazi Ukumbusho wa kifo chake ulipaswa kufanywa mara ngapi. Hata hivyo, aliuanzisha kwenye tarehe ya Pasaka ya Wayahudi, sikukuu ambayo, kwa wanafunzi wake, mahali pake palichukuliwa na Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Pasaka ilikuwa sherehe ya kila mwaka, iliyofanywa Nisani 14. Vivyo hivyo, sherehe za Wayahudi, yaani, Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, Sherehe ya Majuma (Pentekoste), Sherehe ya Vibanda, au ya Kukusanya, na Siku ya Upatanisho zote zilifanywa mara moja kila mwaka.
Je, kutolewa kwa Misa kunazisaidia nafsi zilizo toharani (purgatori)?
Kichapo The Teaching of Christ—A Catholic Catechism for Adults kinasema: “Neno hili ‘toharani’ halimo katika Biblia, wala fundisho la toharani halifundishwi waziwazi katika Biblia. . . . Vitabu vya Mababa vina marejeo mengi si kuhusu kuwako kwa toharani tu, bali pia uhakika wa kwamba waamini waliokufa wanaweza kusaidiwa kwa sala za walio hai, hasa kwa Dhabihu ya Misa.”—Uku. 347, 348.
Kuhusu hali ya wafu, Maandiko Matakatifu yanasema: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhu. 9:5, UV) “Nafsi [“roho,” UV; “yeyote,” BHN] inayofanya zambi, itakufa.” (Eze. 18:4, ZSB) (Ona pia ukurasa wa 102-104, chini ya kichwa “Kifo.”)
-
-
Ukumbusho (Mlo wa Jioni wa Bwana)Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Ukumbusho (Mlo wa Jioni wa Bwana)
Maana: Mlo wa kukumbuka kifo cha Yesu Kristo; kwa hiyo, huo ni ukumbusho wa kifo chake, kifo ambacho kimekuwa na matokeo makubwa kuliko kile cha mtu mwingine yeyote. Hili ndilo tukio pekee ambalo Bwana Yesu Kristo aliwaamuru wanafunzi wake walifanyie ukumbusho. Pia unaitwa Mlo wa Jioni wa Bwana.—1 Kor. 11:20.
Ukumbusho una umuhimu gani?
Yesu aliwaambia hivi mitume wake waaminifu: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Alipokuwa akiwaandikia washiriki wa kutaniko la Kikristo lililozaliwa kwa roho, mtume Paulo aliongeza hivi: “Kila mara mnapokula mkate huu na kunywa kikombe hiki, mnaendelea kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapofika.” (1 Wakorintho 11:26) Kwa hiyo, Ukumbusho unakazia kwa njia ya pekee umuhimu wa kifo cha Yesu Kristo katika kutimiza kusudi la Yehova. Unakazia maana ya kifo cha kidhabihu cha Yesu hasa kuhusiana na agano jipya na matokeo ya kifo chake kwa wale watakaokuwa warithi pamoja naye wa Ufalme wa mbinguni.—Yoh. 14:2, 3; Ebr. 9:15.
Ukumbusho pia unatukumbusha kwamba kifo cha Yesu na jinsi kilivyotimizwa, kupatana na kusudi la Mungu kama lilivyoandikwa katika Mwanzo 3:15 na baadaye katika maandiko mengine, kilitumika kulitetea jina la Yehova. Kwa kudumisha utimilifu kwa Yehova mpaka kifo chake, Yesu alithibitisha kwamba dhambi ya Adamu haikuwa kwa sababu ya kasoro yoyote katika njia ambayo Muumba alimuumba mwanadamu bali kwamba inawezekana kwa mwanadamu kudumisha ujitoaji-kimungu mkamilifu hata akiwa chini ya mkazo mkali. Kwa njia hiyo, Yesu alimtetea Yehova Mungu akiwa Muumba na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu. Zaidi ya hayo, Yehova alikuwa amekusudia kwamba kifo cha Yesu kiandae dhabihu kamilifu ya kibinadamu inayohitajiwa ili kuwafidi watoto wa Adamu, na hivyo kuwawezesha mabilioni ya watu walio na imani waishi milele katika dunia paradiso, na hivyo kutimiza kusudi la kwanza la Yehova na kuonyesha upendo wake mkubwa kwa ajili ya wanadamu.—Yoh. 3:16; Mwa. 1:28.
Yesu alikuwa na mzigo mzito kama nini usiku ule wa mwisho duniani akiwa mwanadamu! Alijua jambo ambalo Baba yake wa mbinguni alikuwa amekusudia kwa ajili yake, lakini alijua pia kwamba alipaswa kujithibitisha kuwa mwaminifu chini ya jaribu. Ikiwa angeshindwa, hiyo ingekuwa shutuma kubwa kwa Baba yake na hasara kwa wanadamu! Kwa sababu ya yote ambayo yangetimizwa kupitia kifo chake, inafaa sana kwamba Yesu aliagiza kikumbukwe.
Mkate na divai vinavyotumiwa kwenye Ukumbusho vinamaanisha nini?
Yesu alisema hivi kuhusu mkate usio na chachu ambao aliwapa mitume wake alipoanzisha Ukumbusho: “Huu unamaanisha mwili wangu.” (Marko 14:22) Mkate huo ulikuwa mfano wa mwili wake mwenyewe wenye nyama usio na dhambi. Huo ungetolewa kwa ajili ya matarajio ya uzima wa wakati ujao wa wanadamu, na katika pindi hii uangalifu wa pekee unaelekezwa kwenye matarajio ya uzima ambao kinafanya yawezekane kwa wale ambao wangechaguliwa kushiriki pamoja na Yesu katika Ufalme wa mbinguni.
Alipokuwa akipitisha divai kwa mitume wake waaminifu, Yesu alisema: “Hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi.” (Marko 14:24) Divai hiyo ilikuwa mfano wa damu yake mwenyewe ya uzima. Kupitia damu yake iliyomwagwa, wale wanaoiamini watasamehewa dhambi. Katika pindi hii Yesu alikuwa akikazia kutakaswa dhambi ambako damu hiyo ingefanya kuwezekane kwa ajili ya wale wanaotarajia kuwa warithi pamoja naye. Maneno yake yanaonyesha pia kwamba kupitia damu hiyo lile agano jipya, kati ya Yehova Mungu na kutaniko la Kikristo lililotiwa mafuta kwa roho, lingeanza kutenda kazi.
Ona pia ukurasa wa 205-207, chini ya kichwa “Misa.”
Ni nani wanaopaswa kula mkate na kunywa divai?
Ni nani waliokula wakati Yesu alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana muda mfupi kabla ya kufa? Ni wale wafuasi kumi na mmoja waaminifu ambao Yesu aliwaambia: “Ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:29) Hao wote walikuwa watu waliokuwa wakialikwa washiriki pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni. (Yoh. 14:2, 3) Wote wanaokula mkate na kunywa divai leo wanapaswa pia kuwa watu ambao Kristo anaingiza katika lile ‘agano kwa ajili ya ufalme.’
Ni wangapi wanaokula? Yesu alisema kwamba ni “kundi dogo” tu ndio wangepewa thawabu ya Ufalme wa mbinguni. (Luka 12:32) Hesabu kamili ni 144,000. (Ufunuo 14:1-3) Kikundi hicho kilianza kuchaguliwa mwaka wa 33 W.K. Basi, kupatana na akili, kungekuwa na hesabu ndogo tu ya wenye kula sasa.
Je, andiko la Yohana 6:53, 54 linaonyesha kwamba ni wale tu wanaokula na kunywa ndio watakaopata uzima wa milele?
Yohana 6:53, 54: “Yesu akawaambia: ‘Kwa kweli kabisa ninawaambia, Ninyi msipoula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uzima ndani yenu wenyewe. Yule ambaye hula mwili wangu na kunywa damu yangu ana uzima wa milele, nami nitamfufua katika siku ya mwisho.’”
Kwa wazi basi, tendo hilo la kula na kunywa linapasa kufanywa kwa njia ya mfano; kama sivyo yule anayetenda hivyo atakuwa akiivunja sheria ya Mungu. (Mwa. 9:4; Mdo. 15:28, 29) Hata hivyo, inafaa kukumbuka kwamba maneno ya Yesu katika Yohana 6:53, 54, hayakusemwa kuhusiana na kuanzishwa kwa Mlo wa Jioni wa Bwana. Kati ya wote waliomsikiliza, hakuna aliyekuwa na wazo lolote kuhusu sherehe ya mkate na divai iliyotumiwa kuwakilisha nyama na damu ya Kristo. Mpango huo haukuanzishwa mpaka mwaka mmoja hivi baadaye, na habari za mtume Yohana kuhusu Mlo wa Jioni wa Bwana hazianzi mpaka baada ya zaidi ya sura saba (katika Yohana 14) katika Injili yenye jina lake.
Basi, mtu anawezaje ‘kuula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake’ kwa njia ya mfano ikiwa si kwa kula mkate na kunywa divai kwenye Ukumbusho? Kumbuka Yesu alisema kwamba wale wanaokula na kunywa kwa njia hiyo watakuwa na “uzima wa milele.” Katika mstari wa 40, alipokuwa akieleza jambo ambalo ni lazima watu wafanye ili wapate uzima wa milele, alisema mapenzi ya Baba yake ni nini? Kwamba “kila mtu ambaye humtazama Mwana na kumwamini awe na uzima wa milele.” Kupatana na akili, basi, mtu ‘huula mwili wake na kunywa damu yake’ katika njia ya mfano kwa kuwa na imani katika nguvu zenye kukomboa za mwili na damu ya Yesu vilivyotolewa katika dhabihu. Wote ambao watapata uzima kamili, iwe mbinguni pamoja na Kristo au katika Paradiso duniani, wanahitaji kuwa na imani.
Ukumbusho unapaswa kusherehekewa mara ngapi na wakati gani?
Yesu hakusema waziwazi ulipaswa kusherehekewa mara ngapi. Alisema tu: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Paulo alisema: “Kwa maana kila mara mnapokula mkate huu na kunywa kikombe hiki, mnaendelea kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapofika.” (1 Kor. 11:26) Maneno “kila mara” si lazima yamaanishe mara nyingi kwa mwaka; yanaweza kumaanisha kila mwaka kwa kipindi cha miaka mingi. Ukifanya ukumbusho wa tukio fulani, kama vile siku ya arusi, au taifa likifanya ukumbusho wa tukio muhimu katika historia yake, hilo hufanywa mara ngapi? Mara moja kwa mwaka katika tarehe ya ukumbusho wa tukio hilo. Hayo yanapatana pia na uhakika wa kwamba Mlo wa Jioni wa Bwana ulianzishwa katika tarehe ya Pasaka ya Wayahudi, ambayo ilikuwa sherehe ya kila mwaka ambayo haikuwa tena lazima ishikwe na Wayahudi waliokuwa wamekuwa Wakristo.
Mashahidi wa Yehova huadhimisha Ukumbusho baada ya jua kutua katika Nisani 14, kulingana na kalenda ya Kiyahudi iliyotumiwa na wengi katika karne ya kwanza. Siku ya Wayahudi huanza wakati jua linapotua na huendelea mpaka jua linapotua siku inayofuata. Kwa hiyo, Yesu alikufa siku ileile aliyoanzisha Ukumbusho kwenye kalenda ya Kiyahudi. Mwanzo wa mwezi wa Nisani ni wakati wa kutua kwa jua baada ya mwezi mpya karibu na siku-mlingano wakati wa masika, mwezi ulipoonekana katika Yerusalemu. Tarehe ya Ukumbusho ni siku 14 baada ya hapo. (Kwa hiyo, huenda tarehe ya Ukumbusho ikakosa kulingana na ile ya Pasaka inayoshikwa na Wayahudi wa siku hizi. Kwa nini? Mwanzo wa miezi yao ya kalenda umewekwa ulingane na tarehe ya mwezi mpya ulio angani, si kulingana na kuonekana kwa mwezi mpya Yerusalemu, ambao huenda ukaonekana baada ya saa 18 mpaka 30. Pia, Wayahudi wengi leo hushika Pasaka siku ya Nisani 15, wala si siku ya 14 kama alivyofanya Yesu kulingana na yaliyoandikwa katika Sheria ya Musa.)
-
-
Kutounga Mkono Upande WowoteKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Kutounga Mkono Upande Wowote
Maana: Msimamo wa wale wasiounga mkono upande wowote wala kusaidia upande wowote kati ya pande mbili au zaidi zinazoshindana. Ni wazi kwamba tangu zamani na hata leo, katika kila taifa na katika hali mbalimbali, Wakristo wa kweli wamejitahidi kutounga mkono hata kidogo mapigano kati ya vikundi vya ulimwengu. Hawawazuii watu wengine wasifanye yale wanayotaka kuhusu kushiriki katika sherehe za kizalendo, kujiunga na jeshi, kujiunga na chama cha kisiasa, kugombea cheo cha kisiasa, au kupiga kura. Lakini wao wenyewe wanamwabudu Yehova peke yake, Mungu wa Biblia; wameweka maisha yao wakfu kabisa kwake nao wanaunga mkono kikamili Ufalme wake.
-