-
Kutumia Habari Ambazo UmepewaFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 43
Kutumia Habari Ambazo Umepewa
BIBLIA inalinganisha kutaniko la Kikristo na mwili wa binadamu. Kila kiungo ni muhimu, lakini ‘vyote havifanyi kazi ileile.’ Kwa hiyo, tufanye bidii tukipewa pendeleo lolote. Hiyo inamaanisha tuelewe hotuba yoyote ambayo tumepewa na kuishughulikia vizuri badala ya kuchukulia kijuu-juu tu habari fulani tukidhani hazipendezi kama habari nyinginezo. (Rom. 12:4-8) Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara ina daraka la kuandaa chakula cha kiroho “kwa wakati ufaao.” (Mt. 24:45) Tukitumia vipawa vyetu kutoa hotuba kwa kufuata maagizo ambayo tumepokea, inaonyesha tunathamini mpango huo. Hiyo inachangia utaratibu mzuri wa kutaniko lote.
Mambo ya Kutaja Katika Hotuba. Kama umepewa habari ya kuzungumzia katika shule, hakikisha unazungumzia habari hiyo wala si mambo mengine. Mara nyingi, utapewa marejeo hususa. Ikiwa hujaagizwa habari hususa za kutumia, unaweza kukusanya habari vile unavyopenda. Lakini, unapotayarisha hotuba, hakikisha hotuba yote inategemea kichwa ulichopewa. Unapofikiria jambo la kutia ndani ya hotuba, wafikirie wasikilizaji pia.
Chunguza kwa makini marejeo ambayo umepewa na maandiko yaliyomo. Kisha fikiria jinsi ya kutumia habari hiyo kwa njia itakayofaidi wasikilizaji. Chagua mambo mawili au labda matatu katika marejeo yaliyochapishwa ambayo yatakuwa mambo makuu katika hotuba yako. Vilevile, katika zile habari ambazo umepewa chagua maandiko ambayo unapanga kusoma na kuzungumzia.
Unapaswa kutumia kiasi gani cha habari zilizo katika marejeo? Tumia tu habari ambayo unaweza kuzungumzia vizuri. Usikose kufundisha vizuri kwa kuzungumzia mambo mengi mno. Kama baadhi ya habari hizo hazichangii kusudi la hotuba yako, tilia maanani sehemu ambazo zitakusaidia kutimiza kusudi lako. Katika zile habari ambazo umepewa, tumia tu habari ambazo zitawaelimisha na kuwafaidi wasikilizaji. Kusudi la kutimiza shauri hili la usemi ni, kutumia habari ambazo umepewa na wala si wingi wa habari utakazozungumzia katika hotuba.
Hotuba si muhtasari tu wa habari ulizopewa. Panga kueleza mambo fulani, kuyafafanua, kutumia mifano, na labda kuonyesha jinsi watu wanavyoweza kuyatumia maishani. Tumia mambo ya ziada kufafanua mambo makuu katika habari ambazo umepewa badala ya kubadilisha habari hizo.
Baadaye ndugu ambao wamestahili kufundisha wanaweza kupewa migawo ya kufundisha katika Mkutano wa Utumishi. Wanafahamu kwamba wanapaswa kutumia vizuri habari ambazo wamepewa badala ya kuzibadilisha na mambo mengine. Vilevile ndugu wanaotoa hotuba za watu wote hupewa mihtasari ya kufuata. Ingawa mihtasari hiyo inamruhusu msemaji kubadilikana, inaonyesha wazi mambo makuu ya kuzungumzia, hoja zinazounga mkono mambo makuu, na maandiko yaliyo msingi wa hotuba. Kujifunza kufundisha ukitumia habari ambazo umepewa ni njia muhimu ya kujitayarishia mapendeleo mengine ya kufundisha.
Mazoezi hayo pia yanaweza kukusaidia kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani yenye maendeleo. Utajifunza kukazia akili habari unayozungumza badala ya kukengeuka na kuzungumzia mambo mengine ambayo huenda yakawa yanapendeza lakini hayachangii mazungumzo hayo. Kwa upande mwingine, ukielewa kusudi la somo hili hutashikilia mno habari mnayojifunza na kukosa kufafanua jambo ambalo huenda mwanafunzi anahitaji kujua.
-
-
Kutumia Maswali VizuriFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 44
Kutumia Maswali Vizuri
MASWALI huhusisha wasikilizaji kwa sababu yanahitaji majibu ya mdomo au ya kimoyomoyo. Maswali yanaweza kukusaidia kuanzisha mazungumzo na kuyafurahia. Ukiwa msemaji na mwalimu, unaweza kutumia maswali kuamsha upendezi wa mtu, kumsaidia mtu asababu kuhusu habari fulani, au kukazia jambo unalosema. Maswali mazuri yanawasaidia wengine kufikiri badala ya kusikiliza tu. Uwe na kusudi fulani akilini, na uulize maswali kwa njia inayokusaidia kutimiza kusudi hilo.
Ili Kuendeleza Mazungumzo. Unapokuwa katika utumishi wa shambani, uwe macho kuona pindi za kuwaomba watu maoni yao ikiwa hawaoni ubaya kuulizwa maswali.
Mashahidi wengi huanzisha mazungumzo yenye kupendeza kwa kuuliza swali kama, “Je, umewahi kufikiria . . . ?” Wakichagua swali ambalo watu wengi wanalifikiria sana, hakika watafurahia utumishi wa shambani. Hata kama mtu hajawahi kusikia swali ambalo umeuliza, bado linaweza kuchochea fikira zake. Tunaweza kuzungumzia mambo mengi kwa kuuliza maswali kama “Unaonaje . . . ?” na “Je, unaamini . . . ?”
Mweneza-evanjeli Filipo alimwendea ofisa wa makao ya kifalme kutoka Ethiopia ambaye alikuwa akisoma kwa sauti unabii wa Isaya. Filipo akamwuliza: “Je, wewe kwa hakika wajua [au, unaelewa] unayoyasoma?” (Mdo. 8:30) Swali hilo lilimwezesha Filipo amweleze kweli kuhusu Yesu Kristo. Mashahidi wengine leo wametumia swali kama hilo kuzungumza na watu ambao wametamani sana kuelewa vizuri kweli ya Biblia.
Watu wengi husikiliza wakipewa nafasi ya kutoa maoni. Baada ya kuuliza swali, sikiliza kwa makini. Uwe mwenye fadhili badala ya kuchambua jibu la mtu huyo. Mpongeze kutoka moyoni inapowezekana. Pindi moja, Yesu alimpongeza mwandishi mmoja ambaye ‘alijibu kwa kutumia akili,’ akamwambia: ‘Hauko mbali na ufalme wa Mungu.’ (Mk. 12:34) Hata kama hukubaliani naye, unaweza kumshukuru kwa kujieleza. Maneno yake yanaweza kukuonyesha mambo unayohitaji kufikiria unapozungumza naye kweli ya Biblia.
Ili Kutokeza Mambo Muhimu. Ikiwa unahutubia watu au unazungumza na mtu, jaribu kutumia maswali yanayoelekeza kwenye mambo muhimu. Hakikisha unauliza maswali ambayo kwa kweli wasikilizaji wangependa kujua majibu yake. Pia unaweza kutumia maswali yanayochochea fikira kwa sababu majibu yake si wazi. Ukitua kifupi baada ya kuuliza swali, inaelekea wasikilizaji watasikiliza kwa hamu zaidi mambo yanayofuata.
Pindi moja nabii Mika alitumia maswali kadhaa. Baada ya kuuliza juu ya takwa la Mungu kwa waabudu wake, nabii huyo aliuliza maswali mengine manne, labda kila swali likiwa na jibu. Maswali hayo yote yanawasaidia wasomaji kutazamia majibu yenye ufahamu wa ndani ambayo nabii huyo anamalizia mazungumzo. (Mika 6:6-8) Je, unaweza kufanya hivyo unapofundisha? Ebu jaribu.
Ili Kusababu Juu ya Habari. Maswali yanaweza kutumiwa kuwasaidia wengine waelewe sababu zinazotolewa. Yehova alifanya hivyo alipotoa matangazo mazito dhidi ya Israeli kama tunavyoona katika Malaki 1:2-10. Kwanza aliwaambia: “Nimewapenda ninyi.” Hawakuthamini upendo huo, akawauliza: “Je, Esau siye ndugu yake Yakobo?” Kisha Yehova akataja hali ya ukiwa ya Edomu ili kuthibitisha kwamba kwa sababu ya uovu wao, Mungu hakupenda taifa hilo. Kisha akaendelea kutoa mifano na kuuliza maswali ili kukazia jinsi ambavyo Israeli limeshindwa kuitikia vizuri upendo wake. Baadhi ya maswali hayo yanaulizwa kana kwamba ni makuhani wasio waaminifu wanayauliza. Mengine ni maswali ambayo Yehova anawauliza makuhani. Mazungumzo hayo yanatugusa moyo na kuvuta uangalifu wetu, na kusababu kunakotumiwa ni wazi kabisa, na ujumbe unaotolewa hauwezi kusahaulika.
Wasemaji wengine huuliza maswali mazuri kwa njia hiyo. Hata ingawa wasikilizaji hawatarajiwi kujibu, wao huyafikiria, kana kwamba wanashiriki katika mazungumzo hayo.
Tunapoongoza mafunzo ya Biblia, tunatumia njia inayomfanya mwanafunzi ashiriki. Bila shaka kuna faida zaidi ikiwa mwanafunzi hasomi tu majibu ambayo yamechapwa. Kwa sauti ya fadhili, tumia maswali ya ziada kusababu na mwanafunzi. Unapozungumzia mambo makuu, mtie moyo atumie Biblia kujibu. Pia unaweza kumwuliza: “Jambo tunalozungumzia linapatanaje na jambo hili jingine ambalo tumejifunza? Kwa nini ni muhimu? Jambo hili liguse maisha yetu kwa njia gani?” Kutumia maswali kwa njia hiyo ni bora kuliko kueleza imani yako au wewe mwenyewe kufafanua jambo kwa urefu mno. Kwa njia hiyo, unamsaidia mwanafunzi kutumia ‘nguvu za kufikiri’ kumwabudu Mungu.—Rom. 12:1.
Ikiwa mwanafunzi haelewi jambo fulani, uwe na subira. Labda anajaribu kulinganisha jambo unalosema na mambo ambayo ameamini kwa miaka mingi. Huenda ikafaa kuzungumzia jambo hilo kwa njia tofauti. Lakini nyakati nyingine unahitaji kusababu tu naye. Tumia Maandiko sana. Tumia mifano. Hali kadhalika, tumia maswali rahisi yanayomsaidia kusababu kwa msingi wa uthibitisho uliopo.
Ili Kutambua Hisia za Moyoni. Watu wanapojibu maswali, nyakati nyingine hawaonyeshi hisia zao za moyoni. Wanaweza tu kukupa majibu ambayo wanafikiri unataka. Unahitaji ufahamu. (Mit. 20:5) Kama Yesu, mwulize hivi: “Je, unaamini hili?”—Yn. 11:26.
Wanafunzi wengi wa Yesu walipokasirika na kumwacha kwa sababu ya jambo alilosema, Yesu aliwaomba mitume maoni yao. Akawauliza: “Nyinyi hamtaki kwenda pia, je, mwataka?” Petro akaonyesha hisia zao za moyoni, akasema: “Bwana, tutaenda zetu kwa nani? Wewe una semi za uhai udumuo milele; na sisi tumeamini na tumekuja kujua kwamba wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.” (Yn. 6:67-69) Pindi nyingine, Yesu aliwauliza wanafunzi wake: “Watu wanasema Mwana wa binadamu ni nani?” Kisha akauliza swali ambalo lingeonyesha maoni yao ya moyoni. “Ingawa hivyo, nyinyi mwasema mimi ni nani?” Petro akasema: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”—Mt. 16:13-16.
Unapoongoza funzo la Biblia, inaweza kufaa kutumia njia hizo kushughulikia hali fulani. Unaweza kumwuliza hivi: “Wanafunzi wenzako (au wafanyakazi wenzako) wanaonaje jambo hili?” Kisha uulize: “Wewe unalionaje?” Ukijua hisia za kweli za mtu, inakuwa rahisi kumsaidia sana ukiwa mwalimu.
Ili Kutia Mkazo. Unaweza kutumia maswali pia kukazia mawazo. Mtume Paulo alifanya hivyo katika Waroma 8:31, 32: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, nani atakayekuwa dhidi yetu? Yeye ambaye hakumwachilia hata Mwana wake mwenyewe bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, kwa nini pia yeye pamoja naye hatatupa sisi kwa fadhili vitu vingine vyote?” Ona kwamba kila swali linategemea maneno anayotangulia kutaja.
Nabii Isaya alionyesha usadikisho thabiti baada ya kuandika hukumu ya Yehova dhidi ya mfalme wa Babiloni, akiongezea kusema: “Maana BWANA wa majeshi amekusudia, naye ni nani atakayelibatili? na mkono wake ulionyoshwa, ni nani atakayeugeuza nyuma?” (Isa. 14:27) Maswali kama hayo huonyesha kwamba jambo linalotajwa haliwezi kukanushwa. Jibu halihitajiwi.
Ili Kufichua Fikira Zisizofaa. Maswali ambayo yamefikiriwa vizuri pia yanasaidia sana kufichua kufikiri kusikofaa. Kabla ya Yesu kumponya mtu fulani, aliwauliza Mafarisayo na wanasheria swali hili: “Je, yaruhusika kisheria kuponya siku ya sabato au sivyo?” Baada ya kumponya, akawauliza swali jingine: “Ni nani kati yenu, ikiwa mwana wake au fahali aanguka ndani ya kisima, hatamtoa nje mara hiyo siku ya sabato?” (Luka 14:1-6) Yesu hakutarajia wamjibu wala hawakumjibu. Maswali hayo yalifichua fikira zao zisizofaa.
Nyakati nyingine, hata Wakristo wa kweli wanaweza kufikiri isivyofaa. Katika karne ya kwanza, wengine katika Korintho walikuwa wakishtaki ndugu zao mahakamani ili kusuluhisha matatizo ambayo wao wenyewe walipaswa kuyasuluhisha kati yao. Mtume Paulo alifanyaje? Aliuliza maswali mengi hususa ili kurekebisha fikira zao.—1 Kor. 6:1-8.
Ukifanya mazoezi, unaweza kujifunza kutumia maswali vizuri. Lakini kumbuka kuonyesha heshima, hasa unapozungumza na watu wenye umri mkubwa, watu ambao huwafahamu, na wenye mamlaka. Tumia maswali kufundisha kweli ya Biblia kwa njia inayovutia.
-
-
Mifano InayofundishaFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 45
Mifano Inayofundisha
MIFANO ni njia yenye nguvu sana ya kufundisha. Mara nyingi inavutia wasikilizaji na kuvuta uangalifu wao. Inachochea fikira za watu. Inachochea hisia na inaweza kugusa dhamiri na mioyo. Nyakati nyingine, unaweza kutumia mifano kushinda tatizo fulani. Pia mifano husaidia sana kukumbuka mambo. Je, wewe hutumia mifano unapofundisha?
Tamathali ni semi fupi ambazo zinaweza kufanya mtu apige picha dhahiri akilini. Ukichagua semi za tamathali kwa makini, maana yake inakuwa wazi. Lakini mwalimu mzuri anaweza kuzifafanua kwa ufupi ili kutia mkazo. Biblia imejaa mifano ambayo unaweza kujifunza.
Anza na Tashbihi na Sitiari. Tashbihi ni tamathali rahisi sana za usemi. Ikiwa unajifunza kutumia mifano, inaweza kufaa kuanza na semi hizi. Kwa kawaida semi hizo hutangulizwa na neno “kama” au “mfano wa.” Tashbihi hulinganisha vitu viwili vilivyo tofauti kabisa lakini vyenye ufanani fulani. Biblia imejaa tamathali zinazotaja mimea, wanyama, na vitu kama nyota na pia mambo yanayohusu wanadamu. Zaburi 1:3 inatuambia kwamba mtu anayesoma Neno la Mungu kwa ukawaida ni “kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji,” mti unaozaa matunda na usionyauka. Mtu mwovu anatajwa kuwa “kama simba” anayeotea windo. (Zab. 10:9) Yehova alimwahidi Abrahamu kwamba mbegu yake ingekuwa nyingi “kama nyota za mbinguni” na “kama mchanga ulioko pwani.” (Mwa. 22:17) Yehova alisema hivi kuhusu uhusiano wa karibu aliokuwa nao na taifa la Israeli: “Kama vile mshipi unavyoshikamana na viuno vya mtu,” ndivyo Alivyofanya Israeli na Yuda kushikamana na Yeye.—Yer. 13:11.
Sitiari pia hukazia ufanano ulioko kati ya mambo mawili yaliyo tofauti kabisa. Lakini sitiari ina mkazo zaidi. Sitiari ni maneno yanayoonyesha kitu fulani kuwa kitu kingine. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nyinyi ndio nuru ya ulimwengu.” (Mt. 5:14) Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi alipokuwa akieleza madhara ya kuongea bila kufikiri: “Ulimi ni moto.” (Yak. 3:6) Daudi alimwimbia hivi Yehova: “Ndiwe genge langu na ngome yangu.” (Zab. 31:3) Kwa kawaida sitiari nzuri haihitaji kufafanuliwa. Ufupi wake hukazia uzito wake. Sitiari inaweza kuwasaidia wasikilizaji kukumbuka jambo kuliko maelezo tu.
Utiaji chumvi wa jambo fulani hutumiwa katika mazungumzo, lakini ni lazima utumiwe kwa busara ama sivyo unaweza kueleweka vibaya. Yesu alitumia tamathali ya aina hiyo kutaja jambo ambalo hatuwezi kusahau alipouliza: “Kwa nini wautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe?” (Mt. 7:3) Kabla ya kujaribu kutumia tamathali ya aina hii, jifunze kutumia tashbihi na sitiari.
Tumia Mifano. Badala ya kutumia tamathali za usemi, unaweza kufundisha kwa kutumia mifano ya hadithi au ya mambo halisi yaliyotendeka. Mara nyingi watu hupita kiasi wanapotumia mifano, kwa hiyo uitumie kwa busara. Mifano inapaswa kutumiwa kutegemeza mambo ambayo kweli ni muhimu, na itumiwe kwa njia inayofanya jambo kuu likumbukwe, wala si kusimulia tu hadithi.
Ingawa si lazima mifano yote iwe mambo yaliyotokea kihalisi, inapasa kuonyesha mitazamo au hali halisi za maisha. Kwa hiyo, Yesu alipokuwa akifundisha jinsi ya kuwatendea watenda-dhambi wenye kutubu, alitoa mfano wa mtu aliyefurahi sana kupata kondoo wake aliyepotea. (Luka 15:1-7) Mtu fulani hakuelewa vizuri amri ya Sheria ya kumpenda jirani. Yesu akamsimulia hadithi ya Msamaria mmoja aliyemsaidia mtu aliyejeruhiwa baada ya kuhani na Mlawi kukosa kumsaidia. (Luka 10:30-37) Ukijifunza kuwa makini kuona mitazamo na matendo ya watu, unaweza kutumia vizuri njia hii ya kufundisha.
Nabii Nathani alimkaripia Mfalme Daudi kwa kusimulia hadithi aliyobuni. Hadithi hiyo ilifaa sana kwa sababu ilimfanya Daudi asiweze kujitetea. Hadithi hiyo ilimhusu tajiri mmoja aliyekuwa na kondoo wengi na maskini mmoja aliyekuwa na kondoo mmoja tu wa kike ambaye alimtunza sana. Daudi aliwahi kuwa mchungaji, basi alielewa kabisa hisia za yule mwenye kondoo mmoja. Daudi akashikwa na ghadhabu ya haki dhidi ya yule tajiri aliyemnyakua kondoo yule mmoja wa maskini. Kisha Nathani akamwambia Daudi wazi: “Wewe ndiwe mtu huyo”! Moyo wa Daudi ukaguswa, akatubu kweli. (2 Sam. 12:1-14) Ukifanya mazoezi, unaweza kushughulikia hali ngumu kwa njia nzuri.
Maandiko yana mifano mingi inayosaidia sana kufundisha. Yesu alifanya hivyo kwa maneno machache aliposema: “Mkumbukeni mke wa Loti.” (Luka 17:32) Yesu alirejelea “siku za Noa” alipofafanua kindani ishara ya kuwapo kwake. (Mt. 24:37-39) Katika Waebrania sura ya 11, mtume Paulo aliwataja kwa majina wanaume na wanawake 16 waliokuwa mifano mizuri ya imani. Unapoifahamu Biblia vizuri, utaweza kutumia mifano mingi mizuri sana katika Maandiko inayozungumzia matukio na watu.—Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11.
Nyakati nyingine inaweza kufaa kukazia jambo kwa kusimulia tukio fulani halisi la nyakati zetu. Lakini, hakikisha unatumia mambo yaliyoonwa ambayo yamethibitishwa na kuepuka yale ambayo yanaweza kumwaibisha msikilizaji yeyote au epuka mambo yenye ubishi ambayo hayahusiani na habari unayozungumzia. Pia kumbuka kwamba jambo lililoonwa linapasa kutimiza kusudi fulani. Usisimulie mambo madogo-madogo yanayoweza kukengeusha watu kutoka kwenye kusudi lako.
Je, Mfano Huo Unaeleweka? Mfano wowote unaotumia unapasa kutimiza kusudi fulani. Je, mfano huo utatimiza kusudi hilo kama huonyeshi jinsi unavyohusiana na habari unayozungumzia?
Yesu alisema wanafunzi wake ni “taa ya ulimwengu,” akafafanua kwa ufupi jinsi taa inavyotumiwa na jinsi usemi huo unavyohusiana na daraka lao. (Mt. 5:15, 16) Baada ya Yesu kutoa mfano wa kondoo aliyepotea, alitaja shangwe inayotokea mbinguni mtu mmoja mwenye dhambi akitubu. (Luka 15:7) Na baada ya Yesu kusimulia ile hadithi ya Msamaria mwenye ujirani, alimwuliza yule mtu swali hususa kisha akamshauri. (Luka 10:36, 37) Katika hali tofauti, Yesu aliwafafanulia watu wanyenyekevu waliotaka kujua mfano kuhusu aina mbalimbali za udongo na ule wa magugu shambani, lakini hakuufafanulia umati mifano hiyo. (Mt. 13:1-30, 36-43) Siku tatu kabla ya kufa, Yesu alitoa mfano unaohusu walimaji wa shamba la mizabibu waliokuwa wauaji. Hakueleza maana ya mfano huo kwa sababu hakukuwa na haja. “Makuhani wakuu na Mafarisayo . . . wakajua kwamba alikuwa akisema juu yao.” (Mt. 21:33-45) Kwa hiyo, mfano wako, maoni ya wasikilizaji, na kusudi lako ni muhimu katika kuamua iwapo utaeleza maana ya mfano huo na kadiri utakavyoufafanua.
Kukuza uwezo wa kutumia mifano vizuri huchukua muda, lakini kuna baraka. Mifano mizuri huvutia akili na kugusa moyo. Matokeo ni kwamba ujumbe wako unakuwa na uzito ambao hauwezi kutokezwa na maneno tu.
-
-
Mifano ya Hali za KawaidaFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 46
Mifano ya Hali za Kawaida
BILA SHAKA ni muhimu kutumia mifano ambayo inapatana na habari unayozungumzia. Lakini ili mifano hiyo iwe na matokeo, ni muhimu pia ifae wasikilizaji.
Wasikilizaji wanahusikaje na aina ya mifano unayotumia unapowahutubia? Yesu Kristo alifanya nini? Yesu alipokuwa akizungumza na umati wa watu au na wanafunzi wake hakutumia mifano ya mambo ambayo hayakujulikana katika Israeli. Watu hawangeelewa mifano kama hiyo. Kwa mfano, Yesu hakutaja maisha katika makao ya kifalme kule Misri wala matendo ya kidini katika India. Lakini alitumia mifano ambayo ilihusu utendaji wa kawaida wa watu katika nchi zote. Alizungumzia kushona nguo, kufanya biashara, kupoteza kitu chenye thamani, na kuhudhuria sherehe za arusi. Alifahamu jinsi ambavyo watu hutenda katika hali mbalimbali, na alitumia vizuri hali hizo katika mifano. (Mk. 2:21; Luka 14:7-11; 15:8, 9; 19:15-23) Kwa kuwa Yesu alifundisha Waisraeli hasa, mara nyingi mifano yake iligusia vitu na utendaji uliokuwa kawaida katika maisha yao. Kwa hiyo, alitaja mambo kama ukulima, jinsi kondoo wanavyomtii mchungaji, na kuhifadhi divai katika ngozi za wanyama. (Mk. 2:22; 4:2-9; Yn. 10:1-5) Pia alitaja mifano ya matukio ambayo watu walielewa kama vile uumbaji wa wanadamu wawili wa kwanza, Furiko la siku za Noa, kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora, kifo cha mke wa Loti, pamoja na mifano mingine. (Mt. 10:15; 19:4-6; 24:37-39; Luka 17:32) Unapochagua mifano ya kutumia, je, wewe pia hufikiria kwa makini mambo ambayo wasikilizaji hutenda kwa ukawaida na desturi zao?
Namna gani kama unazungumza na mtu mmoja au labda watu wachache badala ya watu wengi? Jaribu kuchagua mfano ambao hasa unafaa vizuri watu hao wachache. Yesu alipomhubiria yule mwanamke Msamaria kwenye kisima kimoja karibu na Sikari, alitaja “maji yaliyo hai,” ‘kutopata kiu hata kidogo,’ na “bubujiko la maji linalobubujika ili kutoa uhai udumuo milele”—hizo zote ni semi zinazohusu utendaji wa mwanamke huyo. (Yn. 4:7-15) Na Yesu alipozungumza na wanaume waliokuwa wakiosha nyavu zao, alitumia semi zinazohusu uvuvi. (Luka 5:2-11) Katika hali hizo mbili, Yesu angalitaja mambo ya ukulima kwa sababu watu hao waliishi katika eneo la ukulima, lakini mifano yake ilikuwa na matokeo zaidi kwa sababu alitaja utendaji wao binafsi ili waelewe mambo wazi. Je, unajitahidi kufanya hivyo?
Ingawa Yesu alikazia fikira “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli,” mtume Paulo hakutumwa kwa Israeli tu, bali pia kwa watu wa Mataifa. (Mt. 15:24; Mdo. 9:15) Je, jambo hilo lilibadili mazungumzo ya Paulo? Ndiyo. Katika barua aliyowaandikia Wakristo kule Korintho, alitaja mambo ambayo watu wa Mataifa walifahamu kama mashindano ya kukimbia, mazoea ya kula katika mahekalu ya sanamu, na maandamano ya kusherehekea ushindi.—1 Kor. 8:1-10; 9:24, 25; 2 Kor. 2:14-16.
Je, wewe huchagua kwa uangalifu mifano unayotumia kama Yesu na Paulo? Je, unafikiria desturi na utendaji wa kila siku wa wasikilizaji wako? Ni kweli kwamba ulimwengu umebadilika tangu karne ya kwanza. Watu wengi wanafahamu habari za ulimwengu kupitia televisheni. Mara nyingi wanafahamu hali katika nchi nyinginezo. Ikiwa ndivyo hali ilivyo, si vibaya kutumia habari hizo kama mifano. Hata hivyo, mambo yanayogusa sana mioyo ya watu ni yale yanayohusu maisha yao ya kawaida ya nyumbani, ya familia, kazini, ya chakula, na hali ya hewa.
Ukiona unahitaji kufafanua sana mfano wako, huenda ikawa unazungumzia jambo ambalo wasikilizaji hawalielewi. Mfano kama huo unaweza kufunika kwa urahisi jambo unalofundisha. Basi, wasikilizaji wanaweza kukumbuka mfano lakini wasiweze kukumbuka kweli ya Maandiko uliyokuwa ukijaribu kufundisha.
Yesu alitumia mambo rahisi ya kila siku badala ya kufanya ulinganifu unaotatanisha. Alitumia mambo madogo kufafanua mambo makubwa na mambo rahisi kufafanua mambo magumu. Yesu aliunganisha mambo ya kawaida na kweli za kiroho, akawasaidia watu kushika vizuri zaidi kweli hizo na kuzikumbuka. Huo ni mfano mzuri sana wa kuiga!
-