-
Kutangaza Mnara wa MlinziMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Kutangaza Mnara wa Mlinzi
Lilipotokezwa kwa mara ya kwanza, katika Julai 1879, liliitwa Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence. Gazeti hili, lililokuwa mtetezi wa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, lilichapwa ili kuandaa chakula cha kiroho kwa nyumba ya imani. Ili kukaza fikira kwa udhahiri zaidi juu ya kusudi la gazeti hili, Januari 1, 1909, kichwa chalo kilibadilishwa kuwa The Watch Tower and Herald of Christ’s Presence. Kuanzia Januari 1, 1939, huku likiweka mkazo zaidi juu ya uhakika wa kwamba Kristo alikuwa tayari anatawala kutoka mbinguni akiwa Mfalme, kichwa kilibadilishwa kusomeka The Watchtower and Herald of Christ’s Kingdom. Kisha mnamo Machi 1, 1939, kwa kubadilisha kichwa kuwa The Watchtower Announcing Jehovah’s Kingdom, fikira zilielekezwa kihususa zaidi kwa Yehova akiwa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima, yule aliyempa Mwanae mamlaka ya kutawala.
Lilipotangazwa kwa mara ya kwanza, Watch Tower lilikuwa kichapo cha kurasa nane, kikitokezwa mara moja kwa mwezi. Ukubwa walo uliongezwa hadi kurasa 16 katika 1891, na likawa gazeti la kutokezwa mara mbili kila mwezi katika 1892. Mpangilio wa kurasa 32 ulianzishwa katika lugha nyingi katika 1950.
Kutafsiriwa kwa Watch Tower katika lugha nyinginezo kulianza polepole. Toleo moja la kielelezo lilichapwa katika Kisweden katika 1883 ili litumiwe kuwa trakti. Kuanzia 1886 hadi 1889, chapa ndogo ya gazeti hili ilichapwa katika Kijerumani. Lakini haikuwa hadi 1897 kwamba Watch Tower lilitokea tena katika Kijerumani na likaendelea kutangazwa bila kukoma. Kufikia 1916 lilikuwa likichapwa katika lugha saba—Kidenmark-Kinorway, Kifaransa, Kifinland, Kiingereza, Kijerumani, Kipoland, na Kisweden. Wakati kuhubiriwa kwa habari njema kulipoongeza mwendo zaidi katika 1922, hesabu ya lugha ambazo gazeti hilo lilitangazwa iliongezwa kuwa 16. Hata hivyo, kufikia 1993, lilikuwa likitokezwa kwa ukawaida katika lugha 112—zile zinazotumiwa na sehemu kubwa ya idadi ya watu duniani. Hiyo ilitia ndani si lugha kama vile Kiingereza, Kihispania, na Kijapani tu, ambazo kwazo mamilioni ya nakala za kila toleo zilichapwa, bali pia Kipalau, Kituvalu, na nyinginezo ambazo ni mia chache zilizokuwa zikigawanywa.
-
-
Amkeni!—Gazeti Linalovutia Sana UmmaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Amkeni!—Gazeti Linalovutia Sana Umma
Hapo awali gazeti hilo lilikuwa na kichwa The Golden Age. Toleo la kwanza lilikuwa la Oktoba 1, 1919. Gazeti hilo liliripoti juu ya nyanja nyingi za jitihada za binadamu. Liliwafahamisha watu juu ya yale yaliyokuwa yakiendelea ulimwenguni na likawaonyesha kwamba suluhisho halisi kwa matatizo ya wanadamu ni Utawala wa Mileani wa Kristo, ambao kwa kweli utaleta “muhula bora ajabu” kwa wanadamu. Muundo wa jalada la gazeti hilo ulipata mabadiliko, lakini ujumbe ulibaki uleule. The Golden Age lilibuniwa ili ligawanywe kwa umma, na kwa miaka mingi hesabu ya nakala zilizotokezwa ilikuwa kubwa kuliko ile ya The Watch Tower.
Kuanzia toleo la Oktoba 6, 1937, kichwa kilibadilishwa kuwa Consolation. Hicho kilifaa sana kwa sababu ya uonevu ambao wengi walikuwa wakipata na msukosuko ambao ulimwengu ulijitia ndani yao katika Vita ya Ulimwengu 2. Hata hivyo, kitulizo ambacho gazeti hilo lilitoa, kilikuwa cha aina ile inayovutia wale tu walio na upendo halisi wa ile kweli.
-