-
Manufaa za Habari NjemaMnara wa Mlinzi—2002 | Januari 1
-
-
Manufaa za Habari Njema
“BWANA amenitia mafuta niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo . . .kuwafariji wote waliao.”—ISAYA 61:1, 2.
1, 2. (a) Yesu alijifunua kuwa nani, na jinsi gani? (b) Ni mambo gani yenye kunufaisha yaliyotokana na habari njema alizotangaza Yesu?
SIKU moja ya Sabato mapema katika huduma yake, Yesu alikuwa katika sinagogi huko Nazareti. Kulingana na simulizi hilo, “a[li]pewa hati-kunjo ya nabii Isaya, naye akafungua hiyo hati-kunjo na kupata mahali palipokuwa pameandikwa: ‘Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kutangaza habari njema.’” Yesu aliendelea kusoma ujumbe huo wa kiunabii. Kisha akaketi na kusema: “Leo andiko hili ambalo mmetoka tu kusikia limetimizwa.”—Luka 4:16-21.
2 Kwa kusema hivyo, Yesu alijitambulisha kuwa mweneza-evanjeli aliyetabiriwa, mhubiri wa habari njema na mfariji. (Mathayo 4:23) Naye alitangaza habari njema kama nini! Aliwaambia hivi wasikilizaji wake: “Mimi ni nuru ya ulimwengu. Yeye anifuataye mimi hatatembea kwa vyovyote katika giza, bali atakuwa na nuru ya uhai.” (Yohana 8:12) Pia alisema: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yohana 8:31, 32) Naam, Yesu alikuwa na “semi za uhai udumuo milele.” (Yohana 6:68, 69) Nuru, uhai, uhuru—kwa kweli hayo ni mambo yenye kunufaisha tunayopaswa kuyathamini sana!
3. Ni habari gani njema zilizohubiriwa na wanafunzi wa Yesu?
3 Baada ya Pentekoste 33 W.K., wanafunzi waliendelea na kazi ya Yesu ya kueneza evanjeli. Walihubiri “habari njema [hii] ya ufalme” kwa Waisraeli na kwa watu wa mataifa. (Mathayo 24:14; Matendo 15:7; Waroma 1:16) Wale walioitikia walipata kumjua Yehova Mungu. Walikombolewa kutoka katika utumwa wa kidini na kuwa sehemu ya taifa jipya la kiroho, “Israeli wa Mungu,” ambalo washiriki wake wanatarajia kutawala milele mbinguni pamoja na Bwana wao, Yesu Kristo. (Wagalatia 5:1; 6:16; Waefeso 3:5-7; Wakolosai 1:4, 5; Ufunuo 22:5) Hilo lilikuwa jambo lenye kunufaisha kwelikweli!
Kueneza Evanjeli Leo
4. Kazi ya kuhubiri habari njema inatimizwaje leo?
4 Leo, Wakristo watiwa-mafuta, wanaoungwa mkono na “umati mkubwa” unaoongezeka wa “kondoo wengine,” wanaendelea kutimiza kazi ya kiunabii ambayo hapo awali ilikuwa imepewa Yesu. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Kwa sababu hiyo, habari njema zinahubiriwa kwa kiwango kikubwa zaidi ya wakati mwingine wowote. Katika nchi na maeneo 235, Mashahidi wa Yehova wameenda ‘kuwahubiri wanyenyekevu habari njema; kuwaganga waliovunjika moyo, na kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao. Kutangaza mwaka wa BWANA uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu; kuwafariji wote waliao.’ (Isaya 61:1, 2) Kwa hiyo, kazi ya Kikristo ya kueneza evanjeli inazidi kunufaisha wengi na kuwapa faraja ya kweli “wale walio katika namna yoyote ya dhiki.”—2 Wakorintho 1:3, 4.
-
-
Manufaa za Habari NjemaMnara wa Mlinzi—2002 | Januari 1
-
-
Habari Njema Zinazoleta Manufaa za Milele
6. Ni habari njema gani zinazohubiriwa leo?
6 Mashahidi wa Yehova huhubiri habari bora zaidi ya zote. Wao hufungua Biblia zao na kuwaonyesha watu wenye kupendezwa kwamba Yesu alitoa uhai wake kuwa dhabihu ili kuwawezesha wanadamu wamkaribie Mungu, wasamehewe dhambi, na wawe na tumaini la kupata uhai udumuo milele. (Yohana 3:16; 2 Wakorintho 5:18, 19) Wanatangaza kwamba Ufalme wa Mungu umesimamishwa mbinguni chini ya Yesu Kristo, Mfalme aliyetiwa mafuta, na kwamba hivi karibuni ufalme huo utaondoa uovu duniani na kusimamia kazi ya kurudisha Paradiso. (Ufunuo 11:15; 21:3, 4)
-