-
Kutayarisha Migawo ya ShuleFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Kutayarisha Migawo ya Shule
KILA hotuba katika shule inakupa nafasi ya kufanya maendeleo. Tia bidii sana, na polepole maendeleo yako yatakuwa dhahiri kwako na kwa wengine. (1 Tim. 4:15) Shule itakusaidia kukuza uwezo wako zaidi.
Je, unakuwa na wasiwasi unapofikiria kuhutubu mbele ya kutaniko? Hiyo ni kawaida, hata kama umeshiriki katika shule hii kwa muda mrefu. Lakini kuna mambo fulani ambayo yanaweza kukusaidia kupunguza wasiwasi. Uwe na zoea la kusoma kwa sauti unapokuwa nyumbani. Toa maelezo mara nyingi kwenye mikutano ya kutaniko na ikiwa wewe ni mhubiri, uwe wa kawaida katika huduma ya shambani. Ukifanya hivyo utazoea kusema mbele ya watu. Pia, tayarisha migawo yako mapema, na ufanye mazoezi ya kuzitoa hotuba hizo kwa sauti. Kumbuka kwamba utatoa hotuba mbele ya wasikilizaji wenye urafiki. Kabla ya kutoa hotuba yoyote, sali kwa Yehova. Kwa furaha yeye huwapa roho takatifu watumishi wake wanaomwomba.—Luka 11:13; Flp. 4:6, 7.
Usitarajie kwamba hotuba yako itakuwa bora kabisa. Inachukua muda kuwa msemaji mwenye uzoefu na mwalimu bora. (Mika 6:8) Ikiwa umejiunga na shule hivi karibuni, usitarajie kutoa hotuba kamilifu mara hiyo. Badala yake, fanyia kazi shauri moja la usemi kwa wakati mmoja. Soma sehemu ya kitabu hiki inayozungumzia shauri hilo. Ikiwezekana, fanya mazoezi ambayo yamedokezwa katika sehemu hiyo. Hiyo itafanya ujue mambo yanayohusu shauri hilo kabla ya kutoa hotuba yako kutanikoni. Na utafanya maendeleo.
Jinsi ya Kutayarisha Mgawo wa Usomaji
Kujitayarisha kusoma mbele ya watu kunahusu mambo mengi kuliko tu kuweza kutaja maneno unayosoma. Jitahidi kuelewa kabisa habari hiyo. Mara tu unapopokea mgawo wa usomaji, soma habari hiyo ili uielewe vizuri. Ili uweze kuwasilisha mawazo kwa usahihi na kwa hisia inayofaa, jaribu kuelewa jambo kuu la kila sentensi na wazo kuu la kila fungu. Ikiwezekana, chunguza kamusi ili ujue matamshi sahihi ya maneno usiyoyafahamu. Fahamu kabisa habari hiyo. Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao wadogo kufanya hivyo.
Je, umepata mgawo wa kusoma Biblia au labda mafungu ya Mnara wa Mlinzi? Kama kuna kaseti za kusikiliza katika lugha unazoelewa ambazo zina habari utakayosoma, unaweza kufaidika sana kusikiliza usomaji huo na kufikiria mambo kama matamshi, namna ya kusoma maneno, kutia mkazo, na kubadilisha sauti. Kisha jaribu kutumia sifa hizo unaposoma.
Unapoanza kutayarisha mgawo wako, hakikisha kwamba umesoma kwa makini somo linalozungumzia shauri la usemi ambalo utafanyia kazi. Ikiwezekana, lipitie tena somo hilo baada ya kusoma kwa sauti mgawo wako mara kadhaa. Jaribu kufuata shauri lililoandikwa kwa kadiri iwezekanavyo.
Mazoezi haya yatakusaidia sana katika huduma. Unapokuwa katika utumishi wa shambani, unapata nafasi nyingi za kusomea wengine. Kwa kuwa Neno la Mungu lina uwezo wa kubadili maisha ya watu, ni muhimu kulisoma vizuri. (Ebr. 4:12) Usifikiri kwamba utaweza kufikiria kanuni zote za usomaji mzuri utimizapo migawo michache ya usomaji. Mtume Paulo alimwandikia hivi mzee mmoja Mkristo aliyekuwa na uzoefu wa miaka mingi: “Endelea kujitahidi mwenyewe kusoma mbele ya watu wote.”—1 Tim. 4:13.
Kutayarisha Ukifikiria Kichwa Kikuu na Kikao
Ukipokea mgawo katika shule ambao unahusu kikao, ufanyeje?
Kuna mambo matatu ya kufikiria: (1) habari utakayozungumzia, (2) kikao chako na yule ambaye utazungumza naye, na (3) shauri ambalo unapaswa kufanyia kazi.
Unahitaji kufanya utafiti. Lakini kabla ya kufanya utafiti huo, fikiria sana kikao chako na vilevile yule ambaye utazungumza naye, kwa sababu mambo haya yanahusu sana habari ambayo utatoa na jinsi utakavyoitoa. Utatumia kikao gani? Je, utaonyesha jinsi ya kumhubiria mtu unayemjua? Au utaonyesha jambo unaloweza kusema unapokutana na mtu kwa mara ya kwanza? Je, mtu huyo anakuzidi umri ama wewe unamzidi umri? Anaweza kuwa na maoni gani kuhusu habari unayotaka kuzungumza? Huenda ikawa tayari anajua nini kuhusu habari hiyo? Unatumaini kutimiza kusudi gani katika mazungumzo yenu? Majibu ya maswali hayo yataandaa miongozo muhimu ya kukusaidia kutayarisha.
Utapata wapi habari zinazohusu hotuba yako? Kuna habari inayohusu “Jinsi ya Kufanya Utafiti” kwenye ukurasa wa 33 hadi 38 katika kitabu hiki. Soma sehemu hiyo, kisha utumie vifaa vya kufanyia utafiti vinavyopatikana. Mara nyingi utagundua haraka kwamba kuna habari nyingi kuliko unavyoweza kutumia. Soma kiasi cha habari kinachokuwezesha kutambua mambo uwezayo kupata. Lakini unaposoma, kumbuka kikao utakachotumia katika hotuba yako na vilevile yule ambaye utazungumza naye. Tia alama mambo yanayofaa kutumiwa.
Kabla ya kupanga hotuba yako na hatimaye kuchagua habari ambayo utazungumzia, usome shauri ambalo unafanyia kazi. Mojawapo ya sababu kubwa zinazofanya upewe mgawo wa kutoa hotuba ni kujifunza kufuata shauri hilo.
Ukitoa hotuba kwa wakati uliowekwa, utakuwa na nafasi ya kutoa umalizio wake, kwa kuwa ishara itatolewa wakati muda uliowekwa unapoisha. Lakini tunapokuwa katika huduma ya shambani kwa kawaida hatuwekewi wakati wa kufuata. Basi unapotayarisha, fikiria wakati uliowekewa, lakini hakikisha utafundisha vizuri.
Kuhusu Vikao. Chunguza madokezo yaliyo kwenye ukurasa wa 82, na uchague dokezo moja ambalo unaweza kutumia katika huduma yako na ambalo litakuwezesha kutumia habari ya hotuba yako. Ikiwa umekuwa katika shule kwa muda fulani, chukua nafasi hii kufanya maendeleo na kukuza uwezo zaidi wa kutimiza huduma.
Ikiwa mwangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi amekupa kikao, ukitumie. Vikao vingi huhusu kutoa ushahidi. Ikiwa hujapata kutoa ushahidi katika hali kama hizo zinazoonyeshwa, omba maoni ya wahubiri wengine ambao wamepata kutoa ushahidi katika hali kama hizo. Ikiwezekana, jaribu kufanya mazoezi ya kutoa hotuba yako ukitumia kikao ambacho utatumia katika shule. Hiyo itakusaidia kutimiza kusudi muhimu la mazoezi yako.
Kama Una Mgawo wa Kutoa Hotuba
Ikiwa wewe ni mwanamume, unaweza kupewa mgawo wa kutoa hotuba fupi mbele ya kutaniko. Unapotayarisha hotuba hizo, mambo ya msingi ambayo unahitaji kufikiria yanafanana na yale ambayo tayari yameorodheshwa kuhusu hotuba ya mwanafunzi inayotolewa kwa njia ya maonyesho. Tofauti kubwa iliyopo ni wale unaozungumza nao na jinsi ya kuitoa hotuba hiyo.
Kwa kawaida inafaa kutayarisha habari yako ili ifaidi kila mmoja wa wasikilizaji. Tayari wengi kati ya wahudhuriaji wanajua kweli za msingi za Biblia. Inawezekana kwamba wanafahamu vizuri hotuba yako. Fikiria mambo ambayo tayari wanajua kuhusu habari hiyo. Jaribu kufanya utoaji wako uwafaidi kwa njia fulani. Jiulize: ‘Nawezaje kutumia habari hii kwa njia ambayo itanifanya mimi na wasikilizaji tumthamini Yehova hata zaidi? Habari hii itatusaidiaje kufahamu mapenzi ya Mungu? Habari hii inaweza kutusaidiaje kufanya maamuzi mazuri katika ulimwengu uliojaa tamaa za kimwili?’ (Efe. 2:3) Utafiti unahitajiwa ili kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali haya. Unapotumia Biblia, usisome tu maandiko. Fafanua maandiko unayotumia, na uonyeshe jinsi yanavyoandaa msingi wa kufikia maamuzi. (Mdo. 17:2, 3) Usijaribu kuzungumzia mambo mengi mno. Toa hotuba yako kwa njia itakayofanya wasikilizaji waikumbuke kwa urahisi.
Matayarisho yanatia ndani kufikiria jinsi utakavyotoa hotuba hiyo. Usipuuze jambo hilo. Ufanye mazoezi ya kutoa hotuba yako kwa sauti. Jitihada zako za kujifunza na kufuata mashauri ya usemi zitakusaidia sana kufanya maendeleo. Uwe msemaji mpya au msemaji mwenye uzoefu, tayarisha vizuri ili uweze kutoa hotuba kwa usadikisho na hisia zinazofaa habari yako. Unapotimiza kila mgawo katika shule, kumbuka kwamba kusudi lako ni kutumia zawadi ya usemi uliyopewa na Mungu kumheshimu Yehova.—Zab. 150:6.
-
-
Kutayarisha Hotuba kwa Ajili ya KutanikoFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Kutayarisha Hotuba kwa Ajili ya Kutaniko
PROGRAMU ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi imetayarishwa ili ifaidi kutaniko lote. Pia kuna habari muhimu kwenye mikutano mingine na katika makusanyiko. Kama una hotuba katika mojawapo ya programu hizo, ujue umepewa daraka zito. Mtume Paulo alimhimiza mwangalizi Mkristo Timotheo afikirie ufundishaji wake. (1 Tim. 4:16) Wale wanaohudhuria mikutano ya Kikristo wametenga wakati wao muhimu na wengine wamejitahidi sana kuhudhuria ili wasikilize mafundisho yanayohusu uhusiano wao pamoja na Mungu. Ni pendeleo kama nini kutoa hotuba hizo! Unaweza kushughulikiaje vizuri pendeleo hilo?
Mambo Makuu ya Usomaji wa Biblia
Sehemu hii ya shule inategemea usomaji wa Biblia wa juma hilo. Inapasa kukazia jinsi habari hiyo inavyotuhusu leo. Kama inavyoonyeshwa katika Nehemia 8:8, Ezra na wenzake walisoma Neno la Mungu mbele ya watu, ‘wakaeleza maana yake,’ watu wakafahamu. Wewe pia unapata nafasi ya kufanya hivyo unaposhughulikia mambo makuu ya Biblia.
Utayarisheje mambo makuu? Ikiwezekana, soma sehemu hiyo ya Biblia juma moja au zaidi mapema. Kisha fikiria kutaniko na mahitaji yake. Sali juu ya jambo hilo. Ni mashauri gani, mifano gani, kanuni gani za sehemu hii ya Neno la Mungu zinazoshughulikia mahitaji hayo?
Ni muhimu kufanya utafiti. Je, kuna Watchtower Library kwenye CD-ROM au Watch Tower Publications Index au faharisi ya mwisho wa mwaka kwenye Mnara wa Mlinzi katika lugha unayoelewa? Ikiwa ndivyo, vitumie vizuri. Kwa kufanyia utafiti mambo ambayo tayari yamechapishwa yanayohusu maandiko ambayo umechagua kuzungumzia, unaweza kupata habari zenye kuelimisha, maelezo ya utimizo wa unabii, mambo ambayo maandiko fulani yanafunua kuhusu Yehova, au mazungumzo ya kanuni za Maandiko. Usijaribu kuzungumzia mambo mengi mno. Fikiria maandiko machache tu ambayo umechagua. Ni afadhali kuzungumzia mambo machache na kuyafafanua vizuri.
Pia huenda mgawo wako ukatia ndani kuwaomba wasikilizaji waeleze faida walizopata katika usomaji wa Biblia juma hilo. Walijifunza nini ambacho kitawafaidi katika funzo lao la binafsi na la familia au katika huduma yao au maishani mwao? Ni sifa gani za Yehova ambazo zinaonekana wazi kwa jinsi anavyoshughulika na watu na pia mataifa? Wasikilizaji walijifunza nini ambacho kiliimarisha imani yao na kufanya wamthamini Yehova zaidi? Usizungumzie sana mambo ya ndani yanayotatanisha. Kazia maana ya mambo ambayo umechagua na jinsi yanavyoweza kutumiwa maishani.
Hotuba ya Maagizo
Hii inategemea habari iliyochapishwa katika Mnara wa Mlinzi au Amkeni! au labda kitabu fulani. Kwa kawaida kuna habari nyingi mno kuliko wakati uliowekwa. Utoeje hotuba hii? Kama mwalimu, si kupitia tu habari hiyo. Ni sharti mwangalizi ‘astahili kufundisha.’—1 Tim. 3:2.
Anza kutayarisha kwa kusoma habari hiyo. Soma maandiko. Tafakari. Jaribu kufanya hivyo mapema kabla ya siku ya hotuba yako. Kumbuka kwamba akina ndugu hutiwa moyo kusoma mapema habari itakayozungumziwa. Basi daraka lako ni kuonyesha jinsi wasikilizaji wanavyoweza kutumia habari hiyo wala si kuipitia tu au kuifupisha. Fafanua sehemu muhimu za habari hiyo kwa njia ambayo itafaidi kutaniko.
Kama vile kila mtoto alivyo na utu wake mwenyewe, ndivyo na kila kutaniko lilivyo na hali zake. Mzazi anayefundisha vizuri harudii-rudii tu kumtajia mtoto wake mambo ya maadili kama wimbo. Anasababu na mtoto. Anafikiria utu wa mtoto na matatizo ambayo mtoto huyo anakabili. Vivyo hivyo, walimu kutanikoni hujaribu kuelewa na kushughulikia mahitaji ya wasikilizaji. Lakini, mwalimu mwenye busara anaepuka kutumia mifano ambayo inaweza kuaibisha mmojawapo wa wasikilizaji. Yeye hutaja faida ambazo tayari zimepatikana kwa kutembea katika njia ya Yehova na kukazia shauri la Maandiko ambalo litasaidia kutaniko kushinda matatizo yake.
Mwalimu mzuri hugusa mioyo ya wasikilizaji. Yeye hataji tu mambo bali anafanya wathamini mambo hayo. Mwalimu mzuri anahangaikia sana wale anaowafundisha. Wachungaji wa kiroho wanapaswa kujua kundi. Wakikumbuka kwa upendo matatizo ambayo akina ndugu wanakabili, wataweza kutoa hotuba yenye kutia moyo, wakielewa hali na kuonyesha huruma.
Kama walimu wazuri wanavyojua, ni lazima hotuba iwe na kusudi dhahiri. Hotuba inapasa kutolewa kwa njia ya kwamba mambo makuu yanaeleweka wazi na yanakumbukwa. Inatakikana wasikilizaji waweze kukumbuka mambo yatakayowasaidia maishani mwao.
Mkutano wa Utumishi
Unaweza kukabili ugumu ulio tofauti kidogo unapotoa hotuba inayotegemea Huduma Yetu ya Ufalme. Utaona kwamba mara nyingi utahitajika kuzungumza na wasikilizaji habari ambayo umepewa badala ya wewe kuchagua habari inayofaa. Saidia wasikilizaji wasababu kwa kutumia maandiko ambayo ndiyo msingi wa shauri lolote linalotolewa. (Tito 1:9) Mara nyingi wakati hautoshi na hauruhusu habari za ziada.
Kwa upande mwingine, unaweza kuombwa uzungumzie habari ambayo haipo kwenye Huduma Yetu ya Ufalme. Unaweza kuonyeshwa habari inayopatikana katika Mnara wa Mlinzi, au unaweza kupewa maagizo machache tu. Ukiwa mwalimu, ni juu yako kufikiria jinsi habari hiyo inavyohusu mahitaji ya kutaniko. Huenda ukahitaji kutumia mfano mfupi mzuri au kusimulia jambo fulani lililoonwa ambalo linafaa. Badala ya kusimulia tu habari hiyo, kumbuka kwamba una daraka la kutoa hotuba kwa njia inayochochea kutaniko litimize maagizo ya Neno la Mungu na kufurahia kufanya hivyo.—Mdo. 20:20, 21.
Unapotayarisha hotuba yako, fikiria hali za ndugu kutanikoni. Wapongeze kwa mambo ambayo tayari wanafanya. Wakitumia madokezo ya hotuba yako, shangwe yao inaweza kuongezekaje katika huduma?
Je, hotuba yako ina maonyesho au mahojiano? Ikiwa ndivyo, tayarisha mapema. Ni rahisi kumwomba mtu mwingine afanye matayarisho hayo, lakini mara nyingi hiyo haiwi na matokeo mazuri. Ikiwezekana, fanya mazoezi ya wonyesho au mahojiano kabla ya siku ya mkutano. Hakikisha kwamba unafuata maagizo kabisa unaposhughulikia hotuba yako.
-