-
Mkono wa Yehova Haujawa MfupiUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Na hili ndilo agano kwa upande wangu pamoja nao, niondoleapo mbali dhambi zao.” (Waroma 11:26, 27)
-
-
Mkono wa Yehova Haujawa MfupiUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
19. Yehova anafanya agano gani pamoja na Israeli wa Mungu?
19 Sasa Yehova anafanya agano pamoja na Israeli wa Mungu. Tunasoma hivi: “Tena katika habari zangu, hili ndilo agano langu nao, asema BWANA; roho yangu iliyo juu yako, na maneno yangu niliyoyatia kinywani mwako, hayataondoka kinywani mwako, wala kinywani mwa wana [“wazao,” “NW”] wako, wala kinywani mwa wajukuu wako, asema BWANA, tangu leo na hata milele.” (Isaya 59:21) Iwe maneno hayo yalitumika au hayakutumika kumhusu Isaya mwenyewe, hakika yalitimizwa katika Yesu, aliyehakikishiwa kwamba “ataona uzao wake.” (Isaya 53:10) Yesu alisema yale aliyokuwa amejifunza kutoka kwa Yehova, na roho ya Yehova ilikaa juu yake. (Yohana 1:18; 7:16) Basi ni vizuri kwamba hata ndugu zake na warithi wenzake, ambao ni washirika wa Israeli wa Mungu, wanapokea roho takatifu ya Yehova na kuhubiri ujumbe ambao wamejifunza kutoka kwa Baba yao wa kimbingu. Wote ‘wamefundishwa na Yehova.’ (Isaya 54:13; Luka 12:12; Matendo 2:38) Iwe ni kupitia Isaya au ni kupitia Yesu ambaye Isaya anamfananisha kiunabii, sasa Yehova anafanya agano kwamba hatabadilisha kamwe nafasi yao ichukuliwe na watu wengine, bali atawatumia milele wakiwa mashahidi wake. (Isaya 43:10) Hata hivyo, “wazao” wao ambao pia wanafaidika na agano hilo ni akina nani?
20. Ahadi ya Yehova kwa Abrahamu ilitimizwaje katika karne ya kwanza?
20 Nyakati za kale Yehova alimwahidi Abrahamu hivi: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:18) Kupatana na jambo hilo, mabaki wachache wa Waisraeli wa asili waliomkubali Mesiya waliingia katika mataifa mengi, wakahubiri habari njema juu ya Kristo. Kwa kuanza na Kornelio, watu wengi wasiotahiriwa wa Mataifa yasiyo ya Kiyahudi ‘walijibariki’ kupitia Yesu, Mbegu ya Abrahamu. Wakawa sehemu ya Israeli wa Mungu na sehemu ya pili ya ile mbegu ya Abrahamu. Wao ni sehemu ya “taifa takatifu” la Yehova, ambalo utume wake ni ‘kutangaza kotekote sifa bora kabisa za yeye aliyewaita wao kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.’—1 Petro 2:9; Wagalatia 3:7-9, 14, 26-29.
21. (a) Israeli wa Mungu wametokeza “wazao” gani nyakati za kisasa? (b) “Wazao” hao wanafarijiwaje na agano au mkataba ambao Yehova amefanya pamoja na Israeli wa Mungu?
21 Leo inaonekana kwamba idadi kamili ya Israeli wa Mungu imekusanywa. Na bado, mataifa yanaendelea kubarikiwa—tena sana. Jinsi gani? Ni kwa vile Israeli wa Mungu wamekuwa na “wazao,” yaani wanafunzi wa Yesu walio na tumaini la kupata uhai wa milele katika dunia-paradiso. (Zaburi 37:11, 29) “Wazao” hao wanafundishwa na Yehova pia na kuagizwa katika njia zake. (Isaya 2:2-4) Ingawa hawabatizwi kwa roho takatifu wala hawaonwi kuwa washiriki katika agano jipya, wanaimarishwa na roho takatifu ya Yehova kushinda vipingamizi vyote ambavyo Shetani huwawekea wanapofanya kazi ya kuhubiri. (Isaya 40:28-31) Sasa idadi yao inafikia mamilioni na inaendelea kuongezeka, huku wakitokeza wazao wao wenyewe. Agano au mkataba ambao Yehova amefanya na watiwa-mafuta huhakikishia “wazao” hao kwamba Yehova ataendelea kuwatumia kuwa wasemaji wake hadi milele.—Ufunuo 21:3, 4, 7.
-