-
Kutumia Vizuri VielelezoFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 47
Kutumia Vizuri Vielelezo
KWA NINI utumie vielelezo unapofundisha? Kwa sababu vielelezo hufanya uwe mwalimu bora. Yehova Mungu na Yesu Kristo walitumia vielelezo nasi tunaweza kuwaiga. Vielelezo vinapotumiwa pamoja na maelezo, akili hupokea habari kwa njia mbili. Vielelezo vinaweza kuvuta usikivu wa wasikilizaji na kufanya wakumbuke jambo hilo. Unawezaje kutumia vielelezo unapohubiri habari njema? Unawezaje kuwa na hakika kwamba unatumia vizuri vielelezo?
Jinsi Ambavyo Walimu Wakuu Walitumia Vielelezo. Yehova alifundisha mambo muhimu sana kupitia vielelezo vilivyo rahisi kukumbuka. Siku moja alimleta Abrahamu nje, akasema: “Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. . . . Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.” (Mwa. 15:5) Hata ingawa kwa maoni ya binadamu ahadi hiyo ilionekana kuwa haiwezi kutimizwa, Abrahamu aliguswa moyo sana akaweka imani katika Yehova. Pindi nyingine, Yehova alimtuma Yeremia kwa mfinyanzi akamwambia aingie kwenye karakana yake akatazame jinsi mfinyanzi anavyofinyanga udongo. Hilo ni somo lililoje kuhusu mamlaka ya Muumba juu ya wanadamu! (Yer. 18:1-6) Na, je, kweli Yona angesahau somo la rehema ambalo Yehova alimfundisha kupitia mtango? (Yona 4:6-11) Yehova hata aliwaambia manabii wake waigize ujumbe wake wa unabii wakitumia vitu fulani. (1 Fal. 11:29-32; Yer. 27:1-8; Eze. 4:1-17) Sehemu za hema la kukutania na hekalu ni mifano inayotusaidia kuelewa mambo halisi ya mbinguni. (Ebr. 9:9, 23, 24) Pia Mungu alitumia sana maono ili kutangaza ujumbe muhimu.—Eze. 1:4-28; 8:2-18; Mdo. 10:9-16; 16:9, 10; Ufu. 1:1.
Yesu alitumiaje vielelezo? Mafarisayo na wafuasi wa chama cha Herode walipojaribu kumtega Yesu kwa maneno, aliomba sarafu ya dinari na kuwaonyesha picha ya Kaisari. Akawaeleza kwamba Kaisari apewe vitu vyake na Mungu apewe vitu vyake. (Mt. 22:19-21) Yesu alifundisha somo la kumheshimu Mungu kwa vyote tulivyo navyo kwa kumrejelea mjane mmoja maskini kwenye hekalu ambaye alitoa mchango wa sarafu mbili ndogo, riziki yake yote. (Luka 21:1-4) Pindi nyingine alitumia mtoto mdogo kuwa mfano wa unyenyekevu na wa kutotamani makuu. (Mt. 18:2-6) Alionyesha pia maana ya kuwa mnyenyekevu, kwa kuosha miguu ya wanafunzi wake.—Yn. 13:14.
Njia za Kutumia Vielelezo. Hatuwezi kuwasiliana kwa maono kama Yehova. Lakini, vichapo vya Mashahidi wa Yehova vina picha nyingi zinazomfanya mtu afikiri. Zitumie kuwasaidia watu wanaopendezwa kupiga picha akilini dunia Paradiso ambayo Neno la Mungu linaahidi. Unapoongoza funzo la Biblia la nyumbani, unaweza kumwonyesha mwanafunzi picha inayohusiana na jambo mnalojifunza kisha mwulize anaona nini. Kumbuka kwamba nabii Amosi alipopewa maono fulani, Yehova alimwuliza: “Amosi, unaona nini?” (Amo. 7:7, 8; 8:1, 2) Unaweza kuuliza maswali kama hayo unapowaonyesha watu vielelezo vya picha za kufundishia.
Ukiandika hesabu fulani au ukichora chati fulani kuonyesha tarehe za matukio muhimu, watu wanaweza kuelewa kwa urahisi unabii kama ule wa “nyakati saba” katika Danieli 4:16 na wa “majuma sabini” katika Danieli 9:24. Baadhi ya vichapo vyetu vina vielelezo kama hivyo.
Katika funzo la Biblia la familia unaweza kutumia picha au mchoro ili kufanya mazungumzo juu ya vitu kama vile hema la kukutania, hekalu la Yerusalemu, na hekalu la maono la Ezekieli yawe rahisi kueleweka. Unaweza kupata michoro hiyo katika Insight on the Scriptures, nyongeza ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References, na matoleo ya Mnara wa Mlinzi.
Unaposoma Biblia pamoja na familia yako, tumia vizuri ramani. Fuata hatua kwa hatua safari ya Abrahamu kutoka Uru kupitia Harani hadi Betheli. Chunguza njia ambayo Waisraeli walifuata walipotoka Misri kufikia Nchi ya Ahadi. Tafuta eneo ambalo kila kabila la Israeli lilipewa urithi. Chunguza milki ya utawala wa Solomoni. Fuatisha njia ya Eliya alipotoroka Yezreeli hadi kule nyikani ng’ambo ya Beer-sheba alipotishwa na Yezebeli. (1 Fal. 18:46-19:4) Tafuta majiji na miji ambako Yesu alihubiri. Fuatisha safari za Paulo kama zinavyoonyeshwa katika kitabu cha Matendo.
Vielelezo vinafaa unapowafundisha wanafunzi wa Biblia utendaji wa kutaniko. Unaweza kumwonyesha programu ya kusanyiko na habari ambazo sisi huzungumzia katika makusanyiko. Wengi wamevutiwa walipozuru Jumba la Ufalme au ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Hiyo ni njia nzuri ya kuondoa dhana potovu kuhusu kazi yetu na kusudi lake. Unapowatembeza watu kwenye Jumba la Ufalme, waonyeshe jinsi linavyotofautiana na sehemu nyinginezo za ibada. Kazia kwamba Jumba la Ufalme si jengo la kifahari lakini linafaa hali ya kujifunza. Taja sehemu ambazo hasa zinashughulikia huduma ya kuhubiri kama vile mahali pa kuchukulia vichapo, ramani za maeneo, na masanduku ya michango (tofauti na kupitishwa kwa sahani za sadaka).
Ikiwa video zilizotayarishwa kwa mwelekezo wa Baraza Linaloongoza zinapatikana, zitumie kujenga imani yao katika Biblia, kuwaonyesha utendaji wa Mashahidi wa Yehova, na kuwasaidia kufuata kanuni za Biblia maishani.
Kutumia Vielelezo Mbele ya Watu Wengi. Vielelezo vikitayarishwa vizuri na kuonyeshwa vizuri vinaweza kusaidia sana kufundisha watu wengi. Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara huandaa aina kadhaa za vielelezo kama hivyo.
Kwa kawaida, somo la Mnara wa Mlinzi hutia ndani vielelezo kama vile picha ambazo kiongozi anaweza kutumia kukazia mambo muhimu. Ndivyo ilivyo na vichapo vinavyotumiwa kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko.
Hotuba fulani za watu wote zinaweza kutolewa kwa urahisi kwa kutumia vielelezo vinavyokazia mambo makuu. Lakini utakuwa na matokeo zaidi ukikazia akili mambo yaliyo katika Biblia kwa kuwa wasikilizaji wengi wana Biblia. Ikiwa pindi moja unahitaji kutumia picha au mchoro fulani wa mambo makuu ili kufafanua jambo moja au mambo kadhaa makuu ya hotuba, chunguza mapema uone kama kielelezo hicho kinaweza kuonwa (au kusomwa) na wale ambao wameketi nyuma kwenye jumba. Vielelezo kama hivyo vitumiwe mara chache sana.
Kusudi la vielelezo si kutumbuiza watu tunapozungumza na kufundisha. Tunapotumia vielelezo vinavyofaa, kusudi linapaswa kuwa kukazia mawazo yanayostahili kukaziwa kwa njia ya pekee. Vielelezo hivyo hufaa sana vinaposaidia kufafanua jambo na kufanya lieleweke kwa urahisi, au vinapotumiwa kuthibitisha jambo kabisa. Ukitumia vizuri kielelezo, kinaweza kukazia jambo kabisa hivi kwamba wasikilizaji watakumbuka kielelezo hicho na jambo hilo kwa miaka mingi.
Uwezo wa kusikia na kuona hutusaidia sana kujifunza. Kumbuka jinsi Walimu wakuu wametumia hali ya kusikia na kuona, na ujaribu kuwaiga unapofundisha wengine.
-
-
KusababuFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 48
Kusababu
TUNAFURAHIA jinsi ambavyo Neno la Mungu limebadili maisha yetu, na tunataka wengine pia wafaidike. Na zaidi, tunatambua kwamba wakati ujao wa watu unategemea jinsi wanavyoitikia habari njema. (Mt. 7:13, 14; Yn. 12:48) Tunatamani sana wakubali kweli. Lakini mbali na kuwa na usadikisho thabiti na bidii, tunahitaji vilevile kutumia busara ili tuweze kuwasaidia vizuri.
Kwa kawaida ukifichua kwa madharau fundisho fulani la uwongo ambalo mtu anapenda sana, mtu huyo hatakubali kweli hata umsomee Maandiko mangapi. Kwa mfano, ukishutumu tu sherehe zinazopendwa kwamba ni za kipagani, huenda watu wasibadili maoni yao kuzihusu. Kwa kawaida unaweza kufanikiwa ukisababu naye. Kusababu kunahusisha nini?
Maandiko yanatuambia kwamba ‘hekima ya kutoka juu ni yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu.’ (Yak. 3:17) Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “yenye kukubali sababu” hasa linamaanisha “kukubali maoni ya wengine.” Tafsiri nyingine zinalitafsiri kuwa “upole,” “-enye kufikiria wengine,” au “uvumilivu.” Ona kwamba kusababu kunahusiana na hali ya kufanya amani. Tito 3:2 linataja kukubali sababu pamoja na upole na kuitofautisha na sifa ya kupenda ugomvi. Wafilipi 4:5 linatuhimiza tuwe watu wanaojulikana kwa sifa ya “kukubali sababu.” Mtu anayekubali sababu anafikiria malezi, hali, na hisia za wale anaozungumza nao. Yuko tayari kubadilikana iwapo inafaa. Kushughulika na wengine kwa njia hiyo hufanya wafungue akili zao na mioyo yao ili wasikilize tunaposababu nao juu ya Maandiko.
Uanzie Wapi? Mwanahistoria Luka anaripoti kwamba mtume Paulo alipokuwa Thesalonike, alitumia Maandiko, “akieleza na kuthibitisha kwa marejezo kwamba ilikuwa lazima Kristo kuteseka na kufufuliwa kutoka kwa wafu.” (Mdo. 17:2, 3) Ona kwamba Paulo alifanya hivyo katika sinagogi la Wayahudi. Wasikilizaji waliheshimu Maandiko ya Kiebrania. Ilifaa kuanza mazungumzo kwa jambo walilokubali.
Paulo alipozungumza na Wagiriki katika Areopago huko Athene, yeye hakuanza kwa kunukuu Maandiko. Badala yake, alianza kuzungumzia mambo ambayo walijua na kukubali, na alitumia mambo hayo kuwaongoza kumfikiria Muumba na makusudi Yake.—Mdo. 17:22-31.
Kuna mabilioni ya watu siku zetu ambao hawaoni umuhimu wa Biblia katika maisha yao. Lakini karibu kila mtu anaathiriwa na hali ngumu za mfumo wa leo. Watu wanatamani hali bora. Basi ukihangaikia kwanza jambo linalowatatiza kisha uonyeshe jinsi Biblia inavyoelezea jambo hilo, kusababu kwa njia hiyo kunaweza kuwafanya wasikilize ujumbe wa Biblia kuhusu kusudi la Mungu kwa wanadamu.
Labda mwanafunzi wa Biblia anafuata imani na desturi fulani za kidini kwa sababu wazazi wake wanazifuata. Sasa, mwanafunzi huyo anajifunza kwamba imani hizo na desturi hizo hazimpendezi Mungu, naye anazikataa na kufuata mafundisho ya Biblia. Mwanafunzi huyo atawaelezaje wazazi wake uamuzi wake? Wazazi wake wanaweza kufikiri kwamba kwa sababu anakataa dini yao, anawakataa. Mwanafunzi huyo wa Biblia anaweza kukata kauli ya kwamba kabla ya kueleza sababu ya uamuzi wake kupitia Biblia, anahitaji kuwahakikishia wazazi wake anawapenda na kuwaheshimu.
Wakati wa Kukubali Maoni ya Wengine. Ingawa Yehova ana mamlaka ya kutoa amri, anaonyesha kukubali sababu kwa njia ya pekee sana. Malaika wa Yehova walipokuwa wakimwokoa Loti na familia yake kutoka Sodoma, walimhimiza hivi: “Ujiponye mlimani, usije ukapotea.” Lakini Loti akasihi akisema: “Sivyo, bwana wangu!” Akaomba aruhusiwe kutorokea Soari. Yehova alimsikiliza Loti akamruhusu aende huko; na Soari halikuangamizwa pamoja na majiji mengine. Lakini, baadaye Loti alifuata mwongozo wa awali wa Yehova akahamia milimani. (Mwa. 19:17-30) Yehova alijua Yeye hajakosea, lakini kwa subira alimwachilia Loti mpaka Loti alipotambua jambo hilo baadaye.
Ili sisi pia tufanikiwe kushughulika na wengine, tunahitaji kuwa wenye kusababu. Labda tuna hakika ya kwamba mtu mwingine amekosea, na huenda tuna sababu nzuri sana zinazothibitisha jambo hilo. Lakini haifai nyakati nyingine kumkaza mtu akubali kosa lake. Kukubali sababu hakumaanishi kushusha kanuni za Yehova. Ni afadhali kumshukuru mtu kwa kujieleza au kuachilia mambo fulani yasiyo ya kweli ambayo amesema ili ukazie jambo ambalo litamsaidia msikilizaji. Hata kama anashutumu imani yako, usikasirike. Unaweza kumwuliza kwa nini ana maoni hayo. Sikiliza kwa makini anapojibu. Hiyo itakusaidia ufahamu fikira zake. Na pia inaweza kusaidia kuweka msingi wa mazungumzo mazuri ya wakati ujao.—Mit. 16:23; 19:11.
Yehova amewapa wanadamu uwezo wa kutumia uhuru wao. Anawaruhusu watumie uwezo huo hata ingawa huenda wasiutumie kwa busara. Yoshua alipokuwa msemaji wa Yehova, alisimulia jinsi Mungu alivyotendea Israeli. Kisha akasema: “Nanyi kama mkiona ni vibaya kumtumikia BWANA, chagueni hivi leo mtakayemtumikia; kwamba ni miungu ile ambayo baba zenu waliitumikia ng’ambo ya Mto, au kwamba ni miungu ya wale Waamori ambao mnakaa katika nchi yao; lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia BWANA.” (Yos. 24:15) Mgawo wetu leo ni kutoa “ushahidi,” na tunautoa kwa usadikisho, lakini hatujaribu kuwalazimisha wengine wawe waamini. (Mt. 24:14) Ni lazima wachague wenyewe na hatuwanyimi haki hiyo.
Uliza Maswali. Yesu aliweka mfano mzuri wa kusababu alipozungumza na watu. Alifikiria malezi yao na alitumia mifano ambayo wangekubali kwa urahisi. Pia alitumia vizuri maswali. Maswali yaliwafanya wengine wajieleze na kufunua yaliyo mioyoni mwao. Pia yaliwasaidia kuona sababu za mambo waliyofundishwa.
Mtaalamu mmoja wa Sheria alimwuliza Yesu: “Mwalimu, ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai udumuo milele?” Yesu angaliweza kumjibu mara moja. Lakini alimwuliza mtu huyo maoni yake. “Ni nini limeandikwa katika Sheria? Wewe wasomaje?” Mtu huyo akajibu kwa usahihi. Je, jibu lake sahihi lilimaliza mazungumzo hayo? La. Yesu alimwacha mtu huyo aendelee kuzungumza, na swali ambalo mtu huyo aliuliza lilidokeza kwamba alikuwa akijaribu kujionyesha kuwa mwadilifu. Aliuliza: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu hakufafanua jambo hilo, kwa sababu huenda mtu huyo angempinga kwa sababu ya jinsi Wayahudi walivyowaona watu wa Mataifa na Wasamaria, badala yake alisababu naye kupitia mfano. Ni mfano wa Msamaria mwenye ujirani ambaye alimsaidia msafiri aliyeporwa na kupigwa, ilhali kuhani na Mlawi hawakumsaidia. Yesu alihakikisha mtu huyo ameelewa kwa kumwuliza swali rahisi. Yesu alisababu kwa njia ambayo ilimsaidia mtu huyo aelewe neno “jirani” kwa njia tofauti. (Luka 10:25-37) Huo ni mfano mzuri sana tunaoweza kuiga. Badala ya kuzungumza sana na kumfanya mwenye nyumba asifikiri, jifunze kutumia maswali na mifano kwa njia ya busara ili kumfanya yule anayekusikiliza afikiri.
Toa Sababu. Mtume Paulo alipozungumza katika sinagogi kule Thesalonike, hakusoma tu mambo yaliyopendeza wasikilizaji. Luka anaripoti kwamba Paulo alifafanua, akathibitisha, na kuonyesha matumizi ya jambo alilosoma. Basi “baadhi yao wakawa waamini na kujishirikisha wenyewe na Paulo na Sila.”—Mdo. 17:1-4.
Hata wasikilizaji wawe watu wa aina gani, kusababu nao kunafaidi. Ndivyo ilivyo unapowahubiria watu wa ukoo, unapozungumza na wafanyakazi au wanafunzi wenzako, unapowahubiria hadharani watu usiowafahamu, unapoongoza funzo la Biblia, au unapotoa hotuba kutanikoni. Unaposoma andiko, labda unalielewa vizuri sana lakini huenda mwingine asilielewe. Huenda unashikilia mno maoni yako unapofafanua andiko na kuonyesha matumizi yake. Ingefaa kutenga maneno fulani makuu katika andiko hilo na kuyafafanua, sivyo? Je, unaweza kuthibitisha jambo unalozungumzia kwa kutumia muktadha au andiko jingine lenye habari hiyo? Je, unaweza kutumia mfano kuonyesha sababu za jambo unalosema? Je, maswali yako yanaweza kuwasaidia wasikilizaji waone sababu ya jambo hilo? Kusababu hivyo kunaweza kuwavutia watu na kuwafanya wafikiri.
-