-
Kutumia Kikuza-sautiFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 17
Kutumia Kikuza-sauti
NDUGU na dada zetu Wakristo hujitahidi sana na kutumia muda mwingi kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Ili mikutano iwafaidi, ni lazima waweze kusikia wasemaji vizuri.
Katika Israeli la kale, hakukuwa na vifaa vya kukuza sauti. Musa alipozungumza na taifa la Israeli katika Nyanda za Moabu kabla ya kuingia katika Nchi ya Ahadi, mamilioni ya watu waliwezaje kumsikia? Labda Musa alipitisha habari akitumia watu waliokuwa wakirudia maneno yake, ambao walikuwa wamewekwa mahali fulani-fulani panapofaa katika kambi. (Kum. 1:1; 31:1) Baada ya Waisraeli kuanza kuteka eneo la magharibi la Yordani, Yoshua alikusanya taifa hilo mbele ya Mlima Gerizimu na Mlima Ebali, na inaonekana Walawi walikuwa katika bonde lililotenganisha milima hiyo. Wakiwa pale, watu wote walisikia na kuitikia baraka za Mungu na laana zake walizotangaziwa. (Yos. 8:33-35) Inawezekana watu walitumiwa pindi hii pia kupashana habari, ingawa inaonekana sauti pia iliweza kusambaa kwa urahisi katika eneo hilo.
Miaka 1,500 hivi baadaye wakati ‘umati mkubwa sana ulipokusanyika’ kando ya Bahari ya Galilaya kumsikiliza Yesu, yeye alipanda mashua, akasonga kidogo baharini, akaketi na kuanza kuzungumza na umati. (Mk. 4:1, 2) Kwa nini Yesu alizungumza kutoka mashuani? Inaonekana alifanya hivyo kwa sababu sauti ya mtu husambaa sana juu ya maji matulivu.
Kufikia mwanzoni mwa karne ya 20, idadi ya wale ambao wangeweza kusikia mambo yanayosemwa ilitegemea kiasi cha sauti ya msemaji na jinsi alivyosikika vizuri. Lakini katika miaka ya 1920, watumishi wa Yehova waliweza kuanza kutumia vifaa vya kukuza sauti katika makusanyiko.
Vifaa vya Kukuza Sauti. Vifaa hivyo vinaweza kukuza sana sauti ya msemaji na bado vidumishe vizuri ubora na hali ya sauti yake. Msemaji hahitaji kukaza sauti yake kupita kiasi. Wasikilizaji hawahitaji kukaza sana masikio ili kusikia yanayosemwa. Badala yake wanaweza kusikiliza kwa makini.
Jitihada nyingi hufanywa ili kuhakikisha kuna vifaa vizuri vya kukuza sauti katika makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Na zaidi, Majumba mengi ya Ufalme hutumia vifaa vinavyokuza sauti za wale wanaotoa hotuba, wanaoongoza mikutano, au wanaosoma jukwaani. Na makutaniko mengine yana vikuza-sauti ambavyo hutumiwa na wahudhuriaji wanapotoa maelezo wakati wa mikutano. Kama kutaniko lina kikuza-sauti, jifunze kukitumia vizuri.
Miongozo Fulani ya Msingi. Ili ukitumie vizuri kikuza-sauti, kumbuka mambo yafuatayo: (1) Kwa ujumla kikuza-sauti kinapaswa kuwa sentimeta 10 hadi 15 hivi kutoka mdomo wako. Kikuza-sauti kikiwa karibu sana na mdomo wako, sauti yako itabadilika. Kikiwa mbali sana na mdomo wako, sauti yako haitakuwa wazi. (2) Kikuza-sauti kiwe mbele yako wala si upande. Zungumza tu wakati uso wako umeelekea kikuza-sauti, lakini si wakati umeelekeza uso kulia au kushoto. (3) Ongea kwa sauti ya juu kidogo na kwa mkazo zaidi kuliko unavyozungumza kwa kawaida. Lakini usipige kelele. Vifaa vya kukuza sauti vitainua sauti yako kwa urahisi na hata wale walio mbali watasikia. (4) Ukihitaji kusafisha koo au ukishikwa na kikohozi au chafya, hakikisha umegeuza kichwa kutoka kwenye kikuza-sauti.
Unapotoa Hotuba. Unaposimama utoe hotuba, kwa kawaida kuna ndugu ambaye hurekebisha kikuza-sauti. Anapokirekebisha, simama kwa njia ya kawaida ukitazama wasikilizaji. Weka maandishi yako kwenye kinara cha msemaji, lakini hakikisha kwamba kikuza-sauti hakikuzuii kutazama maandishi yako.
Unapoanza kuzungumza, sikiliza jinsi sauti yako inavyosikika. Je, unaongea kwa sauti ya juu sana, au maneno fulani yanatokeza sauti ya “pu”? Unaweza kusonga nyuma kwa sentimeta 2.5 au 5. Unapotazama kifupi maandishi yako, kumbuka kwamba unapaswa kuzungumza na kusoma wakati tu uso wako umeelekea kikuza-sauti au ukiwa juu kidogo ya kikuza-sauti, lakini uso wako usiwe kamwe chini ya kikuza-sauti.
Unaposoma Jukwaani. Ni vizuri kuinua Biblia au kichapo kingine ili uso wako uelekee wasikilizaji. Huenda ukahitaji kushika kile unachosoma kwa upande fulani kidogo kwa sababu labda kikuza-sauti kitakuwa mbele yako. Yaani, kichwa chako kielekee kidogo upande mwingine wa kikuza-sauti. Ndipo unaposoma, sauti yako iingie moja kwa moja kwenye kikuza-sauti.
Ndugu wengi wanaosoma kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi husoma wakiwa wamesimama, wakitumia kikuza-sauti kilicho kwenye kinara. Hiyo inawawezesha kupumua vizuri na kusoma kwa hisia zaidi. Kumbuka kwamba kusoma mafungu ni sehemu muhimu ya mkutano. Faida ambazo wasikilizaji hupata hutegemea sana usomaji.
Unapotoa Maelezo Mkutanoni. Ikiwa kutaniko lenu linatumia vikuza-sauti wakati wa kutoa maelezo, kumbuka kwamba bado unapaswa kuzungumza kwa njia ya wazi na kwa kiasi kinachofaa cha sauti. Unapotoa maelezo, jaribu kushika mkononi kichapo cha funzo au Biblia. Hiyo itakuwezesha kuona habari hiyo vizuri huku ukiongea kwenye kikuza-sauti.
Katika makutaniko mengine kuna ndugu ambao wana migawo ya kuwapelekea vikuza-sauti wale wanaoitwa kutoa maelezo. Ikiwa ndivyo ilivyo kwenu, endelea kuinua mkono ikiwa umeitwa ili ndugu anayewapokeza kikuza-sauti aone mahali ulipo na kukufikia haraka. Ikiwa mnatumia kikuza-sauti kinachoshikiliwa mkononi, uwe tayari kukichukua. Usianze kuongea kabla ya kikuza-sauti kuwa mahali panapofaa. Ukimaliza kutoa maelezo, mrudishie huyo ndugu kikuza-sauti haraka.
Mnapofanya Onyesho. Tunahitaji kufikiria kimbele jinsi tutakavyotumia kikuza-sauti tunapofanya onyesho. Kikuza-sauti kikiwa kimeshikiliwa na kinara, mikono yako itakuwa huru kufungua Biblia na maandishi. Mkitumia kikuza-sauti mnachoshikilia kwa mkono, mnaweza kuwa huru zaidi kusonga, lakini mtahitaji kupanga ili mwenzako akishike. Mkifanya hivyo mikono yako itakuwa huru kufungua Biblia. Mnahitaji kufanya mazoezi na mwenzako ili ajue jinsi ya kushika kikuza-sauti vizuri. Pia kumbuka kwamba unapokuwa jukwaani usiwageuzie wasikilizaji mgongo, hasa unapoongea.
Katika maonyesho ya Mikutano ya Utumishi, huenda ikawa kuna washiriki kadhaa, na huenda watatembea-tembea pale jukwaani. Kwa hiyo, wanaweza kuhitaji vikuza-sauti kadhaa. Vikuza-sauti hivyo viwekwe mapema mahali panapofaa au wale watakaofanya onyesho wapewe wanapoenda jukwaani. Ni vizuri kufikiria mapema kuweka kikuza-sauti mahali panapofaa na kwa wakati unaofaa. Kufanya mazoezi kabla ya kutoa onyesho kunatokeza nafasi ya kufundisha wale ambao watafanya onyesho jinsi ya kutumia kikuza-sauti vizuri. Ikiwa haiwezekani kufanya mazoezi jukwaani, huenda ikafaa washike kitu kinachotoshana na kikuza-sauti ili kujifunza kukitumia vizuri. Baada ya onyesho, wanapaswa kurudisha vikuza-sauti kwa utaratibu, wakijihadhari wasijikwae kwa kamba za vikuza-sauti wanapoondoka jukwaani.
Kutumia vikuza-sauti vizuri kunahusiana moja kwa moja na mojawapo ya malengo makuu ya mikutano yetu, yaani, kila mmoja kufaidika na mazungumzo yetu ya Neno la Mungu. (Ebr. 10:24, 25) Kwa kujifunza kutumia vikuza-sauti vizuri, sisi mmoja-mmoja tunaweza kutimiza kusudi hilo muhimu.
-
-
Kutumia Biblia Kujibu MaswaliFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 18
Kutumia Biblia Kujibu Maswali
TUNAPOULIZWA maswali yanayohusu imani yetu, maisha yetu, maoni yetu juu ya matukio ya nyakati zetu, na tumaini letu la wakati ujao, sisi hujitahidi kutumia Biblia kujibu. Kwa nini? Kwa sababu Biblia ni Neno la Mungu. Imani yetu inategemea Biblia. Maisha yetu yanategemea Biblia. Maoni yetu kuhusu matukio ya ulimwengu yanategemea Biblia. Tumaini letu la wakati ujao linategemea kabisa ahadi za Biblia zilizopuliziwa.—2 Tim. 3:16, 17.
Tunafahamu sana uzito wa jina letu. Sisi ni Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:12) Kwa hiyo, tunapojibu maswali, tunayajibu kulingana na maoni ya Yehova tunayopata katika Neno lake lililopuliziwa wala hatujibu kulingana na falsafa za wanadamu. Ingawa ni kweli kwamba kila mmoja wetu ana maoni yake kuhusu mambo mbalimbali, sisi huacha Neno la Mungu lirekebishe maoni yetu kwa sababu tunasadiki kabisa kwamba Neno hilo ndilo kweli. Bila shaka, Biblia inaturuhusu kuwa na maoni tofauti-tofauti katika masuala mengi. Badala ya kushurutisha wengine wafuate maoni yetu, sisi tunapenda kufundisha watu kanuni za Maandiko, na hivyo tunawaruhusu wawe na uhuru wa kuchagua kama sisi. Kama mtume Paulo, sisi hujaribu “kukuza utii kwa njia ya imani.”—Rom. 16:26.
Andiko la Ufunuo 3:14 linasema kwamba Yesu Kristo ni “shahidi mwaminifu na wa kweli.” Alijibu maswali na kukabiliana na hali kwa njia gani? Nyakati nyingine alitumia mifano iliyofanya watu wafikiri. Nyakati nyingine aliuliza yule mwenye kuuliza swali jinsi anavyofahamu andiko fulani. Mara nyingi alinukuu maandiko, alitaja jinsi maandiko yanavyosema, au aliyarejelea. (Mt. 4:3-10; 12:1-8; Luka 10:25-28; 17:32) Katika karne ya kwanza, kwa kawaida vitabu vya kukunjwa vya Maandiko vilihifadhiwa katika masinagogi. Hakuna jambo linaloonyesha kwamba Yesu alikuwa na vitabu vyake mwenyewe vya kukunjwa, lakini alijua sana Maandiko na aliyarejelea mara nyingi alipokuwa akifundisha wengine. (Luka 24:27, 44-47) Kwa kweli angeweza kusema kwamba yale aliyofundisha hayakutokana na ubuni wake. Alisema mambo aliyosikia kutoka kwa Baba yake.—Yn. 8:26.
Tunataka kuiga mfano wa Yesu. Hakuna mmoja wetu ambaye amewahi kumsikia Mungu akisema, kama alivyomsikia Yesu. Lakini Biblia ni Neno la Mungu. Tukiitumia kujibu maswali, tunaepuka kujielekezea fikira. Tunaonyesha tumeazimia kabisa kufuata maoni ya Mungu kuhusu kweli badala ya kutoa maoni ya wanadamu wasiokamilika.—Yn. 7:18; Rom. 3:4.
Bila shaka, tamaa yetu si kutumia tu Biblia bali ni kuitumia kwa njia inayomfaidi zaidi msikilizaji. Tunataka asikilize bila kuwa na maoni yenye ubaguzi. Kwa kutegemea maoni yake, unaweza kutaja mambo yanayotokana na Biblia kwa kusema: “Je, hukubali kwamba maneno ya Mungu ndiyo muhimu zaidi?” Au unaweza kusema: “Je, unajua kwamba Biblia inazungumzia swali hili hasa?” Ikiwa unazungumza na mtu ambaye haamini Biblia, unaweza kutumia utangulizi tofauti kidogo. Unaweza kusema: “Ebu nikueleze unabii huu wa kale.” Au unaweza kusema: “Kitabu ambacho kimeenezwa zaidi katika historia kinasema hivi . . . ”
Nyakati nyingine, unaweza kutaja tu jinsi andiko fulani linavyosema. Lakini, ikiwezekana ni afadhali zaidi kufungua Biblia na kuisoma. Mwonyeshe mtu huyo andiko hilo katika Biblia yake hali ikiruhusu. Kutumia Biblia moja kwa moja kwa njia hiyo mara nyingi hugusa sana mioyo ya watu.—Ebr. 4:12.
Wazee Wakristo wana wajibu wa kipekee wa kutumia Biblia wanapojibu maswali. Mojawapo ya sifa za kumstahilisha mtu awe mzee ni “kushika kwa imara lile neno la uaminifu kwa habari ya usanifu wa kufundisha kwake.” (Tito 1:9) Mshiriki wa kutaniko anaweza kufanya maamuzi mazito maishani baada ya kushauriwa na mzee. Ni muhimu shauri litegemee Maandiko. Mfano ambao mzee anaweka unaweza kuwa na uvutano sana juu ya jinsi wengine wanavyofundisha.
-
-
Kuwasaidia Wasikilizaji Kutumia BibliaFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 19
Kuwasaidia Wasikilizaji Kutumia Biblia
KUSUDI letu ni kuelekeza fikira za kila mtu kwenye Neno la Mungu, Biblia. Kitabu hicho kitakatifu ndicho msingi wa ujumbe tunaohubiri, na tunataka watu watambue kwamba yale tunayosema yanatokana na Mungu wala hatusemi mambo yetu wenyewe. Watu wanahitaji kuitumaini Biblia.
Katika Huduma ya Shambani. Unapojitayarisha kwa ajili ya huduma ya shambani, sikuzote chagua andiko moja au zaidi ambalo utawaonyesha wale walio tayari kusikiliza. Hata kama unapanga kutoa kichapo fulani cha Biblia kwa muda mfupi tu, kwa kawaida ni vizuri kusoma andiko linalofaa la Biblia. Biblia ina uwezo mkubwa wa kuelekeza wenye mfano wa kondoo kuliko jambo jingine lolote ambalo tunaweza kusema. Ikiwa hali hazikuruhusu kusoma Biblia, unaweza kuinukuu. Katika karne ya kwanza, vitabu vya kukunjwa vya Maandiko havikupatikana sana. Hata hivyo, Yesu na mitume wake walinukuu sana Maandiko. Hata sisi tunapaswa kujitahidi kushika Maandiko na kuyatumia vizuri katika huduma yetu, nyakati nyingine tukiyanukuu tu.
Ikiwa hali zinakuruhusu kusoma Biblia, uishike vizuri ili mwenye nyumba aweze kufuatana nawe unaposoma. Ikiwa mwenye nyumba anafuatana nawe akisoma Biblia yake mwenyewe, yale anayosoma yanaweza kumfanya aitikie kwa njia nzuri zaidi.
Hata hivyo, ni lazima utambue kwamba baadhi ya watafsiri wa Biblia wamebadili Neno la Mungu. Huenda tafsiri zao hazipatani kwa kila hali na mambo yaliyokuwa katika lugha za awali za Biblia. Tafsiri kadhaa za kisasa zimeondoa jina la Mungu, hazisemi wazi kile ambacho maandishi ya lugha za awali yalisema kuhusu wafu, na zinaficha mafundisho ya Biblia kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia. Ili kuonyesha mtu badiliko ambalo limefanywa, mnaweza kuchunguza maandiko hayo katika Biblia tofauti-tofauti au kuchunguza tafsiri za awali za Biblia za lugha iyo hiyo. Kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kinalinganisha jinsi tafsiri kadhaa zinavyotafsiri maneno makuu ya maandiko ambayo hutumiwa mara nyingi. Mtu yeyote anayependa kweli atafurahi kujua mambo hayo.
Katika Mikutano ya Kutaniko. Wote wasaidiwe kutumia Biblia katika mikutano ya kutaniko. Kuna faida nyingi za kufanya hivyo. Kunawasaidia wasikilizaji wakazie fikira mambo yanayozungumzwa. Kunakazia maneno ya msemaji kwa sababu wasikilizaji wenyewe wanayasoma maneno hayo. Na kufanya hivyo kunawasadikisha wale wanaopendezwa kwamba kwa kweli Biblia ndiyo msingi wa imani yetu.
Wasikilizaji watafuatana nawe unaposoma Maandiko katika Biblia ikiwa tu utawasaidia kufanya hivyo. Mojawapo ya njia bora ya kuwatia moyo kutumia Biblia ni kuwaomba wafuatane nawe unaposoma andiko fulani.
Ni daraka la msemaji kuamua maandiko anayotaka kukazia anapowaomba wasikilizaji wafuatane naye. Inafaa kusoma maandiko yanayokusaidia kufafanua mambo makuu. Kisha kadiri wakati unavyoruhusu, ongezea maandiko mengine machache yanayotegemeza jambo unalozungumzia.
Kwa kawaida, haitoshi tu kutaja andiko fulani wala haitoshi kuwaomba wasikilizaji wafuatane nawe unapolisoma. Ukisoma andiko moja kisha usome jingine mbiombio hata kabla ya wasikilizaji kupata wakati wa kufungua lile la kwanza, upesi watachoka na wataacha kujaribu kufuatana nawe unaposoma Biblia. Uwe na utambuzi. Soma andiko wakati wengi wamelipata.
Fikiria kimbele. Taja vizuri andiko hilo mapema kabla ya kulisoma. Jambo hilo litapunguza wakati unaopotea unapongojea wasikilizaji wafungue Biblia zao. Ingawa hutaweza kuzungumzia mambo mengi sana ukiwapa wasikilizaji wakati wa kufungua Biblia, utawafaidi sana.
-
-
Kutoa Utangulizi Mzuri wa MaandikoFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 20
Kutoa Utangulizi Mzuri wa Maandiko
MAANDIKO ndiyo msingi wa mafundisho yetu katika mikutano ya kutaniko. Pia, maandiko ya Biblia ndiyo msingi wa mahubiri yetu katika huduma ya shambani. Lakini, mafanikio yetu ya kutumia maandiko katika mazungumzo yanategemea kwa kiasi fulani utangulizi tunaotoa kabla ya kuyasoma.
Usirejelee tu andiko na kumwomba mtu afuatane nawe unapolisoma. Unapotaka kutaja andiko, jaribu kutimiza mambo haya mawili: (1) Chochea hamu ya kusoma andiko hilo, na (2) onyesha kusudi la kulisoma. Kuna njia mbalimbali za kutimiza mambo hayo mawili.
Uliza Swali. Njia hii ni bora ikiwa wasikilizaji bado hawajui vizuri jibu la swali unalouliza. Jaribu kuuliza swali kwa njia inayofanya watu wafikiri. Yesu alifanya hivyo. Mafarisayo walipomwendea hekaluni na kujaribu hadharani ujuzi wake wa Maandiko, Yesu aliwauliza: “Nyinyi mwafikiri nini juu ya Kristo? Yeye ni mwana wa nani?” Wakamjibu: “Wa Daudi.” Yesu akawauliza: “Basi, ni jinsi gani, kwamba Daudi kwa upulizio amwita yeye ‘Bwana’?” Kisha akanukuu Zaburi 110:1. Mafarisayo wakanyamazishwa. Lakini, umati ukamsikiliza Yesu kwa furaha.—Mt. 22:41-46.
Unaweza kutumia maswali kama haya kwenye utangulizi wako katika utumishi wa shambani: “Mimi nina jina na wewe una jina. Je, Mungu pia ana jina? Ebu tupate jibu katika Zaburi 83:18.” “Je, kweli itawezekana kuwe na serikali moja inayotawala wanadamu wote? Ebu ona jinsi Danieli 2:44 linavyojibu.” “Je, kweli Biblia inazungumzia hali za siku zetu? Ebu linganisha hali unazoona leo na hali zinazotajwa katika 2 Timotheo 3:1-5.” “Je, kweli kuna wakati ambapo kifo na kuteseka hakutakuwapo tena? Biblia inajibu swali hilo katika Ufunuo 21:4, 5.”
Kutumia maswali vizuri katika hotuba ili kutoa utangulizi mzuri wa maandiko kunaweza kuchochea wasikilizaji kuona maandiko kwa njia tofauti, hata kama ni maandiko wanayofahamu vizuri. Lakini, watafanya hivyo ikiwa tu maswali unayouliza kwa kweli yanawahusu. Hata kama wasikilizaji wanapendezwa na habari unayozungumza, akili zao zinaweza kutangatanga unaposoma maandiko ambayo wamesikia mara nyingi. Ili akili zao zisitangetange, fikiria sana jinsi ya kufanya hotuba yako ivutie.
Taja Tatizo Fulani. Unaweza kutaja tatizo fulani kisha uonyeshe andiko linalotaja suluhisho. Usiwafanye wasikilizaji watarajie suluhisho kubwa kuliko lile watakalopata katika andiko. Mara nyingi andiko huonyesha suluhisho la kadiri fulani tu. Lakini unaposoma andiko, unaweza kuuliza wasikilizaji wafikirie mwongozo unaopatikana katika andiko hilo unaosaidia kukabili tatizo mnalozungumzia.
Vilevile, unaweza kutaja kanuni fulani inayohusu mwenendo mzuri kisha utumie tukio fulani katika Biblia linaloonyesha hekima ya kufuata kanuni hiyo. Ikiwa andiko ambalo wasemaji wengine wanasoma lina mambo mawili hususa (au labda zaidi) ambayo yanahusiana na jambo wanalozungumzia, wao huwaomba wasikilizaji wawe makini kuyaona. Ikiwa inaonekana wasikilizaji fulani hawaelewi jambo unalozungumzia, unaweza kuchochea fikira zao kwa kutaja mambo yanayoweza kufanywa ili kulisuluhisha kisha utumie andiko kuonyesha suluhisho.
Rejelea Biblia. Ikiwa tayari umeamsha upendezi wa wasikilizaji katika habari unayozungumzia na tayari umetaja jambo moja au mambo mawili kuihusu, unaweza kusema hivi kabla ya kusoma andiko: “Ona jinsi Neno la Mungu linavyosema kuhusu jambo hili.” Ukifanya hivyo unaonyesha kwamba jambo unalotaka kusoma linategemea Neno la Mungu.
Yehova alitumia wanaume kama Luka, Paulo, Petro, na Yohana kuandika sehemu fulani za Biblia. Lakini wao ni waandishi tu; Yehova ndiye Mtungaji. Ikiwa unazungumza na watu ambao hawasomi Maandiko Matakatifu, huenda ikafaa zaidi kusema “Neno la Mungu” linasema kuliko kusema “Petro aliandika” au “Paulo alisema” kabla ya kusoma andiko. Ona kwamba nyakati nyingine Yehova alimwamuru Yeremia aseme maneno haya kabla ya kutangaza ujumbe wake: “Sikilizeni neno la BWANA.” (Yer. 7:2; 17:20; 19:3; 22:2) Iwe tunatumia jina la Yehova tunapotaka kusoma andiko au la, kabla ya kumalizia mazungumzo yetu, tujaribu kuonyesha kwamba yaliyomo katika Biblia ni neno lake.
Fikiria Muktadha. Unapaswa kuelewa muktadha unapofikiria utakavyotoa utangulizi wa andiko. Nyakati nyingine unaweza kutaja muktadha, lakini kwa njia nyinginezo ni muktadha unaoweza kuamua maneno utakayotumia. Kwa mfano, je, unaweza kutoa utangulizi wa maneno ya Yobu aliyemcha Mungu kwa njia ile ambayo ungetoa utangulizi wa maneno ya mmojawapo wa wafariji wake bandia? Luka aliandika kitabu cha Matendo, lakini pia ananukuu Yakobo, Petro, Paulo, Filipo, Stefano, na malaika, na vilevile ananukuu Gamalieli na Wayahudi wengine ambao hawakuwa Wakristo. Utasema ni nani aliyesema maneno unayonukuu? Kwa mfano, kumbuka kwamba Daudi hakutunga zaburi zote wala Solomoni hakuandika kitabu chote cha Mithali. Pia ni vizuri kujua mwandishi wa Biblia anazungumza na nani na kwa ujumla anazungumza habari gani.
Tumia Habari za Ziada. Hii ni njia bora ikiwa unaweza kuonyesha kwamba hali zinazohusu simulizi la Biblia unalosoma zinalingana na hali unazozungumzia. Nyakati nyingine unahitaji kutumia habari za ziada ili watu waelewe andiko fulani vizuri. Tuseme unataka kutumia andiko la Waebrania 9:12, 24 katika hotuba inayohusu fidia. Kabla ya kusoma andiko hilo unaweza kufafanua kifupi chumba cha ndani kabisa cha tabenakulo, ambacho maandiko yanaonyesha kinafananisha mahali ambapo Yesu aliingia alipoenda mbinguni. Lakini usitumie habari nyingi sana kiasi cha kufunika andiko ambalo unataka kusoma.
Ili utoe utangulizi wa maandiko kwa njia bora, chunguza jinsi wasemaji wenye ujuzi wanavyofanya. Tazama njia tofauti-tofauti wanazotumia. Ona matokeo ya njia hizo. Unapotayarisha hotuba zako, tambua maandiko makuu na ufikirie kwa makini jambo unalotaka kutimiza unaposoma kila andiko. Panga kwa uangalifu jinsi ambavyo utatoa utangulizi wa kila andiko ili liwe na matokeo bora zaidi. Baadaye, fanya vivyo hivyo na maandiko yote unayotumia. Unapoendelea kuboresha sehemu hii katika hotuba zako, utakuwa ukielekeza fikira zaidi kwenye Neno la Mungu.
-