-
Uwe Mwenye Furaha Waonyeshe Kibali Walio na ShidaMnara wa Mlinzi—1986 | Oktoba 15
-
-
Uwe Mwenye Furaha Waonyeshe Kibali Walio na Shida
“Mwenye kudharau mwanadamu mwenzake anatenda dhambi, lakini mwenye furaha ni yeye anayewaonyesha kibali wenye kusumbuka.”—Mithali 14:21, NW.
1, 2. Ni jambo gani lililotukia kwa jamaa tatu za Ufilipino, nalo linatuongoza tufikirie maulizo gani?
JAMAA tatu za Ufilipino zilipokuwa zikihudhuria mkutano wa Kikristo katika Mkoa wa Pangasina, moto usiotazamiwa uliteketeza nyumba zao zikawa majivu. Waliporudi nyumbani, walijikuta hawana chakula wala mahali pa kulala. Wakristo wenzao, walipopata habari juu ya msiba huo, walifanya haraka kwenda kule wakiwa na chakula na wakawapangia mahali pa kulala katika nyumba za wengine kundini. Asubuhi iliyofuata, Wakristo walifika wakiwa na mianzi na vifaa vingine vya kujengea. Upendo huo wa kidugu uliwavutia sana jirani. Jamaa zile tatu zilivutwa pia kwa njia njema. Moto ule uliharibu nyumba zao, lakini imani yao na sifa nyingine ya Kikristo ziliokoka zikaongezeka kwa sababu ya itikio hilo lenye upendo.—Mathayo 6:33; linganisha 1 Wakorintho 3:12-14.
2 Je! mambo yaliyoonwa kama hili hayachangmshi moyo? Yanajenga imani yetu katika fadhili za kibinadamu na hata zaidi ya hivyo katika Ukristo wa kweli. (Matendo 28:2) Ingawa hivyo, Je! tunauthamini msingi wa Kimaandiko wa ‘kuwatendea watu wote mema kwa njia hiyo; na hasa jamaa ya waaminio’? (Wagalatia 6:10) Na ni kwa njia gani sisi binafsi tunaweza kufanya mengi zaidi kuhusu jambo hilo?
Kielelezo Bora kwa Ajili Yetu
3. Tunaweza kuwa na uhakika juu ya nini kuhusu jinsi Yehova anavyotuhangaikia?
3 Mwanafunzi Yakobo anatuambia hivi: “Kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu hutoka juu.” (Yakobo 1:17, NW) Hiyo ni kweli sana kama nini, kwa maana Yehova anatuandalia vitu tele kwa faidi yetu ya kiroho na kimwili! Lakini, yeye anatanguliza mambo gani kati ya hayo. Ni mambo ya kiroho. Kwa mfano, yeye alitupa sisi Biblia ili tuwe na uongozi wa kiroho na tumaini. Tumaini hilo linategemea zawadi ya kumtoa Mwanaye, ambaye dhabihu yake ndiyo msingi wa kusamehewa kwetu na kuwa na taraja la uzima wa milele.—Yohana 3:16; Mathayo 20:28.
4. Inaonekanaje wazi kwamba Mungu anapendezwa na mahitaji yetu ya kimwili pia?
4 Yehova anapendezwa na masilahi yetu ya kimwili pia. Mtume Paulo alizungumza jambo hilo kwa kuwapa sababu wanaume waliokuwa katika mji wa kale wa Listra. Ingawa wao hawakuwa waabudu wa kweli, hawangeweza kukana kwamba Muumba ‘hakutenda mema, akitupa sisi mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akitushibisha mioyo yetu chakula na furaha.’ (Matendo 14:15-17) Kwa sababu ya upendo, Yehova anatutolea mahitaji yetu ya kiroho na pia anatufanyia uandalizi kwa ajili ya maisha yetu ya kimwili. Je! wewe hufikiri kwamba kutenda hivyo kunashiriki kumfanya awe ndiye yule “Mungu mwenye furaha”?—1 Timotheo 1:11, NW.
5. Tunaweza kujifunza nini kutokana na shughuli za Mungu pamoja na Israeli wa kale?
5 Shughuli za Mungu pamoja na Israeli wa kale zinaonyesha jinsi yeye anavyoangalia kwa usawaziko mahitaji ya kiroho na hali ya kimwili ya waabudu wake. Kwanza, yeye alifanya Sheria ipatikane kwa watu wake. Wafalme wake walipaswa watayarishe nakala yao binafsi ya Sheria, na watu walikusanyika pindi kwa pindi wasikie Sheria yake ikisomwa. (Kumbukumbu la Torati 17:18; 31:9-13) Sheria ilifanya uandalizi kuwe na hema takatifu au hekalu na makuhani wa kushughulikia dhabihu ili watu waweze kuwa na kibali cha Mungu. Waisraeli walikusanyika kwa ukawaida kwa ajili ya siku za sherehe za kiroho, ambazo zilikuwa mambo makuu katika ibada yao ya kila mwaka. (Kumbukumbu la Torati 16:1-17) Kwa sababu ya yote hayo, Waisraeli mmoja mmoja wangeweza kuwa matajiri kiroho mbele za Mungu.
6, 7. Katika Sheria Yehova alionyeshaje kuhangaikia mahitaji ya kimwili ya Waisraeli?
6 Ingawa hivyo, Sheria ilionyesha wazi pia jinsi Mungu anavyoangalia hali za kimwili za watumishi wake. Labda wazo linaloingia akilini mwako ni juu ya sheria walizopewa Israeli kuhusu mipango ya afya na hatua za kupunguza kuenea kwa maambukizo. (Kumbukumbu la Torati 14:11-21; 32:10-14) Hata hivyo haitupasi tusahau maandalizi ya pekee ambayo Mungu alifanya asaidie waliokuwa maskini na wenye shida. Afya mbaya au msiba kama kutokea kwa moto au gharika, ni mambo ambayo yangeweza kuingiza Mwisraeli katika umaskini. Yehova alikubali wazi mle mle ndani ya Sheria yake kwamba si watu wote wangekuwa sawa kiuchumi. (Kumbukumbu la Torati 15:11) Lakini yeye hakuwahurumia tu maskini na wenye shida bali alifanya zaidi ya hilo. Alipanga kuwapa msaada.
7 Uhitaji wa mara hiyo kwa watu kama hao ungekuwa chakula. Kwa hiyo Mungu alielekeza kwamba maskini katika Israeli wawe huru kuokota-okota mazao yaliyosalia katika mashamba ya nafaka na mashamba ya mizabibu au kutokana na mizeituni. (Kumbukumbu la Torati 24:19-22; Mambo ya Walawi 19:9, 10; 23:22) Njia ya Mungu haikutia watu moyo wawe wavivu wala waishi kwa kutegemea kupewa-pewa misaada ya umma hali wangeweza kufanya kazi. Mwokotaji Mwisraeli alipaswa kufanya jitihada, labda atumie saa nyingi akichomwa na jua kali ili akusanye chakula cha siku hiyo. Lakini, haitupasi tukose kuangalia kwamba kwa njia hiyo Mungu aliwapa riziki waliokuwa maskini kwa kuifikiria hali yao.—Linganisha Ruthu 2:2-7; Zaburi 69:33; 102:17.
8. (a) Wayahudi mmoja mmoja walihimizwa wafanye nini kwa ajili ya ndugu zao. (Linganisha Yeremia 5:26, 28) (b) Wewe ungelinganishaje mwelekeo ambao Mungu alihimiza Wayahudi wawe nao na ule wa watu wengi leo?
8 Yehova alizidi kukazia kupendezwa kwake na wenye shida kwa kutoa matangazo rasmi kama lile lililo kwenye Isaya 58:6, 7, NW. Katika wakati ambao Waisraeli fulani wenye kinaya walikuwa wakisingizia tu kwamba wanafunga, nabii wa Mungu alitangaza hivi: “Je! huku siko kufunga ninakochagua mimi? . . . Kuwaacha waliopondwa waende wakiwa huru, na kwamba ninyi watu mvunje katika vipande viwili kila ufito wa nira? Je! si kugawanya mkate wako umpe mwenye njaa, na kwamba uwalete watu wenye kusumbuliwa, wasio na makao ndani ya nyumba yao? Kwamba, ukiona mtu fulani aliye uchi, ni lazima umfunike, na kwamba haikupasi ujifiche kutoka kwa mwili wako mwenyewe?” Watu fulani leo wanalinda kile kinachoweza kuitwa ‘ukanda wa faraja!’ walichojiwekea. Wao wana nia ya kusaidia mtu mwenye uhitaji ikiwa tu kufanya hivyo hakumaanishi kwamba wadhabihu jambo lo lote la kibinafsi au la kuwasumbua. Ni roho tofauti kama nini iliyokaziwa katika maneno ya Mungu kupitia Isaya!—Ona pia Ezekieli 18:5-9.
9. Sheria ilitoa shauri gani juu ya kufanya mikopo, na Mungu alitia moyo juu ya kuwa na mwelekeo gani?
9 Kujali ndugu maskini, Waisraeli kungeweza kuonyeshwa katika kutoa mikopo. Mwisraeli angeweza kutazamia kulipwa riba anapomwazima pesa mtu fulani aliyetaka kuzitumia afanye biashara yake au aipanue. Lakini, Yehova alisema riba isitozwe juu ya pesa alizoazimwa ndugu maskini au sivyo shida yake kubwa ingeweza kumshawishi aingie katika kosa. (Kutoka 22:25; Kumbukumbu la Torati 15:7, 8, 11; 23:19, 20; Mithali 6:30, 31) Mwelekeo wa Mungu juu ya wasiofanikiwa sana ulipasa uwe kiolezo kwa watu wake. Hata tunaahidiwa hivi: “Yeye anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamwazima Yehova, na Yeye atamlipa huyo kwa tendo lake.” (Mithali 19:17, NW) Ebu wazia hilo—kumwazima Yehova, ukiwa na uhakikisho wake kwamba atakulipa kwa wingi!
10. Baada ya kuufikiria mfano wa Mungu, wewe ungeweza kujiulizaje?
10 Hivyo imetupasa sisi sote tuulize hivi: Maoni ya Mungu na kutendea kwake wenye kusumbuka humaanisha nini kwangu? Je! mimi nimekuwa nikijifunza kutokana na kielelezo chake kikamilifu na kujaribu kukiiga? Je! mimi naweza kufanya maendeleo ya kuwa katika mfano wa Mungu katika jambo hili?—Mwanzo 1:26.
Kama Baba, Kama Mwana
11. Maoni ya Yesu yalilinganaje na ya Baba yake? (2 Wakorintho 8:9)
11 Yesu Kristo ndiye “mng’ao wa utukufu wake [Yehova] na chapa ya nafsi yake.” (Waebrania 1:3) Kwa hiyo, tungemtazamia yeye aonyeshe anawajali kama Baba yake wale wanaopendezwa na ibada ya kweli. Hivyo ndivyo alivyofanya. Yesu alionyesha kwamba umaskini unaohitaji kuondolewa zaidi ya mwingine wo wote ni umaskini wa kiroho: “Wenye furaha ni wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao.” (Mathayo 5:3, NW; linganisha Luka 6:20.) Kristo alisema hivi pia: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili mimi nimekuja kuingia ndani ya ulimwengu, kwamba nipaswe kutoa ushuhuda kwa ule ukweli.” (Yohana 18:37, NW) Kwa hiyo, yeye hakujulikana kuwa mfanya-miujiza hasa wala mponyaji bali Mwalimu. (Marko 10:17-21; 12:28-33) Kuhusiana na jambo hilo, angalia Marko 6:30-34. Tunasoma juu ya wakati ambao Yesu alikuwa ametafuta wakati fulani wa faragha ili apumzike kidogo. Ndipo “akaona mkutano mkuu . . . [ambao] walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji.” Yeye alitendaje? “Akaanza kuwafundisha mambo mengi.” Ndiyo, Yesu alijipanua kwa kuitikia uhitaji wao uliokuwa mkubwa zaidi: ukweli ambao kwao wangeweza kuishi milele.—Yohana 4:14; 6:51.
12. Tunaweza kujifunza nini juu ya maoni ya Yesu kutokana na Marko 6:30-34 na Marko 6:35-44?
12 Ingawa Yesu alikaza fikira juu ya mahitaji ya kiroho ya Wayahudi wa hali ya chini, yeye hakupuuza mahitaji yao ya kimwili. Masimulizi ya Marko yanaonyesha kwamba Yesu alikuwa chonjo kuona uhitaji wa chakula halisi. Kwanza mitume walidokeza kwamba umati huo uambiwe waende zao “wakajinunulie chakula.” Yesu hakukubali. Halafu mitume wakautaja uwezekano wa kuchukua nyingine za pesa zilizokuwa za kufanyia kazi yao ambazo walikuwa wakitembea nazo, kisha watumie hizo kununua chakula. Badala ya hivyo, Yesu alitambua kuufanya ule muujiza unaojulikana sana alioutumia kulisha wanaume 5,000, bila kuhesabu wanawake na watoto, kwa kuwapa chakula cha msingi cha mkate na samaki. Watu wengine leo wangeweza kuwa na maoni ya kwamba lilikuwa jambo rahisi Yesu kutosheleza mahitaji ya umati kwa njia ya muujiza. Hata hivyo, tusikose kuuona uhakika wa kwamba yeye alikuwa na hangaikio la kweli, na akachukua hatua.—Marko 6:35-44; Mathayo 14:21.a
13. Yesu alionyesha ushuhuda gani mwingine wa kwamba alipendezwa na masilahi ya watu?
13 Labda wewe umesoma masimulizi ya vitabu vya Injili yanayothibitisha kwamba hisia za Yesu kwa ajili ya watu wasio na mafanikio zilipanuliwa kwa wengi zaidi ya maskini. Yeye alisaidia wagonjwa na wenye kusumbuka pia. (Luka 6:17-19; 17:12-19; Yohana 5:2-9; 9:1-7) Wala hakuwa akiponya wale waliokuwa karibu na yeye tu. Nyakati nyingine alisafiri mahali alikokuwa mgonjwa ili amsaidie.—Luka 8:41-55.
14, 15. (a) Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu alitazamia wafuasi wake waonyeshe wazi mahangaikio kama yake? (b) Ingefaa sisi tujiulize nini?
14 Lakini, Je! waliopaswa kujali mahitaji ya wanafunzi (au watafutaji ukweli) maskini na wenye kusumbuka ni wale tu ambao wangeweza kutoa msaada kwa kufanya miujiza? Hapana. Wanafunzi wote wa Yesu walipaswa wahangaike na kutenda kwa njia yenye kuonyesha hivyo. Kwa mfano, yeye alihimiza mwanamume tajiri aliyetaka uzima wa milele afanye hivi: “Viuze ulivyo navyo vyote, ukawagawanyie maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni.” (Luka 18:18-22) Yesu alishauri hivi pia: “Ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa [mwenye furaha], kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki.”—Luka 14:13, 14.
15 Mkristo ni mfuasi wa Kristo, kwa hiyo kila mmoja wetu angeweza kuuliza hivi: Ni kwa kadiri gani mimi ninaiga mwelekeo na vitendo vya Yesu kuhusu maskini, wenye kusumbuka, wasiofanikiwa sana? Je! mimi naweza kusema kwa unyofu kama mtume Paulo: “Iweni waigaji wangu mimi, kama mimi ninavyoiga Kristo”?—1 Wakorintho 11:1, NW.
Paulo—Mfano Wenye Furaha
16. Ni jambo gani lililompendeza mtume Paulo kwa njia ya pekee?
16 Inafaa kumtaja Paulo katika habari hii, kwa maana yeye pia alikuwa mfano mzuri wa kuigwa. Kama vile ambavyo tungetazamia, kazio lake la msingi lilikuwa mahitaji ya kiroho ya wengine. Yeye alikuwa ‘balozi badala ya Kristo, akiomba wengini hivi, “Mpatanishwe kwa Mungu.” ‘ (2 Wakorintho 5:20, NW) Mgawo wa pekee wa Paulo ulikuwa kuhubiri na kujenga makundi kati ya watu wasio Wayahudi. Yeye aliandika hivi: “Nimekabidhiwa injili ya wasiotahiriwa.—Wagalatia 2:7.
17. Tunajuaje kwamba Paulo alielekeza fikira kwenye mahangaiko ya kimwili pia?
17 Lakini kwa kuwa Paulo alisema alikuwa akiiga Kristo, Je! yeye (kama Yehova na Yesu) aliangalia masumbuko ya kimwili au magumu ya waabudu wenzake? Acheni Paulo mwenyewe ajibu. Katika Wagalatia 2:9, yeye aliendelea kusema ‘Yakobo na Kefa [Petro] na Yohana walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa shirika, ili sisi tuende kwa mataifa.’ Halafu katika mstari ule ule unaofuata Paulo akaongeza hivi: “Tuwakumbuke maskini; nami neno lilo hilo nalikuwa na bidii kulifanya.” (Wagalatia 2:10) Kwa hiyo Paulo alithamini jambo la kwamba, ingawa yeye alikuwa mmisionari-mtume mwenye madaraka kwa makundi mengi, yeye hangeweza kuwa mwenye shughuli mno asiweze kupendezwa na masilahi ya kimwili ya ndugu na dada zake.
18. Ni “maskini” gani ambao inaelekea Paulo alikuwa akitaja katika Wagalatia 2:10, na kwa sababu gani wangalipaswa kufikiriwa?
18 Inaelekea kwamba “maskini” aliosema juu yao katika Wagalatia 2:10 walikuwa Wakristo Wayahudi hasa katika Yerusalemu na Yudea. Mapema kabla ya hapo kulikuwa kumekuwa na “manung’uniko . . . kwa upande wa Wayahudi wenye kusema Kigiriki dhidi ya Wayahudi wenye kusema Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa wakikosa kuangaliwa katika ugawaji wa kila siku” wa chakula. (Matendo 6:1, NW) Hivyo, wakati Paulo alipokuwa akitaja kwamba yeye alikuwa mtume kwa mataifa, alieleza wazi kwamba hakuwa akikosa kujali mtu ye yote katika udugu wa Kikristo.(Warumi 11:13) Yeye alithamini kwamba kutunza akina ndugu kimwili kulitiwa ndani ya maneno haya: “Kusiwe na faraka katika mwili, bali viungo vitunzane kila kiungo na mwenziwe. Na kiungo kimoja kikiumia, viungo vyote huumia nacho.”—1 Wakorintho 12:25, 26.
19. Tuna uthibitisho gani kwamba Paulo alichukua hatua ya kuonyesha kuhangaikia maskini?
19 Wakati Wakristo katika Yerusalemu na Yudea walipotaabika kwa sababu ya umaskini, njaa katika eneo lao, au mateso, makundi fulani ya mbali yalichukua hatua. Bila shaka, ingetazamiwa kwamba walikuwa wakikumbuka ndugu zao wenye uhitaji katika sala za kuomba Mungu awasaidie na kuwafariji. Lakini hawakuachia hapo. Paulo aliandika kwamba “wale katika Makedonia na Akaya wamependezwa kugawana vitu vyao kwa kutoa mchango kwa maskini wa watakatifu katika Yerusalemu.” (Warumi 15:26, 27, NW) Wale waliotolea ndugu zao wenye kusumbuka michango hiyo ya kifedha ‘walikuwa wakitajirishwa katika vitu vyote wapate kuwa na ukarimu wote, umpatiao Mungu shukrani kwa kazi yetu.’ (2 Wakorintho 9:1-13) Je! hicho hakingekuwa kisababishi cha kuwafanya wafurahi?
20. Kwa sababu gani akina ndugu waliotoa michango kusaidia “maskini” wangeweza kuwa wenye furaha?
20 Akina ndugu waliogawana pesa zao na “maskini wa watakatifu katika Yerusalemu” walikuwa na msingi wa ziada wa kupata furaha. Kuwajali wenye kusumbuka kungesaidia wachangaji hao wapate kibali cha Mungu. Tunaweza kuona sababu kwa kuangalia kwamba neno la Kigiriki lililotafsiriwa “mchango” katika Warumi 15:26 na 2 Wakorintho 9:13 lina wazo la “ishara ya ushirika, uthibitisho wa umoja wa kidugu, hata zawadi.” Limetumiwa kwenye Waebrania 13:16, NW linalosema hivi: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana dhabihu kama hizo Mungu anapendezwa sana nazo.”
Je! Sisi Tutakuwa Wenye Furaha?
21. Tunaweza kukata shauri kwamba ni jambo gani litatutolea msingi wa kupata furaha?
21 Katika mazungumzo haya, tumechunguza ushuhuda wa Kimaandiko wa kuonyesha kwamba Yehova Mungu, Yesu Kristo, na mtume Paulo walijali wenye kusumbuka. Tumeona kwamba wote kati yao walitambua kwamba mahitaji ya kiroho ndiyo yanayopasa kuelekezewa fikira kwanza. Lakini ni kweli pia kwamba wote walionyesha kwa njia zenye mafaa kuwa walipendezwa na maskini; wagonjwa, na wale wenye kukosa kufanikiwa. Wangeweza kupata furaha kwa kutoa msaada wenye mafaa. Je! sisi nasi tusifanye hivyo? Paulo mwenyewe alituhimiza “kukumbuka yale maneno ya Bwana Yesu, wakati yeye mwenyewe aliposema, ‘Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.’”—Matendo 20:35, NW.
22. Ni mambo gani ya habari hii ambayo bado yanastahili kuelekezewa fikira zako?
22 Ingawa hivyo, huenda wewe ukauliza hivi: “Ni mambo gani hasa ambayo mimi binafsi naweza kufanya? Naweza kujuaje wale walio na uhitaji kikweli? Naweza kutoaje msaada kwa njia isiyotia moyo kuwa na uvivu, ambayo ni ya fadhili na yenye kufaa, inayofikiria hisia za wengine, na yenye usawaziko pamoja na wajibu wangu wa Kikristo wa kuzieneza habari njema? Makala inayofuata itashughulika na mambo hayo, ikuwekee msingi wa kupata furaha ya ziada.
-
-
Fanya Zaidi ya Kusema Tu: ‘Ukaote Moto na Kushiba’Mnara wa Mlinzi—1986 | Oktoba 15
-
-
Fanya Zaidi ya Kusema Tu: ‘Ukaote Moto na Kushiba’
“Ikiwa . . . mtu wa kwenu [anawaambia ndugu wenye uhitaji], Enendeni zenu kwa amani, mkaote moto na kushiba, lakini asiwape mahitaji ya mwili, yafaa nini?. . . Imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake.”—YAKOBO 2:15-17.
1. Ndugu mmoja katika Naijeria aliingiaje katika uhitaji?
INAHESABIWA kwamba Lebechi Okwaraocha alizaliwa kabla ya mwaka 1880, kwa hiyo umri wake umepita sana miaka mia moja. Yeye alirithi uchawi wa wazazi wake Wanaijeria na akauabudu. Halafu, alipokuwa katika umri wa miaka 80 na kitu, akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alitumia mambo aliyojifunza akabatizwa. Hivyo yeye amekuwa Shahidi kwa miaka karibu 30. Juzijuzi, wazee kutoka kundi lake walimtembelea yeye na mke wake Mwanglikana mwenye umri wa miaka 72 baada ya kumwagika mvua nyingi sana. Wote wawili walikuwa wamekata tumaini—sakafu ya kijumba chao kilichoezekwa kwa nyasi ilikuwa imefunikwa maji, na hawakuwa na watu wa ukoo wao ambao wangewapa mahali pa kulala au kuwasaidia watengeneze sehemu zilizoharibika. Kama wewe ungalikuwako, ungalifanya nini? Kabla ya kujua ni jambo gani lililotukia, acheni tufikirie mashauri fulani ya Biblia.
2. Kwa sababu gani sisi Wakristo tunapendezwa na “matendo mema”?
2 Kristo Yesu “alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili . . . kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema.” (Tito 2:14) Matendo hayo yanategemea yale mahubiri yenye kuokoa uhai yanayohusu Ufalme. (Marko 13:10; Ufunuo 7:9, 10) Lakini, “matendo mema” ya Kikristo yanatia ndani mambo mengi zaidi ya ile kazi ya maana ya kuhubiri, kwa maana Yakobo ndugu mzazi mmoja na Yesu alieleza hivi: “Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo na mawaa.”—Yakobo 1:27.
3, 4. Tunaweza kujifunza nini kutokana na 1 Timotheo sura za 3-5 juu ya “matendo mema,” na hiyo ikiongoza kwenye maulizo gani?
3 Makundi katika karne ya kwanza yalihusika katika aina zote mbili za “matendo mena.” Baada ya kutaja orodha za sifa za waangalizi na watumishi wa huduma, mtume Paulo aliandika katika 1 Timotheo sura ya 3 kwamba “kundi la Mungu aliye hai [ni] nguzo na tegemezo la ukweli.” (1 Timotheo 3:1-15, NW) Yeye alionyesha kwamba Wakristo wanaobaki wakifuata mafundisho haya ya ukweli wangeweza kujiokoa wenyewe na wale wanaowasikiliza. (1 Timotheo 4:16) Halafu Paulo akalizungumza ‘tendo jema’ la kuwatunza kimwili wajane waaminifu waliokuwa ‘hawana kitu kabisa.’—1 Timotheo 5:3-5, NW.
4 Kwa hiyo, zaidi ya kufanya kazi yetu ya kueneza evanjeli, inatupasa tuwe tukielekeza fikiria kwenye “matendo mema,” kama vile ‘kuwatunza yatima na wajane katika dhiki yao.’ Wazee na watumishi wa huduma wanaweza kufanya nini katika habari hiyo, wakiwa ndio wale wenye kuongoza’? (Waebrania 13:17) Wengine kati yetu tunaweza kuwasaidiaje katika jambo hilo? Na sisi binafsi tunaweza kufanya nini tutende “matendo mema” ya namna hiyo?
Wazee Wanaongoza Vizuri
5. Paulo alitimizaje uhitaji wa pekee, na kuna ulinganifu gani wa kisasa?
5 Uhitaji Wa pekee ulipotokea katika Yudea, Paulo, mzee, aliongoza katika kupanga huduma ya usaidizi kwa wenye shida. Uongozi huo ulipunguza sana mvurugo wo wote; vitu vingeweza kugawanywa kwa usawa, kulingana na uhitaji. (1 Wakorintho 16:1-3; Matendo 6:1, 2) Wazee wa kisasa, pia, wameongoza katika kutoa huduma za usaidizi kwa wenye shida baada ya mafuriko yenye maafa, maporomoko ya matope ya milima, mawimbi ya bahari, tufani, au matetemeko ya ardhi, hivyo ‘wakiangalia mambo ya wengine.’—Wafilipi 2:3, 4.
6. Wakati maafa yalipotokea katika Kalifornia U.S.A., wazee waliitikiaje?
6 Gazeti Amkeni! (la Kiingereza) la Oktoba 1986, lilitoa mfano wa Ukristo wa namna hiyo ukifanya kazi. Wazee walichukua hatua wakati ukuta uliobomoka ulipofanya maji ya mto yafurike katika Kalifornia, U.S.A. Wachungaji hao wa kiroho walifanya haraka kwenda kuangalia kundi lao lote waone ni akina nani huenda wakawa wamekosekana au walio na uhitaji wa matibabu, chakula, au mahali pa kulala. Wazee hao waliunganisha jitihada zao na afisi ya makao makuu ya Mashahidi wa Yehova. Halmashauri ya usaidizi kwa wenye shida ilianzishwa, na wakati Mashahidi wenzao walipokuwa wakifika kusaidia, walipangwa katika vikundi-vikundi ili kuondoa takataka na kutengeneza nyumba zilizoharibika. Wazee walisimamia ununuzi na ugawaji wa vifaa pia. Jambo hilo linaonyesha kwamba wakati mahitaji ya pekee yanapotokea, ‘kila mwanafunzi anaweza kuazimu kupeleka msaada kwa kadiri ile anayoweza kutoa’ au kufanya, lakini lingekuwa jambo la hekima kuwauliza waangalizi wa mahali pao wapate kwao mielekezo.—Linganisha Matendo 11:27-30.
7. Ni mahitaji gani yanayopatikana kwa ukawaida zaidi ambayo hata sisi tunapaswa kuitikia?
7 Ingawa wewe (mzee au si mzee) unaweza pindi kwa pindi kuitikia utoe msaada kwa uhitaji mkubwa baada ya maafa, kuna mahitaji yanayopatikana kwa wingi zaidi ambayo yanaweza kuwa ya maana jinsi ile ile—yale yaliyo mle mle kundini mwenu. Kwa sababu huenda mahitaji hayo yasiwe ya kushtua sana kama tukio kubwa la maafa, yanaweza kwa urahisi kutokuangaliwa au kushughulikiwa bila kujali sana. Lakini kwa kweli mahitaji ya mahali ndiyo ya namna iliyotajwa katika Yakobo 2:15-17. Ndiyo, huenda kundi lenu likawa na hali yenye kutokeza jaribu lililo kubwa zaidi la kama ‘imani yako ina matendo, au imekufa nafsini mwako.’
8. Waangalizi wanaweza kuonyeshaje hekima katika kushughulikia mahitaji yaliyo katika kundi?
8 Katika kutoa uongozi, wazee wamepaswa wawe “na hekima na ufahamu.” (Yakobo 3:13) Kwa kutumia hekima wanaweza kulinda kundi na wadanganyifu wanaotoka kwa ndugu huyu kwenda kwa ndugu yule (au kutoka kundi moja kwenda kundi jingine) wakikopa pesa au wakijitungia hadithi ili wapate “msaada” ati. Kwa hekima waangalizi hawaungi mkono uvivu, kwa maana kanuni ya Biblia ni hii: “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.” (2 Wathesalonike 3:10-15) Hata hivyo, wao hawataki ‘kuufunga mlango wa huruma nyororo zao wenyewe’ wala kuongoza ndugu zao wafanye hivyo. (1 Yohana 3:17. NW) Sababu nyingine kwa nini ni lazima waonyeshe hekima ni kwamba Biblia haitupi sisi sheria zisizo na mwisho juu ya kuwatunza wenye uhitaji na wenye kusumbuka. Hali zinatofautiana kipindi hiki na kipindi hiki na mahali hapa na mahali hapa.
9. (a) Wajane Wakristo wenye kustahili walitunzwaje katika karne ya kwanza? (b) Ni msaada wa namna gani ambao wajane hao wanaweza kufaidika nao leo?
9 Kwa mfano, katika 1 Timotheo 5:3-10 Paulo alizungumza juu ya wajane wenye kustahili waliokuwa ‘wameachwa bila kitu kabisa.’ Watu wa ukoo wao walioamini ndio waliokuwa na daraka la kwanza la kuwasaidia; kutokujali wajibu huo kungeweza kuharibu msimamo wa watu wa ukoo pamoja na Mungu. Ingawa hivyo, kama mjane mwenye uhitaji na mwenye kustahili hangeweza kupata msaada kwa njia hiyo, iliwezekana wazee wapange apate msaada fulani wa kimwili kutoka kwenye kundi. Katika nyakati za hivi majuzi, pia, makundi fulani yamesaidia walio na shida hasa katikati yao. Lakini, nchi zilizo nyingi zinatumia kodi ili kuendesha programu za kusaidia watu wazee-wazee, wenye miili dhaifu, au wale walio na nia ya kufanya kazi lakini wasioweza kuipata. Ingawa hivyo huenda wazee Wakristo wakataka kusaidia kwa njia nyingine. Wengine walio na uhitaji wa kweli na ambao wanastahili kabisa kupata zile faida ambazo serikali inatolea watu wote hawazipokei kwa sababu hawajui jinsi ya kupeleka maombi ya msaada huo au ni waoga mno wasiweze kuuomba. Hivyo wazee wanaweza kuuliza habari hizo kwenye mashirika ya kiserikali au wawaendee Mashahidi walio na ujuzi wa mambo hayo. Halafu wanaweza kupanga ndugu au dada hodari asaidie mtu yule mwenye uhitaji kuzipokea faida zinazopatikana.—Warumi 13:1, 4.
Kufanya Mipango ya Kutoa Msaada Wenye Mafaa
10. Wanapolichunga kundi, wazee wanapaswa kuelekeza fikira kwenye nini?
10 Mara nyingi waangalizi walio chonjo ndio wanaokuwa ufunguo wa kuona kwamba Wenye kusumbuka na wenye uhitaji wanapokea msaada kutoka kwa ndugu na dada wenye upendo. Wazee wanapaswa kuwa chonjo kuona mahitaji ya kiroho na kimwili wanapochunga wote walio kundini. Ni wazi kwamba wazee wanaangalia zaidi ‘sala na huduma ya lile neno.’ (Matendo 6:4, NW) Kwa hiyo, wao wangejaribu kupanga mambo ili washiriki wa kundi waliolemewa kitandani au waliolazwa hospitali walishwe kiroho. Wazee wanaweza kupanga mambo yanayosemwa mikutanoni yarekodiwe kwa ajili ya wale wasioweza kuhudhuria. Wazee na watumishi wa huduma wenye kupokezana zamu za kupeleka kanda wameona kwamba ziara zao zinawawezesha kuwapa watu hao zawadi nyingine za kiroho. (Warumi 1:11, 12) Wakati uo huo, wanaweza kuchunguza mahitaji ya mtu ya wakati huo.
11. Toa mfano wa jinsi dada mwenye uhitaji anavyoweza kupangiwa usaidizi.
11 Huenda wakaona kwamba dada fulani mwenye kizuizi cha kimwili au aliye mzee-mzee angeweza kuja kwenye Jumba la Ufalme nyakati nyingine, au ashiriki kwa ufupi katika huduma ya shambani, dada fulani akimsaidia kuoga na kuvaa. (Linganisha Zaburi 23:1, 2, 5.) Waangalizi hata wangeweza kumpa mmoja wao mgawo wa kufanya mipango hiyo. Vivyo hivyo, wanaweza kuomba kundi litokeze wenye kujitolea kusafiri pamoja na mtu mwenye kusumbuliwa au kumsafirisha kwa gari. Kupanga ratiba ya jambo hilo kungefanya mambo yaendeshwe kwa utaratibu hata zaidi.
12. Wengine wanaweza kufanyaje kazi pamoja na waangalizi katika kusaidia wagonjwa au walio wazee-wazee?
12 Huenda wazee wakaona mambo mengine ambayo yangeweza kuhitaji msaada utolewe au mipango yenye upendo ifanywe. Kwa mfano, tuseme kuna dada mzee-mzee au mgonjwa ambaye amekuwa hawezi kutunza nyumba yake kama hapo kwanza. Je! watu fulani kati ya watumishi wa huduma na wengine wangeweza kusaidia? Wakimkatia majani yaliyo katika uwanja wa nyumba yake au kumtengenezea maua aliyopanda huenda akajisikia vizuri zaidi, kwa sababu anajua kwamba sasa nyumba yake haileti suto katika ujirani. Je! bustani inahitaji kupaliliwa au kunyunyiziwa maji? Je! dada fulani anayeenda dukani kununua vitu angeweza kuwa na nia ya kumpitia ili aone anahitaji nini kisha kwenda kumfanyia ununuzi wa vitu vinavyohitajiwa? Kumbuka mitume walipendezwa na kutenda mambo hayo yenye mafaa, nao wakawapanga watu hodari katika kundi wasaidie.—Matendo 6:1-6.
13. Matokeo yalikuwa nini wazee waliposaidia yule ndugu Mnaijeria aliyetajwa mapema?
13 Tendo hilo la hangaikio la Kikristo lingeonyeshwa na wazee waliotajwa mapema ambao, walipokuwa wakifanya ziara ya uchungaji, walimkuta Lebechi Okwaraocha na mke wake wakiwa katika hali ya kusikitisha. Baraza la wazee lilifanya haraka kushughulikia jambo hilo na likajulisha kundi hatua waliyokusudia kuchukua—kujenga upya nyumba hiyo. Ndugu na dada mbalimbali walichanga vifaa na wakashiriki kwa nia katika shughuli hiyo. Katika muda wa juma moja, walijenga kijumba imara, kilichoezekwa kwa mabati. Habari hiyo inayotoka Naijeria inasema:
“Wanakijiji walishangaa na kwa kupenda kwao wakawaletea chakula na vinywaji ndugu na dada waliofanya kazi saa nyingi wamalize kazi hiyo kabla ya mvua kumwagika tena. Wanakijiji wengi walitoa lalamiko lao juu ya vikundi vingine vya kidini, wakasema wao wanapora vita vya watu badala ya kusaidia maskini. Kisa hiki kilikuwa ndiyo maongezi ya mtaa huo. Wanakijiji wameanza kuitikia sana, na mafunzo mengi ya nyumbani ya Biblia yameanzwa.
Ushiriki Wako Katika Haya “Matendo Mema”
14. Tunapaswa kuwa na maoni gani juu ya kufanyia ndugu zetu “matendo mema”?
14 Bila shaka, mara nyingi tunaweza kuitikia kwa faragha na moja kwa moja kuhusu mahitaji ya walio wazee-wazee, wenye udhaifu wa kimwili, waliolazwa hospitali, au wale wanaosumbuliwa na shida kwa njia nyingine walio karibu nasi. Tukiona njia ya kuonyesha Ukristo wa kweli, mbona tusichukue hatua na kujaribu kusaidia? (Matendo 9:36-39) Jambo linalotusukuma sisi, si kukazwa na wengine, bali ni upendo wa Kikristo. Hatua ya kwanza ya kutoa msaada wo wote wenye mafaa ni kupendezwa na watu kikweli na kuwa na huruma. Bila shaka, hakuna ye yote kati yetu anayeweza kufanya watu waliozeeka wawe vijana, kuponya ugonjwa kwa miujiza, wala kufanya hali ya kiuchumi ya wote kundini ilingane. Lakini kwa wazi kabisa inatupasa tuwe na roho ya kuhangaikia na ya kutoa. Tukiwa nayo, kisha tutende kulingana nayo, itatia nguvu kifungo cha upendo kati yetu na wale tunaosaidia. Ilifanya hivyo kati ya Paulo na Onesimo ambaye kwa kulinganishwa alikuwa Mkristo mpya ‘aliyemtumikia Paulo katika vifungo vyake gerezani.’—Filemoni 10-13; Wakolosai 3:12-14; 4:10, 11.
15. Tunaweza kusaidiaje watu fulani wanaostahili ambao wana uhitaji kikweli?
15 Nyakati nyingine tunaweza kuitikia uhitaji wa kimwili kwa kutoa zawadi ya fadhili, iwe imepelekwa bila kujulisha jina la aliyeitoa au imetolewa kwa faragha. Je! ndugu amepoteza kazi yake akawa hawezi kupata nyingine? Je! dada amepatwa na gharama zisizotazamiwa za matibabu; je! yeye amepatwa na aksidenti au vitu vyake vikachukuliwa na wanyang’anyi? Hali zinazofanana na hiyo huenda zikatokea karibu nasi. Tunapotoa “zawadi ya rehema” Baba yetu anayetazama katika siri ataona na kukubali tunavyofanya. (Mathayo 6:1-4, NW) Au, badala ya kutoa pesa, sisi kama Ayubu huenda tukaweza kuwapa maskini mavazi na kumpa mjane au yatima vitu vya kupika au vyakula tulivyopikia nyumbani.—Ayubu 6:14; 29:12-16; 31:16-22.
16. Ni katika njia gani nyingine yenye mafaa msaada unaweza kutolewa nyakati nyingine? Toa mfano.
16 Ujuzi wako au mambo ambayo umejionea mwenyewe kwa kukutana na watu yanaweza kuwa chanzo cha msaada wenye mafaa. Ndugu mmoja alimwuliza Ndugu W——ampe mkopo. Jibu lake la fadhili lilikuwa: ‘Kwa sababu gani wewe unaona kwamba mimi naweza kuwa na pesa zo zote za ziada za kukopesha?’ Jibu alilotoa lilikuwa: ‘Ni kwa sababu wewe unasimamia vizuri zaidi pesa zako.’ Kwa kutumia utambuzi, Ndugu W——aliyekuwa amekopesha wenye uhitaji pesa mara nyingi, alidokeza hivi: ‘Labda jambo ambalo wewe unahitaji kweli kweli ni msaada fulani wa kujua kusimamia pesa zako, nami ningefurahia kukusaidia ikiwa unataka msaada wangu.’ Msaada huo unathaminiwa sana na ndugu wanaohitaji kurekebisha kiwango chao cha maisha kipatane na hali mpya au walio na nia ya kufanya kwa bidii hata kazi ya namna isiyoheshimiwa sana. Bila shaka, ikiwa mkopo unahitajiwa kikweli, ingekuwa vizuri kutia sahihi maandishi ya kumbukumbu ili matatizo yo yote yasitokee baadaye. Hata hivyo ndugu wengi wasio na maelekeo ya kukopa pesa wangethamini sana kupata usaidizi wa kibinafsi kwa namna ya mashauri au kugawiwa ujuzi. (Warumi 13:8) Jambo hilo linaonyeshwa kwa mfano na jambo lililoonwa kutoka Afrika Magharibi linalohusu Emmanuel: Ingawa Emmanuel alikuwa kinyozi aliyezoezwa kazi yake, wenye kunyolewa walikuwa wachache, naye alivunjwa moyo na kutoweza kwake kupata riziki. Halafu mzee aliye chonjo katika kundi akamwuliza Emmanuel kama angefikiria kufanya kazi ya namna nyingine. Yeye akajibu Ndiyo, kwa maana hakutaka kuacha kiburi cha kazi aliyokuwa amesomea kimzuie kufanya hiyo nyingine. Mzee huyo alisema na washirika wake na akapata kazi kwa ajili ya Emmanuel ya kuwa mtumishi hospitalini. Yeye amefanya vizuri katika kazi hiyo na ameweza kusaidia wengine katika kundi.
17. Ni kwa njia gani huenda ukaweza kusaidia ndugu aliye katika hospitali? (Zaburi 41:1-3)
17 Wakati Mkristo mwenzetu anapokuwa katika hospitali au makao ya kutunzia wagonjwa, kunakuwa na nafasi za pekee za kusaidia. Hapa tena, mambo ya msingi ni kupendezwa naye kwa weupe wa moyo na kumjali. Wewe unaweza kuonyesha mambo hayo kwa kuwa na nia ya kusomea mgonjwa huyo vitabu vya Kikristo vyenye kujenga au kumsimulia mambo yaliyoonwa yenye kumtia moyo. Ingawa hivyo, Je! kuna mahitaji ya kimwili unayoweza kusaidia? Katika maeneo fulani, hospitali zinakuwa na kazi nyingi sana hata inakuwa mgonjwa hawezi kuoshwa wala kulishwa isipokuwa mgeni akija kufanya hivyo. Kwa hivyo, madaktari wakikubali, labda unaweza kumletea chakula cha kujenga mwili au kumsaidia aoshe nywele zake au aoge. Je! angethamini kupewa vazi lenye kumpasha moto au sapatu zenye kupasha moto? (2 Timotheo 4:13) Au je! unaweza kujitolea ukamsaidie mgonjwa jambo fulani linalomtia wasiwasi? Labda anahangaikia jinsi atakavyopokea mshahara wake na kulipa gharama zake za utumizi. Unaweza kumsaidia umtulize kwa kufanya hata mambo yaliyo rahisi kama vile kuhakikisha kwamba barua hazijazani nyumbani kwake bila ya yeye kupelekewa, au kwamba mimea aliyoipanda inatiliwa maji, au kwamba vipasha joto nyumbani vimezimwa.
18. Wewe umeazimia ufanye nini kuhusu ndugu walio katika uhitaji?
18 Bila shaka, kila mmoja wetu anaweza kupata njia ambazo tunaweza kufanya maendeleo katika kufanya kwetu zaidi ya kusema tu ‘ukaote moto na kushiba.’ (Yakobo 2:16) Wafikirie ndugu na dada katika kundi lako. Je! kuna watu fulani wenye kustahili walio na uhitaji wa kweli wa vitu vya kimwili, walio wagonjwa, wenye vizuizi vya kimwili, au waliolemewa kitandani? Ni jambo gani ambalo wewe unaweza kufanya kwa njia yenye mafaa usaidie washiriki hao wapendwa wa kundi ambao Kristo alifia? Kuwa na mwelekeo huo kutakusaidia uwe tayari zaidi kuitikia ikiwa magumu yanatokea.
19. (a) Kwa sababu gani usawaziko ni wa maana sana katika jambo hili? (b) Ni wema gani ulio mkubwa zaidi tunaoweza kufanyia wengine, na kwa sababu gani ndivyo ilivyo? (Zaburi 72:4, 16)
19 Kwa kujitahidi kusaidia ndugu zetu, tutakuwa tukithibitisha kwamba imani yetu haikufa. Imani iyo hiyo inatusukuma tutie bidii katika kazi ya Kikristo ya kuhubiri. Tunahitaji kudumisha usawaziko kati ya kusaidia wengine kimwili na kushiriki kwa ukawaida kazi ya Kikristo ya kueneza evanjeli. (Linganisha Mathayo 15:29; 23:23.) Shauri ambalo Yesu aliwapa Martha na Mariamu linaonyesha usawaziko huo. Yeye alisema kwamba kama mtu angekuwa akilinganisha uzito wa vitu vya kimwili na chakula cha kiroho, chakula cha kiroho ndicho kingekuwa “fungu lililo jema,” ambalo halitaondolewa. (Luka 10:39-42) Sikuzote wagonjwa na maskini watakuwapo katika mfumo huu wa mambo. Tunaweza kuwafanyia mambo mema na tunapaswa kutenda hivyo. (Marko 14:7) Hata hivyo, wema ulio bora na wenye kudumu zaidi ambao tunaweza kufanya ni kufundisha wengine juu ya Ufalme wa Mungu. Hilo ndilo jambo ambalo Yesu alikazia fikira. (Luka 4:16-19) Hiyo ndiyo njia ambayo maskini, wagonjwa, wenye kusumbuliwa, wanaweza kupokea kitulizo cha kudumu. Ni furaha kama nini kusaidia ndugu zetu na wengine wategemeze tumaini lao juu ya Mungu na ‘kuushika kwa imara uzima wa kweli kweli.’—1 Timotheo 6:17-19, NW.
Je! Wewe Unakumbuka
◻ Ni nini“matendo mema”yaliyo ya maana zaidi yanayopasa kufanywa na kundi la Kikristo?
◻ Wazee wa mahali wanaweza kutumiaje usawaziko waelekeze fikira juu ya kufanya “matendo mema” yanayohusu hali za kimwili za ndugu zao?
◻ Ni hatua gani zenye mafaa zinazoweza kuchukuliwa na wazee?
◻ Ni mambo gani yenye mafaa ambayo wewe unaweza kushughulikia usaidie ndugu au dada zako walio na uhitaji?
[Sanduku katika ukurasa wa 17]
Kundi Lilijali
Mume na mke waliokuwa wamehamia kundi dogo katika maeneo ya mashambani walitoa habari hii yenye kuamsha fikira:
‘Miaka mitatu iliyopita mke wangu na mimi tuliuza nyumba yetu tukahamia kundi la mbali lililohitaji usaidizi wa ukomavu kwa sababu kulikuwa kumekuwa na matatizo fulani. Upesi mimi nikawa na vyeo vinne vya madaraka. Sisi tulipenda ndugu zetu na tukataka kufanya kazi pamoja nao. Katika muda wa miezi iliyofuata roho ya kundi ikawa na maendeleo, na wazee wawili wazuri sana wakahamia.
‘Mke wangu akaanza kupatwa na matatizo ya afya, na mwaka jana alihitaji kupata upasuaji mkubwa. Siku aliyoingia hospitali, mimi nikalemewa na ugonjwa wa kufura ini. Miezi miwili baadaye, niliachishwa kazi kwa sababu hali ya uchumi katika eneo hilo ilikuwa mbaya sana. Pesa zetu ziliisha, nikawa sina kazi, na huku sisi sote wawili tulikuwa tukijaribu kurudiwa na afya yetu. Nilishuka moyo kwa sababu mkusanyiko wa wilaya ulikuwa ukikaribia nami nilikuwa na sehemu katika programu. Pia nilikuwa na mgawo katika kusanyiko la mzunguko ambalo lingekuja baada ya majuma kadha. Lakini kwa sababu sikuwa na pesa zo zote, sikujua ningewezaje kufika kwenye makusanyiko hayo au hata jinsi ningetunza jamaa yangu. Asubuhi moja mke wangu alienda katika utumishi wa shambani, nami nikaketi nirudie kuifikiria hali yetu.
‘Nilipokuwa nikitazama nje dirishani, nikajiuliza, Tumaini langu katika Yehova limeenda wapi? Mimi nilikuwa nimeambia mke wangu asiwe na wasiwasi, lakini sasa mimi nilikuwa nikianza kutia shaka. Ndipo nikamweleza Yehova kwamba nilikuwa na “imani haba” na kumwomba anisaidie. Nilipomaliza kusali, ndugu mmoja alipiga hodi mlangoni. Alitaka niende naye tukanywe kahawa. Nikamweleza afadhali nisiende, kwa maana ilinipasa kutayarisha sehemu ya mkutano wa usiku huo. Ingawa hivyo, yeye alisisitiza sana akisema kwamba tungeenda kwa dakika chache tu. Basi tukaenda.Tulirudi nusu saa baadaye, nami nilipokuwa nikitoka katika gari lake nikawa nikijisikia vizuri zaidi.
‘Nilipoingia ndani ya nyumba, nikaona kwamba ile meza ya jikoni ilikuwa imejazwa-jazwa vitu vilivyonunuliwa dukani. Nikawaza kwamba bila shaka mke wangu alikuwa ameenda kununua vitu hivyo dukani. “Lakini ngoja kidogo, haingeweza kuwa ni yeye kwa maana hatuna pesa zo zote.” Halafu nikaona bahasha. Upande wa mbele ulikuwa umeandikwa hivi:
“‘Kutoka kwa ndugu na dada zenu, ambao wanawapenda sana. Msiingize zo zote za hizo katika sanduku la michango. Ninyi mmekwisha kuingiziwa zenu tayari.”
‘Sikuweza kuzuia machozi yasinitoke. Mimi niliifikiria ile “imani haba” yangu, na jambo hilo likanifanya nilie zaidi. Halafu mke wangu akaja nyumbani. Mimi nilielekeza kidole changu kwenye chakula na zawadi nyingine zilizokuwapo. Yeye pia akaanza kulia, pamoja na wale dada wawili waliokuwa wamekuja pamoja naye. Sisi tulijaribu kueleza kwamba hatungeweza kukubali vitu vingi namna hiyo, lakini dada wale wakatuambia kwamba hakuna mtu aliyejua ni nani aliyetoa hiki au kile. Kundi zima lilishiriki, nalo lilitaka kufanya hivyo kwa sababu lilijisikia kwamba sisi tulikuwa tumelifundisha jinsi ya kuwapa wengine. Maneno hayo yakatufanya tutoe machozi hata zaidi!’
Baadaye, ndugu huyo alipoandika masimulizi haya, kazi ilikuwa imeendelea kuongezeka-ongezeka. Yeye na mke wake walikuwa wakishiriki utumishi wa painia msaidizi.
[Sanduku katika ukurasa wa 18]
Ushuhuda wa Upendo wa Kikristo
Kundi moja la Mashahidi wa Yehova katika magharibi ya United States lilikabili hali isiyopata kuonekana iliyowaruhusu waonyeshe wazi upendo wa Kikristo, kama ule unaopendekezwa katika Maandiko. Katika eneo lao, sehemu hiyo ya nchi ilifungua kituo cha kutunzia watu waliopooza sana mwili kwa sababu ya kuwa na tatizo katika ubongo. Mmoja wa waakaaji wa kwanza wa kituo hicho alikuwa Gary, mwenye umri wa miaka 25, ambaye hangeweza kutunziwa nyumbani. Ugonjwa huo ulikuwa umempoozesha miguu na mikono yote, na usemi wake uliharibika kidogo pia.
Gary alikuwa amekuwa Shahidi aliyebatizwa kwa miaka saba. Alipokwisha kuingia katika kituo cha afya kipya hicho, alitaka kuhudhuria mikutano ya kundi la mahali hapo. Wazazi wake hawakuishi mbali sana na hapo, na kwa muda fulani walimleta mikutanoni. Lakini kwa sababu ya umri wao ndugu wengine katika kundi walianza kusaidia. Mmoja alikuwa na gari la kuchukulia bidhaa. Kwa hiyo yeye, mke wake, na wasichana wao wawili wakawa wakijitayarisha na kuondoka nyumbani dakika 45 kabla ya mkutano ili waweze kwenda kumchukua Gary. Walikuwa wakimrudisha kwenye kituo cha afya baadaye, hivyo wakawa wakifika nyumbani wakiwa wamechelewa sana.
Ingawa hivyo, jambo fulani lilikuwa likiendelea katika kituo cha afya hicho. Wagonjwa wengine waliopoozeshwa na tatizo la ubongo walionyesha kupendezwa na ukweli wa Biblia. Baada ya muda mfupi wawili wakakubali kujifunza Biblia. Baadaye, wengine pia walionyesha kupendezwa. Lakini wote wangeweza kuletwaje kwenye mikutano? Jamaa nyingine katika kundi ilinunua gari la kuchukulia bidhaa na shirika fulani la kibiashara la Mashahidi wa mahali hapo likafanya gari la tatu la namna hiyo liweze kupatikana. Hata hivyo, nyakati nyingine njia hizo hazikutosha au hazikufaa. Je! Kundi lingeweza kufanya mengi zaidi?
Wazee walizungumza jambo hilo wakakusudia kwamba gari linunuliwe kwa kusudi tu la kuwa likiwaleta mikutanoni na kuwarudisha watu hao wenye vizuizi vya kimwili. Kundi lilikubali na likafurahia kuchanga. Mashahidi wengine kutoka eneo la ujirani waliopata habari za shughuli hiyo walitoa michango pia. Gari lilinunuliwa na kutayarishwa kwa njia ambayo viti vya wagonjwa vyenye magurudumu vingeweza kuchukuliwa ndani yalo.
Sasa, kila mwezi kunakuwa na zamu za Mafunzo ya Kitabu ya Kundi za kuendesha gari hilo kwenda mikutanoni na makusanyikoni. Watu watano wanahudhuria kwa ukawaida kutoka kile kituo cha wagonjwa waliopoozeshwa na tatizo la ubongo, wanne kati yao sasa wakiwa Mashahidi waliobatizwa. Wamekuja kujulikana na kupendwa na ndugu na dada wengi, ambao wanapata furaha ya kusaidia. Jinsi gani? Kwa kuwashikia kitabu cha nyimbo na kuwafungulia maandiko nyakati za mikutano. Kwenye mikusanyiko ya mzunguko na mikusanyiko ya wilaya, hata wanasaidia kuwalisha na kuwatunza wale wasioweza kujifanyia hivyo. Jambo hilo limetokeza hali ha kupendana sana ambayo inachangamsha moyo kweli kweli. Na namna gani juu ya Gary? Sasa yeye anatumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kundi hilo ambalo limeonyesha ushuhuda mkubwa hivyo wa kwamba lina upendo.—Matendo 20:35.
-
-
Kumsifu Yehova kwa MuzikiMnara wa Mlinzi—1986 | Oktoba 15
-
-
Kumsifu Yehova kwa Muziki
KUNA njia nyingi ambazo watumishi wa Yehova wanaweza kutumia wamletee yeye sifa. Bila shaka, kati ya njia zinazopendeza zaidi na kati ya zile zinazoletea moyo wake furaha kubwa ni ile ya ‘kuimba kumfanyia muziki mtamu.’ (Zaburi 105:2, NW) Imeonekana sana kwamba muziki ni moja ya “chapa zinazotambulisha utu wa wanadamu.”
Muziki umeitwa pia “ile zawadi ya kibinadamu isiyo na kifani, ya kugundua ustadi wa kufanya mambo mapya na kuendelea kugundua mwingine.” Wanyama, wawe ni wa mwitu au wa kufugwa, hawana uwezo wa kufanya muziki. Ni kweli kwamba ndege wengine wanaimba nyimbo za kupendeza, lakini wanafanya yote hayo kwa silika tu. Wao hawana ufahamu wa muziki kama vile kasuku wasivyo na ufahamu wa maneno yo yote ambayo huenda wakazoezwa kusema. Lakini sisi tukiwa na muziki wa kupendeza, tunaweza kufikia mioyo ya wengine, kama vile tunavyoweza kupashana habari na akili za wengine kwa kutumia usemi.
Ndiyo, muziki ni zawadi ambayo Muumba amewapa wanadamu, na lo, hiyo ni zawadi kama nini! Uchunguzi uliofanywa hivi majuzi unaonyesha kwamba watoto wachanga
-