-
Ishara za Mwili na za UsoFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 12
Ishara za Mwili na za Uso
WATU wa malezi fulani-fulani hutumia ishara zaidi kuliko watu wa malezi mengine. Lakini, karibu kila mtu hutumia ishara za uso na ishara fulani za mwili wanapoongea na watu wengine au wanapohutubia watu.
Yesu na wanafunzi wake wa mapema walizoea kutumia ishara. Pindi moja, mtu fulani alimwambia Yesu kwamba mama yake na ndugu zake wanataka kuongea naye. Yesu alijibu: “Ni nani mama yangu, na ni nani ndugu zangu?” Biblia inaendelea kusema: “Akinyoosha mkono wake kuelekea wanafunzi wake, akasema: ‘Tazama! Mama yangu na ndugu zangu!’” (Mt. 12:48, 49) Biblia inaonyesha katika Matendo 12:17 na 13:16 kwamba mtume Petro na mtume Paulo pia walitumia ishara, na kuna marejeo mengine kama hayo.
Mbali na sauti, ishara za mwili na za uso huonyesha pia mawazo na hisia. Mtu asipotumia ishara hizo vizuri, watu wanaweza kudhani hajali. Lakini mtu akitumia vizuri sauti yake pamoja na ishara, hotuba yake inakuwa bora sana. Hata kama unazungumza na mwingine kwa simu, ikiwa unatoa ishara nzuri za mwili na za uso, sauti yako itaonyesha zaidi umuhimu wa ujumbe wako na jinsi unavyohisi kuhusu jambo unalosema. Basi, kama unatoa hotuba kwa njia ya maongezi au unasoma, iwe wasikilizaji wanakuangalia au wanaangalia Biblia zao, ni muhimu kutumia ishara za mwili na za uso.
Ishara za mwili na za uso zinapasa kutokea kwa njia ya kawaida, na isionekane ni kama umeziiga kwenye kitabu. Hukujifunza jinsi ya kucheka au kuudhika. Vivyo hivyo ishara zinapasa kuonyesha hisia zako za ndani. Inatakikana ishara zitokee zenyewe zaidi na zaidi.
Kwa ujumla kuna aina mbili za ishara za mwili: ishara za ufafanuzi na za mkazo. Ishara za ufafanuzi huonyesha tendo au ukubwa na pia mahali. Unaposhughulikia ishara katika shule, usitumie ishara moja au mbili tu. Jaribu kutoa ishara kwa njia ya kawaida katika hotuba yote. Kama unashindwa kutoa ishara, unaweza kutafuta maneno yanayoonyesha mahali, umbali, ukubwa, au maneno yanayolinganisha mahali fulani na mahali pengine. Hata hivyo, mara nyingi unahitaji tu kutoa hotuba kwa moyo wako, bila kujali watu wanakuonaje, lakini ukiongea na kufanya mambo kama kawaida yako. Mtu akitulia, ishara zake hutokea zenyewe tu.
Ishara za mkazo huonyesha hisia na usadikisho. Ishara hizo hukazia mambo nazo ni muhimu. Lakini jihadhari! Ni rahisi sana ishara za mkazo ziwe mazoea yasiyotakikana. Ikiwa unatumia ishara ile ile moja kila wakati, inaweza kujitokeza na kuwa jambo kuu badala ya kuboresha hotuba yako. Mwangalizi wa shule akionyesha una tatizo hili, jaribu kutumia ishara za ufafanuzi pekee kwa muda fulani. Baadaye anza kutumia tena ishara za mkazo.
Ili ujue kadiri unavyopasa kutumia ishara za mkazo na mikazo inayofaa, wafikirie wale unaowahutubia. Wasikilizaji wanaweza kufadhaika ukiwanyoshea kidole. Katika jamii fulani-fulani mwanamume hawezi kutumia ishara fulani kuonyesha mshangao, kama vile kufunika mdomo wake kwa mkono kwa sababu kufanya hivyo huonwa kuwa tabia ya kike. Katika sehemu nyingine za ulimwengu, mwanamke hawezi kutumia sana ishara za mkono kwa sababu watu watafikiri hana adabu. Basi katika sehemu kama hizo, hasa akina dada wanahitaji kutumia zaidi ishara za uso. Na katika karibu kila sehemu ya ulimwengu, kutoa ishara zenye kupita kiasi mbele ya watu wachache kunaweza kuonwa kuwa vioja vya kuchekesha.
Unapoendelea kupata ujuzi na kuzoea kutulia unapotoa hotuba, ishara zozote za mkazo unazotumia zitaonyesha hisia zako za ndani, usadikisho wako na unyofu wako. Zitafanya maneno yako yawe na maana.
Ishara ya Uso Wako. Mara nyingi uso wako huonyesha jinsi unavyohisi kwelikweli kuliko sehemu nyingine yoyote ya mwili wako. Macho yako, umbo la mdomo wako, na kichwa chako vinahusika. Pasipo neno lolote, uso unaweza kuonyesha kutojali, machukizo, kutatanika, mshangao, au furaha. Ukionyesha ishara kama hizo unapoongea, zitakazia mambo unayosema. Muumba ameweka zaidi ya misuli 30 usoni mwako. Karibu nusu ya misuli hiyo hutumika unapotabasamu.
Iwe unatoa hotuba jukwaani au unahubiri shambani, unajaribu kuwaeleza watu ujumbe unaopendeza ambao unaweza kufurahisha mioyo yao. Tabasamu ya kutoka moyoni huthibitisha jambo hilo. Kwa upande mwingine, ikiwa uso wako hauonyeshi hisia yoyote, watu wanaweza kutia shaka kama kweli unaamini mambo unayosema.
Na zaidi, tabasamu huonyesha wengine kwamba unawapenda. Tabasamu ni muhimu sana hasa siku hizi ambapo watu huwaogopa wale wasiowafahamu. Tabasamu inaweza kuwastarehesha na kufanya watake kusikiliza zaidi.
-
-
Kuwatazama WasikilizajiFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 13
Kuwatazama Wasikilizaji
MACHO yetu huonyesha maoni yetu na hisia zetu. Yanaweza kuonyesha mshangao au hofu. Yanaweza kuonyesha huruma au upendo. Nyakati nyingine, yanaweza kuonyesha shaka au huzuni. Mtu mmoja mzee alisema hivi kuhusu wenzake waliokuwa wameteseka sana: “Macho yetu yanaonyesha masikitiko yetu.”
Watu wengine wanaweza kukata kauli juu yetu na juu ya mambo tunayosema ikitegemea mahali tunapotazama. Katika jamii nyingi, watu huelekea kumtumaini mtu anayewatazama macho kwa njia ya kirafiki. Kwa upande mwingine, ikiwa mtu anatazama miguu yake tu au vitu vingine badala ya kumtazama mtu anayeongea naye, watu wanaweza kuwa na shaka iwapo anasema kweli au wanaweza kutilia shaka uwezo wake. Na katika jamii nyingine, kumtazama sana mtu mwingine kwa macho kunaonwa kuwa ufidhuli, uchokozi, au ukaidi. Ndivyo ilivyo hasa unapoongea na mtu wa jinsia tofauti au mkuu fulani au mtu yeyote mwenye mamlaka. Na katika maeneo mengine, ni kukosa adabu ikiwa mtu mwenye umri mdogo atazama macho ya mtu mwenye umri mkubwa wanapoongea.
Lakini, mahali ambapo jambo hilo haliudhi, kumtazama mtu machoni unapotaja jambo muhimu kunaweza kukazia jambo hilo akilini mwake. Kufanya hivyo kunaweza kuonyesha kwamba unasadiki unayosema. Ona jinsi Yesu alivyojibu wanafunzi wake waliposhangaa na kusema: “Ni nani kwa kweli awezaye kuokolewa?” Biblia inasema: “Akiwatazama usoni, Yesu akawaambia: ‘Kwa wanadamu hilo haliwezekani, bali kwa Mungu mambo yote yawezekana.’” (Mt. 19:25, 26) Pia Maandiko yanaonyesha kwamba mtume Paulo alitazama kwa makini jinsi wasikilizaji walivyoitikia. Pindi moja, mtu fulani ambaye alikuwa mlemavu tangu kuzaliwa alikuwapo mahali Paulo alikuwa akizungumza. Andiko la Matendo 14:9, 10 linasema: “Mtu huyu alikuwa akisikiliza Paulo akisema, ambaye, alipomkazia macho na kuona alikuwa na imani ya kufanywa apone, alisema kwa sauti kubwa: ‘Simama wima kwa miguu yako.’”
Madokezo ya Kutumia Katika Huduma ya Shambani. Unapokuwa katika huduma ya shambani, uwe mwenye urafiki na mchangamfu unapowafikia watu. Ikiwa inafaa, tumia maswali yanayochochea akili ili kuanzisha mazungumzo kuhusu jambo ambalo linaweza kuwapendeza nyote. Unapofanya hivyo, jaribu kumtazama macho mtu huyo—au angalau mtazame usoni kwa heshima na fadhili. Tabasamu changamfu ya mtu mwenye shangwe ya moyoni huvutia sana. Tabasamu kama hiyo inaweza kumwonyesha wewe ni mtu wa aina gani na kumfanya astarehe zaidi mnapozungumza.
Ikiwa inafaa unaweza kujua jinsi ya kushughulika na mtu huyo kwa kumtazama machoni. Unaweza kutambua kama amekasirika au hapendezwi. Unaweza kutambua kama hakuelewi. Ni rahisi kutambua kama anachoka kukusikiliza. Pia itakuwa dhahiri ikiwa anapendezwa sana. Macho yake yanaweza kukuonyesha unahitaji kurekebisha mwendo wako wa kuongea, kujitahidi zaidi kumhusisha katika mazungumzo, kumaliza mazungumzo au, labda, kumwonyesha jinsi tunavyofanya funzo la Biblia.
Iwe unahubiri au unaongoza funzo la Biblia la nyumbani, jaribu kumtazama kwa heshima mtu unayezungumza naye. Lakini, usimkodolee macho kwani anaweza kuona haya. (2 Fal. 8:11) Lakini kwa njia ya kawaida na ya urafiki, mtazame mtu huyo usoni pindi kwa pindi. Katika nchi nyingi, kufanya hivyo huonyesha kwamba kwa kweli unapendezwa naye. Bila shaka macho yako yatakazia kile unachosoma katika Biblia au kichapo kinginecho kile. Lakini, unaweza kumtazama machoni kifupi unapotaka kukazia jambo. Utaweza kuona itikio lake ikiwa unamtazama pindi kwa pindi unaposoma.
Kama unashindwa kuwatazama watu machoni kwa sababu una haya, endelea kujitahidi. Ukifanya mazoezi, utaweza kuwatazama watu machoni kwa njia ya kawaida, na kuweza kuboresha uwezo wako wa kuwasiliana na wengine.
Unapotoa Hotuba. Biblia inatuambia kwamba kabla ya Yesu kuanza Mahubiri ya Mlimani, ‘aliinua macho yake kuwatazama wanafunzi wake.’ (Luka 6:20) Iga mfano wake. Kama utahutubia watu, watazame na utue kwa sekunde kadhaa kabla ya kuanza hotuba. Mahali pengi, kufanya hivyo kunahusisha kuwatazama baadhi ya wasikilizaji. Kutua kifupi kunaweza kukusaidia kuondoa wasiwasi. Pia kutawasaidia wasikilizaji wajipatanishe na hali yoyote au hisia yoyote ambayo uso wako unaonyesha. Vilevile kutua kifupi kutawawezesha wasikilizaji watulie na kuwa tayari kukusikiliza.
-