-
Mifano InayofundishaFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Nabii Nathani alimkaripia Mfalme Daudi kwa kusimulia hadithi aliyobuni. Hadithi hiyo ilifaa sana kwa sababu ilimfanya Daudi asiweze kujitetea. Hadithi hiyo ilimhusu tajiri mmoja aliyekuwa na kondoo wengi na maskini mmoja aliyekuwa na kondoo mmoja tu wa kike ambaye alimtunza sana. Daudi aliwahi kuwa mchungaji, basi alielewa kabisa hisia za yule mwenye kondoo mmoja. Daudi akashikwa na ghadhabu ya haki dhidi ya yule tajiri aliyemnyakua kondoo yule mmoja wa maskini. Kisha Nathani akamwambia Daudi wazi: “Wewe ndiwe mtu huyo”! Moyo wa Daudi ukaguswa, akatubu kweli. (2 Sam. 12:1-14) Ukifanya mazoezi, unaweza kushughulikia hali ngumu kwa njia nzuri.
Maandiko yana mifano mingi inayosaidia sana kufundisha. Yesu alifanya hivyo kwa maneno machache aliposema: “Mkumbukeni mke wa Loti.” (Luka 17:32) Yesu alirejelea “siku za Noa” alipofafanua kindani ishara ya kuwapo kwake. (Mt. 24:37-39) Katika Waebrania sura ya 11, mtume Paulo aliwataja kwa majina wanaume na wanawake 16 waliokuwa mifano mizuri ya imani. Unapoifahamu Biblia vizuri, utaweza kutumia mifano mingi mizuri sana katika Maandiko inayozungumzia matukio na watu.—Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11.
Nyakati nyingine inaweza kufaa kukazia jambo kwa kusimulia tukio fulani halisi la nyakati zetu. Lakini, hakikisha unatumia mambo yaliyoonwa ambayo yamethibitishwa na kuepuka yale ambayo yanaweza kumwaibisha msikilizaji yeyote au epuka mambo yenye ubishi ambayo hayahusiani na habari unayozungumzia. Pia kumbuka kwamba jambo lililoonwa linapasa kutimiza kusudi fulani. Usisimulie mambo madogo-madogo yanayoweza kukengeusha watu kutoka kwenye kusudi lako.
Je, Mfano Huo Unaeleweka? Mfano wowote unaotumia unapasa kutimiza kusudi fulani. Je, mfano huo utatimiza kusudi hilo kama huonyeshi jinsi unavyohusiana na habari unayozungumzia?
Yesu alisema wanafunzi wake ni “taa ya ulimwengu,” akafafanua kwa ufupi jinsi taa inavyotumiwa na jinsi usemi huo unavyohusiana na daraka lao. (Mt. 5:15, 16) Baada ya Yesu kutoa mfano wa kondoo aliyepotea, alitaja shangwe inayotokea mbinguni mtu mmoja mwenye dhambi akitubu. (Luka 15:7) Na baada ya Yesu kusimulia ile hadithi ya Msamaria mwenye ujirani, alimwuliza yule mtu swali hususa kisha akamshauri. (Luka 10:36, 37) Katika hali tofauti, Yesu aliwafafanulia watu wanyenyekevu waliotaka kujua mfano kuhusu aina mbalimbali za udongo na ule wa magugu shambani, lakini hakuufafanulia umati mifano hiyo. (Mt. 13:1-30, 36-43) Siku tatu kabla ya kufa, Yesu alitoa mfano unaohusu walimaji wa shamba la mizabibu waliokuwa wauaji. Hakueleza maana ya mfano huo kwa sababu hakukuwa na haja. “Makuhani wakuu na Mafarisayo . . . wakajua kwamba alikuwa akisema juu yao.” (Mt. 21:33-45) Kwa hiyo, mfano wako, maoni ya wasikilizaji, na kusudi lako ni muhimu katika kuamua iwapo utaeleza maana ya mfano huo na kadiri utakavyoufafanua.
Kukuza uwezo wa kutumia mifano vizuri huchukua muda, lakini kuna baraka. Mifano mizuri huvutia akili na kugusa moyo. Matokeo ni kwamba ujumbe wako unakuwa na uzito ambao hauwezi kutokezwa na maneno tu.
-
-
Mifano ya Hali za KawaidaFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 46
Mifano ya Hali za Kawaida
BILA SHAKA ni muhimu kutumia mifano ambayo inapatana na habari unayozungumzia. Lakini ili mifano hiyo iwe na matokeo, ni muhimu pia ifae wasikilizaji.
Wasikilizaji wanahusikaje na aina ya mifano unayotumia unapowahutubia? Yesu Kristo alifanya nini? Yesu alipokuwa akizungumza na umati wa watu au na wanafunzi wake hakutumia mifano ya mambo ambayo hayakujulikana katika Israeli. Watu hawangeelewa mifano kama hiyo. Kwa mfano, Yesu hakutaja maisha katika makao ya kifalme kule Misri wala matendo ya kidini katika India. Lakini alitumia mifano ambayo ilihusu utendaji wa kawaida wa watu katika nchi zote. Alizungumzia kushona nguo, kufanya biashara, kupoteza kitu chenye thamani, na kuhudhuria sherehe za arusi. Alifahamu jinsi ambavyo watu hutenda katika hali mbalimbali, na alitumia vizuri hali hizo katika mifano. (Mk. 2:21; Luka 14:7-11; 15:8, 9; 19:15-23) Kwa kuwa Yesu alifundisha Waisraeli hasa, mara nyingi mifano yake iligusia vitu na utendaji uliokuwa kawaida katika maisha yao. Kwa hiyo, alitaja mambo kama ukulima, jinsi kondoo wanavyomtii mchungaji, na kuhifadhi divai katika ngozi za wanyama. (Mk. 2:22; 4:2-9; Yn. 10:1-5) Pia alitaja mifano ya matukio ambayo watu walielewa kama vile uumbaji wa wanadamu wawili wa kwanza, Furiko la siku za Noa, kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora, kifo cha mke wa Loti, pamoja na mifano mingine. (Mt. 10:15; 19:4-6; 24:37-39; Luka 17:32) Unapochagua mifano ya kutumia, je, wewe pia hufikiria kwa makini mambo ambayo wasikilizaji hutenda kwa ukawaida na desturi zao?
Namna gani kama unazungumza na mtu mmoja au labda watu wachache badala ya watu wengi? Jaribu kuchagua mfano ambao hasa unafaa vizuri watu hao wachache. Yesu alipomhubiria yule mwanamke Msamaria kwenye kisima kimoja karibu na Sikari, alitaja “maji yaliyo hai,” ‘kutopata kiu hata kidogo,’ na “bubujiko la maji linalobubujika ili kutoa uhai udumuo milele”—hizo zote ni semi zinazohusu utendaji wa mwanamke huyo. (Yn. 4:7-15) Na Yesu alipozungumza na wanaume waliokuwa wakiosha nyavu zao, alitumia semi zinazohusu uvuvi. (Luka 5:2-11) Katika hali hizo mbili, Yesu angalitaja mambo ya ukulima kwa sababu watu hao waliishi katika eneo la ukulima, lakini mifano yake ilikuwa na matokeo zaidi kwa sababu alitaja utendaji wao binafsi ili waelewe mambo wazi. Je, unajitahidi kufanya hivyo?
Ingawa Yesu alikazia fikira “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli,” mtume Paulo hakutumwa kwa Israeli tu, bali pia kwa watu wa Mataifa. (Mt. 15:24; Mdo. 9:15) Je, jambo hilo lilibadili mazungumzo ya Paulo? Ndiyo. Katika barua aliyowaandikia Wakristo kule Korintho, alitaja mambo ambayo watu wa Mataifa walifahamu kama mashindano ya kukimbia, mazoea ya kula katika mahekalu ya sanamu, na maandamano ya kusherehekea ushindi.—1 Kor. 8:1-10; 9:24, 25; 2 Kor. 2:14-16.
Je, wewe huchagua kwa uangalifu mifano unayotumia kama Yesu na Paulo? Je, unafikiria desturi na utendaji wa kila siku wa wasikilizaji wako? Ni kweli kwamba ulimwengu umebadilika tangu karne ya kwanza. Watu wengi wanafahamu habari za ulimwengu kupitia televisheni. Mara nyingi wanafahamu hali katika nchi nyinginezo. Ikiwa ndivyo hali ilivyo, si vibaya kutumia habari hizo kama mifano. Hata hivyo, mambo yanayogusa sana mioyo ya watu ni yale yanayohusu maisha yao ya kawaida ya nyumbani, ya familia, kazini, ya chakula, na hali ya hewa.
Ukiona unahitaji kufafanua sana mfano wako, huenda ikawa unazungumzia jambo ambalo wasikilizaji hawalielewi. Mfano kama huo unaweza kufunika kwa urahisi jambo unalofundisha. Basi, wasikilizaji wanaweza kukumbuka mfano lakini wasiweze kukumbuka kweli ya Maandiko uliyokuwa ukijaribu kufundisha.
Yesu alitumia mambo rahisi ya kila siku badala ya kufanya ulinganifu unaotatanisha. Alitumia mambo madogo kufafanua mambo makubwa na mambo rahisi kufafanua mambo magumu. Yesu aliunganisha mambo ya kawaida na kweli za kiroho, akawasaidia watu kushika vizuri zaidi kweli hizo na kuzikumbuka. Huo ni mfano mzuri sana wa kuiga!
-