-
Je, Wote Wanaodai Kuwa Wakristo Ni Wakristo Kikweli?Mnara wa Mlinzi—2012 | Machi 1
-
-
Je, Wote Wanaodai Kuwa Wakristo Ni Wakristo Kikweli?
JE, UNAJUA idadi ya Wakristo ulimwenguni? Kulingana na kitabu Atlas of Global Christianity, katika mwaka wa 2010 kulikuwa na Wakristo bilioni 2.3 hivi duniani kote. Lakini kitabu hichohicho kinasema pia kwamba Wakristo hao ni wafuasi wa madhehebu 41,000, kila moja ya madhehebu hayo ikiwa na mafundisho na sheria zake kuhusu mwenendo. Kwa sababu kuna dini nyingi hivyo zinazodai kuwa za Kikristo, tunaelewa ni kwa nini watu fulani wamechanganyikiwa na hata kuvunjwa moyo. Huenda wakajiuliza, ‘Je, wote wanaodai kuwa Wakristo ni Wakristo kikweli?’
Acheni tuchunguze jambo hilo kwa njia tofauti. Kwa kawaida, msafiri hutarajiwa kutambulisha uraia wake kwa ofisa wa uhamiaji aliye mpakani. Pia, anahitaji kuthibitisha yeye ni nani kwa kuonyesha kitu cha kumtambulisha, labda pasipoti. Vivyo hivyo, Mkristo wa kweli anahitaji kufanya mengi zaidi ya kudai tu kwamba anamwamini Kristo. Anahitaji pia kujitambulisha kwa njia nyinginezo. Njia gani hizo?
Neno “Mkristo” lilianza kutumiwa mara ya kwanza muda fulani baada ya mwaka wa 44 W.K. Luka, mwanahistoria aliyeishi nyakati za Biblia aliandika hivi: ‘Kule Antiokia ndiko ambako kwa mara ya kwanza wanafunzi kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo.’ (Matendo 11:26) Ona kwamba wale walioitwa Wakristo walikuwa wanafunzi wa Kristo. Ni nini kinachothibitisha kwamba mtu ni mwanafunzi wa Yesu Kristo? Kamusi ya The New International Dictionary of New Testament Theology inaeleza hivi: “Kuwa mwanafunzi wa Yesu kunamaanisha kwamba mtu amejidhabihu kabisa bila masharti . . . kwa muda wote wa maisha yake.” Hivyo basi, Mkristo wa kweli ni yule anayefuata kikamili na bila masharti mafundisho na maagizo ya Yesu, yule Mwanzilishi wa Ukristo.
Je, inawezekana kuwapata watu kama hao miongoni mwa wengi wanaodai kuwa Wakristo leo? Yesu mwenyewe alisema ni nini ambacho kingewatambulisha wafuasi wake wa kweli? Tunakutia moyo uchunguze jinsi Biblia inavyojibu maswali hayo. Katika makala zinazofuata, tutachunguza mambo matano yaliyotajwa na Yesu ambayo yanawatambulisha wafuasi wake wa kweli. Tutachunguza jinsi Wakristo wa karne ya kwanza walivyotimiza mambo hayo. Na tutajitahidi kuona ni akina nani kati ya wengi wanaodai kuwa Wakristo ambao wanafanya hivyo leo.
-
-
‘Kaeni Katika Neno Langu’Mnara wa Mlinzi—2012 | Machi 1
-
-
‘Kaeni Katika Neno Langu’
“Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”—YOHANA 8:31, 32.
Inamaanisha Nini? “Neno” la Yesu linamaanisha mafundisho yake, ambayo chanzo chake ni cha juu zaidi. Yesu alisema: “Baba mwenyewe aliyenituma amenipa amri kuhusu jambo la kutangaza na la kusema.” (Yohana 12:49) Alipokuwa akisali kwa Baba yake wa mbinguni, Yehova Mungu, Yesu alisema: “Neno lako ni kweli.” Alinukuu Neno la Mungu mara nyingi ili kuunga mkono mafundisho yake. (Yohana 17:17; Mathayo 4:4, 7, 10) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli, ‘wanakaa katika neno lake,’ yaani, wanakubali Neno la Mungu Biblia, kuwa “kweli” na msingi pekee wa imani na matendo yao.
Wakristo wa Mapema Walifanyaje Hivyo? Mtume Paulo, ambaye ndiye Mkristo aliyeandika vitabu vingi zaidi katika Biblia, aliliheshimu Neno la Mungu kama Yesu alivyofanya. Aliandika hivi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.” (2 Timotheo 3:16) Wanaume waliowekwa rasmi ili kuwafundisha Wakristo wenzao walipaswa “kushikamana na Neno la Mungu lililo hakika na lenye kutegemeka.” (Tito 1:7, 9, The Amplified Bible) Wakristo wa mapema walihimizwa wakatae “falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Wakolosai 2:8.
Ni Nani Wanaofanya Hivyo Leo? Katiba ya Vatikani inayoitwa Dogmatic Constitution on Divine Revelation, iliyoanza kutumika mwaka wa 1965 na ambayo imenukuliwa katika kitabu kimoja cha kanisa Katoliki (Catechism of the Catholic Church) inasema hivi: “Kanisa [Katoliki] halifuati tu Maandiko Matakatifu katika kuhakikisha mambo yote yaliyofunuliwa. Kwa hiyo, mapokeo matakatifu na pia Maandiko Matakatifu yanapaswa kukubaliwa na kuheshimiwa kwa ushikamanifu uleule.” Makala moja katika gazeti la Maclean’s ilinukuu kasisi mmoja huko Toronto, Kanada, ambaye aliuliza: “Kwa nini tunahitaji kuongozwa na sauti ya ‘kimapinduzi’ ya miaka elfu mbili iliyopita? Tuna maoni mazuri ajabu, ambayo uzito wake hupungua nyakati zote kwa sababu tunalazimika kuyaunga mkono kwa kutumia Maandiko na maneno ya Yesu.”
Kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema hivi kuhusu Mashahidi wa Yehova: “Wanaiona Biblia kuwa chanzo pekee cha imani na sheria zinazoongoza mwenendo wao.” Hivi karibuni, mwanamume fulani huko Kanada alimkatiza mwanamke fulani Shahidi wa Yehova alipokuwa akijitambulisha. “Ninajua wewe ni nani,” akasema mwanamume huyo huku akiinyooshea kidole Biblia ya Shahidi huyo, “kwa sababu una kitambulisho.”
-
-
“Si Sehemu ya Ulimwengu”Mnara wa Mlinzi—2012 | Machi 1
-
-
“Si Sehemu ya Ulimwengu”
“Ulimwengu umewachukia, kwa sababu wao si sehemu ya ulimwengu.”—YOHANA 17:14.
Inamaanisha Nini? Yesu hakuwa sehemu ya ulimwengu, hivyo hakuunga mkono upande wowote wa mizozo ya kijamii na kisiasa katika siku zake. Alisema hivi: “Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Pia, aliwahimiza wafuasi wake waepuke mitazamo, usemi, na mwenendo unaoshutumiwa na Neno la Mungu.—Mathayo 20:25-27.
Wakristo wa Mapema Walifanyaje Hivyo? Kulingana na mwandishi wa mambo ya kidini, Jonathan Dymond, Wakristo wa mapema “walikataa kushiriki katika [vita]; bila kujali matokeo, iwe wangeshutumiwa, kufungwa gerezani, au kufa.” Walichagua kuteseka badala ya kuunga mkono upande wowote. Maadili yao yaliwafanya wawe tofauti pia. Wakristo waliambiwa: “Kwa sababu ninyi hamwendelei kukimbia pamoja nao katika mwendo huo kwenda kwenye dimbwi lilelile la chini la upotovu, wao wanashangaa na kuendelea kuwatukana ninyi.” (1 Petro 4:4) Mwanahistoria, Will Durant aliandika kwamba Wakristo “walisumbua dhamiri ya ulimwengu huo wa kipagani uliopenda anasa kwa sababu walimwogopa Mungu na walikuwa na mwenendo safi kiadili.”
Ni Nani Wanaofanya Hivyo Leo? Kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema hivi kuhusu msimamo wa Wakristo wa kutounga mkono upande wowote: “Kupatana na maadili, ni hatia kukataa kushiriki vita kwa sababu ya dhamiri.” Makala moja katika gazeti Reformierte Presse inasema kwamba ripoti ya shirika fulani la haki za kibinadamu (African Rights) kuhusu maangamizi ya jamii nzima-nzima huko Rwanda mwaka wa 1994, ilionyesha kwamba dini zote zilihusika, “isipokuwa Mashahidi wa Yehova.”
Akizungumza kuhusu yale Maangamizi Makubwa ya Nazi, mwalimu mmoja wa sekondari alisema hivi kwa huzuni: “Hakuna kikundi au shirika la raia wa kawaida ambalo lilishutumu uwongo mwingi, ukatili, na uovu uliotokea.” Baada ya kuwasiliana na Jumba la Makumbusho la Maangamizi Makubwa la Marekani, aliandika hivi: “Sasa nilikuwa nimepata jibu.” Alitambua kwamba Mashahidi wa Yehova walishikamana kabisa na imani yao hata ingawa waliteswa vikali.
Namna gani maadili yao? Gazeti U.S. Catholic linasema: “Vijana wengi Wakatoliki hawakubaliani na mafundisho ya kanisa yanayopinga kuishi pamoja bila kufunga ndoa kisheria [na] kufanya ngono kabla ya ndoa.” Gazeti hilo linamnukuu mhudumu fulani wa kanisa hilo aliyesema: “Asilimia kubwa ninayoona—nadhani ni zaidi ya asilimia 50—tayari wanaishi pamoja wanapokuja kufunga ndoa kisheria.” Kitabu The New Encyclopædia Britannica kinasema kwamba Mashahidi wa Yehova “wanakazia kufuata viwango vya juu vya maadili maishani mwao.”
-
-
‘Muwe na Upendo Kati Yenu Wenyewe’Mnara wa Mlinzi—2012 | Machi 1
-
-
‘Muwe na Upendo Kati Yenu Wenyewe’
“Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—YOHANA 13:34, 35.
Inamaanisha Nini? Kristo aliwaambia wafuasi wake wapendane jinsi alivyowapenda. Yesu aliwapenda jinsi gani? Aliwapenda watu ijapokuwa siku hizo ubaguzi wa kitaifa na kijinsia ulikuwa umeenea sana. (Yohana 4:7-10) Upendo ulimchochea Yesu kudhabihu wakati, nguvu, na pindi zake za kustarehe ili kusaidia wengine. (Marko 6:30-34) Mwishowe, Kristo alionyesha upendo kwa njia iliyo kubwa zaidi. Alisema: “Mimi ndiye mchungaji mwema; mchungaji mwema huitoa nafsi yake kwa ajili ya kondoo.”—Yohana 10:11.
Wakristo wa Mapema Walifanyaje Hivyo? Katika karne ya kwanza, Wakristo waliitana “ndugu” au “dada.” (Filemoni 1, 2) Watu wa mataifa yote walikaribishwa katika kutaniko la Kikristo, kwa maana waliamini kwamba “hakuna tofauti kati ya Myahudi na Mgiriki, kwa maana kuna Bwana yuleyule juu ya wote.” (Waroma 10:11, 12) Baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., wanafunzi huko Yerusalemu “wa[li]anza kuuza miliki na mali zao na kuwagawia wote mapato hayo, kulingana na vile yeyote alivyokuwa na uhitaji.” Kwa kusudi gani? Ili wale ambao walikuwa wametoka tu kubatizwa wakae Yerusalemu na kuendelea “kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume.” (Matendo 2:41-45) Ni nini kilichowachochea wafanye hivyo? Miaka isiyozidi 200 baada ya kifo cha mitume, Tertullian alinukuu mambo ambayo watu walisema kuhusu Wakristo: “Ona jinsi wanavyopendana . . . na jinsi walivyo tayari kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake.”
Ni Nani Wanaofanya Hivyo Leo? Kitabu The History of the Decline and Fall of the Roman Empire (1837) kinasema kwamba kwa karne nyingi watu wanaodai kuwa Wakristo “wametendeana kwa ukatili sana kuliko jinsi walivyotendewa na watu wasioamini.” Uchunguzi uliofanywa hivi karibuni huko Marekani ulifunua uhusiano mkubwa kati ya watu wanaofuata dini—wengi wao wakidai kuwa Wakristo—na ubaguzi wa kijamii. Katika nchi fulani, mara nyingi wafuasi wa dini fulani hawawafahamu wafuasi wa dini hiyohiyo wanaoishi katika nchi nyingine, na hivyo hawawezi au hawako tayari kuwasaidia waamini wenzao kunapokuwa na uhitaji.
Mwaka wa 2004, baada ya jimbo la Florida kukumbwa na vimbunga vinne katika kipindi cha miezi miwili, mwenyekiti wa Halmashauri ya Kushughulikia Hali ya Dharura huko Florida alifanya uchunguzi ili kuhakikisha kwamba misaada iliyotolewa ilitumiwa ifaavyo. Alisema kwamba hakuna kikundi kingine kilichokuwa na utaratibu kuliko Mashahidi wa Yehova, hivyo akajitolea kutoa misaada ambayo Mashahidi wangehitaji. Mapema katika mwaka wa 1997, kikundi cha wajitoleaji cha Mashahidi wa Yehova kilichokuwa kimebeba madawa, vyakula, na mavazi kilisafiri kwenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ili kuwasaidia ndugu zao Wakristo na watu wengine wenye uhitaji. Mashahidi wenzao barani Ulaya walikuwa wametoa michango mbalimbali yenye thamani ya dola zaidi ya milioni moja za Marekani.
-
-
“Nimewajulisha Jina Lako”Mnara wa Mlinzi—2012 | Machi 1
-
-
“Nimewajulisha Jina Lako”
“Nimelifunua jina lako kwa watu ulionipa kutoka ulimwenguni. . . . Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha.”—YOHANA 17:6, 26.
Inamaanisha Nini? Yesu aliwajulisha watu jina la Mungu kwa kulitumia katika huduma yake. Yesu alipokuwa akisoma Maandiko, kama alivyofanya mara nyingi, alitamka jina la kibinafsi la Mungu. (Luka 4:16-21) Aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: “Baba, jina lako na litakaswe.”—Luka 11:2.
Wakristo wa Mapema Walifanyaje Hivyo? Mtume Petro aliwaambia wanaume wazee huko Yerusalemu kwamba Mungu alikuwa amechukua kutoka katika mataifa “watu kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14) Mtume huyo na wengine walihubiri kwamba “kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” (Matendo 2:21; Waroma 10:13) Pia, walitumia jina la Mungu katika maandishi yao. Mkusanyo wa sheria za Wayahudi unaoitwa The Tosefta, ambao ulikamilishwa karibu mwaka wa 300 W.K., unasema hivi kuhusu maandishi ya Wakristo yaliyoteketezwa na wapinzani: “Wanaviteketeza vitabu vya Waevanjeli na vitabu vya minim [watu wanaodhaniwa kuwa Wakristo Wayahudi]. Vinaruhusiwa viteketee mahali vinapopatikana, . . . pamoja na marejeo ya Jina la Mungu lililo ndani ya vitabu hivyo.”
Ni Nani Wanaofanya Hivyo Leo? Biblia ya Revised Standard Version, iliyoidhinishwa rasmi na Baraza la Kitaifa la Makanisa ya Kristo nchini Marekani, inasema hivi katika utangulizi: “Mazoea ya kutumia jina la kibinafsi la Mungu wa pekee, kana kwamba kuna miungu mingine anayopaswa kutofautishwa nayo, yaliacha kufuatwa katika dini ya Kiyahudi kabla ya enzi ya Ukristo na hayafai kwa imani ya Kanisa la Kikristo la ulimwenguni pote.” Hivyo, Biblia hiyo inatumia jina la cheo “BWANA” badala ya kutumia jina la Mungu. Hivi karibuni, Vatikani iliwaagiza makasisi wake hivi: “Katika sala na nyimbo, jina la Mungu ambalo linawakilishwa na herufi YHWHa za tetragramatoni halipaswi kutumiwa wala kutamkwa.”
Ni nani ambao leo wanatumia na kuwajulisha watu jina la kibinafsi la Mungu? Sergey alipokuwa tineja huko Kyrgyzstan, aliona video iliyosema kwamba jina la Mungu ni Yehova. Kwa miaka kumi hivi, hakulisikia tena jina hilo. Baadaye, Sergey alipohamia Marekani, Mashahidi wawili wa Yehova walimtembelea nyumbani mwake na kumwonyesha jina la Mungu katika Biblia. Sergey alifurahi sana kupata kikundi kilichotumia jina Yehova. Inapendeza kuona kwamba chini ya jina “Yehova Mungu,” kamusi ya Webster’s Third New International Dictionary inatoa ufafanuzi huu: “Mungu mkuu anayetambuliwa kuwa Mungu wa pekee ambaye anaabudiwa na Mashahidi wa Yehova.”
[Maelezo ya Chini]
a Katika Kiswahili, kwa kawaida jina la Mungu linatafsiriwa “Yehova.”
-
-
“Hii Habari Njema ya Ufalme Itahubiriwa”Mnara wa Mlinzi—2012 | Machi 1
-
-
“Hii Habari Njema ya Ufalme Itahubiriwa”
“Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—MATHAYO 24:14.
Inamaanisha Nini? Luka, mwandikaji wa Injili, aliripoti kwamba Yesu ‘alisafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.’ (Luka 8:1) Yesu mwenyewe alisema: ‘Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.’ (Luka 4:43) Aliwatuma wanafunzi wake wahubiri habari njema katika miji na vijiji na baadaye akawaamuru hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Matendo 1:8; Luka 10:1.
Wakristo wa Mapema Walifanyaje Hivyo? Wanafunzi wa Yesu hawakusita kufanya kazi ambayo Yesu aliwapatia. “Kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo.” (Matendo 5:42) Kazi ya kuhubiri haikufanywa tu na kikundi kidogo cha watu walioheshimiwa. Mwanahistoria Neander alisema kwamba “Celsus, mwandishi wa kwanza aliyepinga Ukristo aliwadhihaki wanafunzi wa Yesu kwa kudai kuwa wafumaji wa sufu, washona-viatu, watengeneza-ngozi, watu wa kawaida wasio na elimu yoyote, walikuwa wahubiri wa injili wenye bidii.” Katika kitabu chake kinachoitwa The Early Centuries of the Church, Jean Bernardi aliandika: “[Wakristo] walipaswa kwenda kila mahali na kuzungumza na kila mtu. Kwenye barabara kuu na katika majiji, kwenye maeneo ya umma na nyumbani. Wakiwa wamekaribishwa au la. . . . Hadi miisho ya dunia.”
Ni Nani Wanaofanya Hivyo Leo? Kasisi Mwanglikana David Watson aliandika hivi: “Watu wengi leo hawako tayari kumtumikia Mungu kwa sababu kanisa limekataa kuchukua kwa uzito kazi ya kuhubiri.” Katika kitabu chake Why Are the Catholics Leaving? José Luis Pérez Guadalupe, aliandika kuhusu utendaji wa Wainjilisti, Waadventisti, na wengineo na kusema kwamba “hawahubiri nyumba kwa nyumba.” Aliandika hivi kuhusu Mashahidi wa Yehova: “Wanahubiri nyumba kwa nyumba kwa utaratibu.”
Maoni ya kweli na yenye kupendeza yaliyotolewa na Jonathan Turley yanapatikana katika kitabu Cato Supreme Court Review, 2001-2002: “Unapotaja Mashahidi wa Yehova, mara moja watu wengi wanafikiri kuhusu wahubiri wanaotutembelea nyumbani wakati usiofaa. Kwa Mashahidi wa Yehova, kuhubiri nyumba kwa nyumba si njia pekee ya kueneza imani yao bali ni sehemu muhimu ya imani yao.”
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
Je, Umewatambua Wakristo wa Kweli?
Kwa kutegemea ufafanuzi wa Maandiko yaliyozungumziwa katika mfululizo huu wa makala, unafikiri ni nani ambao leo wanaonyesha sifa zinazowatambulisha Wakristo wa kweli? Ingawa kuna makumi ya maelfu ya vikundi na dini zinazodai kuwa za Kikristo, kumbuka maneno ambayo Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia.” (Mathayo 7:21) Kuwatambua wale wanaofanya mapenzi ya Baba—jambo linalothibitisha kwamba wao ni Wakristo wa kweli—na kushirikiana nao kunaweza kumsaidia mtu apate baraka za milele chini ya Ufalme wa Mungu. Tunakutia moyo uwaombe Mashahidi wa Yehova, yaani, watu waliokupa gazeti hili, wakufundishe mengi zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu na baraka ambazo utaleta.—Luka 4:43.
-