Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Heshimu Ndoa kwa Kuwa Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Januari 15
    • 9 Yehova alimwambia Adamu hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.” (Mwa. 2:24) Hilo linamaanisha nini? Ni lazima mahusiano ya zamani pamoja na marafiki na watu wa ukoo yabadilike. Ni lazima kila mwenzi wa ndoa atumie wakati pamoja na mume au mke wake na kumpa uangalifu. Mtu hapaswi kuendelea kutanguliza marafiki au watu wa ukoo na kupuuza familia yake mpya; na wenzi hao wa ndoa hawapaswi kuruhusu wazazi waingilie maamuzi au mizozano ya familia yao. Ni lazima sasa wenzi hao wa ndoa washikamane pamoja. Huo ndio mwongozo wa Mungu.

      10. Ni nini kitakachowasaidia wenzi wa ndoa wasitawishe ushikamanifu?

      10 Hata katika nyumba ambazo zimegawanyika kidini, ushikamanifu unathawabisha. Dada mmoja mwenye mume ambaye si mwamini alisema hivi: “Ninamshukuru sana Yehova kwa kunifundisha jinsi ya kujitiisha chini ya mume wangu na kumheshimu sana. Kwa sababu ya kuendelea kuwa mshikamanifu, nimefurahia kukaa kwa miaka 47 katika ndoa yenye heshima na upendo wa kudumu.” (1 Kor. 7:10, 11; 1 Pet. 3:1, 2) Kwa hiyo, jitahidi sana kumfanya mwenzi wako wa ndoa ajihisi salama. Kwa maneno na matendo yako, tafuta njia za kumhakikishia mwenzi wako kwamba unamwona kuwa mtu wa maana zaidi duniani. Kwa kadiri ambavyo inakutegemea wewe, usiache mtu yeyote wala kitu chochote kije kati yako na mwenzi wako. (Soma Methali 5:15-20.)

  • Heshimu Ndoa kwa Kuwa Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Januari 15
    • Umoja Unafanya Ndoa Iwe na Nguvu

      11, 12. Akila na Prisila walishirikiana jinsi gani (a) nyumbani, (b) katika kazi yao ya kimwili, na (c) katika huduma ya Kikristo?

      11 Mtume Paulo alipozungumza kuhusu marafiki wake wa karibu Akila na Prisila, hakumtaja mmoja bila kumtaja mwenzake. Wenzi hao wa ndoa wenye umoja ni mfano mzuri unaoonyesha jambo ambalo Mungu alimaanisha aliposema kwamba mume na mke wanapaswa kuwa “mwili mmoja.” (Mwa. 2:24) Sikuzote walifanya mambo pamoja katika nyumba yao, katika kazi yao ya kimwili, na katika huduma ya Kikristo. Kwa mfano, Paulo alipofika Korintho mara ya kwanza, Akila na Prisila walimkaribisha kwa fadhili ili akae katika nyumba yao, ambamo inaelekea aliishi baadaye kwa muda huku akiendelea na utendaji wake. Baadaye, huko Efeso, Akila na Prisila walitumia nyumba yao kwa ajili ya mikutano ya kutaniko na walishirikiana katika kuwasaidia wapya, kama vile Apolo, kukua kiroho. (Mdo. 18:2, 18-26) Kisha, wenzi hao wa ndoa wenye bidii walienda Roma, ambako walitoa tena nyumba yao ili itumiwe kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. Baadaye, walirudi Efeso na kuwatia nguvu akina ndugu.—Rom. 16:3-5.

      12 Kwa muda fulani, Akila na Prisila walishirikiana na Paulo kufanya kazi ya kutengeneza mahema. Kwa mara nyingine tena, tunaona wenzi hao wa ndoa wakishirikiana pamoja bila mashindano wala ugomvi. (Mdo. 18:3) Hata hivyo, bila shaka ndoa yao ilikuwa katika hali nzuri sana ya kiroho kwa sababu ya wakati walioshiriki pamoja katika utendaji mbalimbali wa Kikristo. Walijulikana kotekote kuwa ‘wafanyakazi wenzi katika Kristo Yesu,’ iwe ni Korintho, Efeso, au Roma. (Rom. 16:3) Walishirikiana bega kwa bega ili kuendeleza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme mahali popote ambapo walitumika.

      13, 14. (a) Ni hali gani zinazoweza kuharibu umoja katika ndoa? (b) Taja mambo fulani ambayo wenzi wa ndoa wanaweza kufanya ili kutia nguvu kifungo chao wakiwa “mwili mmoja.”

      13 Kwa kweli, ndoa inakuwa na nguvu wakati wenzi wa ndoa wanapokuwa na umoja katika utendaji mbalimbali na miradi yao. (Mhu. 4:9, 10) Inasikitisha kwamba wenzi wengi wa ndoa leo wanatumia muda mfupi sana pamoja. Kila mmoja wao anafanya kazi yake ya kimwili kwa saa nyingi. Wengine wanasafiri-safiri sana kwa ajili ya kazi yao ya kimwili au wanahamia nchi za kigeni bila mwenzi wao ili kufanya kazi na kutuma pesa nyumbani. Hata wakiwa nyumbani, wenzi fulani wa ndoa wanajikuta wametengana kwa sababu ya muda wanaotumia kutazama televisheni, kufanya mambo wanayopenda, kucheza michezo ya video na michezo mingine, au kutumia Intaneti. Je, ndivyo ilivyo katika nyumba yenu? Ikiwa ndivyo ilivyo, je, mnaweza kurekebisha hali zenu ili mtumie wakati zaidi pamoja? Namna gani mkishirikiana katika kazi za kila siku kama vile kutayarisha vyakula, kuosha vyombo, au kutunza bustani? Je, mnaweza kushirikiana katika kuwatunza watoto au kuwasaidia wazazi wenu wanaozeeka?

      14 Jambo la maana zaidi ni kutumia wakati pamoja kwa ukawaida katika utendaji unaohusiana na ibada ya Yehova. Kuzungumzia andiko la kila siku pamoja na kushiriki katika ibada ya familia ni nafasi bora zaidi za kuhakikisha kwamba familia yenu ina umoja katika fikira na miradi. Mshiriki pia pamoja katika huduma. Ikiwezekana, mjaribu kufanya upainia pamoja, hata ikiwa hali zenu zinawaruhusu kufanya hivyo kwa mwezi mmoja au mwaka mmoja tu. (Soma 1 Wakorintho 15:58.) Dada mmoja ambaye alifanya upainia pamoja na mume wake anasema hivi: “Huduma ni moja ya njia ambazo zilituwezesha kutumia wakati pamoja na kuzungumza kikweli. Kwa sababu sote wawili tulikuwa na mradi mmoja wa kuwasaidia wengine kiroho, nilihisi kwamba tulishirikiana kwa umoja kabisa. Nilimkaribia zaidi si kwa sababu tu ni mume wangu bali pia kwa sababu ni rafiki mzuri.” Unaposhiriki na mwenzi wako katika utendaji wa maana, mapendezi yako, mambo unayotanguliza, na mazoea yako yatapatana hatua kwa hatua na ya mwenzi wako, na mwishowe mtaanza kufikiri, kuhisi, na kutenda mkiwa “mwili mmoja” kama Akila na Prisila.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki