Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tumaini Je, Linaweza Kutusaidia?
    Amkeni!—2004 | Aprili 22
    • Tumaini—Je, Linaweza Kutusaidia?

      DANIEL alikuwa ameugua kansa kwa mwaka mmoja alipokuwa na umri wa miaka kumi tu. Madaktari na rafiki zake wa karibu walikuwa wamekata tamaa. Hata hivyo, Daniel aliendelea kuwa na tumaini. Aliamini kwamba siku moja angekuwa mkubwa na kuwa mtafiti ambaye angesaidia kupata tiba ya kansa. Alitarajia sana kuja kwa daktari ambaye ni mtaalamu wa kutibu aina ya kansa aliyokuwa nayo. Hata hivyo, siku hiyo ilipofika, daktari huyo alilazimika kuvunja safari yake kwa sababu ya hali mbaya ya hewa. Daniel akakata tamaa. Kwa mara ya kwanza, akafadhaika. Akafa siku chache baadaye.

      Kisa cha Daniel kilisimuliwa na mfanyakazi wa afya ambaye alichunguza jinsi kuwa na tumaini au kupoteza tumaini kunavyoathiri afya. Huenda umesikia visa kama hivyo. Kwa mfano, fikiria mzee anayekaribia kufa ambaye anatarajia kwa hamu tukio fulani muhimu ambalo amengojea kwa muda mrefu, labda kutembelewa na mpendwa au sherehe fulani. Tukio hilo linapofika na kupita, mzee huyo hufa baada ya muda mfupi. Ni nini husababisha jambo hilo? Je, ni kukosa tumaini kama wengine wanavyoamini?

      Watafiti wengi wa kitiba husema kwamba matazamio mema, tumaini, na maoni mazuri huboresha maisha na afya ya mtu. Lakini si wote wenye maoni hayo. Watafiti fulani hupinga jambo hilo wakisema kwamba halipatani na sayansi. Wao husema kwamba magonjwa hayawezi kusababishwa na hisia.

      Bila shaka, maoni hayo yanayopinga umuhimu wa tumaini si mapya. Maelfu ya miaka iliyopita, mwanafalsafa Mgiriki Aristotle alipoulizwa maana ya tumaini, alijibu: “Ni ndoto ya mchana.” Na muda mrefu baadaye, mwanasiasa wa Marekani, Benjamin Franklin, alisema hivi waziwazi: “Anayeishi kwa tumaini atakufa njaa.”

      Basi, tumaini ni nini? Je, wakati wote tumaini ni njia ya kujifariji kwa kuota ndoto zisizoweza kutimia? Au, je, tumaini linahusisha mengi zaidi ya ndoto—kitu ambacho sote tunahitaji ili tuwe na afya na furaha, kitu ambacho kina msingi thabiti na manufaa?

  • Kwa Nini Tunahitaji Kuwa na Tumaini?
    Amkeni!—2004 | Aprili 22
    • Kwa Nini Tunahitaji Kuwa na Tumaini?

      VIPI ikiwa Daniel, yule mtoto aliyeugua kansa ambaye alitajwa mwanzoni mwa makala ya kwanza, angedumisha matumaini yake makubwa? Je, angepona kansa? Je, angekuwa hai leo? Hata watu wanaosema tumaini ni muhimu sana hawangedai hivyo. Na hapo kuna jambo muhimu. Tumaini si mambo yote. Tumaini si dawa ya kila kitu.

      Akihojiwa na Shirika la Habari la CBS Dakt. Nathan Cherney alionya kuhusu hatari za kukazia umuhimu wa tumaini kupita kiasi unaposhughulikia watu wagonjwa sana: “Tumesikia kuhusu waume wanaowakemea wake zao eti kwa sababu hawajatafakari vya kutosha, yaani, hawajawa na maoni yanayofaa.” Dakt. Cherney aliongezea hivi: “Maoni hayo yaliwafanya watu wafikiri kimakosa kwamba mtu anaweza kudhibiti ukuzi wa uvimbe wa kansa, na anapodhoofika, huenda wengine wakafikiri kwamba alishindwa kudhibiti uvimbe huo, lakini maoni hayo hayafai.”

      Kwa kweli, wale wanaougua ugonjwa usiotibika wanakabili pambano kali. Bila shaka wapendwa wao hawangependa kuzidisha matatizo yao kwa kuwafanya wahisi kwamba wana hatia. Basi, je, tukate kauli kwamba hakuna haja ya kuwa na tumaini?

      Hapana. Kwa mfano, badala ya kuutibu ugonjwa au kujaribu kurefusha maisha ya wagonjwa, daktari aliyetajwa juu, hupunguza maumivu yao na kuwafanya wastarehe kwa muda ambao watakuwa hai. Madaktari kama hao huamini sana umuhimu wa tiba zinazosaidia mtu kuwa mwenye furaha hata akiwa mgonjwa mahututi. Kuna uthibitisho wa kutosha kwamba tumaini linaweza kufanya hivyo na zaidi.

      Umuhimu wa Tumaini

      Dakt. W. Gifford-Jones, ambaye huandika habari za tiba, anasema: “Tumaini ni tiba yenye nguvu.” Alichunguza matokeo ya utafiti mbalimbali uliofanywa kubainisha umuhimu wa kuwategemeza kihisia watu wenye ugonjwa usio na tiba. Inasemekana kwamba utegemezo huo huwasaidia watu kudumisha tumaini na mtazamo unaofaa. Uchunguzi mmoja wa mwaka wa 1989 ulionyesha kwamba wagonjwa waliotegemezwa hivyo waliishi muda mrefu zaidi, lakini uchunguzi wa karibuni haujathibitisha wazi jambo hilo. Hata hivyo, uchunguzi mbalimbali umethibitisha kwamba wagonjwa wanaotegemezwa kihisia hawashuki moyo sana na hawapati maumivu mengi kama wale wasiotegemezwa.

      Fikiria uchunguzi mwingine uliokazia jinsi tumaini au kutokuwa na tumaini kunavyowaathiri watu wenye ugonjwa wa mishipa ya moyo. Wanaume zaidi ya 1,300 walichunguzwa kwa makini ili kubainisha ikiwa wana tumaini au hawana. Uchunguzi uliofanywa miaka kumi baadaye ulithibitisha kwamba zaidi ya asilimia 12 ya wanaume hao wanaugua ugonjwa fulani wa mishipa ya moyo. Kati ya hao, wale ambao hawakuwa na tumaini walikuwa maradufu ya wale waliokuwa na tumaini. Profesa-msaidizi wa afya na tabia katika Shule ya Afya ya Umma ya Harvard, Laura Kubzansky, anasema hivi: “Uthibitisho mwingi unaounga mkono kwamba ‘kuwa na maoni yanayofaa’ ni muhimu kwa afya hautokani na utafiti wa moja kwa moja, lakini huo ndio uchunguzi wa kwanza wa magonjwa ya moyo unaothibitisha jambo hilo.”

      Uchunguzi mwingine unaonyesha kwamba wale wanaoona afya yao kuwa mbaya hawaponi upesi baada ya upasuaji kama wale wenye maoni yanayofaa. Hata imeonekana kwamba watu wenye maoni mazuri huishi kwa muda mrefu. Utafiti mmoja ulionyesha jinsi wazee wanavyoathiriwa na maoni yanayofaa na yasiyofaa kuhusu kuzeeka. Wazee walipoonyeshwa habari zinazosema kwamba uzee unaleta hekima na uzoefu, walitembea wakiwa na nguvu nyingi zaidi. Matokeo hayo yalikuwa sawa na kufanya mazoezi kwa majuma 12!

      Kwa nini inaonekana kwamba tumaini na maoni mazuri huboresha afya? Huenda wanasayansi na madaktari hawaelewi vizuri akili na mwili wa wanadamu ili kujibu swali hilo kwa usahihi. Hata hivyo, wataalamu wanaochunguza jambo hilo wanaweza kutumia ujuzi wao kukisia. Kwa mfano, profesa mmoja wa mfumo wa neva anasema: “Inapendeza kuwa na furaha na tumaini. Ni hali nzuri ambayo haileti mfadhaiko mwingi, na humfanya mtu awe na afya bora. Hilo ni jambo moja ambalo watu wanaweza kujifanyia ili wajaribu kudumisha afya bora.”

      Huenda madaktari fulani, wanasaikolojia, na wanasayansi wakaona maoni hayo kuwa mapya, lakini si mapya kwa wanafunzi wa Biblia. Karibu miaka 3,000 iliyopita, Mfalme Sulemani mwenye hekima aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi juu ya jambo hilo: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri, lakini roho iliyopondeka huikausha mifupa.” (Methali 17:22) Ona usawaziko unaoonyeshwa hapa. Mstari huo hausemi kwamba moyo wenye shangwe ni dawa ya kila ugonjwa lakini unasema tu ni “dawa nzuri.”

      Kwa kweli, huenda ikafaa kuuliza, Ikiwa tumaini lingekuwa dawa, ni daktari yupi ambaye hangeipendekeza? Isitoshe, zaidi ya kuboresha afya, tumaini lina faida nyingine.

      Jinsi Maoni Mazuri na Mabaya Huathiri Maisha Yako

      Watafiti wamegundua kwamba watu wenye maoni mazuri hufaidika kwa njia nyingi. Wao hufaulu shuleni, kazini, na hata michezoni. Kwa mfano, uchunguzi ulifanywa kuhusu wanawake wanariadha. Makocha walitoa maoni yao kuhusu uwezo wa wanawake hao katika michezo. Wakati huohuo, wanawake hao walichunguzwa kwa makini ili kuona ikiwa wana tumaini. Matokeo yalikuwa kwamba matumaini yao yalionyesha kwa usahihi jinsi walivyofanya michezoni kuliko habari zote zilizotolewa na makocha wao. Kwa nini tumaini lina nguvu nyingi kadiri hiyo?

      Uchunguzi kuhusu maoni mabaya umefunua mambo mengi. Katika miaka ya 1960, uchunguzi ulifunua habari za ajabu kuhusu tabia za wanyama na kuwafanya watafiti kubuni dhana ya “kujifunza kuwa hoi.” Waligundua kwamba wanadamu pia wanaweza kupatwa na hali hiyo. Kwa mfano, katika uchunguzi mmoja kikundi kimoja cha watu kiliwekwa mahali penye kelele na kuambiwa kwamba wanaweza kuzima kelele hizo kwa kubonyeza vidude fulani. Walifaulu kuzizima.

      Kikundi cha pili kiliambiwa kifanye vivyo hivyo, lakini vidude hivyo havikufanya kazi. Kama unavyoweza kuwazia, wengi katika kikundi hicho cha pili walikata tamaa. Baadaye hata hawakutaka kuchukua hatua yoyote. Waliamini kwamba hawangefaulu hata wafanye nini. Hata katika kikundi hicho cha pili, wale waliokuwa na maoni mazuri hawakukata tamaa.

      Dakt. Martin Seligman, aliyesaidia kuanzisha baadhi ya uchunguzi huo aliamua kujitolea kuchunguza maoni mazuri na mabaya. Alichunguza kwa makini maoni ya watu wanaojiona kuwa hawawezi kufaulu. Alikata kauli kwamba maoni hayo mabaya huwazuia watu kufanya mambo mengi maishani au hata kuwafanya wasitende. Seligman anakata kauli hii kuhusu athari za maoni mabaya: “Nimefanya uchunguzi kwa miaka 25 na nimesadiki kwamba tukizoea kuamini kuwa sisi hujiletea mabaya na kila kitu tunachofanya hakitafaulu, kama watu wenye maoni yasiyofaa wanavyoamini, tutapatwa na mabaya hayo kila wakati.”

      Kama ilivyotajwa juu, wengine wanaweza kuona maoni hayo kuwa mapya leo, lakini si mapya kwa wanafunzi wa Biblia. Fikiria methali hii: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Naam, Biblia inaeleza wazi kwamba kuvunjika moyo na mawazo yasiyofaa yatakunyang’anya nguvu za kutenda. Hata hivyo, unaweza kufanya nini ili ushinde maoni mabaya na kuwa na maoni mazuri na tumaini maishani?

      [Picha katika ukurasa wa 4, 5]

      Tumaini linaweza kusaidia sana

  • Unaweza Kushinda Maoni Mabaya
    Amkeni!—2004 | Aprili 22
    • Unaweza Kushinda Maoni Mabaya

      UNAYAONAJE magumu unayokabili? Wataalamu wengi leo wanasema kwamba jibu la swali hilo linaonyesha kwa kiasi kikubwa ikiwa una maoni mazuri au mabaya. Sisi sote hukabili matatizo makubwa maishani, na baadhi yetu hukabili matatizo makubwa kuliko wengine. Hata hivyo, kwa nini watu wengine hushinda magumu, huwa tayari kujaribu tena hali wengine hukata tamaa baada ya kukumbwa na matatizo madogo tu?

      Kwa mfano, wazia unatafuta kazi. Unaenda kuhojiwa na hufanikiwi. Unalionaje jambo hilo baadaye? Huenda ukafikiri kwamba hutakikani na kuona kwamba ni tatizo la kudumu, labda ukisema, ‘Hakuna mtu anayeweza kuajiri mtu kama mimi. Sitapata kazi kamwe.’ Au hata unaweza kuruhusu hali hiyo iathiri maoni yako kuhusu mambo yote maishani na kukata kauli kwamba: ‘Siwezi kufanikiwa kamwe. Mimi ni bure kabisa.’ Hayo ni maoni mabaya sana.

      Kushinda Maoni Mabaya

      Unawezaje kushinda maoni mabaya? Hatua ya kwanza muhimu ni kutambua maoni hayo mabaya. Hatua inayofuata ni kupambana nayo. Tafuta sababu nyingine zinazoonyesha kwa nini hukupata kazi. Kwa mfano, je, ni kweli kwamba hukupata kazi kwa sababu hakuna mtu anayeweza kukuajiri? Au inawezekana kwamba mwajiri alikuwa anatafuta mtu mwenye sifa tofauti na zako?

      Ukichanganua hali kwa njia hiyo, utaondolea mbali maoni mabaya. Je, usipofaulu katika jambo moja, hiyo inamaanisha kwamba huwezi kufaulu kamwe? Au je, unaweza kufikiria sehemu nyingine za maisha yako ambapo umefaulu kwa kiasi fulani, kama vile katika mambo ya kiroho, uhusiano katika familia, au kudumisha marafiki? Jifunze kuondoa akilini mwako maoni mabaya na uyaone kuwa yenye kudhuru. Hata hivyo, je, kweli unaweza kuwa na hakika kwamba hutapata kazi kamwe? Kuna mambo mengine unayoweza kufanya ili kuondolea mbali maoni mabaya.

      Miradi Inayoweza Kukusaidia Kuwa na Maoni Mazuri

      Katika miaka ya karibuni, watafiti wamekuwa na maoni finyu na ya ajabu kuhusu maana ya tumaini. Wanasema kwamba tumaini linahusisha kuamini kwamba utatimiza miradi yako. Kama makala inayofuata inavyoonyesha, tumaini linahusisha mengi zaidi, lakini ufafanuzi huo unaweza kusaidia kwa njia kadhaa. Kuwa na maoni hayo kutatufanya kuwa na miradi inayoweza kutusaidia tuwe na maoni mazuri zaidi.

      Ili tuamini kwamba tunaweza kutimiza miradi ya wakati ujao, tunahitaji kuwa tumefanikiwa kufikia miradi fulani. Ikiwa unahisi kwamba hujafanikiwa, huenda ikafaa ufikirie kwa uzito kuhusu miradi unayojiwekea. Kwanza, una miradi yoyote? Ni rahisi sana kuwa na shughuli nyingi maishani kiasi cha kukosa kufikiria mambo muhimu tunayotaka kutimiza maishani. Kuhusiana na kanuni hiyo muhimu ya kutanguliza mambo fulani, Biblia pia ilisema hivi zamani: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.”—Wafilipi 1:10.

      Tukitambua mambo tunayopaswa kutanguliza, inakuwa rahisi kuweka miradi mbalimbali muhimu kama vile ya kiroho, katika familia, na katika maisha ya kawaida. Hata hivyo, ni muhimu kutoweka miradi mingi sana na kuwa na miradi ambayo tunaweza kutimiza kwa urahisi. Ikiwa ni vigumu sana kufikia mradi fulani, tunaweza kuvunjika moyo na kukata tamaa. Hivyo, ni bora kuugawanya mradi mmoja mkubwa uwe miradi midogo inayoweza kufikiwa kwa muda mfupi.

      “Penye nia pana njia.” Huo ni msemo wa kale na una ukweli fulani. Tunapoweka miradi fulani, tunahitaji nia, yaani tamaa na azimio la kuitimiza. Tunaweza kuimarisha azimio hilo kwa kufikiria faida za miradi yetu na thawabu tutakazopata tunapoitimiza. Bila shaka, matatizo yatatokea lakini tunapaswa kuyaona kama mambo tunayohitaji kukabili wala si vizuizi.

      Hata hivyo, tunahitaji pia kufikiria njia zinazofaa za kutimiza miradi yetu. Mwandishi C. R. Snyder, ambaye amefanya uchunguzi mwingi kuhusu umuhimu wa tumaini anadokeza kwamba mtu anapaswa kufikiria njia mbalimbali za kutimiza mradi fulani. Kwa hiyo njia moja isipofaulu tunaweza kutumia njia ya pili, ya tatu, na kadhalika.

      Snyder pia anapendekeza kujua wakati wa kubadilisha mradi. Ikiwa hatujafaulu kufikia mradi mmoja, tutavunjika moyo tukiendelea kuuhangaikia. Kwa upande mwingine, tukiubadili na mradi mwingine tunaoweza kufikia, tutapata tumaini.

      Biblia ina mfano unaoweza kutusaidia. Mfalme Daudi alikuwa na mradi wa kumjengea Mungu wake Yehova hekalu. Lakini Mungu alimwambia Daudi kwamba mwana wake Sulemani ndiye angepata pendeleo hilo. Badala ya kufuatilia mradi huo juu chini au kununa kwa sababu ya jambo hilo lenye kukatisha tamaa, Daudi alibadili mradi wake. Alitumia nguvu zake kukusanya pesa na vifaa vya ujenzi ambavyo mwana wake alihitaji ili kuukamilisha mradi huo.—1 Wafalme 8:17-19; 1 Mambo ya Nyakati 29:3-7.

      Hata tukifaulu kuimarisha tumaini letu kwa kushinda maoni mabaya na kuwa na miradi inayotusaidia kusitawisha maoni mazuri, huenda bado tukakosa tumaini. Jinsi gani? Mara nyingi sisi hukosa tumaini kwa sababu zisizoepukika. Tunapofikiria matatizo mengi yanayowapata wanadamu—umaskini, vita, ukosefu wa haki, uwezekano wa kuwa wagonjwa na kufa—tunawezaje kudumisha tumaini?

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Ikiwa hukupata kazi uliyotaka, je, unafikiri hutapata kazi kamwe?

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Mfalme Daudi alibadili mradi

  • Unaweza Kupata Wapi Tumaini la Kweli?
    Amkeni!—2004 | Aprili 22
    • Unaweza Kupata Wapi Tumaini la Kweli?

      SAA yako imesimama na inaonekana imeharibika. Unapotaka itengenezwe, inakubidi uchague kati ya mafundi wengi. Unaona matangazo mengi ya biashara, yote yakidai kwa uthabiti kwamba kuna mafundi wanaoweza kutengeneza saa, na madai mengine yanapingana. Namna gani ukitambua kwamba jirani yako ndiye aliyeibuni saa hiyo miaka mingi iliyopita? Isitoshe, anakuambia kwamba yuko tayari kukutengenezea bila malipo. Ni wazi kwamba utamchagua yeye aitengeneze, sivyo?

      Sasa linganisha saa hiyo na uwezo wako wa kutumaini. Ukigundua kwamba unapoteza tumaini, kama vile watu wengi wamepoteza tumaini wakati huu wenye taabu, utapata wapi msaada? Watu wengi wanadai kwamba wanaweza kusuluhisha tatizo hilo lakini mapendekezo mengi wanayotoa yanavuruga na yanapingana. Basi mbona usimwendee Yule aliyewaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kutumaini? Biblia inasema kwamba “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu” na kwamba yuko tayari sana kusaidia.—Matendo 17:27; 1 Petro 5:7.

      Maana Halisi ya Tumaini

      Maoni ya Biblia kuhusu tumaini yanahusisha mengi zaidi kuliko maoni ya kawaida ya madaktari, wanasayansi, na wanasaikolojia wa leo. Maneno ya lugha ya awali yaliyotumiwa katika Biblia ambayo yametafsiriwa “tumaini” yanamaanisha kungojea kwa hamu na kutarajia mema. Tumaini linahusisha mambo mawili. Linatia ndani kutamani mema na pia kuwa na msingi wa kuamini kwamba yatapatikana. Tumaini linalotokana na Biblia si ndoto tu. Linategemea mambo ya hakika na uthibitisho.

      Kwa njia hiyo, tumaini ni sawa na imani, ambayo lazima itegemee uthibitisho wala si imani isiyo na msingi. (Waebrania 11:1) Hata hivyo, Biblia inatofautisha kati ya imani na tumaini.—1 Wakorintho 13:13.

      Kwa mfano: Unapomwomba rafiki mpendwa akufanyie jambo fulani, unaweza kutumaini kwamba atakusaidia. Tumaini lako lina msingi kwa sababu unamwamini rafiki yako, unamjua vizuri, naye hukutendea kwa fadhili na ukarimu. Kuna uhusiano wa karibu kati ya imani na tumaini lako, na sifa hizo zinategemeana ingawa ni tofauti. Unawezaje kumtumaini Mungu jinsi hiyo?

      Msingi wa Tumaini

      Mungu ndiye chanzo cha tumaini la kweli. Katika nyakati za Biblia Yehova aliitwa “tumaini la Israeli.” (Yeremia 14:8) Tumaini lolote lenye kutegemeka ambalo watu wake walikuwa nalo lilitoka kwake; hivyo alikuwa tumaini lao. Tumaini hilo halikutegemea kutamani tu. Mungu aliwapa msingi thabiti wa tumaini. Kwa kushughulika nao kwa karne nyingi, alitoa ahadi nyingi na kuzitimiza. Kiongozi wao Yoshua aliwaambia hivi Waisraeli: “Mnajua vema . . . kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi.”—Yoshua 23:14.

      Miaka mingi imepita na bado Mungu anatimiza ahadi zake. Biblia ina ahadi nyingi za Mungu za kupendeza na inaeleza kwa usahihi jinsi zilivyotimia. Ahadi zake zilizotabiriwa zinategemeka sana hivi kwamba nyakati nyingine husemwa kana kwamba zilitimia tu wakati zilipotabiriwa.

      Ndiyo sababu tunaweza kuiita Biblia kitabu cha tumaini. Unapojifunza jinsi Mungu alivyoshughulika na wanadamu, sababu zako za kumtumaini zinaimarishwa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.”—Waroma 15:4.

      Mungu Hutupatia Tumaini Gani?

      Ni wakati gani tunapohitaji tumaini zaidi? Je, si wakati tunapokabili kifo? Hata hivyo, wakati ambapo mpendwa amekufa ndipo tumaini la wengi hudidimia. Ama kweli kifo hukatisha tamaa zaidi. Kinaandama kila mmoja wetu. Tunaweza kukiepuka kwa muda fulani lakini hatuwezi kukiondoa. Kwa kufaa, Biblia inakiita “adui wa mwisho.”—1 Wakorintho 15:26.

      Basi, tunawezaje kuwa na tumaini mpendwa wetu anapokufa? Mstari wa Biblia unaokiita kifo adui wa mwisho, unasema pia kwamba adui huyo ‘ataangamizwa.’ Yehova Mungu ana nguvu kuliko kifo. Amethibitisha hilo mara nyingi. Vipi? Kwa kuwafufua wafu. Biblia inazungumzia pindi tisa ambapo Mungu alitumia nguvu zake kuwafufua wafu.

      Katika kisa cha kupendeza, Yehova alimpa Mwana wake Yesu nguvu za kumfufua rafiki yake mpendwa, Lazaro, ambaye alikuwa amekufa kwa siku nne. Yesu hakufanya hivyo kisiri bali alifanya hivyo hadharani, mbele ya umati.—Yohana 11:38-48, 53; 12:9, 10.

      Huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini watu walifufuliwa? Je, hawakuzeeka na kufa tena baadaye?’ Bila shaka. Hata hivyo, kutokana na masimulizi hayo yenye kutegemeka kuhusu ufufuo, hatutamani tu kuwaona wapendwa wetu wakiwa hai tena; bali pia tuna sababu ya kuamini kwamba watafufuliwa. Kwa ufupi, tuna tumaini la kweli.

      Yesu alisema: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” (Yohana 11:25) Yeye ndiye atakayepewa nguvu na Yehova za kufufua wafu ulimwenguni pote. Yesu alisema: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Kristo].” (Yohana 5:28, 29) Naam, wote waliomo makaburini wana tumaini la kufufuliwa na kuishi katika paradiso duniani.

      Nabii Isaya alieleza ufufuo kwa njia nzuri sana. Alisema: “Wafu wako wataishi. Maiti wangu—wataamka. Amkeni, pigeni vigelegele kwa shangwe, enyi mnaokaa mavumbini! Kwa maana umande wako ni kama umande wa miholi, na dunia itawaacha hata wale wasiojiweza katika kifo waanguke katika kuzaliwa.”—Isaya 26:19.

      Je, hilo halifariji? Wafu wako katika hali salama kabisa, jinsi mtoto alivyo salama katika tumbo la uzazi la mama yake. Kwa kweli wale walio makaburini wamehifadhiwa vizuri katika kumbukumbu lisiloweza kujaa la Mungu Mweza-Yote. (Luka 20:37, 38) Na karibuni watarudishwa kwenye uhai, waingie katika ulimwengu wenye furaha na uchangamfu kama vile mtoto anayezaliwa anavyokaribishwa na familia yenye upendo! Kwa hiyo, kuna tumaini hata tukikabili kifo.

      Jinsi Tumaini Linavyoweza Kukusaidia

      Paulo anatufundisha mengi kuhusu umuhimu wa tumaini. Alisema kwamba tumaini ni sehemu muhimu ya mavazi ya silaha za kiroho, yaani, kofia ya chuma. (1 Wathesalonike 5:8) Alimaanisha nini? Katika nyakati za Biblia, kwa kawaida askari-jeshi alivaa kofia ya chuma juu ya kofia ya sufu au ya ngozi alipoenda vitani. Kofia hiyo ilimsaidia kukinga kichwa chake kisijeruhiwe na kusababisha kifo. Paulo alikuwa akikazia nini? Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa, ndivyo tumaini linavyolinda akili, yaani, uwezo wetu wa kufikiri. Ikiwa una tumaini thabiti linalopatana na makusudi ya Mungu, utakuwa na amani ya akili hata unapopatwa na magumu. Ni nani asiyehitaji kofia hiyo ya chuma?

      Paulo alitumia mfano mwingine unaohusianisha tumaini na mapenzi ya Mungu. Aliandika hivi: “Tumaini hilo tunalo kama nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara.” (Waebrania 6:19) Paulo alikuwa amevunjikiwa meli mara kadhaa, hivyo alijua umuhimu wa nanga. Mabaharia walipokumbwa na dhoruba walishusha nanga. Ikiwa nanga ingeshikamana kabisa na sakafu ya bahari, huenda meli ingeokoka dhoruba hiyo badala ya kusukumwa hadi ufuoni na kugonga miamba.

      Vivyo hivyo, ikiwa tunaona ahadi za Mungu kuwa tumaini “hakika na imara,” zinaweza kutusaidia kushinda matatizo ya nyakati zetu zenye taabu. Yehova anaahidi kwamba karibuni wanadamu hawatakumbwa na vita, uhalifu, huzuni, au hata kifo. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 10.) Kushikilia tumaini hilo kwaweza kutusaidia kuepuka msiba na kutuchochea kuishi kulingana na kanuni za Mungu badala ya kufuata roho ya ukosefu wa adili iliyoenea sana ulimwenguni leo.

      Tumaini ambalo Yehova anatoa linakuhusu wewe binafsi pia. Anataka uishi kama vile alivyokusudia. Anataka “watu wa namna zote waokolewe.” Jinsi gani? Kwanza kila mtu anapaswa “kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Wachapishaji wa gazeti hili wanakusihi upate ujuzi kuhusu kweli ya Neno la Mungu, ujuzi ambao utakuwezesha kupata uzima. Tumaini ambalo Mungu atakupa linapita matumaini yoyote yale ambayo ulimwengu unaweza kukupa.

      Ukiwa na tumaini hilo hutakata tamaa kamwe kwa kuwa Mungu anaweza kukupa nguvu unazohitaji kutimiza miradi yoyote uliyoweka ambayo inapatana na kusudi lake. (2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:13) Je, huhitaji tumaini kama hilo? Kwa hiyo, ikiwa unahitaji tumaini, au umekuwa ukilitafuta, jipe moyo. Tumaini liko karibu. Unaweza kulipata!

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

      Sababu za Kuwa na Tumaini

      Habari hizi zilizo katika Biblia zinaweza kuimarisha tumaini lako:

      ◼ Mungu anaahidi wakati ujao wenye furaha.

      Neno lake linasema kwamba dunia yote itakuwa paradiso itakayokaliwa na familia ya wanadamu yenye umoja na furaha.—Zaburi 37:11, 29; Isaya 25:8; Ufunuo 21:3, 4.

      ◼ Mungu hawezi kusema uwongo.

      Anachukia uwongo wa kila aina. Yehova ni mtakatifu wala hana hatia hata kidogo, kwa hiyo hawezi kusema uwongo.—Methali 6:16-19; Isaya 6:2, 3; Tito 1:2; Waebrania 6:18.

      ◼ Mungu ana nguvu zisizo na kikomo.

      Yehova pekee ndiye mweza-yote. Hakuna kitu chochote ulimwenguni kinachoweza kumzuia kutimiza ahadi zake.—Kutoka 15:11; Isaya 40:25, 26.

      ◼ Mungu anataka uishi milele.

      —Yohana 3:16; 1 Timotheo 2:3, 4.

      ◼ Mungu anatutakia mema.

      Yeye hazingatii kasoro na makosa yetu, bali anaangalia sifa zetu nzuri na jitihada zetu. (Zaburi 103:12-14; 130:3; Waebrania 6:10) Anatumaini kwamba tutafanya mema naye hufurahi tunapofanya hivyo.—Methali 27:11.

      ◼ Mungu anaahidi kukusaidia kutimiza miradi inayopatana na kusudi lake.

      Watumishi wake hawapaswi kukata tamaa. Mungu hutoa kwa ukarimu roho yake takatifu, ambayo ndiyo kani yenye nguvu zaidi, ili itusaidie.—Wafilipi 4:13.

      ◼ Mungu anapaswa kutumainiwa.

      Kwa kuwa yeye hutegemeka na ni mwaminifu kabisa, hatakutamausha kamwe.—Zaburi 25:3.

      [Picha katika ukurasa wa 12]

      Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa, ndivyo tumaini linavyolinda akili

      [Picha katika ukurasa wa 12]

      Kama nanga, tumaini thabiti linaweza kukuimarisha

      [Hisani]

      Courtesy René Seindal/Su concessione del Museo Archeologico Regionale A. Salinas di Palermo

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki