Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Nisome Biblia?
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2017 | Na. 1
    • Mwanamke akichukua Biblia kwenye rafu

      HABARI KUU | JINSI YA KUFAIDIKA ZAIDI UNAPOSOMA BIBLIA

      Kwa Nini Nisome Biblia?

      “Nilifikiri kwamba Biblia ni ngumu sana kuielewa.”​—Jovy

      “Nilihisi kwamba kusoma Biblia kunachosha.”​—Queennie

      “Nilipotazama ukubwa wa Biblia, nilikosa kabisa hamu ya kuisoma.”​—Ezekiel

      Je, umewahi kuhisi kama watu waliotajwa hapo juu kuhusu kusoma Biblia? Kwa watu wengi, kusoma Biblia kunaoneka kuwa jambo lenye kuchosha. Lakini namna gani ukijua kwamba Biblia inaweza kukusaidia kuwa na maisha yenye furaha na ya kuridhisha zaidi? Na vipi ukijua kwamba kuna mambo unayoweza kufanya ili ufurahie zaidi kuisoma Biblia? Je, utakuwa tayari kuisoma na kuona jinsi inavyoweza kukunufaisha?

      Chunguza maelezo machache ya wale ambao wamefaidika kwa kuisoma Biblia.

      Ezekiel, mwenye umri wa miaka 20 hivi anasema: “Zamani, nilikuwa kama mtu anayeendesha gari bila kujua mahali hususa anakoenda. Lakini kusoma Biblia kumenisaidia kupata kusudi la maisha. Biblia ina ushauri unaofaa ninaotumia kila siku.”

      Frieda, mwenye umri wa miaka 20 hivi anaeleza: “Nilikuwa mwenye hasira. Lakini kwa sababu ya kuisoma Biblia, nimejifunza jinsi ya kujidhibiti. Hilo limefanya iwe rahisi kwangu kupatana na wengine, na sasa nimekuwa na marafiki wengi.”

      Eunice, mwanamke mwenye umri wa miaka 50 hivi, alisema: “Biblia inanisaidia kuboresha utu wangu, na imenisaidia kuacha mazoea fulani mabaya.”

      Wasomaji hao pamoja na mamilioni ya watu wengine wamejifunza kwamba kusoma Biblia kunaweza kukusaidia uwe na maisha yenye furaha zaidi. (Isaya 48:17, 18) Miongoni mwa faida unazoweza kupata kwa kusoma Biblia ni (1) kufanya maamuzi mazuri, (2) kupata marafiki wa kweli, (3) kushughulika na mkazo kwa njia nzuri, na (4) muhimu zaidi, kujifunza ukweli kumhusu Mungu. Ushauri wa Biblia unatoka kwa Mungu, kwa hiyo huwezi kupata hasara kwa kuufuata. Mungu hawezi kamwe kutoa ushauri mbaya.

      Jambo muhimu ni kujua jinsi unavyoweza kuanza kusoma. Ni mapendekezo gani unayoweza kutumia ili uweze kuanza kusoma Biblia na kufurahia usomaji wako?

  • Nianze Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2017 | Na. 1
    • HABARI KUU | JINSI YA KUFAIDIKA KATIKA USOMAJI WAKO

      Mwanamke akisali kabla ya kusoma Biblia
      Nianze Jinsi Gani?

      Unaweza kufanya ili ufurahie usomaji wako wa Biblia na kufaidika zaidi? Chunguza mapendekezo matano ambayo yamewasaidia watu wengi.

      Andaa mazingira mazuri. Tafuta mazingira tulivu. Epuka mambo yanayoweza kukukengeusha unaposoma. Kusomea mahali penye mwanga wa kutosha na hewa safi kunaweza kufanya ufaidike zaidi.

      Uwe na mtazamo mzuri. Kwa kuwa Biblia ina ujumbe kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni, utafaidika zaidi ukiwa na mtazamo kama wa mtoto aliye tayari kufundishwa na mzazi wake mwenye upendo. Ikiwa una mtazamo au maoni yasiyofaa kuihusu Biblia, ondoa mtazamo huo ili uweze kufundishwa na Mungu.—Zaburi 25:4.

      Sali kabla ya kuanza kusoma. Biblia ina mawazo ya Mungu, kwa hiyo tunahitaji msaada wake ili kuielewa. Mungu ameahidi kuwapa “roho takatifu wale wanaomwomba.” (Luka 11:13) Roho takatifu itakusaidia kuelewa mawazo ya Mungu. Baada ya muda, itakusaidia kuelewa hata “mambo mazito ya Mungu.”—1 Wakorintho 2:10.

      Soma ili uelewe. Usisome tu ili kumaliza sehemu fulani. Tafakari kwa kina mambo unayosoma. Jiulize maswali kama haya: ‘Mtu huyu ninayesoma habari zake alikuwa na sifa gani? Ninaweza kutumiaje habari hii maishani mwangu?’

      Uwe na malengo hususa. Ili ufaidike na usomaji wa Biblia, uwe na lengo la kujifunza mambo hususa yatakayoboresha maisha yako. Unaweza kujiwekea malengo kama vile: ‘Kujifunza mengi kumhusu Mungu.’ ‘Kuboresha utu wangu, kuwa mume au mke bora.’ Kisha, chagua sehemu za Biblia zitakazokusaidia kutimiza malengo hayo.a

      Mapendekezo hayo matano yatakusaidia kuanza kuisoma Biblia. Lakini unaweza kufanya nini ili ufurahie zaidi usomaji wako? Makala inayofuata inatoa mapendekezo kadhaa.

      a Ikiwa hujui jinsi ya kupata habari za Biblia kuhusu mambo hayo, wasiliana na Mashahidi wa Yehova nao watafurahi kukusaidia.

      JINSI YA KUFAIDIKA KATIKA USOMAJI WAKO

      • Soma taratibu

      • Tafakari unayosoma na uwazie matukio hayo

      • Elewa muktadha wa mistari unayosoma

      • Tafuta mambo ya kujifunza katika usomaji wako

  • Ni Nini Kitakachofanya Nifurahie Kusoma Biblia?
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2017 | Na. 1
    • Mwanamke akitumia vifaa vya kujifunzia anaposoma Biblia

      HABARI KUU | JINSI YA KUFAIDIKA ZAIDI UNAPOSOMA BIBLIA

      Ni Nini Kitakachofanya Nifurahie Kusoma Biblia?

      Je, kusoma Biblia kunakuchosha au kunakufurahisha? Yote hayo yanategemea njia unayotumia katika usomaji wako. Acheni tuchunguze mambo unayoweza kufanya ili uongeze hamu ya kusoma na ufurahie zaidi.

      Chagua tafsiri sahihi na yenye lugha inayoeleweka. Ikiwa unasoma habari fulani yenye maneno magumu au yasiyoeleweka, ni wazi kwamba hutafurahia usomaji huo. Kwa hiyo, chagua Biblia yenye lugha rahisi kueleweka ambayo itagusa moyo wako. Wakati huohuo, Biblia hiyo inapaswa kuwa tafsiri sahihi na inayotegemeka.a

      Tumia teknolojia ya kisasa. Leo, Biblia inapatikana katika nakala zilizochapishwa, na pia katika mfumo wa vifaa vya elektroniki. Baadhi ya Biblia zinaweza kusomwa mtandaoni au kupakuliwa na kusomwa kupitia kompyuta, tablet, au simu. Baadhi ya programu za elektroniki zina mfumo unaoweza kukusaidia kulinganisha mistari ya Biblia inayohusu jambo unalosoma au hata kulinganisha tafsiri kadhaa. Ikiwa unapenda kusikiliza badala ya kusoma, Biblia pia inapatikana katika rekodi za kusikiliza kwa baadhi ya lugha. Wengi hupenda kusikiliza wanapotumia usafiri wa umma, wanapofua nguo, au wanapofanya kazi nyingine yoyote inayowaruhusu kusikiliza. Kwa nini usijaribu njia inayokufaa?

      Tumia vifaa vya kujifunzia Biblia. Vifaa vya kujifunzia Biblia vinaweza kukusaidia ufaidike zaidi na usomaji wako. Kuna ramani za nchi zinazotajwa katika Biblia, ambazo zitakusaidia kujua mahali ambapo jambo unalosoma lilitukia na hivyo kukuwezesha kuwazia matukio. Makala mbalimbali, kama zile zinazopatikana kwenye gazeti hili au sehemu yenye kichwa “Mafundisho ya Biblia” iliyo kwenye tovuti ya jw.org/sw, zinaweza kukusaidia kuelewa maana ya mistari mbalimbali ya Biblia.

      Tumia njia mbalimbali kusoma Biblia. Ikiwa kusoma Biblia kuanzia mwanzo hadi mwisho kunaoneka kuwa kunachosha, jaribu kusoma sehemu fulani za Biblia ambazo zinakuvutia. Pia, unaweza kutumia njia ya kusoma habari zinazohusu mtu mmoja-mmoja kati ya wale wanaotajwa katika Biblia. Mfano mmoja wa jinsi ya kufanya hivyo umeonyeshwa katika sanduku lenye kichwa, “Chimba Katika Biblia kwa Kuwajua Watu Wanaotajwa Humo.” Njia nyingine ni kusoma habari fulani hususa, moja baada ya nyingine, au kusoma kulingana na mfuatano wa matukio. Unaonaje ukitumia njia moja kati ya hizo?

      a Wengi wameona kwamba Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni sahihi, inategemeka, na ni rahisi kusoma. Biblia hiyo inachapishwa na Mashahidi wa Yehova, na inapatikana katika lugha zaidi ya 130. Unaweza kupakua nakala yako katika tovuti ya jw.org/sw au kupakua programu ya JW Library. Au wasiliana na Mashahidi wa Yehova wakuletee nakala ya Biblia.

      CHIMBA KATIKA BIBLIA KWA KUWAJUA WATU WANAOTAJWA HUMO

      Baadhi ya wanawake waaminifu

      Abigaili

      1 Samweli sura ya 25

      Esta

      Esta sura ya 2-5, 7-9

      Hana

      1 Samweli sura ya 1-2

      Maria

      (Mama ya Yesu) Mathayo sura ya 1-2; Luka sura ya 1-2; pia soma Yohana 2:1-12; Matendo 1:12-14; 2:1-4

      Rahabu

      Yoshua sura ya 2, 6; pia soma Waebrania 11:30, 31; Yakobo 2:24-26

      Rebeka

      Mwanzo sura ya 24-27

      Sara

      Mwanzo sura ya 17-18, 20-21, 23; pia soma Waebrania 11:11; 1 Petro 3:1-6

      Baadhi ya wanaume washikamanifu

      Abrahamu

      Mwanzo sura ya 11-24; pia soma 25:1-11

      Daudi

      1 Samweli sura ya 16-30; 2 Samweli sura ya 1-24; 1 Wafalme sura ya 1-2

      Yesu

      Vitabu vya Injili vya Mathayo, Marko, Luka, na Yohana

      Musa

      Kutoka sura ya 2-20, 24, 32-34; Hesabu sura ya 11-17, 20, 21, 27, 31; Kumbukumbu la Torati sura ya 34

      Noa

      Mwanzo sura ya 5-9

      Paulo

      Matendo sura ya 7-9, 13-28

      Petro

      Mathayo sura ya 4, 10, 14, 16-17, 26; Matendo sura ya 1-5, 8-12

      VIFAA VYA KUJIFUNZIA BIBLIA VILIVYOANDALIWA NA MASHAHIDI WA YEHOVA

      • JW.ORG​—Tovuti hii ina vipengele vingi vya kujifunzia, kutia ndani sehemu ya “Majibu ya Maswali ya Biblia.” Pia, inaeleza jinsi ya kupakua programu ya JW Library

      • “Ona Nchi Nzuri”​—Broshua hii ina ramani na picha za maeneo yanayotajwa katika Biblia

      • Insight on the Scriptures​—Ni mabuku mawili ya ensaiklopidia ya Biblia yenye ufafanuzi wa kina kuhusu watu, maeneo, na lugha iliyotumiwa katika Biblia

      • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”​—Kitabu hiki cha kujifunzia kinaeleza ni lini, wapi, na sababu ya kuandikwa kwa kila kitabu cha Biblia, pia, kinaeleza kwa ufupi ujumbe ulio katika kila kitabu

      • Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?​—Ni kitabu kidogo chenye utafiti wa kina unaothibitisha kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho

      • Biblia​—Ina Ujumbe Gani?​—Ni broshua yenye kurasa 32 inayoeleza kifupi habari kuu zilizo katika Biblia

  • Biblia Inawezaje Kuboresha Maisha Yangu?
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2017 | Na. 1
    • Mume na mke wakisaidiana kazi jikoni

      HABARI KUU | JINSI YA KUFAIDIKA ZAIDI UNAPOSOMA BIBLIA

      Biblia Inawezaje Kuboresha Maisha Yangu?

      Biblia si kitabu cha kawaida tu. Ni kitabu chenye mashauri kutoka Muumba wetu. (2 Timotheo 3:16) Ujumbe wake unaweza kutunufaisha sana. Kwa kweli, Biblia yenyewe inasema hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.” (Waebrania 4:12) Ina nguvu za kuboresha maisha yetu katika njia kuu mbili. Kwanza, inatoa mwongozo wa maisha ya kila siku, na pili inatusaidia kumjua Mungu na ahadi zake.—1 Timotheo 4:8; Yakobo 4:8.

      Jinsi inavyoweza kuboresha maisha yako sasa. Biblia inaweza kukusaidia hata katika mambo ya kibinafsi, kwa kuwa inatoa mwongozo unaofaa kuhusu mambo yafuatayo.

      • Mahusiano na watu wengine. —Waefeso 4:31, 32; 5:22, 25, 28, 33.

      • Afya na hali ya kihisia. —Zaburi 37:8; Methali 17:22.

      • Maadili.—1 Wakorintho 6:9, 10.

      • Hali ya uchumi.—Methali 10:4; 28:19; Waefeso 4:28.a

      Wenzi fulani wa ndoa waliooana hivi karibuni huko Asia wamefaidika sana na ushauri wa Biblia wenye thamani. Kama ilivyo kwa wenzi wengi wapya, wao walikuwa wakipambana kurekebisha tofauti zao za utu na kuboresha mawasiliano. Hivyo, waliamua kuanza kutumia yale waliyojifunza katika Biblia. Walipata matokeo gani? Vicent, ambaye ni mume katika familia hiyo alisema hivi: “Mambo niliyojifunza katika Biblia yamenisaidia kushugulikia changamoto za ndoa yetu kwa upendo. Kuishi kulingana na Biblia kumetusaidia kuwa na maisha yenye furaha.” Mke wake, Annalou, anakubaliana naye. Anasema hivi: “Kusoma mifano inayotajwa katika Biblia kumetusaidia. Sasa nina furaha na nimeridhika na hali ya ndoa na malengo yetu maishani.”

      Kumjua Mungu. Mbali na kueleza kuhusu ndoa, Vicent alisema hivi pia: “Kusoma Biblia, kunafanya nijihisi nikiwa karibu zaidi na Yehova.” Maelezo ya Vicent yanakazia kwamba Biblia inaweza kukusaidia umjue Mungu vizuri. Kwa kufanya hivyo, utanufaika na ushauri wake, na jambo muhimu zaidi ni kwamba utakuwa rafiki yake. Nawe utajifunza kwamba Mungu anaeleza kuhusu wakati ujao ulio mzuri, ambao tutafurahia “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima wa milele. (1 Timotheo 6:19) Hilo ni tumaini zuri sana ambalo huwezi kulipata katika kitabu kingine chochote.

      Ukiendelea kusoma Biblia kwa ukawaida, wewe pia utapata faida hizo, yaani, utaboresha maisha yako na utamjua Mungu vizuri. Hata hivyo, unaposoma Biblia, huenda ukajiuliza maswali mengi. Ukikabili hali hiyo, kumbuka mfano mzuri wa ofisa Mwethiopia aliyeishi miaka 2,000 hivi iliyopita. Alikuwa na maswali mengi kuhusu Biblia. Kwa hiyo, alipoulizwa ikiwa anaelewa mambo anayosoma, alijibu hivi: “Kwa kweli, ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?”b Kisha, bila kusita akakubali msaada kutoka kwa Filipo, mwalimu mzuri wa Biblia, ambaye alikuwa mwanafunzi wa Yesu. (Matendo 8:30, 31, 34) Vivyo hivyo, ikiwa unapenda kujua mengi kuhusu Biblia, tunakualika utume ombi lako kwenye mtandao kupitia www.jw.org/sw au kupitia anwani zilizo kwenye gazeti hili. Unaweza pia kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova au kutembelea Jumba la Ufalme lililo jirani na mahali unakoishi. Je, unaweza kuanza kusoma Biblia leo? Ukifanya hivyo, Biblia itakuongoza kwenye maisha bora sana!

      Ikiwa una shaka kama unaweza kuitumaini Biblia, tafadhali tazama video fupi yenye kichwa, Tunawezaje Kuwa na Hakika Kwamba Yale Yaliyoandikwa Katika Biblia Ni ya Kweli? Unaweza kuipata katika tovuti ya jw.org/sw, kisha, bofya kitufe cha Kutafuta, na uingize jina la video hiyo

      a Ili kupata habari zaidi kuhusu ushauri wa Biblia, tembelea tovuti yetu ya, jw.org/sw. Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MAJIBU YA MASWALI YA BIBLIA.

      b Pia, soma makala kwenye gazeti hili yenye kichwa “Kuelewa Maandiko Kimakosa, Je, Ni Tatizo Dogo?”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki