-
Yehova ni Mungu wa MaaganoMnara wa Mlinzi—1998 | Februari 1
-
-
Miaka kadhaa baadaye, baada ya kuitahini imani ya Abrahamu—hata kufikia hatua ya utayari wake wa kumtoa Isaka mwana wake mpendwa akiwa dhabihu—Yehova aliirudia ahadi yake kwa Abrahamu akisema hivi: “Katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako [“mbegu yako,” NW] kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako [“mbegu yako,” NW] utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako [“mbegu yako,” NW] mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwanzo 22:15-18) Mara nyingi ahadi hiyo iliyopanuliwa huitwa agano la Kiabrahamu, nalo lile agano jipya la baadaye lingeunganishwa kwa ukaribu pamoja nalo.
7. Idadi ya mbegu ya Abrahamu ilianza kuongezekaje, na ni hali gani zilizowaongoza kuwa wakazi huko Misri?
7 Baada ya muda, Isaka alikuwa na wavulana mapacha, Esau na Yakobo. Yehova alimchagua Yakobo kuwa mzazi wa zamani wa Mbegu Iliyoahidiwa. (Mwanzo 28:10-15; Waroma 9:10-13) Yakobo alikuwa na wana 12. Kwa wazi, sasa ulikuwa wakati wa mbegu ya Abrahamu kuanza kuongezeka. Wana wa Yakobo walipokuwa watu wazima, wengi wakiwa na familia zao wenyewe, njaa kuu iliwalazimisha wote kuhamia huko Misri ambako, kwa mwongozo wa kimungu, mwana wa Yakobo, Yosefu, alikuwa ametayarisha njia. (Mwanzo 45:5-13; 46:26, 27) Baada ya miaka michache, hiyo njaa kuu katika Kanaani ilipungua. Lakini familia ya Yakobo ilikaa Misri—hapo kwanza wakiwa wageni-waalikwa lakini baadaye wakiwa watumwa. Haikuwa hadi mwaka wa 1513 K.W.K., miaka 430 baada ya Abrahamu kuvuka Eufrati, ambapo Musa aliwaongoza wazao wa Yakobo kutoka Misri hadi kwenye uhuru. (Kutoka 1:8-14; 12:40, 41; Wagalatia 3:16, 17) Yehova sasa angelipa uangalifu wa pekee agano lake pamoja na Abrahamu.—Kutoka 2:24; 6:2-5.
“Agano la Zamani”
8. Yehova alifanya nini na wazao wa Yakobo katika Sinai, nalo lilihusuje agano la Kiabrahamu?
8 Yakobo na wanawe walipohamia Misri, walikuwa familia iliyo pana, lakini wazao wao waliondoka Misri wakiwa jamii kubwa ya makabila yenye watu wengi. (Kutoka 1:5-7; 12:37, 38) Kabla ya kuwaleta Kanaani, Yehova aliwaongoza kuelekea kusini hadi chini ya mlima fulani ulioitwa Horebu (au, Sinai) Arabuni. Hapo, alifanya agano pamoja nao. Hilo lilikuja kuitwa “agano la zamani” kwa kulihusisha “agano jipya.” (2 Wakorintho 3:14) Kwa njia ya hilo agano la zamani, Yehova alitekeleza kwa njia ya kielezi utimizo wa agano lake pamoja na Abrahamu.
9. (a) Yehova aliahidi mambo gani manne kupitia agano la Kiabrahamu? (b) Ni matazamio gani zaidi yaliyowezeshwa na agano la Yehova pamoja na Israeli, na kwa masharti gani?
9 Yehova alieleza Israeli masharti ya agano hilo kwa kusema: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” (Kutoka 19:5, 6) Yehova alikuwa ameahidi kwamba mbegu ya Abrahamu (1) ingepata kuwa taifa kubwa, (2) ingepewa ushindi dhidi ya adui zake, (3) ingerithi nchi ya Kanaani, na (4) ingekuwa njia ambayo kwayo mataifa yangebarikiwa. Sasa alifunua kwamba ikiwa wangezitii amri zake, wao wenyewe wangeweza kurithi baraka hizo wakiwa watu wake wa pekee, Israeli, “ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” Je, Waisraeli walikubali kuingia katika agano hilo? Walijibu kwa umoja hivi: “Hayo yote aliyoyasema BWANA tutayatenda.”—Kutoka 19:8.
10. Yehova aliwapangaje Waisraeli kuwa taifa, naye alitarajia nini kwao?
10 Kwa sababu hiyo, Yehova aliwapanga Waisraeli kuwa taifa. Aliwapa sheria zilizoongoza ibada na maisha ya kijamii. Pia aliwaandalia tabenakulo (baadaye, akawapa hekalu katika Yerusalemu) na ukuhani wa kutoa utumishi mtakatifu katika hilo tabenakulo. Kushika hilo agano kulimaanisha kuzitii sheria za Yehova, na hasa, kumwabudu yeye pekee. Ya kwanza kati ya Amri Kumi ambazo ndizo zilizokuwa kiini cha sheria hizo ilikuwa: “Mimi ni BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa. Usiwe na miungu mingine ila mimi.”—Kutoka 20:2, 3.
Baraka Kupitia Agano la Sheria
11, 12. Ahadi katika agano la zamani zilitimizwa kuelekea Israeli katika njia gani?
11 Je, ahadi katika agano la Sheria zilitimizwa kuelekea Israeli? Je, Israeli lilipata kuwa “taifa takatifu”? Wakiwa wazao wa Adamu, Waisraeli walikuwa watenda-dhambi. (Waroma 5:12) Hata hivyo, chini ya Sheria, dhabihu zilitolewa ili kufunika dhambi zao. Kuhusu dhabihu zilizotolewa katika Siku ya Kufunika ya kila mwaka, Yehova alisema hivi: “Siku hiyo upatanisho utafanywa kwa ajili yenu, ili kuwatakasa [“safisha,” NW]; nanyi mtatakaswa [“mtakuwa safi,” NW] na dhambi zenu zote mbele za BWANA.” (Mambo ya Walawi 16:30) Kwa hiyo, lilipokuwa lenye uaminifu, Israeli lilikuwa taifa takatifu, lililosafishwa kwa ajili ya utumishi wa Yehova. Lakini hali hiyo ya usafi ilitegemea kutii kwao Sheria na kutoa dhabihu kwa kuendelea.
12 Je, Israeli lilipata kuwa “ufalme wa makuhani”? Tangu mwanzo kabisa, lilikuwa ufalme, Yehova akiwa Mfalme wa kimbingu. (Isaya 33:22) Zaidi, agano la Sheria lilitia ndani maandalizi kwa ajili ya umaliki wa kibinadamu, hivi kwamba baadaye Yehova aliwakilishwa na wafalme waliotawala huko Yerusalemu. (Kumbukumbu la Torati 17:14-18) Lakini, je, Israeli lilikuwa ufalme wa makuhani? Lilikuwa na ukuhani uliotoa utumishi mtakatifu kwenye tabenakulo. Lile tabenakulo (baadaye, hekalu) lilikuwa kitovu cha ibada safi kwa ajili ya Waisraeli na pia kwa ajili ya wasio Waisraeli. Nalo taifa lilikuwa njia ya pekee ya kupata kweli iliyofunuliwa kwa wanadamu. (2 Mambo ya Nyakati 6:32, 33; Waroma 3:1, 2) Waisraeli wote waaminifu, wala si makuhani wa Kilawi tu, walikuwa “mashahidi” wa Yehova. Israeli lilikuwa “mtumishi,” wa Yehova aliyefanyizwa ili ‘azitangaze sifa zake.’ (Isaya 43:10, 21) Wageni wengi wanyenyekevu waliona nguvu za Yehova kwa niaba ya watu wake na kuvutiwa na ibada safi. Wakapata kuwa wageuzwa-imani. (Yoshua 2:9-13) Lakini kabila moja tu ndilo kwa kweli lililotumikia likiwa makuhani watiwa-mafuta.
Wageuzwa-Imani Katika Israeli
13, 14. (a) Kwa nini yaweza kusemwa kwamba wageuzwa-imani hawakuwa washiriki katika agano la Sheria? (b) Wageuzwa-imani walikujaje kuwa chini ya agano la Sheria?
13 Hao wageuzwa-imani walikuwa na msimamo gani? Yehova alipofanya agano lake, lilikuwa tu pamoja na Israeli; wale wa “kundi kubwa la watu waliochangamana mno,” wajapokuwapo, hawakutajwa kuwa washiriki. (Kutoka 12:38; 19:3, 7, 8) Wazaliwa wao wa kwanza hawakutiwa ndani wakati ambapo hesabu ya bei ya fidia kwa ajili ya mzaliwa wa kwanza wa Israeli ilipigwa. (Hesabu 3:44-51) Miongo kadhaa baadaye nchi ya Kanaani ilipogawanywa kati ya makabila ya Waisraeli, hakuna kitu chochote kilichowekwa kando kwa ajili ya waamini wasio-Waisraeli. (Mwanzo 12:7; Yoshua 13:1-14) Kwa nini? Kwa sababu agano la Sheria halikufanywa pamoja na wageuzwa-imani. Lakini wanaume wageuzwa-imani walitahiriwa kwa kutii Sheria. Walishika kanuni zake, wakanufaika na maandalizi yake. Wageuzwa-imani na vilevile Waisraeli wakaja kuwa chini ya agano la Sheria.—Kutoka 12:48, 49; Hesabu 15:14-16; Waroma 3:19.
14 Kwa kielelezo, mgeuzwa-imani akiua mtu fulani kiaksidenti angeweza, kama vile Mwisraeli, kukimbilia jiji la makimbilio. (Hesabu 35:15, 22-25; Yoshua 20:9) Katika Siku ya Kufunika dhabihu ilitolewa “kwa ajili ya mkutano wote wa Israeli.” Wakiwa sehemu ya hilo kutaniko, wageuzwa-imani walishiriki katika matukio hayo na walifunikwa na hiyo dhabihu. (Mambo ya Walawi 16:7-10, 15, 17, 29; Kumbukumbu la Torati 23:7, 8) Wageuzwa-imani walishirikiana kwa ukaribu sana na Israeli lililokuwa chini ya Sheria hivi kwamba kwenye Pentekoste mwaka wa 33 W.K ‘ufunguo wa kwanza wa ufalme’ ulipotumiwa kwa niaba ya Wayahudi, wageuzwa-imani walinufaika pia. Tokeo ni kwamba, “Nikolausi, mgeuzwa-imani wa Antiokia,” akawa Mkristo na alikuwa miongoni mwa “wanaume saba wenye kuthibitishwa” waliowekwa rasmi ili kushughulikia mahitaji ya kutaniko la Yerusalemu.—Mathayo 16:19; Matendo 2:5-10; 6:3-6; 8:26-39.
Yehova Abariki Mbegu ya Abrahamu
15, 16. Agano la Yehova pamoja na Abrahamu lilitimizwaje chini ya agano la Sheria?
15 Wazao wa Abrahamu wakiwa wamepangwa kuwa taifa chini ya Sheria, Yehova aliwabariki kulingana na ahadi yake kwa huyo mzee wa ukoo. Mwaka wa 1473 K.W.K., Yoshua, mwandamizi wa Musa, aliongoza Israeli hadi Kanaani. Mgawanyo wa nchi uliofuata miongoni mwa makabila ulitimiza ahadi ya Yehova ya kuipa mbegu ya Abrahamu hiyo nchi. Israeli lilipokuwa lenye uaminifu, Yehova alitimiza ahadi yake ya kulipa ushindi juu ya adui zake. Hilo hasa lilikuwa kweli wakati wa utawala wa Mfalme Daudi. Kufikia wakati wa Solomoni mwana wa Daudi, sehemu ya tatu ya agano la Kiabrahamu ilitimizwa. “Yuda na Israeli walikuwa wengi kama mchanga wa pwani kwa wingi, wakila, na kunywa, na kufurahi.”—1 Wafalme 4:20.
16 Ingawa hivyo mataifa wangejibarikije kupitia Israeli, mbegu ya Abrahamu? Kama vile tayari imetajwa, Israeli walikuwa watu wa pekee wa Yehova, mwakilishi wake miongoni mwa mataifa. Upesi kabla ya Israeli kuingia Kanaani, Musa alisema hivi: “Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake.” (Kumbukumbu la Torati 32:43) Wageni wengi waliitikia. “Kundi kubwa la watu waliochangamana mno” tayari walikuwa wamefuata Israeli kutoka Misri, wakashuhudia nguvu za Yehova nyikani, wakasikia mwaliko wa Musa wa kushangilia. (Kutoka 12:37, 38) Baadaye, Ruthu Mmoabi aliolewa na Boazi Mwisraeli, naye akawa mzazi wa zamani wa Mesiya. (Ruthu 4:13-22) Yehonadabu Mkeni na wazao wake na yule Mwethiopia Ebed-meleki walijitofautisha kwa kushikamana sana na kanuni za haki wakati ambapo Waisraeli wa asili hawakuwa waaminifu. (2 Wafalme 10:15-17; Yeremia 35:1-19; 38:7-13) Chini ya Milki ya Uajemi, wageni wengi walipata kuwa wageuzwa-imani na kupigana pamoja na Israeli dhidi ya adui zake.—Esta 8:17, kielezi-chini.
Agano Jipya Lahitajiwa
17. (a) Ni kwa nini Yehova aliukataa ufalme wa Israeli wa kaskazini na wa kusini? (b) Ni nini kilichoongoza kwenye kukataliwa kabisa kwa Wayahudi?
17 Hata hivyo, ili lipokee utimizo kamili wa ahadi ya Mungu, taifa la Mungu la pekee lilipaswa kuwa lenye uaminifu. Halikuwa hivyo. Ni kweli, kulikuwa na Waisraeli wa imani yenye kutokeza. (Waebrania 11:32–12:1) Hata hivyo, katika pindi nyingi hilo taifa liligeukia miungu ya kipagani, likitumaini kunufaika kimwili. (Yeremia 34:8-16; 44:15-18) Watu mmoja-mmoja waliitumia vibaya Sheria au kuipuuza tu. (Nehemia 5:1-5; Isaya 59:2-8; Malaki 1:12-14) Baada ya kifo cha Solomoni, Israeli liligawanyika kuwa ufalme wa kaskazini na wa kusini. Ufalme wa kaskazini ulipothibitika kuwa wenye kuasi kabisa, Yehova alitangaza hivi: “Kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi.” (Hosea 4:6) Ufalme wa kusini pia uliadhibiwa vikali kwa sababu ya kuthibitika kwake kutokuwa mwaminifu kwa agano. (Yeremia 5:29-31) Wayahudi walipomkataa Yesu akiwa Mesiya, hali kadhalika Yehova aliwakataa. (Matendo 3:13-15; Waroma 9:31–10:4) Mwishowe, Yehova alifanya mpango mpya ili atekeleze utimizo kamili wa agano la Kiabrahamu.—Waroma 3:20.
18, 19. Yehova alifanya mpango upi mpya ili agano la Kiabrahamu liweze kutimizwa kwa njia kamili?
18 Mpango huo mpya ulikuwa agano jipya. Yehova alikuwa ametabiri hilo aliposema hivi: “Angalia, siku zinakuja, asema BWANA, nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda . . . Agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema BWANA; Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”—Yeremia 31:31-33.
19 Hilo ndilo agano jipya ambalo Yesu alirejezea katika Nisani 14, 33 W.K. Pindi hiyo, alifunua kwamba agano lililoahidiwa lilikuwa karibu kufanywa kati ya wanafunzi wake pamoja na Yehova, Yesu akiwa mpatanishi. (1 Wakorintho 11:25; 1 Timotheo 2:5; Waebrania 12:24) Kupitia agano hilo jipya, ahadi ya Yehova kwa Abrahamu ingekuwa na utimizo wenye utukufu na wenye kudumu, kama vile tutakavyoona kwenye makala inayofuata.
-
-
Baraka Kubwa Zaidi Kupitia Agano JipyaMnara wa Mlinzi—1998 | Februari 1
-
-
Mataifa Yabarikiwa Kupitia Mbegu ya Abrahamu
5, 6. Katika utimizo wa msingi na wa kiroho wa agano la Kiabrahamu, ni nani aliye Mbegu ya Abrahamu, na ni taifa jipi lililokuwa la kwanza kupokea baraka kupitia yeye?
5 Yehova alimwahidi Abrahamu hivi: “Katika uzao wako [“mbegu yako,” NW] mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:18) Chini ya agano la zamani, wageni wengi wenye tabia-pole walibarikiwa kupitia ushirikiano wao na Israeli, mbegu ya kitaifa ya Abrahamu. Hata hivyo, katika utimizo wake wa kimsingi na wa kiroho, Mbegu ya Abrahamu ilikuwa mtu mmoja aliye mkamilifu. Paulo alieleza hilo aliposema hivi: “Ahadi zilisemwa kwa Abrahamu na kwa mbegu yake. Haisemi: ‘Na kwa hizo mbegu,’ kama katika kisa cha nyingi za namna hiyo, bali kama katika kisa cha moja: ‘Na kwa mbegu yako,’ ambaye ni Kristo.”—Wagalatia 3:16.
6 Ndiyo, Yesu ndiye Mbegu ya Abrahamu, na kupitia Yeye mataifa hupokea baraka iliyo bora zaidi kuliko yoyote ambayo iliwezekana kwa Israeli la kimwili. Kwa kweli, taifa la kwanza kupokea baraka hiyo lilikuwa Israeli lenyewe. Mara baada ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., mtume Petro alikiambia kikundi cha Wayahudi hivi: “Nyinyi ndio wana wa manabii na wa agano ambalo Mungu aliagana pamoja na baba zenu wa zamani, akimwambia Abrahamu, ‘Na katika mbegu yako familia zote za dunia zitabarikiwa.’ Baada ya kumwinua Mtumishi wake, Mungu alimtuma kwenu kwanza ili kuwabariki nyinyi kwa kugeuzia mbali kila mmoja kutoka kwenye vitendo vyenu viovu.”—Matendo 3:25, 26.
7. Ni mataifa yapi yaliyobarikiwa kupitia Yesu, Mbegu ya Abrahamu?
7 Punde si punde hiyo baraka ilipanuliwa kuwafikia Wasamaria kisha kuwafikia Wasio-Wayahudi. (Matendo 8:14-17; 10:34-48) Wakati fulani kati ya mwaka wa 50 na wa 52 W.K., Paulo aliwaandikia Wakristo waliokuwa Galatia katika Asia Ndogo hivi: “Andiko, likitangulia kuona kwamba Mungu angetangaza watu wa mataifa kuwa waadilifu kwa sababu ya imani, lilitangaza habari njema kimbele kwa Abrahamu, yaani: ‘Kupitia wewe mataifa yote yatabarikiwa.’ Kwa sababu hiyo wale washikamanao sana na imani wanakuwa wenye kubarikiwa pamoja na Abrahamu mwaminifu.” (Wagalatia 3:8, 9; Mwanzo 12:3) Ijapokuwa Wakristo wengi katika Galatia walikuwa “watu wa mataifa,” walibarikiwa kupitia Yesu kwa sababu ya imani yao. Katika njia gani?
8. Kwa Wakristo wa siku ya Paulo, kubarikiwa kupitia Mbegu ya Abrahamu kulitia ndani nini, na mwishowe, ni wangapi waliopokea baraka hiyo?
8 Paulo aliwaambia hivi Wakristo Wagalatia, hata wawe wa malezi gani: “Ikiwa nyinyi ni wa Kristo, kwa kweli nyinyi ni mbegu ya Abrahamu, warithi kuhusiana na ahadi.” (Wagalatia 3:29) Kwa Wagalatia hao, baraka kupitia Mbegu ya Abrahamu ilitia ndani kuwa kwao washiriki katika agano jipya na pia kuwa warithi-wenzi wa Yesu, washiriki pamoja na Yesu katika mbegu ya Abrahamu. Hatujui idadi ya watu wa Israeli la kale. Twajua tu kwamba lilikuja kuwa “kama mchanga wa pwani kwa wingi.” (1 Wafalme 4:20) Hata hivyo, twajua idadi ya mwisho ya washiriki wa Yesu katika hiyo mbegu ya kiroho—144,000. (Ufunuo 7:4; 14:1) Washiriki hao 144,000 hutoka katika “kila kabila na ulimi na watu na taifa” la wanadamu na hushiriki katika kuwatolea wengine zaidi baraka za hilo agano la Kiabrahamu.—Ufunuo 5:9.
-